Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Unaweza Kuishi Miaka Ngapi?

Unaweza Kuishi Miaka Ngapi?

WAKATI Harriet alikufa katika mwaka wa 2006, alikuwa na miaka karibu 175. Bila shaka, Harriet hakuwa mwanadamu. Alikuwa kobe wa visiwa vya Galapagos, na aliishi katika bustani ambamo wanyama wanafugwa huko Australia. Harriet aliishi miaka mingi sana, ukimulinganisha na sisi wanadamu. Lakini ukimulinganisha na viumbe wengine, kobe huyo hakuwa na maisha marefu kabisa. Tuchunguze mifano fulani.

  • Wachunguzi fulani katika inchi ya Ufini (Finlande), wanasema kwamba kiumbe wa baharini anayeitwa kome, anaweza kuishi miaka 200.

  • Kiumbe wa baharini anayeitwa chaza mara nyingi anaishi zaidi ya miaka 100 na hata imeripotiwa kwamba ameishi zaidi ya miaka 400.

  • Miti mbalimbali, kama vile aina fulani ya musindano, muti mukubwa sana ambao unaitwa sequoia, na aina fulani ya muvinje na musonobari, inaishi kwa maelfu ya miaka.

Lakini wanadamu, ambao wanaonwa kuwa uumbaji muzuri zaidi kati ya uumbaji wote duniani, wanaishi tu miaka 80 ao 90, ijapokuwa wanajikaza sana ili kurefusha maisha yao!

Unawaza namna gani, je, miaka 80 ao zaidi ndio miaka ambayo tunaweza kutumainia kuishi kabisa? Ao je, kuna uwezekano kwamba tunaweza kuishi miaka mingi zaidi? Watu wengi wanatumaini kwamba sayansi na teknolojia ya kiganga vina siri ya kuishi muda murefu zaidi.

Je, Sayansi Inaweza Kusaidia Kurefusha Maisha Yetu?

Sayansi imesaidia sana katika mambo ya afya na maendeleo ya teknolojia ya kiganga. Gazeti moja (Scientific American) linasema hivi: “Watu wachache sana [huko Amerika] wanakufa kutokana na magonjwa ya kuambukiza ao matatizo ya kuzaa. Hesabu ya watoto ambao wanakufa tangu mwaka wa 1960 imeshuka kufikia 75 juu ya 100.” Lakini sayansi imeshindwa kurefusha miaka ya maisha yetu. Habari nyingine ya gazeti hilo inasema hivi: “Hata kisha makumi ya miaka ya uchunguzi, uzee ni jambo ambalo halijaeleweka mupaka sasa.” Hata hivyo, “mambo ya hakika yanaonyesha kwamba uzee unaweza kutokea wakati programu za chembe za uriti ambazo zinafanya mutu aendelee kukomaa zinaacha kufanya kazi.” Habari hiyo inaendelea kusema hivi: “Ikiwa kuzeeka kunatokana kwanza kabisa na chembe za uriti, ni wazi kwamba siku moja itawezekana kuzuia kuzeeka.”

“Hata kisha makumi ya miaka ya uchunguzi, uzee ni jambo ambalo halijaeleweka mupaka sasa”

Katika uchunguzi wao wa kutafuta sababu kubwa ambazo zinafanya watu wazeeke, kutia ndani uchunguzi wa magonjwa yanayotokana na uzee, wanasayansi fulani wanaendelea kuchunguza mabadiliko ambayo yanatokea katika chembe yaliyovumbuliwa hivi karibuni. Mabadiliko hayo yanaitwa epijenetiki. Epijenetiki ni nini?

Chembe zilizo hai zina habari kuhusu chembe za uriti, ambazo zinahitajiwa ili kutokeza chembe mupya mbalimbali. Nyingi kati ya habari hizo zinapatikana ndani ya jenomu, neno ambalo linamaanisha ADN (deoksiribonyukilia asidi) zote zilizo ndani ya chembe moja. Hata hivyo, hivi karibuni, wanasayansi wamechunguza kwa uangalifu sana namna nyingine ya utendaji mbalimbali unaofanyika ndani ya chembe, ni kusema, epijenomu. Epijenetiki ni elimu inayochunguza utendaji huo mbalimbali wenye kushangaza unaofanyika ndani ya chembe, na mabadiliko yanayotokana na muchanganyiko wa utendaji huo ndani ya chembe.

Molekuli ao chembe ndogo kabisa ambazo zinafanyiza epijenomu ni tofauti kabisa na ADN. Ijapokuwa ADN inafanana na ngazi ambayo inajipinda-pinda, ao misokoto miwili, epijenomu ni mufumo wa alama za kemikali, ao vibandiko, alama ambazo zinashikana na ADN. Epijenomu inafanya kazi gani? Kama vile kiongozi anayeongoza kikundi cha wanamuziki, epijenomu inaongoza namna habari za chembe za uriti zinavyotumika. Vibandiko vya molekuli vinachochea vikundi vya chembe za uriti kufanya kazi ao kuacha kufanya kazi kulingana na uhitaji wa chembe na pia mambo ya inje ya chembe, kama vile chakula, mahangaiko, na sumu. Uvumbuzi mbalimbali wa hivi karibuni kuhusu epijenomu umetokeza mabadiliko katika sayansi za biolojia, mabadiliko ambayo yanahusianisha epijenetiki na magonjwa fulani na hata uzee.

Muchunguzi wa mambo ya epijenetiki anayeitwa Nessa Carey, anasema hivi: “[Mambo yanayohusiana na epijenetiki] ndiyo yanatokeza magonjwa, kuanzia ugonjwa mubaya wa akili unaoitwa schizophrenia mupaka ugonjwa unaoshambulia sehemu zinazounganisha viungo vya mwili, na pia kuanzia ugonjwa wa kansa mupaka maumivu makali yanayodumu.” Na “kwa hakika [mambo yanayohusiana na] epijenetiki yanachangia pia kuzeeka.” Kwa hiyo, uchunguzi unaofanywa kuhusu epijenetiki unaweza kusaidia kutengeneza dawa zinazofaa ili kufanya afya iwe nzuri, kupiganisha magonjwa, kutia ndani kansa, na hivyo kufanya watu waishi miaka mingi zaidi. Hata hivyo, kwa sasa, hakuna matumaini makubwa ya kupata dawa hizo wakati ujao. Carey anasema hivi: “Bado tunaendelea na njia zetu za zamani [za kupiganisha uzee], ni kusema, kula mboga nyingi za majani na kufanya mazoezi mengi ya mwili.”

Sababu gani basi watu wanajikaza sana ili kurefusha maisha yao? Sababu gani tunataka kuishi milele? Gazeti moja la Uingereza (The Times) linauliza hivi: “Sababu gani duniani pote watu wanahangaikia sana kupata njia ya kuepuka kifo, iwe ni kupitia kutokufa, ufufuo, maisha baada ya kifo ao kuzaliwa upya katika mwili mwengine?” Kama tutakavyoona sasa, jibu la ulizo hilo litatusaidia kuelewa sababu ya kweli inayofanya watu wazeeke.

Sababu Gani Tunataka Kuishi Milele?

Kwa maelfu ya miaka, watu wenye akili wamejaribu kupata jibu kwa ulizo hilo. Je, kuna maelezo yenye kueleweka na yenye kutosheleza yanayopatana na namna mwili wetu umeumbwa na tamaa yetu ya asili ya kuishi milele? Mamilioni ya watu wanaweza kujibu ndiyo bila kusita! Sababu gani? Katika Biblia, wamepata majibu yenye kutosheleza kabisa kuhusu namna mwanadamu alivyoumbwa.

Tangu kitabu cha Mwanzo, Biblia inaeleza waziwazi kwamba wanadamu wako tofauti kabisa na viumbe wengine, ijapokuwa wana mambo fulani yanayofanana na viumbe hao. Kwa mufano, katika andiko la Mwanzo 1:27, tunasoma kwamba Mungu aliumba wanadamu kwa mufano wake. Namna gani hivyo? Aliwapa uwezo wa kuonyesha upendo, haki, na hekima. Na kwa sababu yeye ni Mungu anayeishi milele, aliweka ndani yetu tamaa ya kuishi milele. Andiko la Mhubiri 3:11 linasema kwamba “ameweka hiyo milele ndani ya mioyo yao.”—Union Version.

Uwezo wa ubongo wa mwanadamu, zaidi sana uwezo wa ubongo wa kujifunza mambo, unahakikisha kwamba wanadamu waliumbwa ili waishi miaka mingi zaidi ya ile wanayoishi leo. Kitabu kimoja kinachozungumuzia uwezo wa ubongo (The Encyclopedia of the Brain and Brain Disorders) kinasema kwamba uwezo wa ubongo wa mwanadamu wa kuweka mambo “hauna mipaka.” Sababu gani ubongo ungekuwa na uwezo huo ikiwa haukumbwa ili utumiwe? Kwa kweli, katika njia nyingi, namna wanadamu wameumbwa inaonyesha kusudi ambalo Mungu alikuwa nalo tangu mwanzoni kwa ajili ya wanadamu. Kwa hiyo, sababu gani tunazeeka, tunateseka, na tunakufa?

Sababu Gani Tunazeeka na Tunakufa?

Mwanaume na mwanamuke wa kwanza walikuwa na miili mikamilifu na uhuru wa kuchagua. Inasikitisha kwamba walitumia vibaya uhuru huo kwa kumuasi Muumbaji wao. * (Mwanzo 2:16, 17; 3:6-11) Kukosa kumutii Mungu, ao zambi, kuliwafanya wawe na hatia kubwa na haya. Zambi hiyo ilileta matokeo mabaya katika miili yao, na ikatokeza hali isiyoweza kuepukika na iliyoelekeza polepole kwenye kifo. Andiko la 1 Wakorintho 15:56 linasema hivi: ‘Muchomo unaotokeza kifo ni zambi.’

Kulingana na sheria za asili za uriti, wazao wote wa Adamu na Eva waliriti kutokamilika na mwelekeo wa kufanya zambi, ao mambo yaliyo mabaya. Andiko la Waroma 5:12 linasema hivi: ‘Kupitia mutu mumoja zambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia zambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya zambi.’

Tunaweza kusema nini kutokana na yale ambayo yametajwa hapo juu? Tunaweza kusema hivi: Siri ya kuishi milele haiwezi kupatikana hata siku moja katika vyumba vya uchunguzi wa kisayansi. Ni Mungu tu ndiye anaweza kumaliza matokeo mabaya ya zambi. Lakini, je, atafanya hivyo? Biblia inajibu waziwazi ndiyo!

“Yeye . . . Atameza Kifo Milele”

Tayari Mungu amefanya jambo la maana sana ili kuondoa zambi na kifo. Alituma Yesu Kristo ili atoe uzima wake kwa ajili yetu. Namna gani kifo cha Yesu kinaweza kutusaidia? Yesu alizaliwa akiwa mukamilifu na ‘hakufanya zambi.’ (1 Petro 2:22) Kwa hiyo, alikuwa na haki ya kuendelea kuishi milele akiwa mwanadamu mukamilifu. Alifanya nini na uzima wake mukamilifu? Aliutoa bila kulazimishwa ili kulipia zambi zetu. Kwa kweli, Yesu alitoa uzima wake kuwa “fidia [ao zabihu ya ukombozi] badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Hivi karibuni, zabihu hiyo ya ukombozi itatumiwa kabisa kwa ajili yetu. Zabihu hiyo inaweza kukuletea faida gani? Fikiria maandiko haya:

  • ‘Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamutoa Mwana wake muzaliwa​-pekee, ili kila mutu anayemuamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.’​—Yohana 3:16.

  • “Yeye kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.”​—Isaya 25:8.

  • “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”​—1 Wakorintho 15:26.

  • “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena.”​—Ufunuo 21:3, 4.

Unaweza kuishi miaka ngapi? Jibu la Biblia ni wazi: Wanadamu wanaweza kuwa na tumaini la kuishi milele​—tumaini ambalo litatimia kisha Mungu kuondoa mabaya yote duniani. (Zaburi 37:28, 29) Yesu alikuwa akifikiria tumaini hilo nzuri alipomuambia mwanaume aliyetundikwa kwenye muti karibu naye hivi: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”​—Luka 23:43.

Kwa kweli, tamaa ya mwanadamu ya kuishi milele inaeleweka na inapatana na namna tuliumbwa. Mungu alituumba tukiwa na tamaa hiyo! Zaidi ya hilo, atatimiza tamaa hiyo. (Zaburi 145:16) Hata hivyo, tunapaswa kutimiza mambo ambayo tunaombwa kufanya. Kwa mufano, tunapaswa kuwa na imani katika Mungu. Andiko la Waebrania 11:6 linasema hivi: ‘Bila imani haiwezekani kamwe kumupendeza [Mungu] vema, kwa maana yule anayemukaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye ni musawabishaji wa wale wanaomutafuta kwa bidii.’ Imani kama hiyo si kuamini tu bila ushuhuda, lakini ni usadikisho wa akili unaotegemea ujuzi wa kweli kabisa ulio katika Biblia. (Waebrania 11:1) Ikiwa unapenda kuwa na imani hiyo, tafazali, zungumuza na Mashahidi wa Yehova walio katika eneo lenu ao fungua adresi yetu ya Internete www.jw.org.

^ Uasi wa Adamu na Eva ulitokeza maulizo mazito juu ya haki ya Mungu ya kutawala. Maulizo hayo, ambayo yanaonyesha sababu gani Mungu anaacha watu wateseke kwa muda, yanazungumuziwa katika kitabu kinachosaidia kujifunza Biblia chenye kichwa Biblia Inafundisha Kabisa Nini? Soma kitabu hicho kwenye adresi yetu ya Internete www.jw.org.