Marko 4:1-41

4  Naye akaanza tena kufundisha kando ya bahari.+ Na umati mkubwa sana ukakusanyika karibu naye, hivi kwamba akapanda ndani ya mashua akaketi baharini, lakini umati wote kando ya bahari ulikuwa pwani.+  Kwa hiyo akaanza kuwafundisha mambo mengi kwa mifano+ na kuwaambia katika kufundisha kwake:+  “Sikilizeni. Tazama! Mpandaji alienda kupanda.+  Naye alipokuwa akipanda, mbegu fulani zikaanguka kando ya barabara, na ndege wakaja wakazila.+  Na mbegu nyingine zikaanguka mahali penye miamba ambapo, bila shaka, hapakuwa na udongo mwingi, nazo zikachipuka mara moja kwa sababu ya kutokuwa na udongo wenye kina.+  Lakini jua lilipochomoza, zikaungua, na kwa sababu hazikuwa na mzizi zikanyauka.+  Na mbegu nyingine zikaanguka katikati ya miiba, na ile miiba ikamea na kuzisonga, nazo hazikuzaa tunda lolote.+  Lakini nyingine zikaanguka kwenye udongo mzuri,+ nazo zikamea na kuongezeka, zikaanza kuzaa matunda, nazo zilikuwa zikizaa matunda 30, na 60 na 100.”+  Kwa hiyo akaongeza neno hili: “Yule aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”+ 10  Basi alipokuwa peke yake, wale waliomzunguka pamoja na wale kumi na wawili wakaanza kumuuliza juu ya mifano hiyo.+ 11  Naye akaanza kuwaambia: “Ninyi mmepewa siri takatifu+ ya ufalme wa Mungu, lakini kwa wale walio nje mambo yote yanatukia kwa mifano,+ 12  ili, ingawa wanatazama, watazame na bado wasione, na, ingawa wanasikia, wasikie na bado wasielewe, wala wasigeuke kamwe na kusamehewa.”+ 13  Tena akawaambia: “Hamjui mfano huo, kwa hiyo basi mtaelewa namna gani mifano mingine yote? 14  “Mpandaji hulipanda neno.+ 15  Basi, hawa ndio wale walio kando ya barabara ambapo lile neno limepandwa, lakini mara tu baada ya kulisikia Shetani huja+ na kuliondoa neno lililopandwa ndani yao.+ 16  Vivyo hivyo hawa ndio wale waliopandwa mahali penye miamba: mara tu baada ya kulisikia neno, wanalipokea kwa shangwe.+ 17  Lakini hawana mzizi ndani yao wenyewe, bali wao huendelea kuwako kwa wakati fulani; kisha mara tu dhiki au mateso yanapotokea kwa sababu ya lile neno, wao hukwazika.+ 18  Bado kuna wengine wanaopandwa katikati ya miiba; hawa ndio ambao wamelisikia neno,+ 19  lakini mahangaiko+ ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri+ na tamaa+ za mambo yale mengine hupenya na kulisonga neno, nalo hukosa kuzaa matunda.+ 20  Mwishowe, wale waliopandwa kwenye udongo mzuri ndio wale wanaolisikiliza neno na kulipokea vizuri na kuzaa matunda mara 30 na 60 na 100.”+ 21  Naye akaendelea kuwaambia: “Je, taa huletwa ili kuwekwa chini ya kikapu cha kupimia au chini ya kitanda? Je, hailetwi ili kuwekwa juu ya kinara cha taa?+ 22  Kwa maana hakuna jambo lililofichwa ila kwa kusudi la kupata kufunuliwa; hakuna lililositiriwa kwa uangalifu ila kwa kusudi la kuja kutokea wazi.+ 23  Yeyote aliye na masikio ya kusikiliza, na asikilize.”+ 24  Tena akawaambia: “Sikilizeni kwa makini mambo ambayo mnasikia.+ Kwa kipimo mnachopimia, mtapimiwa hicho,+ ndiyo, mtaongezewa zaidi.+ 25  Kwa maana aliye na kitu ataongezewa; lakini yule ambaye hana kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.”+ 26  Kwa hiyo akaendelea kusema: “Katika njia hii ufalme wa Mungu ni kama vile mtu anapotupa mbegu kwenye udongo,+ 27  naye hulala usingizi usiku na huamka mchana, na ile mbegu huota na hukua na kuwa ndefu, naye hajui ni jinsi gani hasa.+ 28  Udongo wenyewe hutokeza matunda hatua kwa hatua, kwanza jani, kisha suke, mwishowe nafaka iliyo kamili katika suke. 29  Lakini mara tu matunda yanaporuhusu, yeye huutia mundu, kwa sababu wakati wa mavuno umefika.” 30  Naye akaendelea kusema: “Tutaufananisha ufalme wa Mungu na nini, au tutauweka katika mfano gani?+ 31  Kama mbegu ya haradali, ambayo ilipopandwa katika udongo ilikuwa ndiyo mbegu ndogo zaidi kuliko zote duniani+​— 32  lakini baada ya kupandwa, humea na kuwa kubwa zaidi kuliko mboga nyingine zote na hutokeza matawi makubwa,+ hivi kwamba ndege wa mbinguni+ wanaweza kupata makao chini ya kivuli chake.”+ 33  Kwa hiyo alikuwa akisema nao lile neno kwa mifano+ mingi ya namna hiyo, kwa kadiri walivyoweza kusikiliza. 34  Kwa kweli, hakuwa akisema nao bila mfano, lakini kwa faragha alikuwa akiwaeleza wanafunzi wake mambo yote.+ 35  Na siku hiyo, ilipokuwa jioni, akawaambia: “Na tuvuke mpaka ukingo ule mwingine wa bahari.”+ 36  Kwa hiyo, walipokuwa wamekwisha kuuruhusu umati uondoke, wakamchukua katika mashua, kama vile alivyokuwa, na kulikuwa na mashua nyinginezo pamoja naye.+ 37  Sasa kukatokea dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi, na mawimbi yakawa yakiipiga mashua kwa nguvu, hivi kwamba karibu mashua ifunikwe na maji.+ 38  Lakini yeye alikuwa katika tezi, akiwa amelalia mto. Kwa hiyo wakamwamsha na kumwambia: “Mwalimu, je, hujali kwamba tuko karibu kuangamia?”+ 39  Ndipo akaamka, akaukemea upepo na kuiambia bahari: “Nyamaza, utulie!”+ Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.+ 40  Kwa hiyo akawaambia: “Kwa nini mna moyo wa woga? Je, bado hamna imani yoyote?” 41  Lakini wakaogopa isivyo kawaida, nao wakawa wakiambiana: “Kwa kweli huyu ni nani, kwa sababu hata upepo na bahari zinamtii?”+

Maelezo ya Chini