Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuna Sababu ya Kuwa na Tumaini?

Je, Kuna Sababu ya Kuwa na Tumaini?

Je, Kuna Sababu ya Kuwa na Tumaini?

“Tatizo moja katika ndoa zenye matatizo makubwa ni kushikilia sana wazo la kwamba hali haiwezi kuwa bora. Wazo hilo ni kipingamizi kwa sababu huzuia jitihada yoyote yenye kujenga.”—DAKT. AARON T. BECK.

HEBU jiwazie ukiwa na maumivu na umeenda kwa daktari ili uchunguzwe. Una wasiwasi—na kwa sababu nzuri. Kwani, afya yako—hata uhai wako—huenda ukawa hatarini. Tuseme kwamba baada ya uchunguzi, daktari akupa habari njema kwamba ijapokuwa hali yako ni mbaya, yaweza kutibiwa. Kwa kweli, daktari akujulisha kwamba iwapo utashikamana na utaratibu unaofaa wa mlo na mazoezi, unaweza kutazamia kupona. Kwa hakika utahisi umetulizwa sana na utafurahia kufuata ushauri wake!

Linganisha hali hiyo na habari tunayozungumzia hapa. Je, ndoa yako ina matatizo makubwa? Bila shaka, kila ndoa hupatwa na matatizo na kutoafikiana. Kwa hivyo, kuwa na pindi yenye mkazo katika uhusiano wenu hakumaanishi kuwa ndoa yenu haina upendo. Lakini vipi hali hiyo ikiendelea kwa majuma, miezi, au hata miaka? Ikiwa ndivyo, una sababu ya kuhangaika, kwa kuwa hilo si jambo dogo. Kwa kweli hali ya maisha ya ndoa yaweza kuathiri kila sehemu ya maisha yako—na ya watoto wako. Kwa mfano, inaaminika kwamba matatizo ya ndoa yaweza kuchangia sana matatizo kama vile kushuka-moyo, uzembe kazini, na watoto kufeli mitihani shuleni. Na kuna mengi zaidi. Wakristo hutambua kwamba uhusiano wao na wenzi wao wa ndoa waweza kuathiri uhusiano wao na Mungu.—1 Petro 3:7.

Uhakika wa kuwa kuna matatizo katika ndoa yenu haimaanishi hakuna tumaini. Kukabili mambo hakika kuhusu maisha ya ndoa—kwamba kutakuwa na magumu—kwaweza kusaidia wenzi wa ndoa kuona mambo kihalisi na kutafuta suluhisho. Mume anayeitwa Isaac asema hivi: “Sikujua kwamba kwa kawaida kiwango cha furaha katika maisha ya ndoa hupanda na kushuka. Nilifikiri sisi tuna kasoro fulani!”

Hata ikiwa ndoa yako imefikia hatua ya kukosa upendo, inaweza kuokolewa. Ni kweli kwamba athari za kihisia-moyo zenye kusababishwa na uhusiano wenye matatizo zaweza kuwa mbaya sana, hasa ikiwa matatizo yameendelea kwa miaka mingi. Licha ya hilo, kuna sababu yenye nguvu ya kuwa na tumaini. Nia ni ya maana sana. Hata watu wawili walio katika ndoa yenye matatizo makubwa waweza kuboresha hali iwapo wanathamini uhusiano wao. *

Kwa hivyo jiulize, ‘Tamaa yangu ya kuwa na uhusiano wenye kuridhisha ina nguvu kadiri gani?’ Je, wewe na mwenzi wako mko tayari kujitahidi kuboresha ndoa yenu? Dakt. Beck, aliyenukuliwa awali, asema hivi: “Nimeshangaa mara nyingi ninapoona uhusiano unaoonekana kuwa mbaya ukibadilika wenzi wanapojitahidi kufanyia kazi udhaifu wao na kuimarisha sifa nzuri za ndoa yao.” Lakini vipi ikiwa mwenzi wako hakuungi mkono kuiboresha ndoa yenu? Au vipi ikiwa mwenzi wako anaonekana hang’amui kwamba kuna tatizo? Je, juhudi yako binafsi ya kuboresha hali itaambulia patupu? La, hasha! “Ukifanya mabadiliko fulani,” asema Dakt. Beck, “hilo laweza kumchochea mwenzi wako kufanya mabadiliko—na huwa hivyo mara nyingi.”

Usikate kauli upesi kwamba hilo haliwezekani katika ndoa yako. Maoni yasiyofaa kama hayo huenda yakawa ndiyo tisho kubwa zaidi kwa ndoa yako! Mmoja wenu hana budi kuchukua hatua ya kwanza. Je, inaweza kuwa wewe? Ukiimarisha juhudi zako, huenda mwenzi wako akaona umuhimu wa kukuunga mkono ili kuifanya ndoa yenu iwe na furaha.

Hivyo basi, unaweza kufanya nini—ukiwa peke yako au mkiwa nyote wawili—ili kuokoa ndoa yenu? Biblia inasaidia sana kujibu swali hilo. Acheni tuone inavyofanya hivyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ingawa hivyo, katika visa fulani vibaya zaidi, huenda kukawa na sababu halali za kumfanya mume na mke waachane. (1 Wakorintho 7:10, 11) Isitoshe, Biblia inaruhusu talaka kwa msingi wa uasherati. (Mathayo 19:9) Kumtaliki au kutomtaliki mwenzi asiye mwaminifu ni uamuzi wa kibinafsi, na wengine hawapaswi kumlazimisha mwenzi asiye na hatia kufanya uamuzi wowote.—Ona kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, ukurasa 158-161, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.