Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Ninawezaje Kuhubiri?’

‘Ninawezaje Kuhubiri?’

‘Ninawezaje Kuhubiri?’

Ulimwenguni pote, tuna mifano yenye kuvutia ya ndugu na dada ambao wanashiriki kwa uaminifu katika kazi ya kuhubiri licha ya kukabiliana na matatizo makubwa ya afya. Kwa mfano, mfikirie Dalia, ambaye anaishi huko Vilnius, mji mkuu wa Lithuania.

Dalia ni dada mwenye umri wa miaka 30 hivi. Tangu azaliwe amekuwa akikabiliana na ugonjwa wa kupooza kwa ubongo. Ugonjwa huo umemfanya apooze na kuwa na tatizo kubwa la kuzungumza. Matokeo yake ni kwamba ni watu wa familia yake tu ndio wanaoweza kumwelewa vizuri. Dalia anaishi na mama yake, Galina, ambaye anashughulikia mahitaji yake. Ingawa maisha ya Dalia yamejaa matatizo na mahangaiko, anadumisha mtazamo mzuri. Hilo linawezekanaje?

Galina anaeleza: “Mwaka 1999, binamu yangu Apolonija alikuja kututembelea. Tuligundua kwamba Apolonija, ambaye ni Shahidi wa Yehova, aliijua Biblia yake vizuri, na Dalia akaanza kumuuliza maswali mengi. Muda si muda, Dalia akaanza kujifunza Biblia. Mara kwa mara, nilijiunga nao katika funzo hilo ili kusaidia kutafsiri yale ambayo Dalia alikuwa akisema. Hata hivyo, niligundua kwamba Dalia alikuwa akifaidika na kila jambo ambalo alikuwa akijifunza. Muda mfupi baadaye, mimi pia nikaomba kujifunza Biblia.”

Dalia alipokuwa akiendelea kuelewa kweli za Biblia vizuri, jambo moja lilianza kumsumbua tena na tena. Hatimaye, akamuuliza Apolonija: “Mtu kama mimi​—aliyepooza​—anawezaje kuhubiri?” (Mt. 28:19, 20) Kwa utulivu, Apolonija akamhakikishia Dalia hivi: “Usiogope. Yehova atakusaidia.” Na kwa kweli, Yehova husaidia.

Hivyo basi, Dalia anahubiri jinsi gani? Anatumia njia mbalimbali. Dada Wakristo humsaidia kuandika barua zenye ujumbe wa Biblia. Kwanza, Dalia huwaeleza akina dada mawazo yake. Kisha, dada hao wanaandika barua ikiwa na mawazo yake. Pia, Dalia anahubiri kwa kutuma ujumbe mfupi wa simu. Na ikiwa hali ya hewa ni nzuri, washiriki wa kutaniko wanamtoa nje ili awahubirie watu ambao wanakutana nao kwenye bustani za kupumzikia na barabarani.

Dalia na mama yake wamezidi kufanya maendeleo ya kiroho. Wote walijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa Novemba 2004. Mnamo Septemba 2008, kikundi cha lugha ya Kipolandi kilianzishwa huko Vilnius. Kwa kuwa kikundi hicho kilikuwa na uhitaji wa wahubiri wengi wa Ufalme, Dalia na mama yake walijiunga na kikundi hicho. Dalia anasema hivi: “Miezi fulani mimi huwa na wasiwasi ikiwa sijatoka kwenda kuhubiri. Lakini baada ya kusali kwa Yehova kuhusu jambo hilo, mtu fulani hufanya mpango ili aende katika mahubiri pamoja nami.” Dada yetu mpendwa Dalia anahisije kuhusu hali yake? Anasema hivi: “Ugonjwa umepooza mwili wangu, lakini haujapooza akili zangu. Ninafurahi sana kuwaambia wengine kumhusu Yehova!”