Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Kuvumilia Jaribu Lolote Lile!

Tunaweza Kuvumilia Jaribu Lolote Lile!

Tunaweza Kuvumilia Jaribu Lolote Lile!

JE, WEWE unakabili jaribu lolote maishani mwako? Je, jaribu hilo linakatisha tamaa na unashindwa kulivumilia? Je, wakati mwingine hata unahofu kwamba jaribu lako si la kawaida na haliwezi kutatuliwa? Ikiwa ndivyo, usivunjike moyo! Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu anaweza kutusaidia kukabiliana na majaribu yoyote yale.

Biblia inatambua kwamba watumishi wa Mungu ‘watakutana na majaribu ya namna mbalimbali.’ (Yakobo 1:2) Ona kwamba zamani neno “mbalimbali” (Kigiriki poi·kiʹlos) lilimaanisha “-a aina tofauti-tofauti” au “-a rangi tofauti-tofauti,” jambo linalokazia kwamba “kuna majaribu ya aina mbalimbali.” Hata hivyo Yehova anatutegemeza ili tuweze kuvumilia majaribu yote hayo. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hilo?

‘Fadhili Zisizostahiliwa za Mungu Zinaonyeshwa kwa Njia Mbalimbali’

Mtume Petro anasema kwamba Wakristo ‘wanahuzunishwa na majaribu ya namna mbalimbali.’ (1 Petro 1:6) Baadaye, kwenye barua yake iliyoongozwa na roho ya Mungu alisema kwamba “fadhili zisizostahiliwa za Mungu” zinaonyeshwa “kwa njia mbalimbali.” (1 Petro 4:10) Usemi “kwa njia mbalimbali” una maana ileile ya neno la Kigiriki cha awali. Akitoa maoni kuhusu neno hilo msomi mmoja wa Biblia anasema hivi: “Hilo ni wazo lenye kushangaza sana. . . . Kuzungumzia neema [au, fadhili zisizostahiliwa] za Mungu kwa kutumia neno la Kigiriki poikilos, kunamaanisha kwamba hakuna jaribu lolote ambalo mwanadamu atakabiliana nalo ambalo fadhili za Mungu haziwezi kulitatua.” Anaendelea kusema: “Hakuna hali yoyote, tatizo lolote, uhitaji wowote au dharura yoyote katika maisha ambayo neema za Mungu haziwezi kushughulikia na kushinda. Neno poikilos hutuwezesha kuona neema nyingi za Mungu, ambazo kwa kweli zinatosha kutusaidia kuvumilia majaribu yote.”

Fadhili Hutusaidia Kuvumilia Majaribu

Kulingana na Petro, njia moja ambayo fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinaonyeshwa ni kupitia watu mbalimbali katika kutaniko la Kikristo. (1 Petro 4:11) Kila mtumishi wa Mungu ana zawadi za kiroho au kipawa ambacho anaweza kutumia kuwatia moyo wale wanaokabili majaribu. (Waroma 12:6-8) Kwa mfano, baadhi ya washiriki wa kutaniko ni walimu wazuri wa Biblia. Maneno yao yenye ufahamu yanatia moyo na kuwachochea wengine wavumilie. (Nehemia 8:1-4, 8, 12) Wengine hufanya ziara za uchungaji kwa ukawaida kwenye nyumba za wale wanaohitaji msaada. Ziara hizo huimarisha na ‘kufariji mioyo.’ (Wakolosai 2:2) Waangalizi wanapofanya ziara hizo zenye kuimarisha imani wanatoa zawadi ya tunda la roho. (Yohana 21:16) Bado kuna wengine kutanikoni ambao huonyesha sifa yao ya uchangamfu, huruma, na wororo wanaposhughulika na waamini wenzao ambao wamehuzunishwa na majaribu. (Matendo 4:36; Waroma 12:10; Wakolosai 3:10) Hisia-mwenzi na utegemezo unaoonyeshwa na ndugu na dada hao wapendwa ni wonyesho wa aina “mbalimbali” za fadhili zisizostahiliwa za Mungu.—Methali 12:25; 17:17.

“Mungu wa Faraja Yote”

Zaidi ya yote, Yehova hutoa faraja. Yeye ni “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.” (2 Wakorintho 1:3, 4) Hekima inayopatikana katika Neno la Mungu na nguvu inayotolewa na roho yake takatifu, ni njia muhimu ambazo Yehova hutumia kujibu sala zetu za kuomba msaada. (Isaya 30:18, 21; Luka 11:13; Yohana 14:16) Tunaweza kutiwa moyo na ahadi hii ambayo mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kutoa: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

Fadhili zisizostahiliwa za Mungu zinaweza kutusaidia kuvumilia aina yoyote ile ya majaribu. (Yakobo 1:17) Msaada hususa unaopatikana kwa wakati unaofaa ambao Yehova anatoa kwa watumishi wake hata wakabili jaribu la aina gani, ni uthibitisho wa “hekima ya Mungu ya namna nyingi sana.” (Waefeso 3:10) Je, hukubaliani na jambo hilo?

[Picha katika ukurasa wa 31]

Yehova anatusaidia kuvumilia majaribu