Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sababu Iliyonifanya Niache Kazi Yenye Pesa Nyingi

Sababu Iliyonifanya Niache Kazi Yenye Pesa Nyingi

Sababu Iliyonifanya Niache Kazi Yenye Pesa Nyingi

Limesimuliwa na Martha Teresa Márquez

NILIPENDA sana kuimba, na hata niliimba kwenye redio nilipokuwa mtoto. Masomo yangu yalifikia tu shule ya nasari (shule ya chekechea), lakini baadaye nilipata mafunzo ya kuimba huko Mexico City chini ya msimamizi wa okestra ya nchi nzima.

Mnamo 1969, nilipokuwa na umri wa miaka 24, rafiki yangu aliyekuwa mcheza-dansi alinikaribisha niimbe kwenye mkahawa ulioitwa La Rampa Azul ambao wakati huo ulikuwa maarufu sana. Niliimba wimbo uliojulikana sana Cucurrucucú Paloma wa mtungaji nchini Mexico anayeitwa Tomás Méndez, na wasikilizaji waliufurahia sana. Huo ndio uliokuwa mwanzo wa kazi yangu. Niliimba peke yangu nikitumia jina Romelia Romel.

Nilifanya kazi pamoja na Tomás Méndez, na pia watungaji na waimbaji wengine wa Mexico wenye ustadi, kama vile Cuco Sánchez na Juan Gabriel. Nilifurahi sana kuona jina langu likiandikwa kwenye vibao vikubwa vya matangazo na magazetini. Niliimba kwenye vilabu vya usiku, kwenye redio, na nilipokuwa katika ziara huko Mexico na Belize. Pia nilifanya kazi pamoja na mtumbuizaji maarufu wa Mexico Leonorilda Ochoa wakati ambapo kipindi chake cha televisheni kilikuwa bado kipya nchini.

Baada ya muda nilianza kupata umaarufu na nikaanza kupata mshahara mzuri, kiasi cha kwamba ningeweza kufurahia kujinunulia vitu vyenye thamani kama vile vito, koti zilizotengenezwa kwa ngozi ya kicheche, na nyumba nzuri. Nilikuwa na kila kitu, lakini sikuwa na furaha. Nilihisi kwamba maisha yangu ni matupu. Ingawa nililelewa katika dini ya Katoliki, niliaibika kwenda kanisani. Nilijihisi nikiwa mchafu sana kwa sababu ya maisha yangu yasiyo na maadili.

Jinsi Nilivyoanza Kumpenda Yehova

Nilipokuwa nikifanya mazoezi ya rekodi yangu ya kwanza, nilimweleza rafiki yangu aliyeitwa Lorena Wong, mwimbaji wa nyimbo za ranchera, kuhusu hisia zangu. Nilimwambia kwamba ningependa kuwa mtawa wa kike na kuwasaidia watu wanaohitaji msaada. “Eti mtawa? Umerukwa na akili!” akasema.

Kisha akaniuliza: “Je, unajua jina la Mungu?”

Nikamjibu, “Ni Bwana Yesu Kristo.”

Akaniambia, “Hapana, jina lake ni Yehova. Yesu ni Mwana wake.”

“Eti Yehova?” nikamwuliza. Jina hilo lilikuwa geni kabisa kwangu. Lorena alinipa Biblia na akaniahidi kwamba angemtuma mwalimu wake, ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova, anitembelee. *

Kila mara nilipomwona Lorena nilimwuliza, “Mwalimu wako atakuja lini?” Nilikuwa na njaa ya kiroho.

Nilianza kujisomea Biblia na nikaona kweli kwamba jina la Mungu ni Yehova. (Zaburi 83:18) Nilishangaa sana. Pia, nilisoma zile Amri Kumi na nikashangazwa na ile iliyosema: “Usifanye uzinzi.” (Kutoka 20:14) Wakati huo, nilikuwa nikiishi na mwanamume aliyekuwa na mke, ambaye pia alikuwa baba ya mwana wangu mwenye umri wa miezi minane. Huyo alikuwa mtoto wangu wa pili. Tayari nilikuwa nimezaa mwana na mwanamume mwingine ambaye pia hatukuwa tumefunga ndoa.

Siku moja nilipokuwa nikijizoeza wimbo kwa ajili ya kipindi fulani kipya, mlango wa nyumba yangu ulibishwa. Kumbe alikuwa mwalimu wa Lorena, Mauricio Linares, pamoja na mke wake. Walinionyesha kusudi la Mungu kwa ajili ya wanadamu na wakaniachia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. * Nilikisoma chote kwa usiku mmoja ingawa niling’ang’ana kuelewa maneno magumu. Hapo ndipo nilipoanza kumpenda Yehova.

Nabadili Maisha Yangu

Mashahidi waliponisaidia kujifunza Biblia na kuboresha uwezo wangu wa kusoma, nilitambua kwamba lazima nibadili maisha yangu ili nimpendeze Yehova. Hatua kwa hatua nilitupa sanamu zangu, medali, na hirizi za bahati njema, hata ingawa vilikuwa vya dhahabu.

Ilikuwa vigumu hasa kuacha kuvuta sigara na kunywa kupita kiasi. Nilipopita kwenye duka lililokuwa likiuza kileo, mdomo wangu ungejaa mate. Nililazimika kujitenga na marafiki wangu wote, kwa sababu walinipa vinywaji na kunikaribisha kula na kunywa katika mikahawa ya hali ya juu. Nilijua kwamba hilo lingenifanya nitumie kileo vibaya.

Pia ilikuwa vigumu kwangu kuacha kuhudhuria karamu za watu matajiri na maarufu. Nilipokaribishwa kwenye karamu ya siku ya kuzaliwa ya mchezaji wa ndondi maarufu kutoka Cuba, nilisali hivi: “Yehova nitaenda kwa mara ya mwisho tu. Sitaenda tena kwenye tukio kama hili wala sitajihusisha katika mwenendo ambao haukupendezi.” Nami sijawahi kufanya hivyo tena.

Nilivunja uhusiano wangu na baba ya mtoto wangu wa pili. Nilifanya hivyo licha ya kwamba alikuwa na utajiri mwingi na aliniahidi kwamba angenipa vitu vingi ikiwa singemwacha. Ilikuwa vigumu sana kwangu kufanya hivyo kwa kuwa nilimpenda, naye alijua hivyo. Aliniambia hivi kwa kiburi: “Mimi ndiye Mungu wako! Mimi ndiye Kristo wako!”

Nilimjibu hivi, “Huenda wakati fulani ulikuwa, lakini sasa Yehova ndiye Mungu wangu.” Alinitisha kwamba angeninyang’anya mwana wake na kuniumiza.

Wakati huo watu fulani waliniambia kwamba kuimba ni kazi tu kama kazi nyingine, kwa hiyo, ningeweza kuwa Shahidi na bado niimbe. Hata hivyo, wengine walinikumbusha hivi, “Hakuna chochote kitakachokulinda usivute sigara, usitumie kileo, au kukuzuia usiathiriwe na ukosefu wa maadili wa mashabiki wako.” Nilitambua hekima ya maneno hayo.

Nilipokuwa mwimbaji mashuhuri, watu walinipa pesa nyingi ili kunishawishi kufanya mambo yasiyofaa. Niliazimia kwamba sitashawishiwa hivyo tena. Kwa hiyo, mnamo 1975, nilivunja mkataba wangu wa kutembelea China, na miezi sita baadaye nikabatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova.

Magumu na Shangwe

Ningeruzuku familia yangu kwa njia gani? Sikuwa na elimu yoyote na sikujua kufanya kazi yoyote isipokuwa kuimba. Dada yangu mkubwa, Irma, na watoto wake watatu, kutia ndani wana wangu wawili wachanga walikuwa wakinitegemea. Tulilazimika kutoka kwenye nyumba yangu ya bei ghali na kuhamia nyumba yenye vyumba viwili vidogo. Lilikuwa badiliko kubwa kutoka kwa maisha ya hali ya juu na kuanza kuishi maisha magumu. Kwa muda fulani, dada yangu na watoto walinidhihaki na kunichochea niendelee na kazi ya kuimba, lakini niliazimia kufanya yote niliyohitaji kufanya ili nimtumikie Yehova.

Nilianza kuuza vitu vyangu vyenye thamani, yaani, vito, koti, na gari langu, na pesa tulizopata ndizo zilizoturuzuku. Baada ya muda, pesa hizo zilikwisha. Ili tuepuke kudhulumiwa na baba ya mwana wangu wa pili, mnamo 1981 tulihamia jiji fulani upande mwingine wa nchi ambako hangeweza kutupata.

Mashahidi katika jiji hilo walinifundisha jinsi ya kutengeneza aina fulani ya sambusa, donati, na vyakula vingine vya kuuza. Baadaye niliajiriwa kwenye kiwanda na nikawa nikifanya kazi usiku. Lakini kazi hiyo ilikuwa ikinizuia nisihudhurie mikutano ya Kikristo na iliathiri utumishi wangu kwa Mungu. Kwa hiyo, mwishowe nilijiuzulu na nikaanza kupika sambusa nikiwa nyumbani. Ningezibeba katika vikapu na kuziuza barabarani. Nimeweza kujiruzuku kwa njia hiyo katika utumishi wa wakati wote.

Uamuzi Ambao Sijawahi Kujutia

Watu wanaponiuliza jinsi ninavyohisi kwa kuacha kazi nzuri ya kuimba, ninawaambia kuwa hakuna chochote ninachoweza kubadili na ujuzi niliopata kumhusu Yehova na uelewaji wa makusudi yake ya ajabu. Imekuwa shangwe kwangu kuwaona wana wangu wakifanya maendeleo na kupata ujuzi wa Biblia, wakijiweka wakfu kwa Yehova, na kisha kuoa waamini wenzao. Wana wangu wawili, wakisaidiwa na wake zao, wanajitahidi kuwalea watoto wao ili wamtumikie Mungu wetu, Yehova.

Kwa karibu miaka 30 nimekuwa painia, kama Mashahidi wa Yehova wanavyowaita wale wanaoshiriki katika kazi ya kuhubiri wakati wote. Kwa msaada wa Mungu nimefaulu kuwasaidia watu wengi sana, kutia ndani dada yangu mkubwa Irma na binti yake, wajifunze kweli za Biblia na kuweka maisha yao wakfu kwa Mungu. Ninapata shangwe kubwa sana ninapokutana na “watoto wangu wa kiroho” na kuwaona bado wakiendelea kutembea katika kweli, na wengi wao wakiwa mapainia. (3 Yohana 4) Leo, nikiwa na umri wa miaka 64, ninajifunza Biblia pamoja na watu 18.

Ile hisia niliyokuwa nayo nilipokuwa mwimbaji mwenye umri mdogo kwamba maisha yangu ni matupu, na tamaa ya kuwasaidia wengine imetoshelezwa kwa kutii amri ya Yesu ya ‘kwenda kufanya wanafunzi.’ (Mathayo 28:19, 20) Ninashukuru kama nini kwamba Yehova amenitegemeza miaka hii yote na bado anaendelea kufanya hivyo! Kwa kweli, ‘nimeonja na kuona ya kuwa yeye ni mwema.’—Zaburi 34:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Baadaye Lorena Wong alikuja kuwa Shahidi wa Yehova.

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na wana wangu, wake zao, na dada yangu mkubwa, ambaye tunashirikiana kufanya upainia

[Picha katika ukurasa wa 26]

Bado ninapika sambusa na kuziuza barabarani ili nijiruzuku ninaposhiriki katika utumishi wa wakati wote