Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ni chini ya hali gani ingefaa mwanamke Mkristo ajifunge kitambaa kichwani kwa sababu za kidini?

Mtume Paulo aliandika hivi: “Kila mwanamke ambaye husali au hutoa unabii kichwa chake kikiwa hakijafunikwa huaibisha kichwa chake.” Kwa nini? Kwa sababu ya kanuni ya Biblia ya ukichwa: “Kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” Kwa kawaida wanaume ndio wenye daraka la kusali au kuhubiri katika kutaniko la Kikristo. Kwa hiyo, mwanamke Mkristo anaposhughulikia mambo yanayohusu ibada ambayo kwa kawaida yangefanywa na mume wake au na mwanamume aliyebatizwa, anapaswa kujifunga kitambaa kichwani.—1 Wakorintho 11:3-10.

Huenda kukatokea hali fulani katika ndoa ambapo mke Mkristo angelazimika kufunga kitambaa kichwani. Kwa mfano, familia inapokutana pamoja kwa ajili ya funzo la Biblia au kwa ajili ya chakula, kwa kawaida mume ndiye hufundisha na kutoa sala kwa Mungu kwa niaba ya familia. Hata hivyo, iwapo mume si mwamini, huenda mke akachukua daraka hilo. Kwa hiyo, anaposali kwa sauti kwa niaba yake mwenyewe au kwa niaba ya wengine, au anapoongoza funzo la Biblia pamoja na watoto wake mumewe akiwepo, dada Mkristo anapaswa kufunga kitambaa kichwani. Ikiwa mume wake hayupo, mke hahitaji kujifunga kitambaa kichwani, kwa kuwa Mungu amempa mamlaka ya kufundisha watoto.—Mithali 1:8; 6:20.

Namna gani ikiwa katika familia kuna mvulana ambaye ni mtumishi wa Yehova Mungu aliyejiweka wakfu na kubatizwa? Kwa kuwa mvulana huyo ni mshiriki wa kutaniko la Kikristo, anapaswa kufundishwa na wanaume. (1 Timotheo 2:12) Ikiwa baba yake ni mwamini, basi mwana huyo anapaswa kufundishwa naye. Hata hivyo, ikiwa baba hayupo, basi mama anapaswa kufunga kitambaa kichwani anapoongoza funzo la Biblia pamoja na mvulana aliyebatizwa na watoto wengine. Anaweza kuamua iwapo atamruhusu mwana huyo aliyebatizwa kutoa sala wakati wa funzo au wa chakula. Huenda dada huyo akahisi kwamba mwana wake hajakomaa vya kutosha na hivyo akaamua kutoa sala yeye mwenyewe. Akiamua kusali kwenye pindi hizo, anapaswa kufunga kitambaa kichwani.

Huenda wanawake Wakristo wakahitaji kujifunga kitambaa kichwani wanaposhughulikia migawo fulani kutanikoni. Kwa mfano, kwenye mikutano ya utumishi katikati ya juma, huenda kusiwepo mwanamume aliyebatizwa, isipokuwa tu akina dada. Huenda kukawa na pindi ambapo hakuna wanaume waliobatizwa katika mikutano ya kutaniko. Ikiwa dada atalazimika kushughulikia migawo ambayo kwa kawaida hushughulikiwa na ndugu kwenye mikutano ya kutaniko au kwenye mkutano wa utumishi wa shambani, anapaswa kufunga kitambaa kichwani.

Je, wanawake Wakristo wanapaswa kufunga kitambaa kichwani wanapotafsiri hotuba za Biblia katika lugha nyingine au katika lugha ya ishara, au wanaposoma hadharani mafungu ya kitabu kinachozungumzia habari za Biblia ambacho kinatumiwa kwenye mkutano wa kutaniko? La. Akina dada wanaoshughulikia migawo hiyo hawafundishi au kusimamia wengine. Vivyo hivyo, si lazima akina dada wafunge kitambaa kichwani wanapofanya maonyesho, kusimulia mambo yaliyoonwa, au kutoa hotuba za wanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

Ingawa ni daraka la wanaume waliobatizwa kufundisha katika kutaniko, daraka la kuhubiri na kufundisha nje ya kutaniko ni la wanaume na wanawake pia. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Kwa hiyo si lazima mwanamke Mkristo afunge kitambaa kichwani anapozungumza Neno la Mungu na mwanamume ambaye si Shahidi, hata kama ameambatana na mwanamume ambaye ni Shahidi wa Yehova.

Hata hivyo, hali ni tofauti kwenye funzo la Biblia la nyumbani linalofanywa kwa ukawaida, na ambapo kuna mwanamume aliyebatizwa. Kwa kuwa funzo hilo huwa limepangwa kimbele, mwenye kuongoza anafundisha na kusimamia. Chini ya hali hizi, funzo hilo ni kama mkutano wa ziada. Dada akiongoza funzo hilo akiwa pamoja na ndugu aliyebatizwa, anapaswa kufunga kitambaa kichwani. Hata hivyo, ndugu aliyejiweka wakfu na kubatizwa anapaswa kutoa sala. Dada hapaswi kutoa sala iwapo kuna ndugu aliyejiweka wakfu isipokuwa ndugu huyo awe ni bubu au kuna sababu nyingine za kipekee.

Huenda pindi kwa pindi dada Mkristo akaandamana kwenye funzo la Biblia na mwanamume ambaye ni mtangazaji wa Ufalme asiyebatizwa. Dada akipenda, anaweza kumwomba mhubiri huyo aongoze funzo hilo. Lakini kwa kuwa mhubiri huyo hawezi kumwakilisha dada aliyebatizwa ifaavyo katika sala kwa Yehova, ingefaa dada huyo atoe sala. Ikiwa dada ndiye anayeongoza funzo na kutoa sala, anapaswa kufunga kitambaa kichwani. Hata ikiwa mhubiri huyo wa kiume hajabatizwa, watu ambao si Mashahidi humwona kuwa mshiriki wa kutaniko kwa sababu anahubiri.

Mtume Paulo aliandika hivi: “Mwanamke apaswa kuwa na ishara ya mamlaka juu ya kichwa chake kwa sababu ya malaika.” Naam, dada Wakristo wana pendeleo la kuwa vielelezo vizuri kwa mamilioni ya malaika ambao wanaendelea kujitiisha kwa Yehova. Inafaa kama nini kwa wanawake Wakristo kufunga kitambaa kichwani inapokuwa lazima kufanya hivyo!

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kujifunga kitambaa kichwani ni ishara ya kuheshimu ukichwa