Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vita Vilivyobadili Maisha Yangu

Vita Vilivyobadili Maisha Yangu

Vita Vilivyobadili Maisha Yangu

SIMULIZI LA MICHAEL MOLINA

‘Jamhuri ya Viet Nam ilimpa Molina, Ofisa wa cheo cha chini cha manowari, medali yenye umbo la msalaba ya Vietnam,’ likaripoti gazeti la kijeshi “Tester,” la Maryland, Marekani. ‘Baadaye, Molina alipewa medali ya dhahabu yenye umbo la nyota kama tuzo lake la pili la kumpongeza kwa sababu ya ujasiri na bidii yake katika mapigano mengine makali ya kijeshi. Juni 6, 1968, Molina alijishindia medali nyingine ya dhahabu yenye umbo la nyota alipozuia kikosi muhimu kisiangamizwe na wapiganaji wa kuvizia wa Viet Cong.’

KWA ujumla, nilishiriki katika vita 284 na nikapewa nishani 29. Sasa ninatumikia nikiwa mhudumu Mkristo katika vita tofauti, ambavyo Biblia inasema hivi kuvihusu: “Silaha za vita vyetu si za kimwili.” (2 Wakorintho 10:4) Acheni niwaeleze jinsi nilivyofanya mabadiliko maishani.

Jiji la Chicago liko kaskazini mwa Illinois, Marekani, ambalo sikuzote ni kana kwamba linapigwa na pepo kali zinazotoka kwenye Ziwa Michigan. Siku niliyozaliwa huko, Februari 1, 1947, kulikuwa na upepo na pia baridi kali sana. Kwa kuwa baba yangu alikuwa ametoka tu kupigana kwenye Vita vya Pili vya Ulimwengu, madaktari wawili wa kijeshi walimsaidia mama kujifungua. Nilipokuwa na umri wa miaka kumi, wazazi wangu walihamisha familia yetu hadi Los Angeles, California, ambako walinipeleka mimi, kaka yangu, na dada yangu kwenye shule fulani ya Wakatoliki.

Nikiwa mdogo nilikuwa nikicheza besiboli na kandanda mitaani na kwenye maeneo yasiyo na majengo, na pia nilijifanya kuwa askari nikitumia bunduki za mbao. Miaka ya 1960, nilipoanza shule ya upili, ilikuwa miaka ya mabadiliko makubwa ya fikira na mitazamo. Kuuawa kwa viongozi wa kijamii na kisiasa, kutia ndani kupigwa risasi kwa rais wa Marekani mwaka wa 1963; na vilevile maandamano, kuteketeza bendera ya Marekani, na maandamano yenye jeuri, yalikuwa mambo ya kawaida. Nilipokuwa shuleni, mimi na wanadarasa wenzangu tulikuwa na wasiwasi kuhusu kuandikishwa jeshini.

Muda mfupi baada ya kuhitimu shule ya upili mwaka wa 1966, nilipokea barua ya kunitaka niende kupimwa kitiba na nikapatikana kuwa na afya nzuri. Hata hivyo, badala ya kuandikishwa katika jeshi la nchi kavu, nilijiunga na jeshi la wanamaji. Kwa kuwa nilivutiwa na helikopta, nilijitolea kufanya kazi na kikosi kipya cha wanamaji wanaotumia helikopta kushambulia maadui. Mnamo Novemba 1967, muda mfupi baada ya kupokea mazoezi ya msingi, nilijikuta Saigon, mji mkuu wa Vietnam.

Mambo Niliyojionea Vitani Hapo Mwanzoni

Baada ya muda mfupi, nilipelekwa kwenye uwanja mdogo wa ndege, ambako kulikuwa na helikopta nne aina ya Huey. Baadhi ya kikosi cha askari wenzetu cha mabaharia 30 walilala kwenye uwanja huo wa ndege, hali wengine wetu tulipelekwa kulala kwenye jumba la orofa mbili lililokuwa umbali wa kilometa 16. Usiku wa kwanza, niliamka kwa ghafula huku risasi zikipenya kwenye jengo hilo. Nilijibingirisha kutoka kitandani mwangu na kulala chali sakafuni kwa sekunde chache. Niliposikia mlio wa risasi juu yangu, nilitafuta njia inayoelekea kwenye ngazi na nikafaulu kufika kwenye paa, ambako mtu fulani alinipa bunduki. Tulipigana usiku kucha, tukiwa na nguo za ndani bila viatu.

Baada ya siku tatu za mapigano makali, huku tukiwa tumezingirwa na kutenganishwa na wengine, tulimaliza chakula na maji tuliyokuwa nayo na risasi zetu nyingi. Ofisa aliyekuwa akitusimamia alitoa agizo hili: “Jua likichomoza tu, tutakimbia mara moja hadi kwenye uwanja wa ndege.” Ilitubidi kuvuka mji mdogo uliokuwa ukiteketea. Tungeweza kusikia risasi zikifyatuliwa, kutia ndani mlio wa bunduki zinazomimina risasi tulipokuwa tukipita katika mji huo. Maiti zilitapakaa kila mahali.

Hatimaye tulifika kwenye uwanja wetu wa ndege, ambako hali haikuwa afadhali. Tulichimba mashimo haraka-haraka kuzunguka uwanja huo wa ndege na kujaribu kujihami. Mara kadhaa jeshi la Vietcong lilivamia uwanja wetu mdogo wa ndege, na kuua watu wengi, kutia ndani kamanda wetu mkuu. Nilikaa ndani ya shimo kwa majuma kadhaa bila kubadili mavazi au kuoga. Kisha tukahamishwa kwa helikopta hadi kituo kingine.

Baada ya kupigana siku hizo za kwanza-kwanza, niliazimia kuwa mpiga-mizinga wa helikopta. Nilizoezwa kwa siku chache na nikawa sehemu ya kikosi hicho cha ndege. Mapigano ya bunduki yalikuwa ya kawaida; nyakati nyingine nilienda vitani mara tatu au nne kwa siku.

Matokeo ya Vita

Nilishtuka kuona watu wengi sana wameuawa. Wakati huohuo, nilifikiria kuhusu maandamano ya kupinga vita huko nyumbani. Je, hatukuwa tukipigania uhuru? Je, hatukuwa tukihatarisha maisha yetu ili wengine waishi maisha bora? Hata hivyo, nilijiuliza kama kulikuwa na sababu nzuri ya kupigana vita hivyo. Ni nani angenufaishwa navyo? Raia wa Vietnam? Walikuwa wamevumilia vita kwa miaka mingi hata kabla hatujaenda huko. Sasa watu wengi zaidi walikuwa wanakufa na kuteseka.

Nilikuwa na umri mdogo na sikuelewa siasa zilizochochea vita hivyo. Hata sikuwa na wakati wa kufikiria siasa hizo. Nilijua tu kwamba nilikuwa na vita vya kupigana na kazi ya kufanya kwa kuwa nilikuwa nimezoezwa kufanya hivyo. Wanajeshi wa majini walikuwa wakisema, “Tulizoezwa kupigana, si kufikiri.” Hata hivyo, nilijiambia kwamba ikiwa nitaokoka, nitafanya uchunguzi mkali ili kujua sababu iliyotupeleka huko.

Vita vya Vietnam vilifanya nianze kutumia kitu fulani chenye uraibu, yaani, dawa za kulevya. Nilipokuwa tineja, nilivuta sigara, nikanywa bia na wiski mwisho-juma na kwenda kwenye karamu. Lakini sikuwa nimewahi kutumia dawa za kulevya. Mambo yalibadilika nilipokuwa Vietnam. Wanajeshi wenzangu walisema: “Mike, mbona usitumie dawa hizi? Si kesho utauawa tu.” Kwa hiyo, pindi fulani nilikubali kuzitumia.

Bila shaka, haifai kutumia dawa za kulevya unapokuwa vitani, na niliapa kwamba singezitumia kabla ya kwenda vitani. Hata hivyo, niliporudi nyumbani, bado nilikuwa na tamaa ya kutumia dawa za kulevya, na nikaanza kuzitumia.

Narudi Kutoka Vitani

Nilipotoka Vietnam na kurudi nyumbani huko California mnamo Oktoba 1970, mtazamo wangu kuhusu maisha ulikuwa umebadilika sana. Ingawa nilikuwa nimejiunga na jeshi ili kupigania uhuru, nilihisi kwamba nilikuwa nimetumiwa vibaya. Nilirudi nikiwa mchungu na mwenye chuki nyingi. Singeweza kuchangamana na watu na sikuwa mzalendo tena.

Nilivuta bangi siku nzima na kutumia dawa nyingine za kulevya huku nikitengeneza pikipiki yangu katika gereji ya wazazi wangu. Nilishuka moyo hata zaidi nilipotafakari kuhusu hali yangu na kufikiria mambo yaliyotukia huko Vietnam. Dhamiri yangu ilianza kunisumbua. Nilitamani sana kuchunguza kile kilichofanya Vita vya Vietnam vipiganwe.

Serikali iliwapa wale waliotumikia jeshini fedha ili waendeleze elimu yao, kwa hiyo nilijiunga na chuo fulani jijini na baadaye nikajiunga na Chuo Kikuu cha Taifa cha California huko Los Angeles. Nikiwa huko, nilipata marafiki ambao walikuwa wameandamana kupinga vita vya Vietnam, na vilevile wale waliopigana katika vita hivyo. Tulizungumza kwa kirefu kuhusu vita na hali za ulimwengu. Hakuna yeyote aliyekuwa na majibu yenye kuridhisha; sote tulitatanika.

Jitihada za Kusaidia Watu na Kutafuta Msaada

Kwa kweli, wengi wetu walikuwa na matatizo ya kihisia na kiakili. Nilichochewa kufanya jambo fulani ili kusaidia watu. Kwa hiyo, nikiwa kwenye chuo nilisomea mambo ambayo husababisha matatizo ya akili. Kwa kuwa nilikuwa nimejihusisha sana na vita na mauaji, niliamua kufanya kazi kama njia ya kulipia mambo niliyofanya. Kwa hiyo nilianza kufanya kazi katika hospitali ya watu wenye matatizo ya akili.

Wanafunzi wengi katika chuo kikuu walitumia dawa za kulevya, nami niliona kwamba ndizo zilikuwa kisababishi cha matatizo mengi. Nilitaka kuendeleza masomo yangu na kusaidia wale waliokuwa na matatizo ya akili hospitalini. Kwa hiyo niliacha kutumia dawa zote za kulevya na kutumia wakati na nguvu zangu kusoma na kufanya kazi. Hata hivyo, nikiwa mtaalamu wa magonjwa ya akili na kihisia, niliona wagonjwa wangu wenye matatizo ya akili wakifanya maendeleo madogo sana.

Baada ya kufadhaishwa sana na mfumo wa mambo na kusumbuliwa na dhamiri yangu, nilitafuta kitulizo. Nilianza kusali na kwenda kanisani. Sikuona misa iliyofanywa katika Kanisa Katoliki kuwa na mafundisho yanayoweza kunisaidia. Kwa hiyo nilianza kwenda kanisani usiku. Nilikuwa nikiingia kanisani, kuwasha mshumaa, na kusali mbele ya sanamu. Sanamu hizo zilitia ndani Yesu akining’inia msalabani na pia Maria akiwa na upanga kwenye moyo wake, na sanamu nyingine za “watakatifu.”

Nilianza kuwaza: ‘Kanisa ni mahali penye kushusha moyo sana. Je, kweli roho ya Mungu inaweza kuwa hapa?’ Nilihitaji majibu na kitia moyo. Nilikuwa nimeona mateso ya kutosha. Kwa hiyo usiku fulani niliondoka kanisani na kwenda kusali kwenye bustani. Niliangalia nyota na labda kwa mara ya kwanza katika maisha yangu nilijaribu kuwasiliana kwa unyoofu na Muumba wangu.

Kujifunza Kweli ya Biblia

Mwisho-juma mmoja nilienda kumtembelea Gary, rafiki yangu wa muda mrefu ili kuepa mkazo wa kazi ya hospitali. Siku moja tulitumia muda fulani kutazama televisheni sebuleni. Taarifa ya habari ilikuwa ikizungumzia jitihada za kumng’atua mamlakani Rais Nixon. Tulizungumzia ufisadi katika sehemu zote za maisha, nami nikataja kwamba nilihisi kuwa nimedanganywa kuhusiana na vita vya Vietnam.

Alva, mke wa rafiki yangu, alisikia mazungumzo hayo na akaja kutoka jikoni. Alisema kwamba mambo tuliyokuwa tukizungumzia yalikuwa yakitimiza unabii wa Biblia. “Matatizo ya rais yanahusianaje na unabii wa Biblia?” nikauliza. Alva alisema kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu mikononi mwa Yesu Kristo utachukua mahali pa serikali zote zenye ufisadi na kwamba watu wataishi milele kwa amani katika dunia itakayogeuzwa kuwa paradiso. (Danieli 2:44; Ufunuo 21:3, 4) Alva alizungumza kuhusu Sala ya Bwana, ambayo tunaomba Ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yafanywe duniani kama mbinguni.—Mathayo 6:9, 10.

Niliona kwamba kwa kweli tunahitaji mwongozo wa Mungu ili kuwa na serikali bora na amani ya kweli duniani. (Mhubiri 8:9; Yeremia 10:23) Kuhusu uwezekano wa kuishi milele, nilikumbuka kuwa nilikuwa nimejifunza kwamba atomu zinazofanyiza mwili wetu hutengenezwa upya baada ya muda mfupi sana. Ingawa mambo fulani ambayo Alva alisema yalionekana kuwa yasiyowezekana, nilikuwa na hamu ya kutaka kujua. Nilitaka kulipia madhara yote niliyokuwa nimesababisha na kusaidia kupunguza mateso ya wengine. Alva alipendekeza niende kwenye Jumba la Ufalme, ambako ningejifunza mambo mengi zaidi.

Bill Akina, alikuwa mhudumu wa wakati wote katika kutaniko. Alitumika katika jeshi la wanamaji wakati wa vita vya pili vya ulimwengu, kwa hiyo nilihisi kwamba angeweza kunielewa. Isitoshe, aliifahamu Biblia, na yeye na mke wake walitumia Biblia kujibu maswali yangu. Nilipoendelea kujifunza na Bill, ningeweza kuona kwamba ingawa nilikuwa na nia nzuri ya kuwasaidia watu waliokuwa hospitalini, ningeweza kuwapa tu kitulizo cha muda. Kwa upande mwingine, kuwasaidia watu wapate ujuzi sahihi wa Biblia kungemaanisha uzima wa milele ikiwa wangekuwa na imani na kuishi kupatana na ujuzi huo.—Yohana 17:3.

Bill alinifunza Biblia akitumia kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele. Mnamo Julai 1974, nilibatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Mungu. Miezi sita baadaye nikawa painia, kama waitwavyo waeneza-injili wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Wakati huohuo, niliacha masomo yangu kwenye chuo kikuu na nikaacha kufanya kazi kwenye hospitali. Ili kujitegemeza katika kazi ya hiyo ya kuhubiri, nilifanya kazi ya usafi na udumishaji wa benki usiku. (1 Wathesalonike 4:11) Marafiki na watu wa familia yangu walifikiri nimerukwa na akili.

Baada ya kufanya upainia huko California kwa mwaka mmoja hivi, nilianza kufikiria jinsi ninavyoweza kutumiwa zaidi katika utumishi wa Yehova. Niliamua kuweka mradi wa kutumikia katika eneo la kigeni nikiwa mishonari. Baada ya kufanya upainia kwa miaka michache, nilipokea mwaliko wa kujiunga na Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) ambayo wakati huo ilifanyiwa Brooklyn, New York. Nilikuwa katika darasa la 66 la shule hiyo na nikahitimu Machi 11, 1979, huko Long Island City, New York.

Mabadiliko ya Mgawo

Nilipewa mgawo wa kwenda Guatemala, Amerika ya Kati, ambako nilitumikia nikiwa mmishonari kwa mwaka mmoja hivi. Kisha nikaalikwa kufanya kazi ya kuchapisha katika matbaa ndogo kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika mji mkuu, Guatemala City. Mnamo 1981, nilimwoa Lupita, painia mwenyeji, naye akaalikwa kujiunga nami kwenye ofisi ya tawi. Baadaye mnamo 1996, tuliacha kuchapisha vichapo nchini Guatemala tulipoanza kupokea vichapo vyetu vyote kutoka kwenye ofisi ya tawi ya Mexico.

Binti yetu mdogo, Stephanie, alizaliwa mwaka wa 1984, hata hivyo niliendelea kutumikia kwenye ofisi ya tawi. Niliendelea kutumikia huko pia hata baada ya Lupita kujifungua Mitchell mwaka wa 1987. Haijawa rahisi kuishi mbali na ofisi ya tawi na kusafiri kila siku umbali wa kilometa kumi hivi. Lakini limekuwa pendeleo kutumikia kwenye ofisi ya tawi, na familia yangu imeniunga mkono kwa dhati.

Sasa Lupita na Stephanie ni mapainia, naye Mitchell ni mhudumu aliyebatizwa. Atamaliza masomo yake kwenye chuo cha ufundi mwaka huu, na ana mradi wa kufuatia huduma ya wakati wote. Ninajua kwamba tuna mapendeleo haya ya pekee, si kwa sababu ya vipawa vyetu, bali kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Yeye ni Mungu mwenye upendo, na atamtumia yeyote aliye na nia na anayetegemea mwongozo wake.

Nyakati nyingine sisi huulizwa tunawezaje kuwa katika huduma ya wakati wote na wakati huohuo kujitegemeza. Sisi hufanya kazi tunapokuwa likizoni. Lakini mbali na hayo, sikuzote tumejaribu kuwa na ‘jicho rahisi’ kuhusiana na vitu vya kimwili, huku tukimtegemea Yehova atusaidie, tukimtumaini, na kutafuta mwongozo wake daima.—Mathayo 6:25-34; Methali 3:5.

Kubeba bunduki kulifanya nihisi kuwa na mamlaka, kwa hiyo mimi hujaribu kusitawisha unyenyekevu daima. Mfumo wa mambo wa Shetani ulinifunza kuchukia, kuua, kushuku watu, kuwa mwenye jeuri, na mwenye kujitetea. Lakini Yehova amenionyesha rehema na fadhili zenye upendo na ninamshukuru sana kwa jambo hilo. Sasa nimeazimia kuendelea kutojifunza vita tena na kuwapenda na kuwahurumia watu wote.—Mathayo 5:43-45; Isaya 2:4.

Haijawa rahisi kufanya mabadiliko. Hata hivyo, nimejifunza kuishi maisha yenye amani zaidi. Kwa msaada wa Mungu nimefaulu pia kukabiliana na ndoto mbaya zinazosababishwa na mambo niliyojionea vitani. Ninatazamia kwa hamu wakati ambapo vita havitakuwepo. (Zaburi 46:9) Hadi wakati huo ufike, ninashukuru kwa kupata pendeleo la kutumikia katika kazi inayookoa uhai ya kusaidia watu wajifunze kumhusu Mpaji wetu mkuu wa uhai, Yehova Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nilikuwa mpiga-mizinga wa helikopta

[Picha katika ukurasa wa 14]

Nikiwa na Bill Akina na mke wake, Eloise, 1978

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiendesha mashini ya kuchapisha katika ofisi ya tawi ya Guatemala, 1982

[Picha katika ukurasa wa 15]

Leo, nikiwa na Lupita, Mitchell, na Stephanie

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikihubiri na mke wangu