Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kifo—Je, Kweli Ndio Mwisho?

Kifo—Je, Kweli Ndio Mwisho?

Kifo—Je, Kweli Ndio Mwisho?

MNAMO Februari (Mwezi wa 2) 1987, mwanamume mwenye umri wa miaka 85 aliyekuwa na ugonjwa wa figo, aliacha kutumia mashine ya kusafisha damu iliyokuwa ikimsaidia kuishi. Majuma mawili baadaye, alikufa kwa utulivu nyumbani huku mwanaye wa pekee akiwa kando yake.

Muda wao wa mwisho pamoja uliwapa nafasi ya kuzungumzia jambo walilokuwa wamezungumzia mapema: Je, wafu wanaweza kuishi tena? Baba aliyekuwa na elimu ya juu alikuwa na mashaka kuhusu jambo hilo. Aliamini fundisho la mageuzi na alichukizwa na unafiki wa kidini. Aliamini kwamba mambo ya Mungu hayawezi kujulikana.

Akitamani kumfariji na kumpa tumaini baba yake, mwana huyo alimwonyesha kwa nini wafu wanaweza kuishi tena. Kifo chake kilipokaribia, baba huyo alikubali kwamba angetamani kuishi tena akiwa mwenye afya na nguvu.

Faraja Tunapokabili Kifo

Watu wengi wangetamani kuishi tena ikiwa wangerudishiwa afya na nguvu katika ulimwengu ulio na amani. Wanadamu ni tofauti na wanyama ambao wanafafanuliwa katika Biblia kuwa “wasiofikiri” au “viumbe wanaoongozwa na silika.” (2 Petro 2:12; New International Version) Sisi huwazika wafu. Sisi tunafikiri kuhusu wakati ujao. Sisi hatutaki kuzeeka, kuwa wagonjwa, na kufa. Hata hivyo, mambo hayo huwapata wanadamu.

Tunahuzunishwa tunapofikiria kwamba sisi au mpendwa wetu anaweza kufa. Hata hivyo, Biblia inatutia moyo tukabiliane na kifo kwa ujasiri inaposema: “Ni afadhali kwenda katika nyumba ya maombolezo kuliko kwenda katika nyumba ya karamu.” Inaongezea hivi: “Aliye hai anapaswa kuliweka jambo hilo moyoni mwake.” (Mhubiri 7:2) Kwa nini tuliweke jambo hilo moyoni au tufikirie kifo kwa uzito?

Sababu moja ni kwamba tumezaliwa na tamaa ya kuishi na kufurahia maisha ya amani na usalama. Hakuna mtu anayetaka kufa au kutokuwepo. Ni vigumu sana kufikiria kwamba tutaacha kuishi. Biblia inaeleza sababu inaposema: “[Mungu] ameweka umilele katika akili ya mwanadamu,” au “ndani ya moyo wao.” (Mhubiri 3:11, Revised Standard Version) Tunataka kuishi, si kufa. Hebu fikiria kuhusu hilo: Je, tamaa hiyo ingekuwa yenye nguvu sana ikiwa Muumba hakukusudia tuishi milele? Je, tunaweza kuishi tena tukiwa na afya na furaha milele?

Kwa Nini Tuamini?

Mwaka jana, gazeti AARP The Magazine, linalochapishwa na Shirika la Marekani la Wastaafu, lilikuwa na makala yenye kichwa “Uhai Baada ya Kifo.” Watu wengi wenye umri wa zaidi ya miaka 50 walihojiwa na “asilimia 73 hivi wanakubaliana na maneno haya, ‘Ninaamini kwamba kuna uhai baada ya kifo.’” Kwa upande mwingine, gazeti hilo liliripoti kwamba karibu asilimia 25 walikubaliana na maneno haya, “Ninaamini kwamba nikifa, huo ndio mwisho.” Lakini je, kweli hivyo ndivyo watu wanataka kuamini?

Katika makala hiyohiyo, Tom ambaye ni Mkatoliki kutoka New York, aliripotiwa kusema hivi: “Viongozi wa kidini wanahubiri kwamba kuna uhai baada ya kifo. Mimi hujiambia, kila mtu ana maoni yake. Kwa hiyo, mtu hujiamulia atakachoamini. Mimi huhudhuria Misa. Ninaishi kana kwamba kuna uhai baada ya kifo lakini siamini hilo. Ikiwa kunao, basi nitafaidika.”

Kama vile Tom, watu wengi wana mashaka kama baba aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii alimwambia mwanaye hivi mara nyingi: “Kuwa na imani ya kidini ni sawa kwa watu wanaoshindwa kukubali kwamba kifo ni jambo halisi.” Hata hivyo, yeye pamoja na watu wengine walio na mashaka wamelazimika kukubali kwamba kumwamini Muumba mwenye nguvu zote kunatoa majibu kuhusu miujiza isiyoeleweka kwa njia nyingine yoyote.

Kwa mfano, majuma matatu tu baada mimba kutungwa, kiini-tete cha mwanadamu huanza kutokeza chembe za ubongo. Chembe hizo huongezeka haraka sana, mara nyingine hata kufikia 250,000 kwa dakika. Miezi tisa baadaye, mtoto huzaliwa akiwa na uwezo wa ajabu wa kujifunza. Mwanabiolojia wa molekuli James Watson alisema kwamba ubongo wa mwanadamu ndicho “kitu tata zaidi ambacho tumepata kugundua katika ulimwengu wetu.”

Watu wengi hustaajabu wanapofikiria maajabu kama hayo. Vipi wewe? Je, kutafakari kuhusu mambo hayo kumekusaidia kujibu swali hili lililoulizwa na mtu fulani miaka mingi iliyopita: “Mtu akifa, je, anaweza kuishi tena?” Mtu huyo alimjibu Mungu hivi kwa uhakika: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.”—Ayubu 14:14, 15.

Kwa kweli, tuna sababu ya kuchunguza uthibitisho unaoonyesha kwamba inawezekana kuishi baada ya kifo.