Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, kazi ya kuhubiri inayofanywa sasa itafikia mwisho lini?

Yesu alisema hivi: “Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mwisho” katika mstari huu na mstari wa 6 na 13, ni teʹlos. Neno hilo linarejelea mwisho kabisa wa ulimwengu wa Shetani katika vita vya Har–​Magedoni. (Ufu. 16:​14, 16) Hivyo, tutaendelea kuhubiri habari njema hadi kabla tu ya mwisho huo. Hilo linarekebisha uelewaji wetu wa awali.

Zamani, tulielewa kwamba tutaacha kuhubiri habari njema dhiki kuu itakapoanza kwa kuharibiwa kwa Babiloni Mkubwa. (Ufu. 17:​3, 5, 15, 16) Tuliamini kwamba, tukio hilo lingeashiria mwisho wa “mwaka [wa mfano] wa nia njema ya Yehova.” (Isa. 61:2) Tulifikiri pia kwamba wale ambao wangeokoka dhiki kuu, ni wale ambao wangethibitisha uaminifu wao kwa Yehova kabla ya tukio hilo. Tuliwalinganisha watu hao na Wayahudi waliookoka uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Watu hao walikuwa wametiwa alama ya kuokoka mapema kwa sababu walimwabudu Yehova na walichukia uovu. (Eze. 5:11; 9:4) Hata hivyo, ulinganisho huo haupatani na maneno ya Yesu yanayopatikana katika Mathayo 24:​14, yanayoonyesha kwamba huenda watu watakuwa na nafasi ya kukubali habari njema hadi kabla tu ya mwisho kabisa kwenye vita vya Har–​Magedoni.

Uelewaji wetu uliorekebishwa wa Mathayo 24:14 unarekebisha pia uelewaji wetu wa ujumbe unaofananishwa na mvua ya mawe uliotabiriwa katika Ufunuo 16:21. Uchunguzi zaidi umeonyesha kwamba maandiko hayo mawili yanapatana. Jinsi gani? Tunapata jibu la swali hilo kupitia jinsi watu wanavyoitikia ujumbe wa Ufalme. Mtume Paulo aliandika kwamba kwa “wale wanaookolewa,” ujumbe huo ni habari njema, yaani, “harufu ya uzima.” Lakini kwa maadui wa Mungu ni habari mbaya, yaani, “harufu ya kifo.” (2 Kor. 2:​15, 16) Wanachukia ujumbe wa Ufalme kwa sababu unafunua ukweli kuhusu ulimwengu wao—kwamba ni mwovu, unatawaliwa na Shetani, na hivi karibuni utaharibiwa.—Yoh. 7:7; 1 Yoh. 2:17; 5:19.

Ona pia kwamba mvua hiyo ya mawe ya mfano itakuwa “kubwa mno.” Hilo linadokeza kwamba wakati wa dhiki kuu, huenda ujumbe wetu wakati huo ukawa mkali au mzito zaidi, yaani, jina la Yehova litajulikana zaidi kuliko wakati mwingine wowote. (Eze. 39:7) Wakati huo, baada ya uharibifu wa Babiloni Mkubwa, je, baadhi ya watu watavutiwa na ujumbe huo, kama mtu anavyovutiwa na harufu tamu? Hilo linawezekana. Huenda wakakumbuka au kujifunza kwamba kwa miaka mingi Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakitangaza kuhusu mwisho wa dini za uwongo.

Kwa kulinganisha, fikiria kilichotokea katika Misri ya kale baada ya yale Mapigo Kumi. Baada ya Yehova “[kutekeleza] hukumu dhidi ya miungu yote ya Misri,” “kundi kubwa lenye mchanganyiko” wa watu wasio Waisraeli, lilijiunga na watu wake. (Kut. 12:​12, 37, 38) Huenda wageni hao waliamua kwenda na watu wa Yehova baada ya kuona yale Mapigo Kumi ambayo Musa aliwaonya kuhusu yakitimia.

Yeyote atakayeamua kujiunga na watu wa Yehova baada ya uharibifu wa Babiloni Mkubwa, atakuwa na pendeleo la kuwatendea mema ndugu za Kristo ambao bado watakuwa duniani. (Mt. 25:​34-36, 40) Bila shaka, fursa hiyo ya kuhukumiwa kuwa kondoo itaisha muda mfupi kabla ya vita vya Har–​Magedoni, wakati watiwa-mafuta watakapopokea thawabu yao ya mbinguni.

Uelewaji huu uliorekebishwa unaonyesha kwa njia kubwa upendo na rehema nyingi ambazo Yehova anazo. Naam, “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Pet. 3:9.