Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wanawake Wanapaswa Kuwa Wahudumu?

Je, Wanawake Wanapaswa Kuwa Wahudumu?

Maoni ya Biblia

Je, Wanawake Wanapaswa Kuwa Wahudumu?

“NINASHANGAZWA na kukasirishwa kwamba bado wanawake hawatawazwi,” akaandika mwanamke Mkatoliki katika gazeti USA Today. Watu wengi wana maoni kama yake. Isitoshe, kuna wanawake katika dini fulani ambao ni wahudumu, makasisi, maaskofu, na marabi.

Dini zote, iwe zinaunga mkono kwamba wanawake hawapaswi kuwa wahudumu au zinasema kwamba wanapaswa kuhubiri kanisani, zinadai kwamba zinafuata Maandiko. Hata hivyo, Biblia haiungi mkono maoni yote hayo. Kwa nini? Ili kujibu, acheni tuchunguze kwanza jinsi Biblia inavyotumia neno “mhudumu.”

Wahudumu wa Karne ya Kwanza

Neno “mhudumu” linaleta wazo gani akilini mwako? Watu wengi hufikiria kuhusu kiongozi wa kidini, awe mwanamume au mwanamke, anayeongoza kutaniko katika ibada. Lakini Biblia hutumia neno hilo katika maana pana. Mfikirie mwanamke Mkristo anayeitwa Fibi, ambaye mtume Paulo alimtaja kuwa “dada yetu, ambaye ni mhudumu wa kutaniko lililo katika Kenkrea.”—Waroma 16:1.

Je, unaweza kumwazia Fibi akisimama mbele ya kutaniko huko Kenkrea, akiongoza ibada ya kidini? Fibi alihudumu kwa njia gani? Katika barua yake kwa Wafilipi, Paulo anaandika kwamba wanawake fulani “wamefanya kazi ya kueneza injili . . . pamoja nami.”—Italiki ni zetu; Wafilipi 4:2, 3, Biblia Habari Njema.

Njia ya msingi ambayo Wakristo katika karne ya kwanza walieneza injili ilikuwa “hadharani na nyumba kwa nyumba.” (Matendo 20:20) Wale walioshiriki katika kazi hiyo walikuwa wahudumu. Walitia ndani wanawake kama vile Prisila. Yeye pamoja na mume wake, ‘walimfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu’ mwanamume fulani aliyemwogopa Mungu ambaye hakuwa amebatizwa kuwa Mkristo. (Matendo 18:25, 26) Kama tu Fibi—na wanawake wengine—Prisila pia alikuwa mhudumu mwenye matokeo.

Daraka Lenye Kuheshimika

Je, kazi ya kuhubiri hadharani ilikuwa kazi ya hali ya chini ambayo ilipaswa kuachiwa wanawake huku wanaume wakifanya kazi ile muhimu ya kulisimamia kutaniko? La hasha, kwa sababu mbili zifuatazo. Kwanza, Biblia inaonyesha wazi kwamba Wakristo wote—kutia ndani wanaume wenye madaraka mazito kutanikoni—walipaswa kushiriki katika huduma ya hadharani. (Luka 9:1, 2) Pili, huduma ya hadharani ilikuwa, na bado ndiyo njia ya msingi ambayo Wakristo wote, iwe ni wanaume au wanawake, hutimiza amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote na kuwafundisha.’—Mathayo 28:19, 20.

Kuna daraka lingine muhimu ambalo wanawake fulani wanatimiza kutanikoni. Paulo aliandika hivi: “Wanawake wenye umri mkubwa wawe . . . walimu wa yaliyo mema; ili kuziamsha akili za wanawake vijana wawapende waume zao, wawapende watoto wao.” (Tito 2:3, 4) Hivyo, wanawake wakomavu walio na uzoefu katika maisha ya Kikristo wana pendeleo la kuwasaidia wanawake wachanga, wasio na uzoefu wakomae. Hilo pia ni daraka zito, lenye kuheshimika.

Kufundisha Kutanikoni

Hata hivyo, Biblia haisemi mahali popote kwamba wanawake wanapaswa kufundisha mbele ya kutaniko. Badala yake, mtume Paulo aliwaagiza “wakae kimya katika mikutano.” Kwa nini? Aliandika kwamba sababu moja ni ili mambo yafanyike “kwa heshima na kwa utaratibu.” (1 Wakorintho 14:34, 40, BHN) Ili mambo kutanikoni yaendeshwe kwa utaratibu, Mungu amegawia kikundi kimoja daraka la kufundisha. Hata hivyo, mtu hapewi pendeleo la kusimamia kutaniko kwa sababu tu yeye ni mwanamume; daraka hilo linapewa wanaume ambao kwa kweli wanastahili. *1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9.

Je, daraka ambalo Mungu amewapa wanawake linawavunjia heshima? La. Kumbuka kwamba Yehova Mungu amewaweka rasmi wafanye kazi muhimu, ile ya kutoa ushahidi hadharani kumhusu yeye. (Zaburi 68:11) Kati ya Mashahidi wa Yehova leo, wanaume na wanawake wanaohudumu hadharani wamewasaidia mamilioni ya watu watubu na kupata wokovu. (Matendo 2:21; 2 Petro 3:9) Hilo ni jambo muhimu sana!

Utaratibu uliowekwa kwa ajili ya wanaume na wanawake unachangia amani na heshima kati yao. Kwa mfano: Macho na masikio hufanya kazi pamoja ili kumsaidia mtu avuke barabara yenye magari mengi. Vivyo hivyo, wanaume na wanawake wanapotimiza mapenzi ya Mungu kulingana na madaraka ambayo wamegawiwa, Mungu hulibariki kutaniko kwa amani.—1 Wakorintho 14:33; Wafilipi 4:9. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ona pia kwamba mamlaka ya mwanamume kutanikoni ina mipaka. Anajitiisha kwa Kristo na lazima atende kupatana na kanuni za Biblia. (1 Wakorintho 11:3) Wale walio na madaraka kutanikoni wanapaswa pia ‘kujitiisha kwa mmoja na mwenzake,’ wakijinyenyekeza na kushirikiana.—Waefeso 5:21.

^ fu. 15 Wanapoheshimu daraka ambalo Mungu amewapa wanaume kutanikoni, wanawake Wakristo huwawekea malaika mbinguni mfano mzuri.—1 Wakorintho 11:10.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Wanawake walifundisha kwa njia gani katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza?—Matendo 18:26.

● Ni nani ambao wamewekwa rasmi kusimamia kutaniko?1 Timotheo 3:1, 2.

● Mungu ana maoni gani kuhusu huduma ambayo wanawake Wakristo wanatimiza leo?—Zaburi 68:11.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Yehova mwenyewe anasema neno hili; wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.”—ZABURI 68:11