Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wapata Somo Kutoka kwa Simulizi la Loida

Wapata Somo Kutoka kwa Simulizi la Loida

Wapata Somo Kutoka kwa Simulizi la Loida

MAKALA “Loida Aacha Kukimya” (Mei 8, 2000) iliwachochea wasomaji wetu wengi kutuandikia. Mioyo ya wengi iliguswa sana na simulizi hilo la kweli kuhusu msichana mchanga mwenye ugonjwa wa kupooza ubongo ambaye hangeweza kuwasiliana hadi alipokuwa na umri wa miaka 18. Yafuatayo ni baadhi ya maelezo tuliyopokea.

“Nililia sana niliposoma ujumbe wa Loida kwa familia yake alipoweza kuwasiliana hatimaye. Nitajitahidi sana kuiga ujasiri na uthabiti aliokuwa nao licha ya hali zake ngumu.”—K. G.

“Nina afya bora kabisa, lakini nyakati nyingine mimi hujikuta nikilalamika kuhusu mambo fulani-fulani. Baada ya kusoma kuhusu Loida, nilisali kwa Yehova, nikimwomba msamaha kwa sababu ya kukosa kuthamini vitu nilivyo navyo.”—R. H.

“Mnamo mwaka wa 1980 ndugu yangu mdogo alizaliwa akiwa na matatizo mengi ya kiafya, kutia ndani kupooza kwa ubongo, naye hawezi kuongea. Simulizi hilo lilitia familia yangu moyo kutokata tamaa, hata hali ziwe ngumu namna gani.”—L. W.

“Mimi ni msichana mwenye umri wa miaka 14, nilifikiri daima kwamba ni mimi tu niliye na matatizo. Ningependa kumwona Loida akiwa na afya njema na kuongea naye katika Paradiso. Yeye ni mmojawapo wa watu walio katika orodha yangu ya watu ninaopanga kukutana nao na kuwa marafiki milele.”—R. K.

“Makala hiyo ilinigusa moyo. Nimelazimika kuvumilia magonjwa mbalimbali ya kiakili na ya kihisia-moyo. Kusoma kuhusu namna ambavyo Loida anatazamia sana ulimwengu mpya wa Mungu hunifanya nitamani hata zaidi kuwa katika ulimwengu huo.”—P. B.

“Mimi pia nina ugonjwa wa kupooza ubongo, lakini sina tatizo la kuongea. Makala hiyo hunisaidia nitambue kwamba Yehova anaona yote yanayotupata na anathamini kila mmoja wetu kwa sababu ya yale ambayo kila mmoja anaweza kufanya katika kumtumikia.”—D. J.

“Lililonigusa zaidi ni kusoma namna Loida alivyoweka wakfu maisha yake kwa Yehova akiwa na umri mdogo na namna anavyoshiriki pia kazi ya kuhubiri. Wale kati yetu walio na afya bora zaidi waweza kujifunza somo kutokana na Loida kwa njia nyingi.”—A. R.

“Simulizi la Loida limenifanya nijitahidi kuwafikiria wengine zaidi na kile ninachoweza kuwafanyia. Sitaki kabisa kupuuza pendeleo langu la kuweza kuongea na wengine kumhusu Yehova Mungu.”—B. M.

“Ni makala ya pekee kama nini! Twafahamu wenzi wawili katika kutaniko jirani walio na binti mwenye ugonjwa wa kupooza ubongo. Nitawatumia kadi leo na kuwaeleza kwamba ninawathamini kwelikweli na yote wanayomfanyia binti yao.”—T. G.

“Ninaposhuka moyo, nyakati nyingine mimi huwa na ubinafsi, lakini Loida anapendezwa kipekee na wengine. Najitahidi kufanya hivyohivyo. Nahitaji pia kujitahidi kumwiga Loida na kusali kwa Yehova ninapohisi nimelemewa.”—N. D.

“Nina umri wa miaka 14, nami nina ugonjwa wa pumu. Nyakati nyingine mimi hudhani kwamba ugonjwa wangu ni mbaya kuliko magonjwa yote, lakini niliposoma simulizi hilo, nilijifunza kwamba sivyo ilivyo. Asanteni kwa ajili ya simulizi hilo lenye kuhuzunisha na lenye kufurahisha pia ambalo hutupa tumaini.”—M. C.