Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunapaswa “Kumjibu Kila Mtu” Jinsi Gani?

Tunapaswa “Kumjibu Kila Mtu” Jinsi Gani?

“Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, . . . ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”KOL. 4:6.

1, 2. (a) Simulia kisa kinachoonyesha umuhimu wa kuuliza maswali yaliyochaguliwa vizuri. (Tazama picha kwenye ukurasa huu.) (b) Kwa nini hatuhitaji kuogopa kuzungumzia habari ngumu?

MIAKA kadhaa iliyopita, dada Mkristo alikuwa akizungumza na mume wake asiye mwamini kuhusu Biblia. Zamani, mume huyo alikuwa mfuasi wa dini fulani ya Kikristo. Walipokuwa wakizungumza, mume alisema kwamba anaamini Utatu. Mke alipotambua kwamba huenda mume hajui maana ya fundisho la Utatu, kwa busara alimuuliza hivi: “Je, unaamini kwamba Mungu ni Mungu, Yesu ni Mungu, na roho takatifu ni Mungu; nao si Mungu watatu bali Mungu mmoja?” Mume alishangaa na kujibu hivi: “Hapana, siamini hivyo!” Kisha wakawa na mazungumzo mazuri kuhusu jinsi Mungu alivyo kikweli.

2 Kisa hicho kinaonyesha umuhimu wa kuuliza kwa busara maswali yaliyochaguliwa vizuri. Kinakazia pia jambo hili muhimu: Hatuhitaji kuogopa kuzungumzia habari ngumu kama vile Utatu, moto wa mateso, au kuwapo kwa Muumba. Tukimtegemea Yehova na kutumia mazoezi anayoandaa, tunaweza kutoa jibu lenye kusadikisha linaloweza kugusa mioyo ya wasikilizaji wetu. (Kol. 4:6) Acheni sasa tuchunguze wahubiri wenye ustadi hutumia njia gani kuzungumzia habari kama hizo. Tutachunguza  jinsi ya (1) kuuliza maswali yatakayomchochea mtu kujieleza, (2) kujadiliana kwa kutumia Maandiko, na (3) kutumia mifano ili kukazia jambo kuu.

ULIZA MASWALI ILI UWACHOCHEE WASIKILIZAJI KUJIELEZA

3, 4. Kwa nini ni muhimu kutumia maswali ili kuelewa anachoamini mtu? Toa mfano.

3 Maswali yanaweza kutusaidia kuelewa mambo ambayo mtu anaamini. Kwa nini hilo ni muhimu? Andiko la Methali 18:13 linasema hivi: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” Kwa kweli, kabla ya kumfafanulia mtu maoni ya Biblia kuhusu fundisho fulani, tunapaswa kujaribu kuelewa anachoamini hasa. Tusipofanya hivyo, huenda tukatumia muda mwingi kuzungumzia jambo ambalo haamini!—1 Kor. 9:26.

4 Tuseme kwamba tunazungumza na mtu kuhusu fundisho la moto wa mateso. Si kila mtu anayeamini kwamba kuna mahali halisi penye moto wa mateso. Wengi wanaamini kwamba ni hali ya mtu kutokuwa na uhusiano mzuri na Mungu. Hivyo, tunaweza kusema hivi: “Kwa kuwa watu wana maoni tofauti kuhusu moto wa mateso, ningependa kusikia maoni yako.” Baada ya kusikiliza jibu lake, itakuwa rahisi kumsaidia kuelewa maoni ya Biblia kuhusu habari hiyo.

5. Maswali yanaweza kutusaidiaje kuelewa kwa nini mtu anaamini fundisho fulani?

5 Maswali yanayoulizwa kwa busara yanaweza pia kutusaidia kujua kwa nini mtu anaamini fundisho fulani. Kwa mfano, namna gani tukikutana na mtu anayesema haamini kuwapo kwa Mungu? Huenda ikawa rahisi kufikiri kwamba mtu huyo ameathiriwa na mambo aliyojifunza shuleni, kama vile nadharia ya mageuzi. (Zab. 10:4) Hata hivyo, baadhi ya watu hawamwamini Mungu kwa sababu wameona au kukabili mateso makali sana maishani mwao. Kwa sababu hiyo, huenda ikawa vigumu kwao kuamini kwamba kuna Muumba mwenye upendo. Hivyo, ikiwa mwenye nyumba ana shaka kuhusu kuwapo kwa Mungu, tunaweza kumuuliza hivi: “Je, umekuwa ukiamini hivyo sikuzote?” Akisema hapana, tunaweza kumuuliza ikiwa kuna jambo fulani hususa lililomfanya atilie shaka kuwapo kwa Mungu. Jibu lake linaweza kutusaidia kujua njia bora ya kumsaidia kiroho.—Soma Methali 20:5.

6. Tunapaswa kufanya nini baada ya kuuliza swali?

6 Baada ya kuuliza swali, tunahitaji kusikiliza kwa makini mtu anapojibu na kuonyesha kwamba tunaelewa hisia zake. Kwa mfano, labda mtu atasema kwamba msiba fulani uliompata ndio uliomfanya awe na shaka kuhusu kuwapo kwa Muumba mwenye upendo. Kabla ya kumthibitishia kwamba kuna Mungu, tunapaswa kumhurumia na kumwambia kwamba si vibaya kuuliza kwa nini tunateseka. (Hab. 1:2, 3) Tukiongea naye kwa subira na upendo, tunaweza kumchochea atake kujifunza mengi zaidi. *

JADILIANA KWA KUTUMIA MAANDIKO

Ustadi wetu kwenye huduma unategemea nini Hasa? (Tazama fungu la 7)

7. Kwa kadiri kubwa, ustadi wetu katika huduma unategemea nini?

7 Acheni sasa tuchunguze jinsi tunavyoweza kujadiliana kwa kutumia Maandiko. Kwa kweli, Biblia ndicho kifaa muhimu zaidi katika huduma yetu. Inatusaidia kuwa na ‘uwezo kamili, na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Tim. 3:16, 17) Kwa kadiri kubwa, ustadi wetu katika huduma hautegemei idadi ya maandiko tunayosoma, bali jinsi tunavyojadiliana na kufafanua maandiko tunayosoma. (Soma Matendo 17:2, 3.) Kwa mfano, fikiria hali tatu zifuatazo.

8, 9. (a) Tunaweza kutumia njia gani kujadiliana na mtu anayeamini kwamba Yesu ni Mungu? (b) Ni njia gani nyingine yenye matokeo unayotumia kujadiliana na watu kuhusu jambo hilo?

 8 Hali ya kwanza: Tunakutana na mtu katika huduma anayeamini kwamba Yesu ni Mungu. Ni maandiko gani tunayoweza kutumia ili kujadiliana kuhusu jambo hilo? Tunaweza kumwomba asome maneno haya ya Yesu yaliyonukuliwa katika Yohana 6:38: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.” Baada ya kusoma andiko hilo, tunaweza kumuuliza hivi: “Ikiwa Yesu ni Mungu, ni nani aliyemtuma Yesu kutoka mbinguni? Je, si ni wazi kwamba Huyo aliyemtuma ni mkuu kuliko Yesu? Kwa kweli, anayemtuma mwingine ni mkuu kuliko anayetumwa.”

9 Tunaweza pia kusoma Wafilipi 2:9. Katika andiko hilo, mtume Paulo anataja alichofanya Mungu baada ya Yesu kufa na kufufuliwa. Andiko hilo linasema hivi: “Mungu alimpandisha [Yesu] kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine.” Ili kumsaidia mtu aelewe andiko hilo, tunaweza kuuliza hivi: “Ikiwa kabla ya kufa Yesu alilingana na Mungu, na baadaye Mungu akampandisha kwenye cheo cha juu zaidi, je, huoni kwamba hilo linamfanya Yesu awe mkuu kuliko Mungu? Lakini je, kuna yeyote aliye mkuu kuliko Mungu?” Ikiwa mtu huyo anaheshimu Neno la Mungu na ana moyo mnyoofu, huenda njia hiyo ya kufikiri ikamchochea kuchunguza zaidi jambo hilo.—Mdo. 17:11.

10. (a) Tunawezaje kujadiliana na mtu anayeamini fundisho la moto wa mateso? (b) Ni njia gani nyingine yenye matokeo unayotumia kujadiliana na watu kuhusu moto wa mateso?

10 Hali ya pili: Mwenye nyumba ambaye ni mfuasi mwenye bidii wa dini anaamini kwamba watu wabaya watateswa milele katika moto wa mateso. Huenda anaamini hivyo kwa kuwa anatamani kuona waovu wakiadhibiwa kwa sababu ya matendo yao mabaya. Tutatumiaje maandiko kujadiliana na mtu anayeamini hivyo? Kwanza, tunaweza kumhakikishia kwamba waovu wataadhibiwa. (2 The. 1:9) Kisha, tunaweza kumwomba asome andiko la Mwanzo 2:16 na 17 linaloonyesha kwamba adhabu ya dhambi ni kifo. Tunaweza kueleza kwamba wanadamu wote wanazaliwa wakiwa watenda-dhambi kwa sababu ya dhambi ya Adamu. (Rom. 5:12) Hata hivyo, tunaweza kutaja kwamba Mungu hakusema lolote kuhusu adhabu ya moto wa mateso. Kisha tunaweza kumuuliza hivi: “Ikiwa Adamu na Hawa walikabili hatari ya kuteswa milele, je, halingekuwa tendo la haki ikiwa Mungu angewaonya mapema?” Halafu tunaweza kusoma andiko la Mwanzo 3:19. Katika andiko hilo, Mungu anataja adhabu  ambayo Adamu na Hawa wangepata baada ya kutenda dhambi. Lakini hakusema lolote kuhusu moto wa mateso. Badala yake, alimwambia Adamu kwamba angerudi mavumbini. Tunaweza kuuliza hivi: “Je, ingekuwa ni haki kwa Mungu kumwambia Adamu kwamba angerudi mavumbini ikiwa kwa kweli angeenda katika moto wa mateso?” Ikiwa mtu huyo yuko tayari kusikiliza, maswali hayo yanaweza kumsaidia kufikiria kwa uzito zaidi jambo hilo.

11. (a) Tunaweza kutumia njia gani kujadiliana na mtu anayeamini kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni? (b) Ni njia gani nyingine yenye matokeo unayotumia kujadiliana na watu kuhusu kwenda mbinguni?

11 Hali ya tatu: Katika huduma yetu, tunakutana na mtu anayeamini kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni. Imani hiyo inaweza kuathiri jinsi mwenye nyumba anavyoifafanua Biblia. Kwa mfano, tuseme kwamba tunataka kuzungumza naye kuhusu andiko la Ufunuo 21:4. (Soma.) Huenda mtu huyo akadhani kwamba baraka zinazotajwa katika mstari huo ni kwa ajili ya wale watakaoishi mbinguni. Tunawezaje kujadiliana naye? Badala ya kusoma maandiko zaidi ili kutoa uthibitisho, tunaweza kukazia fikira wazo lililo katika andiko hilo. Linasema kwamba “kifo hakitakuwapo tena.” Tunaweza kumuuliza ikiwa anakubali kwamba ni lazima jambo liwepo ili isemwe kwamba halitakuwapo tena. Inaelekea kwamba atakubali hilo. Kisha tunaweza kutaja kwamba hakuna kifo mbinguni; watu hufa duniani tu. Basi, ni wazi kwamba andiko la Ufunuo 21:4 linarejelea baraka za wakati ujao hapa duniani.—Zab. 37:29.

TUMIA MIFANO KUKAZIA JAMBO KUU

12. Kwa nini Yesu alitumia mifano?

12 Yesu alitumia maswali na pia mifano alipohubiri. (Soma Mathayo 13:34, 35.) Mifano ya Yesu ilifunua nia ya wale waliomsikiliza. (Mt. 13:10-15) Pia, mifano ilifanya mafundisho ya Yesu yavutie na kukumbukwa. Tunawezaje kutumia mifano tunapofundisha?

13. Tunaweza kutumia mfano gani kuonyesha kwamba Mungu ni mkuu kuliko Yesu?

13 Kwa kawaida, mifano rahisi hufaa zaidi. Kwa mfano, tunapoeleza kwamba Mungu ni mkuu kuliko Yesu, tunaweza kujaribu njia ifuatayo. Tunaweza kutaja kwamba Mungu na Yesu walitumia mfano wa familia ili kuonyesha uhusiano wao. Mungu alimrejelea Yesu kuwa Mwana wake, naye Yesu alimrejelea Mungu kuwa Baba yake. (Luka 3:21, 22; Yoh. 14:28) Kisha, tunaweza kumuuliza mwenye nyumba hivi: “Ikiwa unataka kunifundisha kwamba watu wawili wanalingana, ni uhusiano gani wa familia utakaotumia ili nielewe?” Huenda mwenye nyumba akasema kwamba atatumia uhusiano wa mapacha au watoto wa familia moja. Akijibu hivyo, tunaweza kumwambia kwamba mfano huo ni mzuri. Kisha tunaweza kumuuliza hivi: “Ikiwa mimi na wewe tunaweza kutumia mfano huo kuonyesha uhusiano wa watu wanaolingana, je, si ni wazi kwamba Yesu, yule Mwalimu Mkuu, angetumia mfano huo? Hata hivyo, alimrejelea Mungu kuwa Baba yake. Basi, Yesu alionyesha wazi kwamba Mungu ameishi kwa muda mrefu zaidi na ana mamlaka kuliko yeye.”

14. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba ni jambo lisilopatana na akili kwa Mungu kumtumia Ibilisi kuwatesa watu katika moto wa mateso?

14 Fikiria mfano mwingine. Baadhi ya watu wanaamini kwamba Shetani ndiye “anayesimamia” moto wa mateso. Mfano ufuatao unaweza kumsaidia mzazi kuona kwamba si jambo linalopatana na akili kwa Mungu kumtumia Ibilisi kuwatesa watu katika moto wa mateso. Tunaweza kuuliza hivi: “Tuseme kwamba mtoto wako ni mkaidi sana na anafanya mambo mengi mabaya. Utafanya nini?” Inaelekea mzazi  huyo atasema kwamba atamrekebisha mtoto wake. Huenda atajaribu tena na tena kumsaidia kuacha kutenda mabaya. (Met. 22:15) Kisha, tunaweza kumuuliza mzazi huyo atafanya nini mtoto wake akikataa kubadilika. Wazazi wengi watasema kwamba watamwadhibu. Halafu tunaweza kuuliza hivi: “Vipi ukijua kwamba mtu fulani mwovu ndiye aliyemchochea mtoto wako kuwa mkaidi?” Bila shaka mzazi huyo atamkasirikia mtu huyo. Ili kukazia jambo kuu, tunaweza kumuuliza hivi: “Kwa kuwa unajua kwamba mtu fulani mwovu ndiye aliyemchochea mtoto wako kuwa mkaidi, je, utamwomba mtu huyo amwadhibu mtoto wako?” Bila shaka atasema kwamba hawezi kufanya hivyo. Basi, ni wazi kwamba Mungu hawezi kumtumia Shetani kuwaadhibu watu walewale ambao Ibilisi mwenyewe amewashawishi kufanya mambo mabaya!

DUMISHA MAONI YENYE USAWAZIKO

15, 16. (a) Kwa nini hatupaswi kutarajia kwamba kila mtu atakubali ujumbe wa Ufalme? (b) Je, ni lazima tuwe na kipaji ili tufundishe kwa ustadi? Eleza. (Tazama pia sanduku lenye kichwa “ Mfululizo Unaotusaidia Kujibu.”)

15 Tunajua kwamba si kila mtu atakayekubali ujumbe wa Ufalme. (Mt. 10:11-14) Wengine hawatakubali hata tukiuliza maswali yanayofaa, tukitumia njia bora ya kujadiliana nao, na hata tukitumia mifano bora kabisa. Kwa kweli, ni wachache tu waliokubali mafundisho ya Yesu, yule Mwalimu mkuu zaidi aliyepata kuishi duniani!—Yoh. 6:66; 7:45-48.

16 Kwa upande mwingine, tunaweza kuwa stadi katika huduma yetu hata ikiwa tunahisi kwamba hatuna kipaji cha kufundisha. (Soma Matendo 4:13.) Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba ‘wale wote walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele’ watakubali habari njema. (Mdo. 13:48) Hivyo, na tuendelee kusitawisha na kudumisha maoni yenye usawaziko kuhusu sisi wenyewe na wale tunaowahubiria habari njema ya Ufalme. Acheni tutumie kikamili mazoezi anayoandaa Yehova huku tukiwa na uhakika kwamba tutanufaika na kuwanufaisha wale wanaotusikiliza. (1 Tim. 4:16) Yehova anaweza kutusaidia kujua jinsi tunavyopaswa “kumjibu kila mtu.” Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, njia moja itakayotusaidia kufanikiwa katika huduma yetu ni kufuata ile inayoitwa Kanuni Bora.

^ fu. 6 Tazama makala yenye kichwa “Je, Inawezekana Kuamini Kuna Muumba?” katika Mnara wa Mlinzi, Oktoba 1, 2009.