Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Huuliza

Ninaweza Kukabilianaje na Mfadhaiko Shuleni?

Ninaweza Kukabilianaje na Mfadhaiko Shuleni?

“Kadiri unavyokua mfadhaiko unaopata shuleni haupungui badala yake unapata sababu nyingine tu za kufadhaika.”—James, New Zealand. *

“Nilipata mkazo mwingi sana shuleni hivi kwamba mara nyingi nilitaka kulia na kupiga mayowe.”—Sharon, Marekani.

JE, UNAHISI kwamba wazazi wako hawaelewi mfadhaiko unaopata shuleni? Ni kweli kwamba huenda wazazi wako wakakuambia huhitaji kulipa mkopo wa benki, kulisha familia, au kumpendeza mwajiri. Hata hivyo, inaelekea unahisi kwamba ukiwa shuleni unapata mfadhaiko sawa tu na wazazi wako au hata zaidi.

Huenda safari ya kwenda na kutoka shuleni ikaleta mfadhaiko. “Mara nyingi, vita vilitokea kwenye basi la shule,” anasema Tara, anayeishi Marekani. “Dereva angesimamisha basi na kila mtu angelazimika kushuka. Sote tungechelewa kwa nusu saa hivi.”

Je, mfadhaiko huisha unapofika shuleni? La hasha! Huenda umekabiliana na hali kama zinazotajwa hapa chini.

Mfadhaiko unaosababishwa na walimu.

“Walimu wangu wanataka nifaulu na kupata alama za juu zaidi, nami ninashinikizwa kuwapendeza.”—Sandra, Fiji.

“Walimu huwashinikiza wanafunzi wafanye vema katika masomo, hasa ikiwa mwanafunzi ana vipawa fulani. Walimu huwakaza sana wafaulu.”—April, Marekani.

“Hata ingawa una miradi mizuri maishani, walimu fulani wanakufanya uhisi kwamba hufai usipofuatilia miradi ya masomo ambayo wao wanafikiri kwamba unapaswa kufuatilia.”—Naomi, Marekani.

Unaathiriwaje na mfadhaiko unaosababishwa na walimu?

Mfadhaiko unaosababishwa na wanafunzi wenzako.

“Katika shule ya sekondari, wanafunzi wana uhuru zaidi na ni waasi zaidi. Usipojiunga nao, wanakuona kuwa mshamba.”—Kevin, Marekani.

“Kila siku, mimi hushawishiwa kunywa vileo na kufanya ngono. Wakati mwingine ni vigumu kukataa kujiunga nao.”—Aaron, New Zealand.

“Sasa nina umri wa miaka 12, na jambo linalonifadhaisha zaidi ni kwamba ninashinikizwa niwe na rafiki wa jinsia tofauti. Kila mtu shuleni huniuliza, ‘Utakaa mseja mpaka lini?’”—Alexandria, Marekani.

“Nilishinikizwa niwe na rafiki wa kiume. Nilipokataa, walisema kwamba mimi ni shoga. Na wakati huo, nilikuwa na umri wa miaka kumi tu!”—Christa, Australia.

Unaathiriwaje na mfadhaiko unaosababishwa na wanafunzi wenzako?

Mfadhaiko kuhusu maoni ya wanafunzi wenzako unapowaambia kuhusu imani yako ya kidini.

“Ni vigumu kuwaeleza wanafunzi wenzako kuhusu imani yako kwa sababu hujui watakuonaje baadaye. Unahofia kwamba watakuona kuwa tofauti.”—Carol, Hawaii.

“Katika shule za msingi na za sekondari, wanafunzi wanajihusisha na dawa za kulevya, ngono, na pombe. Inafadhaisha sana kwa kuwa hutaki wanafunzi wenzako wakudhihaki kwa sababu unaishi kulingana na viwango vya Biblia.”—Susan, Marekani.

Unaathiriwaje na masuala yanayohusu imani yako?

Mambo mengine yanayosababisha mfadhaiko.

Tia alama kando ya jambo linalokuathiri zaidi au uandike jambo lingine linalokuathiri.

  • Mitihani inapokaribia

  • Kazi za shuleni

  • Wazazi wanatarajia utimize mengi

  • Kutimiza matarajio yako mengi

  • Kuonewa au kutendewa vibaya kingono

  • Mengine ․․․․․

Hatua Tano za Kupunguza Mfadhaiko

Si jambo linalopatana na akili kutarajia kwamba hutapatwa na mfadhaiko wowote ukiwa shuleni. Ni kweli kwamba mfadhaiko unaweza kumfanya mtu ahangaike. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname.” (Methali 12:25) Lakini usiruhusu mfadhaiko ufanye moyo wako uiname. Siri ni kujifunza jinsi ya kukabiliana na mfadhaiko wako kwa njia nzuri.

Kukabiliana na mfadhaiko ni kama kunyanyua vyuma. Ili afaulu, mnyanyua-vyuma anahitaji kujitayarisha vizuri. Ananyanyua vyuma kwa njia inayofaa na anaepuka kunyanyua vyuma vizito sana. Akifanya hivyo, atakuwa na misuli yenye nguvu bila kuumiza mwili wake. Kwa upande mwingine, akikosa kuchukua hatua hizo, anaweza kuumiza misuli au hata kuvunja mfupa.

Vivyo hivyo, unaweza kukabiliana na mfadhaiko na kufanya kazi unazohitaji kufanya bila kujiumiza. Kwa njia gani? Chukua hatua zifuatazo:

  1. Tambua visababishi hususa. Methali moja yenye hekima inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Lakini huwezi kujificha kutokana na mfadhaiko kabla hujatambua kisababishi. Hivyo, pitia tena mambo uliyoandika hapo juu. Ni jambo gani linalokuathiri zaidi?

  2. Fanya utafiti. Kwa mfano, ikiwa kazi nyingi za shule zinakufadhaisha, chunguza mapendekezo yaliyo katika makala “Vijana Huuliza—Nawezaje Kupata Wakati wa Kufanya Kazi za Shule?” katika toleo la Amkeni! la Januari 22, 2004 (22/1/2004). Ikiwa unahisi unashinikizwa ufanye ngono na mwanafunzi mwenzako, utapata shauri linalofaa katika makala “Vijana Huuliza—Nifanyeje Nikiombwa Nifanye Ngono?” katika toleo la Amkeni! la Machi (Mwezi wa 3) 2007.

  3. Jitayarishe mapema. Ikiwa unafadhaishwa na jinsi wanafunzi wenzako watakavyoitikia utakapowaambia kuhusu imani yako ya kidini, usingoje hadi watakapokuuliza ili uanze kufikiria jambo la kusema. (Methali 29:25) Kelsey, mwenye umri wa miaka 18 anasema hivi: “Kile kimenisaidia kukabiliana na mfadhaiko huo ni kujitayarisha mapema. Nilikuwa nimetayarisha jinsi nitakavyowaeleza imani yangu.” Aaron, mwenye umri wa miaka 18 anayeishi Ubelgiji, alifanya vivyo hivyo. “Nilifikiria mapema kuhusu maswali ambayo ningeulizwa, kisha nikatayarisha majibu ya maswali hayo,” anasema. “Kama singefanya hivyo, singekuwa na ujasiri wa kuzungumza kuhusu imani yangu.”

  4. Usiahirishe. Matatizo hayatokomei unapoyapuuza. Badala yake, yanazidi kuwa makubwa na hivyo kuongeza mfadhaiko wako. Kwa mfano, ikiwa wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, kujitambulisha mapema iwezekanavyo kutakulinda. Marchet, ambaye sasa ana umri wa miaka 20 anasema: “Kila mwaka shule zilipofunguliwa, mimi nilianzisha mazungumzo kuhusu habari ambayo ninajua itanipa nafasi ya kueleza viwango vya Biblia. Niligundua kwamba nisipojitambulisha mara moja kuwa mimi ni Shahidi, ingekuwa vigumu kufanya hivyo baadaye. Ilikuwa rahisi zaidi nilipoeleza imani yangu na kujitahidi kuishi kupatana nayo mwaka mzima.”

  5. Omba msaada. Hata mnyanyua-vyuma mwenye nguvu sana ana mipaka ya uzani anaoweza kuinua. Wewe pia una mipaka. Lakini huhitaji kubeba mzigo huo mzito peke yako. (Wagalatia 6:2) Kwa nini usizungumze na wazazi wako au Wakristo wengine wakomavu? Waonyeshe majibu uliyoandika mwanzoni mwa makala hii. Jadiliana nao jinsi wanavyoweza kukusaidia kukabiliana na baadhi ya mikazo hiyo. Liz, anayeishi Ireland alimwambia baba yake kuhusu hofu ya kudhihakiwa kwa sababu ya imani yake ya kidini. Liz anasema hivi: “Kila siku, baba yangu alisali pamoja nami kabla ya kunipeleka shuleni. Siku zote hilo lilinifanya nihisi nikiwa salama.”

Je, Kuna Mfadhaiko Unaofaa?

Amini usiamini, ni vizuri kufadhaika wakati fulani. Kwa nini? Huenda hilo likawa ishara ya bidii yako na kwamba dhamiri yako inafanya kazi. Ona jinsi Biblia inavyomfafanua mtu ambaye inaonekana hafadhaiki hata kidogo. “Ewe mvivu, utalala hapo mpaka lini? Utaamka lini katika usingizi wako? Wasema: ‘Acha nilale kidogo tu, acha nisinzie kidogo! Niache nikunje mikono nipumzike kidogo!’ Wakati huo umaskini utakuvamia kama mnyang’anyi, ufukara utakufuata kama jambazi.”—Methali 6:9-11, BHN.

Heidi, mwenye umri wa miaka 16 anakata kauli hivi, “Huenda mikazo unayokabili shuleni ikaonekana kuwa mibaya sana, lakini utakabili mikazo hiyohiyo kazini.” Ni kweli kwamba si rahisi kukabiliana na mfadhaiko, lakini unapokabiliana nao kwa njia inayofaa, mfadhaiko hautakudhuru. Badala yake, unaweza kuboresha utu wako.

 

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

  • Ni dalili gani zitakazoonyesha kwamba una mfadhaiko?

  • Kwa nini mfadhaiko unaongezeka unapotazamia ukamilifu kutoka kwako na kwa wengine?

  • Unaweza kuzungumza na nani unapohisi umelemewa na mfadhaiko?