Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SEHEMU YA KUULIZA MAULIZO | IRÈNE HOF LAURENCEAU

Muganga Anayepasua Mifupa Anaeleza Imani Yake

Muganga Anayepasua Mifupa Anaeleza Imani Yake

Muganga Irène Hof Laurenceau anafanya kazi ya kupasua mifupa katika inchi ya Uswisi. Wakati fulani, alikuwa na mashaka ikiwa kuna Mungu. Lakini miaka fulani kisha hapo alifikia kutambua kwamba kuna Mungu na kwamba yeye ndiye Muumbaji wa uzima. Gazeti Amuka! lilimuuliza kuhusu kazi yake na imani yake.

Ni nini kilikufanya upendezwe na sayansi?

Nilipokuwa mutoto, nilivutiwa sana na mazingira. Nilikomalia huko Richterswil, kijiji kimoja chenye kupendeza sana cha Uswisi kilicho pembeni ya Bahari Zurich. Wazazi wangu na ndugu zangu wakubwa walikuwa wananitembeza na kunieleza juu ya viumbe na mimea tuliyoona njiani wakati wa matembezi yetu.

Sababu gani ulisoma masomo ya kupasua mifupa?

Kwa wakati fulani, baba yangu alitumika kama musaidizi katika chumba cha kupasua watu kwenye hospitali ya kijiji chetu. Mambo ambayo aliona yalimuchochea kusema kwa uchangamufu kuhusu kazi ya upasuaji. Uchangamufu wake ulinichochea sana na kisha mimi pia nikachagua kusoma masomo ya upasuaji. Nilifuata masomo ya upasuaji wa mifupa kwa sababu ninapenda namna mifupa inafanyizwa na namna inafanya kazi katika mwili. Waganga wanaopasua mifupa wanapaswa kufikiri kama fundi ili kurekebisha mifupa, misuli, na kano ao mishipa inayotuwezesha kutikisika.

Zaidi ya yote, ninafurahi wakati ninaona wagonjwa ambao ninatunza wanapona. Kwa kweli, ninapenda sana kusaidia watu.

Sababu gani ulikuwa na mashaka ikiwa kuna Mungu?

Nilianza kuwa na mashaka nilipokuwa kijana, na mambo mawili hasa ndiyo yalinifanya niwe na mashaka. Jambo la kwanza, nilitambua kwamba walimu fulani wa dini kwenye kanisa walikuwa na mwenendo mubaya, na jambo hilo lilinisumbua sana. Jambo la pili, kwenye masomo, walimu wangu fulani wa somo la biolojia waliamini fundisho la mageuzi, fundisho ambalo nilifikia kukubali baadaye, zaidi sana nilipoenda kwenye masomo ya juu.

Sababu gani ulikubali fundisho la mageuzi?

Niliwaamini walimu wangu. Zaidi ya hiyo, nilifikiri kwamba mambo yenye kufanana katika muundo wa miili ya aina fulani za viumbe yalionyesha kwamba walitokana na chanzo kimoja na kwamba mabadiliko ya chembe za uriti yanatokeza aina mupya.

Lakini, ulibadilisha mawazo yako. Sababu gani?

Rafiki fulani alinialika kwenye mukutano wa Mashahidi wa Yehova. Nilivutiwa sana na urafiki ambao nilionyeshwa na washiriki wa kutaniko na mafundisho mbalimbali yenye kujenga. Kisha hapo, mwanamuke mumoja mwenye kuvutia wa kutaniko alinitembelea, na nikamuuliza, “Namna gani ninaweza kuwa na uhakika ikiwa Biblia ina habari za kweli?”

Alinionyesha unabii mbalimbali wa Biblia kuhusu mambo mengi yanayotokea katika siku zetu. Mufano mumoja ni unabii wa Yesu ambao unaonyesha kwamba katika siku za mwisho za ulimwengu huu kungekuwa na vita kati ya mataifa, ‘matetemeko makubwa ya inchi,’ na magonjwa ya kuambukiza na upungufu wa chakula. * Pia mwanamuke huyo alizungumuzia unabii mbalimbali ambao ulitabiri kwamba mwenendo wa watu ungekuwa mubaya sana na kwamba watu wangekuwa na tamaa mbaya na mambo mengine mabaya sana ambayo tunaona leo. * Bila kukawia, nilianza kujifunza Biblia kwa bidii na nikatambua haraka kwamba mambo ambayo Biblia inatabiri yanatimia sikuzote. Pia nilianza kuchunguza upya mawazo yangu juu ya namna uzima ulianza.

Je, uchunguzi wako juu ya mambo ya kiganga ulikusaidia kufikiri sana juu ya namna uzima ulianza?

Ndiyo. Nilipoanza kujifunza Biblia, nilikuwa ninafanya uchunguzi juu ya upasuaji wa magoti. Kuanzia mwishoni mwa miaka kati ya 1961 na 1970, wanasayansi walianza kuelewa waziwazi zaidi namna magoti yanavyofanya kazi kwa njia ya ajabu. Walitambua kwamba goti letu halijikunje tu upande mumoja. Lakini, linaweza kujikunja katika pande zote, na hivyo kuwezesha goti kuzunguka huku na huku kwa njia ambayo inatuwezesha kutembea, kucheza, kuteleza kwenye barafu, na kufanya mambo mengine mengi.

Kwa muda wa miaka 40, wachunguzi wamejaribu kutengeneza goti la mufano. Lakini kwa sababu goti la mwanadamu linafanya kazi kwa njia ya ajabu sana, hilo linafanya iwe vigumu kuliiga. Zaidi ya hilo, vinapolinganishwa na goti letu, vitu vinavyotengenezwa na mwanadamu havidumu kwa muda murefu. Hata ikiwa wanatumia vitu vya hali ya juu zaidi, watengenezaji hao wanafurahi sana ikiwa vitu ambavyo wanatengeneza vinadumu miaka 20. Bila shaka, goti letu linafanyizwa na chembe zenye uzima ambazo zinaendelea kujifanya upya. Kulingana na mimi, goti halionyeshe kwamba vitu vilijitokeza vyenyewe kupitia mageuzi, lakini linaonyesha hekima ya Mungu.

Tuseme nini juu ya kubadilika kwa viumbe na mambo yenye kufanana katika muundo wa miili ya aina fulani za viumbe?

Mambo yenye kufanana katika muundo wa miili ya aina fulani za viumbe yanaonyesha kwamba viumbe hivyo viliumbwa na Muumbaji mumoja. Zaidi ya hilo, kubadilika kwa viumbe hakufanye viumbe hivyo viwe na muundo wa mwili ulio muzuri zaidi ambao unavifanya viwe vya aina nyingine ya hali ya juu zaidi. Lakini, kubadilika huko kwa viumbe kuna mwelekeo wa kuharibu chembe za uriti. Bila shaka, aksidenti inaweza kutimiza kusudi fulani la maana. Kwa mufano, treni inaweza kuanguka ndani ya daraja ao kilalo na kukiharibu, na hivyo kulinda muji ili usivamiwe na jeshi la maadui. Lakini aksidenti hiyo haikufanya hali ya muji huo iwe nzuri zaidi. Ni vilevile, kubadilika kwa viumbe hakufanye muundo wa miili ya viumbe hivyo uwe muzuri zaidi. Na kubadilika huko hakuwezi kutokeza hata siku moja kitu fulani kilichoumbwa kwa njia ya ajabu kama goti la mwanadamu, ambalo ni moja tu kati ya sehemu nyingi za mwili wa mwanadamu ambazo zimeumbwa kwa njia ya ajabu.

Kubadilika kwa viumbe hakuwezi kutokeza hata siku moja kitu fulani kilichoumbwa kwa njia ya ajabu kama goti la mwanadamu

Sababu gani umekuwa Shahidi wa Yehova?

Nilipoanza kufuata kanuni za Biblia, maisha yangu yalibadilika sana. Zaidi ya hilo, katika mwaka wa 2003, nilienda kwenye mukusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova na kwenye mukusanyiko huo niliona kwamba Mashahidi wa Yehova ni familia yenye umoja kabisa, niliona umoja huo hata kati ya wahuzuriaji ambao walikuwa hawajakutana bado. Wahuzuriaji hao walionyeshana upendo wa kweli, na mimi nilitaka kuwa mumoja wao.