Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo wa Kweli Wanaliheshimu Neno la Mungu

Wakristo wa Kweli Wanaliheshimu Neno la Mungu

“Neno lako ni kweli.”​—YOH. 17:17.

1. Ulipozungumza na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, ni jambo gani kuu ambalo uliona linawafanya kuwa tofauti na vikundi vingine vya kidini?

FIKIRIA wakati ulipokuwa na mazungumzo ya maana kwa mara ya kwanza na Shahidi wa Yehova. Unakumbuka nini kuhusu mazungumzo hayo? Wengi wangejibu, ‘Nilivutiwa sana kuona Shahidi huyo akitumia Biblia ili kujibu maswali yangu yote.’ Tulifurahi kama nini kujua kusudi la Mungu kuelekea dunia, inakuwaje tunapokufa, na tumaini la ufufuo kwa ajili ya wapendwa wetu waliokufa!

2. Taja baadhi ya sababu zinazokufanya uithamini Biblia.

2 Hata hivyo, tulipoendelea kujifunza, tulitambua kwamba Biblia ina mengi zaidi kuliko majibu tu ya maswali yetu kuhusu uhai, kifo, na wakati ujao. Tulianza kuithamini Biblia na kuiona kuwa kitabu chenye manufaa zaidi ulimwenguni. Mashauri ya Biblia hayabadiliki, na wale wanaoyafuata kwa makini watakuwa na maisha yenye furaha na mafanikio. (Soma Zaburi 1:1-3.) Sikuzote Wakristo wa kweli wameikubali Biblia, “si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 The. 2:13) Kuchunguza kwa ufupi historia kutakazia tofauti kati ya wale wanaoliheshimu kikweli Neno la Mungu na wale wanaolipuuza.

SUALA GUMU LATATULIWA

3. Ni suala gani ambalo lilitishia umoja wa kutaniko la Kikristo katika karne ya kwanza, na ni nini kilichokuwa hatarini?

3 Miaka 13 baada ya mtu wa kwanza wa Mataifa asiyetahiriwa, Kornelio, kutiwa mafuta na roho takatifu, suala fulani lilitokea ambalo lilitishia kuharibu umoja wa kutaniko la Kikristo. Watu wengi wa Mataifa walikuwa wakikubali imani ya Kikristo. Swali lilikuwa, Je, wanaume wangepaswa kutahiriwa kulingana na desturi ya Wayahudi kabla ya kubatizwa? Hilo halikuwa swali rahisi kwa Myahudi kujibu. Wayahudi ambao walifuata Sheria hawangeweza hata kuingia ndani ya nyumba ya mtu wa Mataifa, wala kushirikiana kwa uchangamfu na mtu huyo. Wakristo Wayahudi walikuwa tayari wakiteswa vikali kwa sababu ya kuacha dini yao ya asili. Ikiwa sasa wangewakaribisha miongoni mwao watu wa Mataifa wasiotahiriwa, hilo lingeongeza tu uadui kati ya Wayahudi waliofuata Sheria na Wakristo na hivyo kufanya Wakristo walaumiwe zaidi.​—Gal. 2:11-14.

4. Ni nani walioitwa ili kutatua suala hilo, na kuhusu hilo, ni maswali gani ambayo yangejitokeza katika akili za watazamaji?

4 Katika mwaka wa 49 W.K., mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu, wao wenyewe wakiwa Wayahudi waliotahiriwa, ‘walikusanyika pamoja ili waliangalie jambo hilo.’ (Mdo. 15:6) Mkutano wao ulikuwa, si kama mikutano ya kidini yenye kuchosha na ambayo hujadili mambo mengi yasiyo na maana, bali ulikuwa mkutano wenye kuchochea kuhusu mafundisho ya Biblia. Kila mtu aliyekuwepo alitoa maoni yake kuhusu suala hilo. Je, wangeruhusu mapendezi ya mtu binafsi au ubaguzi uathiri uamuzi wao? Je, wanaume hao wazee wenye kutegemeka wangeahirisha uamuzi wao hadi chuki ya kidini dhidi ya Wakristo katika Israeli iwe imepungua? Au je, wangelegeza hatimaye msimamo wao na kukubali jambo fulani ambalo kwa kweli hawakuamini kwamba lilikuwa sawa ili tu wafikie makubaliano?

5. Ni katika njia gani muhimu mkutano huo huko Yerusalemu katika mwaka wa 49 W.K. unatofautiana na makongamano ya kanisa yaliyofanywa katika karne zilizofuata?

5 Katika makongamano ya kidini leo, ni jambo la kawaida kwa viongozi wa kidini kulegeza msimamo wao au kufanya kampeni ya kuungwa mkono katika makongamano hayo. Hata hivyo, katika mkutano uliofanywa huko Yerusalemu, mitume na wanaume wazee hawakulegeza msimamo wao; wala hawakufanya kampeni ya kuungwa mkono. Badala yake, kwa ujumla wote walifikia uamuzi mmoja. Hilo lingewezekanaje? Sababu ni kwamba hata ingawa walikuwa na maoni yaliyotofautiana, wote waliokuwepo waliliheshimu Neno la Mungu, na walitumia maandiko hayo matakatifu ili kutatua suala hilo.​—Soma Zaburi 119:97-101.

6, 7. Maandiko yalitumiwaje kutatua suala la tohara?

6 Andiko ambalo liliwasaidia kutatua suala hilo lilikuwa Amosi 9:11, 12. Kama linavyonukuliwa katika Matendo 15:16, 17, andiko hilo linasomeka hivi: “Nitarudi na kukijenga upya kibanda cha Daudi ambacho kimeanguka chini; nami nitayajenga upya mabomoko yake na kukisimamisha tena, ili watu wanaobaki wamtafute Yehova kwa bidii, pamoja na watu wa mataifa yote, watu wanaoitwa kwa jina langu, asema Yehova.”

7 Huenda mtu akabisha na kusema hivi, ‘lakini ngoja kidogo, andiko hilo halisemi kwamba haikuwa lazima kwa waamini wa Mataifa kutahiriwa.’ Hilo ni kweli. Lakini hata Wakristo Wayahudi wangelielewa andiko hilo kwa njia hiyo. Kwa nini? Kwa sababu Wakristo Wayahudi waliwaona watu wa Mataifa waliotahiriwa kuwa ndugu zao, tofauti na jinsi walivyowaona wale ambao hawakuwa wametahiriwa. (Kut. 12:48, 49) Kwa mfano, kulingana na tafsiri ya Bagster ya Septuajinti, andiko la Esta 8:17 linasomeka hivi: “Watu wengi wa Mataifa walitahiriwa na wakawa Wayahudi.” Hivyo, Maandiko yalipotabiri kwamba wale waliobaki wa nyumba ya Israeli (Wayahudi na Wayahudi wageuzwa-imani waliotahiriwa) pamoja na “watu wa mataifa yote” (watu wa Mataifa wasiotahiriwa) wangekuja kuwa taifa moja kwa ajili ya jina la Mungu, ujumbe ulikuwa wazi. Watu wa Mataifa waliotaka kuwa Wakristo hawakuhitaji kutahiriwa.

8. Kwa nini ujasiri ulihitajiwa ili kufikia uamuzi ambao ulifanywa?

8 Wakristo hao wanyoofu waliongozwa na Neno la Mungu na pia roho yake na hivyo wakafikia “kauli moja.” (Mdo. 15:25) Hata ingawa inaelekea uamuzi huo ungewafanya Wakristo Wayahudi wateswe zaidi, wale waliokuwa waaminifu walifuata kwa ujasiri uamuzi uliotegemea kabisa Biblia.​—Mdo. 16:4, 5.

TOFAUTI YAWA WAZI ZAIDI

9. Ni jambo gani kuu ambalo lilichangia mafundisho ya uwongo kuharibu ibada ya kweli, na ni fundisho gani muhimu la Kikristo ambalo lilipotoshwa?

9 Mtume Paulo alitabiri kwamba baada ya kifo cha mitume, imani ya Kikristo ingechafuliwa na mafundisho ya uwongo. (Soma 2 Wathesalonike 2:3, 7.) Miongoni mwa wale ambao hawangevumilia “fundisho lenye afya” kulikuwa na watu fulani wenye mapendeleo. (2 Tim. 4:3) Katika siku zake, Paulo aliwaonya wazee hivi: “Kutoka katikati yenu ninyi wenyewe watu watasimama na kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:30) Kitabu The New Encyclopædia Britannica kinaeleza hivi kuhusu sababu moja kuu iliyofanya Wakristo fulani waanze kufikiri kwa njia yenye kupotoka: “Wakristo waliosoma kwa kiasi fulani falsafa ya Kigiriki walianza kuhisi uhitaji wa kueleza imani yao kwa kutumia falsafa hiyo, kwa sababu ya kutosheleza tamaa yao ya kupenda elimu na pia ili kuwasaidia wapagani wenye elimu kukubali Ukristo.” Fundisho moja muhimu la Kikristo ambalo lilipotoshwa na wazo la kipagani lilihusu utambulisho wa Yesu Kristo. Biblia inamwita Mwana wa Mungu; lakini wale waliopenda sana falsafa ya Kigiriki walisisitiza kwamba yeye ni Mungu.

10. Suala kuhusu utambulisho wa Kristo lingetatuliwa jinsi gani?

10 Baadaye, viongozi wa kanisa walijadiliana kuhusu fundisho hilo katika makongamano mengi ya kanisa. Suala hilo lingetatuliwa kwa urahisi sana ikiwa wajumbe wangeyapa Maandiko uzito unaofaa, lakini wengi wao hawakufanya hivyo. Kwa kweli, wengi wao walikuwa tayari wamefanya uamuzi wao hata kabla ya kufika kwenye makongamano hayo, na hata baada ya makongamano hakuna jambo lolote ambalo lingeweza kamwe kubadili misimamo yao. Maamuzi yaliyofanywa katika makongamano hayo hayakurejelea kamwe Maandiko.

11. Mamlaka ya wale walioitwa eti Mababa wa Kanisa yalipewa uzito gani, na kwa nini?

11 Kwa nini Maandiko hayakutumiwa kikamili zaidi katika makongamano hayo? Mwanahistoria Charles Freeman anasema kwamba wale walioamini kuwa Yesu ni Mungu “waliona ni vigumu kukanusha maneno mengi ya Yesu ambayo yanaonyesha kwamba alijitiisha kwa Mungu Baba.” Kwa sababu hiyo, mapokeo ya kanisa na maoni ya viongozi wa kanisa yalionekana kuwa muhimu zaidi kuliko vitabu vya Injili. Hadi leo hii, viongozi wengi wa kanisa wanafikiri maneno ambayo hayakuongozwa na roho ya Mungu ya wale wanaoitwa eti Mababa wa Kanisa ni muhimu zaidi kuliko Neno la Mungu! Ikiwa umewahi kuzungumza na mwanachuo wa kidini kuhusu fundisho la Utatu, inaelekea umetambua jambo hilo.

12. Ni ushawishi gani mbaya ambao maliki alikuwa nao?

12 Maliki au watawala wa Roma walikuwa na ushawishi mkubwa juu ya makongamano hayo. Kwa mfano, Profesa Richard E. Rubenstein aliandika hivi kuhusu Kongamano la Nisea: “Konstantino aliwatajirisha sana [maaskofu]. Baada ya muda usiozidi mwaka mmoja, maliki mpya alikuwa amewarudishia maaskofu vitu vyao vyote au kuwajengea upya makanisa yao yote, akawapa tena kazi na heshima ambayo walikuwa wamepokonywa . . . Aliwapa makasisi wa Kikristo mapendeleo ambayo hapo awali yalikuwa ya makuhani wapagani.” Kwa sababu hiyo, “Konstantino alikuwa na ushawishi mkubwa, na labda hata uwezo wa kubadili maamuzi makubwa ya Kongamano la Nisea.” Charles Freeman alithibitisha hivi: “Sasa katika kongamano la awali iliamuliwa kwamba maliki anapaswa kuingilia kati si tu kuliimarisha Kanisa bali pia kuongoza mafundisho ya Kanisa.”​—Soma Yakobo 4:4.

13. Ni mambo gani ambayo unafikiri yalikuwa na ushawishi mbaya juu ya viongozi wa kanisa karne nyingi baadaye hivi kwamba wakapuuza mafundisho yaliyo wazi ya Biblia?

13 Viongozi wa kanisa walipokuwa na tatizo la kujua Yesu Kristo ni nani hasa, watu wengi wa kawaida hawakuwa na tatizo hilo. Sababu ni kwamba watu hao wa kawaida walielewa vizuri na kukubali mambo waliyosoma katika Maandiko. Lakini viongozi wa kanisa badala yake walitaka pesa na mamlaka ambayo walipewa na maliki, na hivyo wakaipuuza Biblia. Gregory wa Nyssa, ambaye alikuwa kiongozi wa kidini wakati huo, alitoa maelezo yanayoshutumu jinsi watu wa kawaida, kama vile wauza-nguo, wabadilishaji wa pesa, wauza-mboga na matunda, na watumishi, walivyozungumza kuhusu dini. Gregory hakupendezwa na wazo la kwamba watu wa kawaida wengi walieleza kuwa Mwana ni tofauti na Baba, kwamba Baba ni mkuu zaidi kuliko Mwana, na kwamba Mwana aliumbwa lakini hakuumbwa kutokana na kitu chochote. Watu wa kawaida waliweza kufafanua kweli hizo kwa kutumia Biblia. Hilo ni jambo ambalo Gregory wa Nyssa na viongozi wa kanisa hawakuwa wakifanya. Walipaswa kuwasikiliza watu hao wa kawaida!

“NGANO” NA “MAGUGU” VYAKUA PAMOJA

14. Kwa nini tunaweza kukata kauli kwamba kuanzia karne ya kwanza na kuendelea, sikuzote kumekuwepo na Wakristo wa kweli watiwa-mafuta duniani?

14 Katika mfano mmoja, Yesu alionyesha kwamba kuanzia karne ya kwanza na kuendelea, kungekuwa na Wakristo wa kweli watiwa-mafuta duniani. Aliwalinganisha Wakristo hao na “ngano” iliyokuwa ikikua katikati ya “magugu.” (Mt. 13:30) Bila shaka, hatuwezi kusema kwa uhakika ni watu gani au vikundi gani vilivyokuwa sehemu ya jamii ya ngano ya watiwa-mafuta, lakini tunaweza kuthibitisha kwamba sikuzote kulikuwepo watu fulani ambao walitetea kwa ujasiri Neno la Mungu na kufunua mafundisho ya uwongo ya kanisa. Acheni tuchunguze mifano michache.

15, 16. Taja baadhi ya watu walioliheshimu Neno la Mungu.

15 Askofu Mkuu Agobard wa Lyons, Ufaransa, aliyeishi kati ya mwaka wa 779 na 840 W.K., alilaumu ibada ya sanamu, zoea la kuweka makanisa wakfu kwa watakatifu, na ibada na matendo ya kanisa yasiyopatana na Maandiko. Askofu Claudius, aliyeishi wakati uleule na Askofu Agobard, yeye pia alikataa mapokeo ya kanisa na akapinga zoea la kutoa sala kwa ajili ya watakatifu na kuabudu mabaki ya watakatifu. Katika karne ya 11, Msaidizi wa askofu, Berengarius wa Tours, Ufaransa, alifukuzwa kanisani kwa sababu ya kukataa fundisho la Kanisa Katoliki la kwamba mkate na divai vinageuka kimuujiza na kuwa mwili na damu halisi ya Yesu. Zaidi ya hayo, alifundisha kwamba Biblia ina mamlaka kuu zaidi kuliko mapokeo ya kanisa.

16 Peter wa Bruys na Henry wa Lausanne, walioishi katika karne ya 12, walikuwa wanaume wengine wawili ambao waliipenda kweli ya Biblia. Peter aliacha ukasisi kwa sababu aliamini kwamba mafundisho ya Kanisa Katoliki ya ubatizo wa watoto, mkate na divai kugeuka kimuujiza na kuwa mwili na damu halisi ya Yesu, sala kwa ajili ya wafu, na ibada ya msalaba, hayakupatana na Maandiko. Katika mwaka wa 1140, Peter alichomwa moto hadi kufa kwa sababu ya imani yake. Henry, ambaye alikuwa mtawa, alilaumu matendo mapotovu na ibada ya uwongo kanisani. Alikamatwa mwaka wa 1148 na kufungwa jela maisha yake yote.

17. Ni hatua gani muhimu zilizochukuliwa na Waldo na wafuasi wake?

17 Karibu na wakati huo ambao Peter wa Bruys aliuawa kwa kuchomwa moto akiwa hai kwa sababu ya kuthubutu kulilaumu kanisa, mtu fulani alizaliwa ambaye baadaye angekuwa na ushawishi wenye nguvu juu ya kuenezwa kwa kweli za Biblia. Jina lake la pili lilikuwa Valdès, au Waldo. * Tofauti na Peter wa Bruys na Henry wa Lausanne, Valdès hakuwa kasisi, lakini alilithamini sana Neno la Mungu hivi kwamba akaacha vitu vyake vya kimwili na akafanya mipango ili sehemu fulani za Biblia zitafsiriwe katika lugha ya watu wa kawaida huko kusini-mashariki mwa Ufaransa. Baadhi ya watu walifurahi sana kusikia ujumbe wa Biblia katika lugha yao wenyewe hivi kwamba wao pia wakaacha vitu vyao vya kimwili na kutumia maisha yao kuhubiri kweli za Biblia kwa wengine. Viongozi wa kanisa walikasirishwa sana na jambo hilo. Katika mwaka wa 1184 wanaume na wanawake hao wenye bidii, ambao baadaye waliitwa Wawaldo, walitengwa na papa na wakafukuzwa na askofu kutoka katika nyumba zao. Tendo hilo kwa kweli lilisaidia tu kueneza ujumbe wa Biblia katika maeneo mengine. Wakati huo, katika sehemu nyingi za Ulaya kulikuwepo na wafuasi wa Waldo, Peter wa Bruys, na Henry wa Lausanne na pia watu wengine ambao walijitenga wenyewe na kanisa. Wateteaji wengine wa kweli ya Biblia walitokea katika karne nyingi zilizofuata: John Wycliffe (aliyeishi kuanzia karibu mwaka wa 1330 hadi 1384), William Tyndale (aliyeishi kuanzia karibu mwaka wa 1494 hadi 1536), Henry Grew (aliyeishi kuanzia karibu mwaka wa 1781 hadi 1862), na George Storrs (aliyeishi kuanzia karibu mwaka wa 1796 hadi 1879).

“NENO LA MUNGU HALIFUNGWI”

18. Eleza mbinu ya kujifunza Biblia ambayo ilitumiwa na wanafunzi wanyoofu wa Biblia katika karne ya 19 na kwa nini ilikuwa na matokeo mazuri.

18 Ingawa walifanya yote wawezayo, maadui wa kweli ya Biblia hawakuweza kuzuia kweli hiyo isienezwe. “Neno la Mungu halifungwi,” linasema andiko la 2 Timotheo 2:9. Katika mwaka wa 1870, kikundi cha wanafunzi wanyoofu wa Biblia kilianza kutafuta kweli. Walijifunza jinsi gani? Mmoja wao angetokeza swali. Wangeweza kuzungumzia swali hilo. Wangetafuta maandiko yote yanayohusiana na jambo hilo, na kisha, walipotosheka na upatani wa maandiko hayo, wangekubaliana hatimaye kuhusu jibu la swali hilo na kuliandika. Je, hilo halikuhakikishii kwamba kama mitume na wanaume wazee wa karne ya kwanza, wanaume hao waaminifu, “mababu zetu wa kiroho” wa mwishoni mwa miaka ya 1800, walikuwa wameazimia kupatanisha kabisa mafundisho yao na Neno la Mungu?

19. Andiko la mwaka wa 2012 ni lipi, na kwa nini linafaa?

19 Biblia bado ndio msingi wa mafundisho yetu. Tukiwa na hilo akilini, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova limechagua maneno haya yenye uhakikisho ya Yesu kuwa andiko letu la mwaka wa 2012: “Neno lako ni kweli.” (Yoh. 17:17) Kwa kuwa kila mtu anayetaka kupata kibali cha Mungu anapaswa kutembea katika kweli, sote basi na tuendelee kujitahidi kuongozwa na Neno la Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Nyakati nyingine Valdès aliitwa Pierre Valdès au Peter Waldo, lakini jina lake la kwanza haliwezi kuthibitishwa.

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Andiko letu la mwaka wa 2012: “Neno lako ni kweli.” ​—Yoh. 17:17

[Picha katika ukurasa wa 7]

Waldo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wycliffe

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tyndale

[Picha katika ukurasa wa 7]

Grew

[Picha katika ukurasa wa 7]

Storrs