Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msaada kwa Mzazi Asiye na Mwenzi wa Ndoa

Msaada kwa Mzazi Asiye na Mwenzi wa Ndoa

Msaada kwa Mzazi Asiye na Mwenzi wa Ndoa

“Watoto wangu wanaporudi nyumbani na kunikumbatia na kuniambia kwamba wananipenda ndipo ninapofurahi sana kuwa na watoto.”DORIS, MAMA ASIYE NA MUME, MWENYE WATOTO WAWILI.

WAZAZI wasio na wenzi wa ndoa wanaweza kutiwa moyo wanaposoma maneno haya katika Biblia: “Watoto ni baraka na zawadi kutoka kwa BWANA.” (Zaburi 127:3, Contemporary English Version) Mungu huwapenda watoto wanaolelewa na mzazi mmoja kama anavyowapenda watoto wengine. Muumba wetu anataka familia za mzazi mmoja zifaulu. Biblia inasema hivi kumhusu: “Huwategemeza yatima na mjane.” (Zaburi 146:9) Wazazi wasio na wenzi wa ndoa wanaweza kuwa na hakika kwamba Mungu yu tayari kuwasaidia.

Mtoto ana haki ya kulelewa katika familia yenye upendo na amani ili aweze kukomaa kimwili, kihisia, na kiroho. Ni daraka na pendeleo la kila mzazi kutumiwa na Mungu kumzoeza mtoto.

Wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa wameona kwamba ni muhimu kutoa sala za moyoni, kufuata kanuni za Biblia bila kigeugeu, na kumtumaini Yehova kabisa. Jambo hilo linalingana na himizo linalopatikana katika Zaburi 55:22: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza.”

Mara kwa mara, nyanya na babu, wazee wa kutaniko, na wazazi katika kutaniko la Kikristo, ambao wamefaulu kulea watoto, huenda wakaweza kusaidia familia yenye mzazi mmoja kushinda magumu. Ni kweli kwamba watu wa ukoo na waabudu wenzi wanaweza kuwasaidia sana wazazi wasio na wenzi wa ndoa, lakini Mungu amempa mzazi daraka la kumlea mtoto. *

Jambo la kufurahisha ni kwamba wazazi wengi wasio na wenzi wa ndoa wamefaulu kushinda magumu na kulea watoto wenye kutegemeka, wenye mwenendo mzuri, na wenye kumcha Mungu. Mwandishi wa Amkeni! aliwahoji baadhi yao. Mambo kadhaa ambayo wazazi hao walitaja yameorodheshwa hapa chini.

Kupanga kazi za nyumbani vizuri. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu hujitahidi kupanga kazi za nyumbani na shughuli mbalimbali vizuri. Kupanga mambo vizuri na kufanya mambo kwa utaratibu ni muhimu sana. Biblia inasema hivi: “Mawazo ya wenye bidii huuelekea utajiri tu.”—Mithali 21:5.

Kuwajibika kutunza familia. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu wanaona familia zao kuwa muhimu sana. Wao hutanguliza mahitaji ya watoto wao wala si mahitaji yao wenyewe.—1 Timotheo 5:8.

Kuwa na kiasi ni muhimu. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu hawapuuzi matatizo wala hawayatii chumvi; wao hutafuta suluhisho. Wao hutambua magumu na kuyashughulikia bila kujihurumia wala kuhisi uchungu.

Mawasiliano mazuri. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu hujitahidi kuwa na mawasiliano mazuri. Wao huwatia moyo watoto waeleze waziwazi mawazo na hisia zao bila kuficha. Baba mmoja asiye na mke anasema hivi kuwahusu watoto wake: “Ninaongea nao kila ninapopata nafasi. Tunafurahia kuwa pamoja tunapotayarisha chakula cha jioni. Ndipo wanaponieleza mambo yaliyomo mioyoni mwao.”

Kujitunza. Ijapokuwa wana shughuli nyingi mno, wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu, hutambua kwamba ni lazima wajitunze wenyewe pia kiroho, kihisia, na kiafya. Ethel, mama aliyetalikiwa mwenye watoto wawili, alieleza hivi: “Ninajaribu kuweka kando wakati kwa ajili yangu mwenyewe. Kwa mfano, wakati rafiki yangu mmoja anapowafundisha watoto kucheza ala fulani ya muziki, ninapata saa moja ya kupumzika. Wakati huo mimi huketi chini bila kuwasha televisheni.”

Maoni yanayofaa. Wazazi wasio na wenzi wa ndoa ambao wamefaulu wana maoni yanayofaa kuhusu daraka lao na juu ya maisha kwa ujumla. Wao huona kwamba katika hali ngumu kunaweza kuwa na faida fulani. Mama mmoja asiye na mume anasema hivi: “Mimi nimegundua kwamba kulea watoto wangu nikiwa peke yangu kunaweza kufurahisha pia.”

Wale Waliofaulu

Je, kanuni zilizotajwa juu, zinafanya kazi? Naam, kama tunavyoweza kuona kutokana na masimulizi mengi kuwahusu wazazi ambao wamefaulu kulea watoto wao wakiwa peke yao. Gloria, mama aliyetalikiwa, ambaye alitajwa katika makala ya kwanza, anafanya kazi ya kuajiriwa huko Uingereza na alilea wana wawili na binti mmoja akiwa peke yake. Wote watatu wakawa wahudumu Wakristo wa wakati wote, ambao hutumia maisha yao kufundisha Biblia. Alipoulizwa jinsi alivyofaulu, Gloria alieleza hivi: “Jambo gumu hasa lilikuwa kuongoza funzo la Biblia lenye kupendeza kwa ukawaida. Nilitaka watoto wawe wenye furaha, wawe na amani akilini, waridhike, na kulindwa na mitego. Nilipata kazi ya usiku. Nilitaka kuwa pamoja na watoto kila nilipoweza. Kabla ya kwenda kazini, tulitoa sala pamoja, kisha nikawalaza. Nilipokuwa kazini mama yangu mdogo alilinda nyumba.

Gloria aliwasaidiaje watoto wake kutanguliza mambo muhimu maishani? Aongeza: “Lengo langu kuu lilikuwa kutanguliza mambo ya kiroho. Hatukuwa na fedha nyingi, na sikuficha jambo hilo kwa watoto. Kila jambo ambalo niliwaomba wafanye, nilikuwa tayari kulifanya mwenyewe pia, na wote walikuwa tayari kusaidia.” Akikumbuka jinsi alivyodumisha uhusiano mzuri pamoja na watoto wake, Gloria anasema hivi: “Nilifaulu kwa sababu tulifanya mambo pamoja. Hakuna aliyejitenga katika chumba chake. Tulipika pamoja, na tulisafisha na kupamba nyumba pamoja. Tulifanya kila kitu kwa kiasi. Sikuzote nilihakikisha kwamba tulipata nafasi ya kujiburudisha pia.”

Carolyn, mama asiye na mume mwenye mwana mdogo anayeitwa Joseph, anafurahia kuona maendeleo yake. Nini kinachomsaidia kufaulu? “Sisi husoma Biblia kabla ya kulala,” anasema, “baadaye mimi humwuliza maswali kuhusu yale aliyojifunza. Isitoshe, sisi huchunguza mafungu fulani katika vichapo vya Biblia na kuona jinsi tunavyoweza kutumia mambo hayo katika maisha yetu. Jambo hilo humsaidia Joseph anapokabili matatizo, kama vile kuchokozwa shuleni.” Carolyn anakubali kwamba maisha yake si rahisi, lakini hajihisi mpweke. Anasema hivi: “Nahitaji kujikakamua, lakini nahisi kwamba Yehova amenisaidia sana. Mimi hutiwa moyo pia katika kutaniko la Kikristo.”

Masimulizi ya maelfu ya mama wasio na waume kama vile Gloria na Carolyn, yanaonyesha kwamba kanuni za Biblia zinategemeka. Tangu zamani kanuni hizo zimewasaidia wazazi kulea watoto wenye sifa nzuri na wenye nguvu kiroho. (Mithali 22:6) Inawezekana kufaulu! Mzazi asiye na mwenzi wa ndoa anapatwa na magumu mengi yanayompa fursa za kufanya maendeleo na kuwasaidia wengine. Kumtegemea Mungu kikamili na kutumaini msaada wake ni njia bora ya kushinda magumu yanayowakabili wazazi wasio na wenzi wa ndoa.—Zaburi 121:1-3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Habari zaidi kuhusu jinsi familia za mzazi mmoja zinavyoweza kufaulu zinapatikana katika kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, sura ya 9, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Funzo la Biblia la familia limewasaidia watoto watatu wa Gloria kuwa wahudumu Wakristo wa wakati wote. Wanatazama barua na picha iliyotumwa na mwana wake mkubwa, ambaye ni mishonari

[Picha katika ukurasa wa 12]

Carolyn na mwana wake, Joseph