Luka 16:1-31

16  Ndipo akaendelea kuwaambia wanafunzi pia: “Mtu fulani alikuwa tajiri naye alikuwa na msimamizi-nyumba,+ na huyo akashtakiwa kwake kuwa anapoteza mali zake.+  Kwa hiyo akamwita na kumwambia, ‘Ni nini hili ninalosikia juu yako? Toa hesabu+ ya usimamizi wako, kwa maana huwezi tena kuisimamia nyumba.’  Ndipo huyo msimamizi akasema moyoni mwake, ‘Nitafanya nini, kwa kuwa bwana+ wangu atauondolea mbali usimamizi wangu? Sina nguvu za kutosha kulima, ninaona aibu kuombaomba.  Ah! Najua nitakalofanya, ili, nitakapoondolewa kwenye usimamizi, watu wanipokee nyumbani mwao.’+  Naye akaita kila mmoja wa wale wenye deni la bwana wake, akamwambia wa kwanza, ‘Unadaiwa kiasi gani na bwana wangu?’  Akasema, ‘Vipimo 100 vya bathi vya mafuta ya zeituni.’ Akamwambia, ‘Chukua hati yako ya mapatano, uketi uandike upesi 50.’  Halafu, akamwambia mwingine, ‘Na wewe, unadaiwa kiasi gani?’ Akasema, ‘Vipimo 100 vya kori vya ngano.’ Akamwambia, ‘Chukua hati yako ya mapatano uandike 80.’  Na bwana wake akamsifu yule msimamizi, kwa sababu alikuwa ametenda kwa hekima inayotumika,+ ingawa si mwadilifu; kwa maana wana wa mfumo huu wa mambo wana hekima zaidi kwa njia inayotumika kuelekea kizazi chao wenyewe kuliko vile walivyo wana wa nuru.+  “Pia, ninawaambia ninyi, Jifanyieni rafiki+ kupitia mali+ zisizo za uadilifu, ili, zitakapopunguka wawapokee ninyi katika makao ya milele.+ 10  Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo zaidi ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu ambaye si mwaminifu katika lililo dogo zaidi si mwaminifu katika lililo kubwa pia.+ 11  Kwa hiyo, ikiwa ninyi hamjajionyesha wenyewe kuwa waaminifu kuhusiana na mali zisizo za uadilifu, ni nani atakayewakabidhi ninyi kilicho cha kweli?+ 12  Na ikiwa ninyi hamjajionyesha wenyewe kuwa waaminifu kuhusiana na kilicho cha mwingine,+ ni nani atakayewapa ninyi kilicho chenu wenyewe? 13  Hakuna mtumishi wa nyumbani anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana, ama atamchukia mmoja na kumpenda mwingine, au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kuwa watumwa wa Mungu na wa Mali.”+ 14  Sasa Mafarisayo, waliokuwa wapenda-pesa, walikuwa wakisikiliza mambo yote hayo, nao wakaanza kumcheka kwa dharau.+ 15  Kwa hiyo akawaambia: “Ninyi ni wale mnaojitangaza kuwa waadilifu mbele ya macho ya wanadamu,+ lakini Mungu anaijua mioyo+ yenu; kwa sababu kilichoinuka sana kati ya wanadamu ni chukizo machoni pa Mungu.+ 16  “Sheria na Manabii walikuwa mpaka Yohana.+ Tangu wakati huo na kuendelea ufalme wa Mungu unatangazwa kuwa habari njema, na kila namna ya mtu anajitahidi kuufikia.+ 17  Kwa kweli, ni rahisi zaidi mbingu na dunia kupitilia mbali+ kuliko nukta+ moja ya herufi ya Sheria kupita bila kutimizwa.+ 18  “Kila mtu anayemtaliki mke wake na kuoa mwingine anafanya uzinzi, naye anayemwoa mwanamke aliyetalikiwa kutoka kwa mume anafanya uzinzi.+ 19  “Lakini mtu+ fulani alikuwa tajiri, naye alikuwa akijipamba kwa mavazi ya zambarau na kitani, akijifurahisha siku baada ya siku kwa fahari.+ 20  Lakini mwombaji fulani aliyeitwa Lazaro alikuwa akiwekwa kwenye lango lake, akiwa amejaa vidonda 21  naye alikuwa akitamani kujishibisha kwa vitu vilivyokuwa vikianguka kutoka kwenye meza ya yule tajiri. Ndiyo, pia, mbwa walikuwa wakija na kuviramba vidonda vyake. 22  Baadaye yule mwombaji akafa+ naye akachukuliwa na malaika mpaka kifuani+ pa Abrahamu.+ “Pia, yule tajiri akafa+ na kuzikwa. 23  Na katika Kaburi* akayainua macho yake, akiteswa sana,+ naye akamwona Abrahamu kwa mbali na Lazaro akiwa kifuani pamoja naye. 24  Kwa hiyo akaita na kusema, ‘Baba Abrahamu,+ nihurumie, umtume Lazaro achovye ncha ya kidole chake katika maji aupoze ulimi wangu,+ kwa sababu nimo katika maumivu makali katika moto huu unaowaka vikali.’+ 25  Lakini Abrahamu akasema, ‘Mwanangu, kumbuka kwamba ulipokea kwa ukamili vitu vyako vyema katika maisha yako, lakini Lazaro alipokea mabaya. Hata hivyo, sasa anapata faraja hapa lakini wewe umo katika maumivu makali.+ 26  Na mbali na mambo yote haya, shimo+ kubwa limewekwa kati yetu na ninyi,+ hivi kwamba wale wanaotaka kuvuka kutoka hapa kuja kwenu hawawezi, wala watu hawawezi kuvuka kutoka huko kuja kwetu.’+ 27  Ndipo akasema, ‘Ikiwa ni hivyo ninakuomba, baba, umtume kwenye nyumba ya baba yangu, 28  kwa maana nina ndugu watano, ili apate kuwapa ushahidi kamili, ili wao pia wasiingie mahali hapa pa mateso.’ 29  Lakini Abrahamu akasema, ‘Wana Musa+ na Manabii;+ na wawasikilize hao.’+ 30  Ndipo akasema, ‘Kwa kweli, hapana, baba Abrahamu, lakini mtu fulani kutoka kwa wafu akiwaendea watatubu.’ 31  Lakini akamwambia, ‘Ikiwa hawamsikilizi Musa+ na Manabii, wala hawatasadikishwa ikiwa mtu fulani atafufuliwa kutoka kwa wafu.’ ”

Maelezo ya Chini

Hadesi. Tazama Nyongeza 4.