Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Amani Kati ya Watu wa Nia Njema”

“Amani Kati ya Watu wa Nia Njema”

“Utukufu katika vilele vilivyo juu kwa Mungu, na juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.”​—LUKA 2:14.

Kwa nini watu fulani husherehekea Krismasi?

Kila mwaka, papa na viongozi wengine wa kidini huhubiri ujumbe wa amani, wakitumaini kwamba majira ya Krismasi yatatimiza tangazo hili la malaika: “Juu ya dunia amani kati ya watu wa nia njema.” Wengine hupanga safari za kidini ili kwenda mahali fulani patakatifu na kusheherekea.

Kwa nini ni vigumu kufanya hivyo?

Mara nyingi, amani wakati wa Krismasi huwa ni ya muda mfupi tu. Kwa mfano, Desemba 1914, wakati bara Ulaya lilipokuwa katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, wanajeshi wa Uingereza na wa Ujerumani walitoka kwenye mahandaki yao na kusheherekea Krismasi pamoja. Walikula, wakanywa, na kuvuta sigara pamoja. Pia, walicheza mpira wa miguu. Hata hivyo, amani hiyo haikudumu kwa muda mrefu. Katika barua iliyotoka vitani, mwanajeshi wa Uingereza alisimulia kwamba mwanajeshi wa Ujerumani alimwambia: “Leo tuna amani. Kesho utaipigania nchi yako; na mimi nitaipigania nchi yangu.”

Ni kanuni gani za Biblia zinazoweza kutusaidia?

“Kuna mtoto ambaye amezaliwa kwetu . . . Naye ataitwa jina . . . Mkuu wa Amani. Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.” (Isaya 9:6, 7) Je, hutiwi moyo na unabii huo kumhusu Yesu Kristo? Yesu hakuzaliwa duniani ili kuleta amani ya siku moja kila mwaka. Akiwa Mtawala aliye mbinguni, ataleta amani ya kweli ambayo itadumu milele.

“Kupitia kwangu [Yesu] mpate kuwa na amani. Ulimwenguni mna dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Hata leo, Yesu anawasaidia wafuasi wake kuwa na amani. Ni kweli kwamba Wakristo wana dhiki. Hata hivyo, kwa msaada wa Biblia, wanaelewa ni kwa nini watu wanateseka na jinsi Yesu atakavyoleta amani yenye kudumu. Kwa hiyo, wanafurahia kuwa na amani ya akili.

Kwa kutii maneno ya Yesu, Mashahidi wa Yehova​—kutoka kila taifa, rangi, jamii, au lugha—​wanafurahia amani hiyo. Jionee mwenyewe kwa kuhudhuria mikutano kwenye Jumba lao la Ufalme. Kama watu wengine wengi, huenda utakubali kwamba amani hiyo ni bora kuliko amani yoyote inayotokana na Krismasi.

Mashahidi wa Yehova wameunganishwa kwa sababu ya amani licha ya rangi au lugha yao. Jionee mwenyewe kwa kuhudhuria mikutano kwenye Jumba lao la Ufalme