Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kuepukaje Hatari za Vituo vya Maongezi vya Intaneti?

Ninaweza Kuepukaje Hatari za Vituo vya Maongezi vya Intaneti?

Vijana Huuliza . . .

Ninaweza Kuepukaje Hatari za Vituo vya Maongezi vya Intaneti?

“Nilizungumza kwenye vituo vya Intaneti kwa ukawaida kwa saa tatu au nne kwa siku. Nyakati nyingine ningezungumza kwa muda wa saa sita au saba mfululizo.”—José. *

SAWA na mahali pengine popote ambapo watu wasiojuana huchangamana, vituo vya Intaneti vya maongezi hutokeza hatari unazohitaji kujua. Kwa mfano, ikiwa ungetembelea jiji fulani, bila shaka ungejaribu kutambua maeneo hatari na kuyaepuka.

Ndivyo ilivyo unapotumia vituo vya Intaneti vya maongezi. Katika toleo la Amkeni! la Septemba 22, hatari mbili za vituo hivyo zilitajwa, yaani, uwezekano wa kukutana na watu wanaowavizia wengine kingono na kushawishiwa kuwa mdanganyi. Pia kuna hatari nyingine unazopaswa kufikiria. Lakini kwanza kabisa, vituo vya maongezi vimepangwaje?

Vimepangwa kwa Kusudi Fulani

Kwa kawaida vituo vya maongezi vimepangwa kulingana na habari itakayovutia kikundi fulani cha watu. Vingine vinaweza kupangwa kwa ajili ya mashabiki wa mchezo fulani. Huenda vingine vikawa vya kuzungumzia kipindi fulani cha televisheni. Na bado huenda vingine vikapangwa kwa ajili ya watu wanaodai kuwa wa dini fulani.

Ikiwa wewe ni Shahidi wa Yehova, huenda udadisi ukakuchochea kuzuru kituo cha maongezi kinachodai kuwa mahali ambapo vijana Mashahidi kutoka sehemu zote ulimwenguni wanaweza kupata marafiki wapya. Ni mradi unaofaa kutafuta marafiki miongoni mwa vijana walio na imani kama yako. Hata hivyo, vituo hivyo vina hatari zisizoonekana waziwazi kwa Wakristo. Hatari zipi?

Hupotoa Maadili

Kijana anayeitwa Tyler anasema, “Nilikuwa nikizungumza na watu niliodhani kwamba wote walikuwa Mashahidi wa Yehova. Lakini baada ya muda, baadhi ya watu hao walianza kukashifu imani yetu. Punde si punde, nilitambua kwamba watu hao walikuwa waasi-imani.” Watu hao walijaribu kuchambua maadili ya wale waliodai kuwa waamini wenzao.

Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, alionya kwamba baadhi ya wafuasi wake wangewapinga wenzao. (Mathayo 24:48-51; Matendo 20:29, 30) Mtume Paulo aliwaita watu hao wa wakati wake ndugu wa uwongo na kusema kwamba ‘waliingia ndani kimya-kimya’ ili kuwadhuru wale walio katika kutaniko la Kikristo. (Wagalatia 2:4) Mwandikaji wa Biblia, Yuda anasema kwamba ‘waliingia ndani kisirisiri’ wakiwa na lengo la ‘kuzigeuza fadhili zisizostahiliwa za Mungu wetu kuwa kisingizio cha mwenendo mpotovu.’ (Yuda 4) Pia anawataja kuwa kama “miamba iliyofichwa chini ya maji.”—Yuda 12.

Ona kwamba Paulo na Yuda wanataja mbinu za ujanja ambazo mara nyingi hutumiwa na waasi-imani. Waandikaji hao wa Biblia walisema kwamba waasi-imani hao ‘waliingia ndani kimya-kimya’ au ‘kuingia ndani kisirisiri’ wakiwa na lengo la kupotosha kiadili wale walio katika kutaniko la Kikristo. Leo, vituo vya maongezi huwapa watu hao waliopotoka nafasi nzuri ya kuficha hila zao. Kama miamba iliyofichwa chini ya maji, Wakristo hao wa uwongo huficha nia yao halisi kwa kujifanya kuwa wanapendezwa na vijana Mashahidi. Lakini lengo lao ni kuvunja imani ya wale wasio macho.—1 Timotheo 1:19, 20.

Gazeti hili, na pia vichapo vingine vya Mashahidi wa Yehova, vimetoa onyo mara kwa mara kuhusu hatari hiyo. * Kwa hiyo, ukizungumza na mtu yeyote katika vituo vinavyodaiwa kuwa vya Mashahidi wa Yehova, hata kama mtu huyo si mwasi-imani, anapuuza mashauri yanayotegemea Biblia. Je, kweli ungependa kufanya urafiki na watu wanaoamua kupuuza mwongozo unaotegemea Biblia?—Methali 3:5, 6; 15:5.

Mtego wa Kujitenga

Jambo jingine unalopaswa kufikiria kuhusu vituo vya maongezi ni muda ambao watu hutumia kwenye vituo hivyo. José aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, anasema: “Nyakati nyingine nilijishughulisha sana na vituo vya maongezi hivi kwamba nilisahau kula.”

Huenda usinaswe sana na vituo hivyo kama José. Hata hivyo, ili upate wakati wa kuzungumza kwenye vituo hivyo vya Intaneti, lazima ununue wakati kutoka kwenye utendaji mwingine. Utendaji ambao huenda ukaathiriwa mara moja si kazi ya shule, au kazi zako za nyumbani. Huenda mawasiliano pamoja na familia yenu ndiyo yatakayoathiriwa kwanza. Adrian anayeishi Hispania, anasema: “Baada ya chakula, ningeondoka sebuleni mara moja na kwenda kupiga gumzo kwenye Intaneti. Nilinaswa sana na vituo vya maongezi hivi kwamba nilikuwa karibu sana kuacha kuzungumza na familia yetu.”

Ikiwa unatumia wakati mwingi sana kwenye vituo vya maongezi, huenda pia ukawa unajitenga na watu walio muhimu kwako. Biblia inatoa onyo hili linalofaa: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Yaelekea watu unaokutana nao kwenye vituo vingi hawatakutia moyo uishi kupatana na hekima inayotumika ambayo inapatikana katika Biblia. Kuna uwezekano mkubwa kwamba watakutia moyo ufuatie mapendezi ya kibinafsi nao watakushawishi uache kuishi kupatana na viwango vya adili vya Kikristo.

Ni kweli kwamba huenda ukashawishiwa na vituo vya maongezi kwa kuona kuwa ni rahisi zaidi kuzungumza kwenye Intaneti kuliko kuwasiliana na familia yenu. Huenda rafiki zako kwenye vituo hivyo wakaonekana kuwa na hamu ya kusikia maoni yako kuhusu mambo mbalimbali na huenda wakajieleza waziwazi. Kwa upande mwingine, huenda familia yenu ikaonekana kuwa yenye shughuli nyingi kutoweza kusikiliza mahangaiko yako na huenda isijieleze waziwazi.

Hata hivyo, jiulize hivi: ‘Je, kweli rafiki zangu kwenye Intaneti wanajua mimi ni mtu wa aina gani? Je, kweli wanapendezwa na hali yangu njema ya siku zijazo?’ Yaelekea washiriki wa familia yenu watahangaikia zaidi afya yako ya kihisia-moyo na ya kiroho. Ikiwa wazazi wako wanajitahidi kuishi kupatana na viwango vya Biblia, wanapendezwa kikweli kuwasiliana nawe. (Waefeso 6:4) Ukiwaeleza hisia zako kwa heshima, huenda ukashangaa kuona jinsi watakavyoitikia kwa fadhili.—Luka 11:11-13.

Kuepuka Hatari

Huenda ukawa na sababu nzuri za kutembelea vituo vya maongezi—kwa mfano, labda umepewa mradi fulani wa shule. * Ikiwa ndivyo, unaweza kuepuka hatari kwenye vituo hivyo kwa kufuata tahadhari rahisi zifuatazo.

Kwanza, epuka kutumia kompyuta iliyounganishwa na Intaneti kwenye chumba chako. Kufanya hivyo ni sawa na kuranda-randa kwenye barabara yenye giza katika jiji usilolifahamu, utakuwa unajitafutia matatizo. Badala yake, weka kompyuta hiyo mahali palipo wazi ambapo wengine wanaweza kuona unapoitumia.

Pili, jitahidi kuwa na mawasiliano mazuri na wazazi wako kwa kuwaonyesha vituo unavyotembelea na kuwaeleza sababu inayofanya utembelee kituo fulani hususa. Pia, jiwekee muda utakaotumia kwenye kompyuta, kisha uufuate.

Tatu, weka programu za kompyuta zitakazokulinda usishambuliwe kingono kwa kuchuja ujumbe unaotumiwa. Ukianza kushawishiwa kuhusu mambo ya ngono kwenye Intaneti, wajulishe wazazi au mwalimu wako mara moja. Katika nchi fulani watu wazima wanaojua kwamba wewe ni kijana na bado wanakutumia ujumbe wa kukushawishi kingono au kukutumia habari nyingine chafu wanavunja sheria. Wanapaswa kuripotiwa kwa polisi.

Isitoshe, usitoe jina lako, anwani, jina la shule yako, au namba yako ya simu kwa mtu unayekutana naye kwenye vituo vya maongezi. Na usikubali kamwe kukutana uso kwa uso na mtu uliyezungumza naye kwenye kituo cha Intaneti.

Ingawa yaliandikwa maelfu ya miaka iliyopita, maneno haya ya Mfalme Sulemani mwenye hekima yanahusu hatari zinazotokana na vituo vya maongezi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.”—Methali 22:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina fulani yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kwa hekima, waonyeshe wazazi wako vituo unavyotembelea