Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Desturi za Kale Katika Mexico ya Leo

Desturi za Kale Katika Mexico ya Leo

Desturi za Kale Katika Mexico ya Leo

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI MEXICO

DESTURI na imani za kale za kidini bado zinafuatwa katika Mexico ya leo ambapo watu wanatumia simu za mkononi na Intaneti. Kwa karne nyingi, desturi fulani za Wenyeji wa Asili wa Amerika zilichanganywa na Ukatoliki. Kwa kweli, bado desturi hizo ni sehemu muhimu ya ibada ya Wakatoliki wa Mexico.

Kwa mfano, kila mwaka, Novemba 2, watu wengi huko Mexico huenda kwenye makaburi ili kukumbuka Siku ya Nafsi Zote, ambayo pia inaitwa Siku ya Wafu. Wao huwaachia wapendwa wao waliokufa maua, chakula, na kileo. Wengine hata hupanga wanamuziki wacheze nyimbo ambazo wapendwa wao walipenda kusikiliza. Pia Wakatoliki wengi hujenga madhabahu katika nyumba zao na wanaweza kuweka picha za mpendwa wao aliyekufa.

Kichapo Enciclopedia de México kinasema kwamba inaonekana mazoea fulani yaliyohusu sherehe za wafu “yana mambo fulani yaliyokuwa katika sherehe za Wenyeji wa Asili wa Amerika zilizofanywa katika miezi ya ochpaniztli na teotleco, wakati ambapo maua ya cempasúchil na vyakula vilivyotengenezwa kwa unga wa mahindi vilitolewa kwa manes [roho za wafu] wakati ambapo mavuno yangekuwa yamekusanywa, yaani, mwishoni mwa Oktoba na mwanzoni mwa Novemba.” Kama ensaiklopidia hiyo inavyoonyesha, desturi fulani hufuata sherehe zinazofanana na zile zilizokuwapo wakati wa kipindi cha kabla ya Wahispania, ambazo zilitia ndani sherehe zenye shamrashamra.

Ibada ya Sanamu

Desemba (Mwezi wa 12) 12 ni sikukuu ya Wakatoliki wa Mexico. Siku hiyo maelfu ya mahujaji kutoka sehemu mbalimbali za Mexico hukusanyika kwenye kanisa la Bikira wa Guadalupe lililo kwenye Mlima Tepeyac huko Mexico City. Wengi wao hutembea kwa siku nyingi, wakisali kwa Bikira huyo. Wanapowasili, wao huingia kanisani wakiwa wamepiga magoti (juu) na kutoa maua ya waridi.

Leo, sanamu za Bikira wa Guadalupe hupatikana pia katika nyumba za watu na vilevile katika vituo vya basi na maeneo mengine ya umma. Bikira wa Guadalupe ameitwa “Mama ya Mungu” na “Msichana Mweusi wa Tepeyac.” Tangu karne ya 16, mara nyingi waumini wamesema kwamba Bikira huyo ameponya na kufanya miujiza mingine.

Chanzo cha Ibada ya Bikira

Ibada ya mungu huyo wa kike pamoja na mambo mengine yanayohusiana na sikukuu hiyo, ilianza na ibada ya mungu-mama wa Azteki anayeitwa Cihuacóatl, ambaye pia anaitwa Tonantzin, jina linalomaanisha “Mama Yetu Mdogo.” Kitabu México a través de los siglos (Historia ya Mexico) kinasema kwamba Waazteki wa zamani walileta mungu huyo, pamoja na mwana wake Huitzilopochtli, huko Tenochtitlán, ambao ulikuwa mji mkuu wa Milki ya Azteki, ambayo sasa ni Mexico City.

Wahispania waliharibu hekalu la Cihuacóatl, lililo kwenye Mlima Tepeyac. Kulingana na mapokeo, miaka 40 hivi baada ya Columbus kufika kwenye bara hilo, Bikira wa Guadalupe alimtokea Mwenyeji wa Asili wa Amerika, Juan Diego. Inasemekana kwamba aliomba madhabahu ijengwe mahali hapo kwa ajili yake.

Cihuacóatl aliheshimiwa sana na Waazteki. Inasemekana kwamba alikuwa na nywele ndefu, ambazo hazikuwa zimesukwa na alivaa nguo ndefu nyeupe. Hekalu lake lilikuwa mlango mfupi sana hivi kwamba mtu angeweza tu kuingia akiwa amepiga magoti. Akiwa ndani, mtu angeona sanamu yake iliyokuwa imezungukwa na sanamu nyingine na hivyo kumfanya aonekane kuwa “mama . . . wa miungu.”

Sherehe ya Cihuacóatl ilitia ndani kutoa dhabihu za wanadamu, kucheza dansi, na misafara ya askari-jeshi waliovaa “maua ya waridi mikononi, shingoni, na vichwani.” Zawadi hizo ziliachwa juu ya hekalu kama dhabihu kwa Huitzilopochtli. Wenyeji fulani wa Asili wa Amerika, kutia ndani wengi kutoka Guatemala, wangetembea kwa zaidi ya kilomita elfu moja kwenda kwenye sikukuu ya Cihuacóatl.

Je, Ni Muhimu Kuchunguza Chanzo cha Ibada?

Ni wazi kwamba ibada ya sanamu ya Kikatoliki ya Bikira wa Guadalupe imetokana na desturi za watu ambao hawakumwabudu Mungu wa kweli wa Biblia. (Zaburi 83:18) Je, hilo liathiri maoni yetu kuhusu ibada hiyo? Je, ni muhimu kuchunguza chanzo cha ibada?

Mtume Paulo alitoa shauri hili lenye hekima kuhusu jambo hilo: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini. . . . Kuna upatano gani kati ya Kristo na Beliali? Au mtu mwaminifu ana fungu gani na asiye mwamini?” Paulo alisema hivi pia: “Hakikisheni mambo yote; shikeni sana yaliyo mazuri.”—2 Wakorintho 6:14, 15; 1 Wathesalonike 5:21.

Kitia-moyo hicho kinafaa leo pia. Tunapaswa kutafakari ibada yetu kwa Mungu na kujiuliza: ‘Je, ibada yangu inafuata kabisa mafundisho ya Neno la Mungu, Biblia? Au je, ina sehemu fulani ambazo zimetokana na ibada ya watu wanaotumikia miungu ya uwongo?’ Mtu anayetaka kumpendeza Yehova, Mungu wa kweli, atatafuta majibu ya maswali hayo.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mahujaji wakiwasili katika kanisa la Bikira wa Guadalupe

[Picha katika ukurasa wa 23]

Wanamuziki makaburini siku ya Novemba 2