Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtumikia Mungu kwa Bidii na Shangwe

Kumtumikia Mungu kwa Bidii na Shangwe

Kumtumikia Mungu kwa Bidii na Shangwe

YEHOVA anataka uwe na shangwe. (Zab. 100:2) Ukiwa mmoja wa watumishi wake, inaelekea wewe pia una shughuli nyingi sana. Labda hukuwa na shughuli nyingi hivyo kabla hujaweka maisha yako wakfu kwa Mungu, lakini sasa huenda madaraka ya kimwili na ya kiroho yakakufanya uhisi umelemewa. Huenda hata ukahisi kwamba una hatia unapokosa kutimiza mambo yote uliyopanga kutimiza. Unaweza kupata jinsi gani usawaziko unaofaa na kuendelea kuwa na “shangwe ya Yehova”?—Neh. 8:10.

Unaishi katika nyakati za hatari na hivyo unakabili mikazo mingi, basi unahitaji kuwa na ratiba nzuri. Kuhusiana na hilo, shauri hili la mtume Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu linafaa sana: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.”—Efe. 5:15, 16.

Kupatana na shauri hilo lenye hekima, unaweza kupanga jinsi gani miradi unayoweza kutimiza na kusawazisha funzo la kibinafsi, daraka la kuitunza familia, utumishi wa shambani, kazi ya kimwili, na shughuli nyingine za lazima?

Je, unakumbuka shangwe uliyokuwa nayo ulipojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa? Ulikuwa na shangwe kwa sababu ulipata ujuzi kumhusu Yehova na makusudi yake. Huenda ulijifunza kwa bidii kwa miezi mingi na hivyo ukapata shangwe na uelewaji huo. Bila shaka, jitihada hizo zote hazikuwa za bure. Funzo hilo lilibadili maisha yako na kuyaboresha.

Ili uendelee kuwa na shangwe, unahitaji kuendelea kujilisha kiroho. Ikiwa unajikaza sana ili upate wakati wa kusoma na kujifunza Biblia, chunguza ratiba yako. Kujifunza na kutafakari hata kwa dakika chache tu kila siku kutakusaidia kuwa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova, na bila shaka utapata shangwe nyingi.

Watumishi wengi wa Mungu wanaweza kununua wakati fulani wanaotumia kwa ajili ya mambo yasiyo ya maana sana na kuutumia kufanya mambo ya maana. Jiulize, ‘Ninatumia wakati mwingi kadiri gani kusoma magazeti ya kilimwengu, kutazama televisheni, kusikiliza muziki, au kufuatia burudani fulani ninayopenda?’ Mambo hayo yanaweza kufurahisha ikiwa tu yanafanywa kwa usawaziko. (1 Tim. 4:8) Ukitambua kwamba una tatizo la kupanga wakati wako vizuri, rekebisha ratiba yako.

Adam, ambaye ni mume, baba mwenye watoto watatu, na mzee wa kutaniko, anaeleza kinachomsaidia: “Ninajitahidi kuishi maisha rahisi. Ninaepuka burudani na vitu vya kimwili vinavyohitaji wakati mwingi. Si kwamba ninaishi maisha ya kujinyima, lakini ninafurahia tu burudani ya kawaida.”

Kutafakari kuhusu matokeo mazuri ya maamuzi yako kunaweza kukusaidia kupata tena shangwe yako na kuendelea kuwa na mtazamo mzuri. Kwa mfano, Mariusz, mzee wa kutaniko mwenye watoto watatu, anasema hivi: “Nilipoanza kujifunza Biblia, nilianza kuwa na mtazamo mzuri kuhusu wakati ujao. Bado ninakabili matatizo mara kwa mara, na ni Yehova tu anayejua mengi ya matatizo hayo. Lakini kwa sababu ya utegemezo wake, ninatazamia wakati ujao nikiwa na shangwe.”

Kama kisa cha Mariusz kinavyoonyesha, kuwa na mtazamo mzuri hakutaondoa mahangaiko yote. Lakini mtazamo mzuri unaweza kukusaidia ujihisi vizuri na upambane vizuri zaidi na matatizo ya maisha. Tunasoma hivi: “Siku zote za mwenye kuteseka ni mbaya, lakini mtu aliye mchangamfu moyoni huwa na karamu sikuzote.” (Met. 15:15) Tafakari pia kuhusu upendo ambao tayari Mungu amekuonyesha. Kutafakari kuhusu upendo huo kunaweza kujenga upendo wako kwa Mungu na kuongeza shangwe yako ya kimungu.—Mt. 22:37.

Kumtanguliza Yehova na mambo ya kiroho maishani kunaongeza shangwe katika familia. Kuonyesha sifa za Kikristo kunapunguza matatizo ya kutoelewana na kunaisaidia familia kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na wenye kupendeza zaidi. Hivyo, familia yote itafurahia hali ya umoja na nyumba yenu itakuwa na amani ya kweli.—Zab. 133:1.

Kushiriki katika utendaji wa kiroho mkiwa familia kunaleta shangwe nyingi ya kweli. Mariusz anaeleza hivi: “Ninathamini sana wakati tunaotumia pamoja tukiwa familia. Mke wangu ananiunga mkono kabisa. Inapowezekana, anaambatana nami katika huduma ya shambani au ninaposafisha uwanja kabla ya makusanyiko, na pia anaambatana nami ninapoenda kutoa hotuba za watu wote katika makutaniko mengine. Jambo hilo linanitia moyo.”

Maandiko yanawaamuru Wakristo waandalie familia zao mahitaji ya kimwili. (1 Tim. 5:8) Lakini ikiwa kazi ya kimwili inachukua nguvu na wakati mwingi sana, inaweza kukufanya upoteze shangwe katika utumishi wa Mungu. Sali kwa Yehova kuhusu jambo hilo. (Zab. 55:22) Wakristo fulani wameamua kwamba ili watangulize Ufalme wa Mungu wanahitaji kutafuta kazi nyingine. Hakuna Mkristo anayepaswa kuruhusu faida za kifedha anazopata kwa kufanya kazi inayohitaji nguvu na wakati mwingi sana zimzuie kufuatilia mambo ya kiroho ambayo ni ya maana zaidi.—Met. 22:3.

Unaweza kunufaika ukiandika faida na hasara zote za kazi yako ya sasa au kazi unayofikiria kuanza. Bila shaka, ungependa kupata mshahara mzuri na kazi yenye kuridhisha. Hata hivyo, je, kazi yako ya sasa inakusaidia kujenga hali ya kiroho ya familia yako? Chunguza kwa uzito mambo yote, na ufanye maamuzi ambayo yanaonyesha kwamba unatanguliza uhusiano wako pamoja na Yehova.

Ikiwa kazi yako ya sasa inakuzuia kukua kiroho, unahitaji kurekebisha hali zako. Wakristo wengi wamefanya mabadiliko makubwa ili wapate wakati wa mambo ya kiroho. Ndugu mmoja huko Poland anasema hivi: “Pindi moja sikuwa na jambo lingine la kufanya ila kuacha kazi katika kampuni moja kwa kuwa mara nyingi nilisafiri kwa sababu za kibiashara. Sikuwa na wakati wa kutosha kushughulikia ipasavyo mambo ya kiroho au kuitunza familia yangu.” Sasa anapata riziki kwa kufanya kazi ambayo haihitaji nguvu na wakati wake mwingi sana.

Pata Shangwe kwa Kuwasaidia Wengine

Yesu alisema kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Wakristo wana nafasi nyingi za kutoa kwa njia hiyo. Nyakati nyingine, ili upate shangwe na kumletea mtu mwingine shangwe unahitaji tu kutabasamu kwa uchangamfu, kumsalimu kwa mkono, au kumshukuru kutoka moyoni kwa sababu ya jitihada anazofanya katika mgawo wake wa kiroho.

Mtume Paulo aliwatia moyo hivi Wakristo wenzake: “Semeni kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika, tegemezeni walio dhaifu.” (1 The. 5:14) Watu waliohuzunika wanaweza kuhisi kwamba hawawezi kukabiliana na matatizo kwa nguvu zao wenyewe. Je, unaweza kuwasaidia watu kama hao? Ukiona kwamba mmoja wa ndugu zako anapoteza shangwe yake katika utumishi wa Yehova, jitahidi kumtia moyo. Kufanya hivyo kutakutia moyo pia. Matatizo fulani hayawezi kutatuliwa na mwanadamu yeyote. Hata hivyo, unaweza kumhurumia kutoka moyoni ndugu yako na kumhimiza ategemee msaada wa Yehova ambao haushindwi kamwe. Wale wanaomtegemea hawatakata tamaa kamwe.—Zab. 27:10; Isa. 59:1.

Hatua nyingine inayofaa ni kumwalika yule ambaye anaonekana hana shangwe ahubiri pamoja nawe. Yesu alipowatuma wale wanafunzi 70, aliwatuma “wawili-wawili.” (Luka 10:1) Je, huamini kwamba kwa kufanya hivyo alituandalia njia ya kutiana moyo? Je, unaweza kuiga kielelezo hicho leo kwa kuwasaidia Wakristo wengine wapate tena shangwe?

Leo kuna mambo mengi ambayo yanaweza kutufanya tuhangaike. Hata hivyo, Paulo anatuhimiza hivi: “Shangilieni sikuzote katika Bwana. Mara nyingine tena nitasema, Shangilieni!” (Flp. 4:4) Kwa sababu unampenda Mungu, unamtii, na unavumilia unapoendelea kufanya kwa bidii kazi ambayo amekupa, maisha yako yana kusudi. Hilo linakuletea shangwe. Na zaidi ya hayo, Yehova anakusaidia kushughulika na mikazo na matatizo ambayo unakabili.—Rom. 2:6, 7.

Kwa macho ya imani, tunatambua jinsi tulivyo karibu sana kuingia katika ulimwengu mpya ambao Yehova anaahidi. Ulimwengu huo mpya utatuletea baraka na sababu nyingi kama nini za kushangilia! (Zab. 37:34) Kwa hiyo, tunaweza kushangilia, na kuendelea kukazia fikira jinsi Yehova anavyotubariki sana hata sasa. Hivyo, tunaweza ‘kumtumikia Yehova kwa kushangilia.’—Zab. 100:2.

[Mchoro katika ukurasa wa 8]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Huenda ukahitaji kurekebisha ratiba yako ili uendelee kuwa na shangwe

BURUDANI na TAFRIJA

KUITUNZA NYUMBA na FAMILIA

KAZI

MIKUTANO YA KIKRISTO

FUNZO LA KIBINAFSI

HUDUMA

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, unaweza kuwasaidia wengine kupata tena shangwe?