Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Mungu

Je, Jina Lako Limeandikwa Katika “Kitabu cha Kumbukumbu cha Mungu”?

Je, Jina Lako Limeandikwa Katika “Kitabu cha Kumbukumbu cha Mungu”?

JE, YEHOVA huona jitihada za waabudu wake za kumpendeza? Bila shaka, anaona! Lakini yeye huona zaidi ya matendo na maneno yao ya kumtukuza. Anatambua hata wanapofikiria kwa uthamini kumhusu yeye. Kwa kweli, Yehova hatawasahau kamwe watu wake na yale waliyofanya. Tunawezaje kuwa na uhakika? Tunapata jibu katika maneno yaliyoandikwa na nabii Malaki.​—Soma Malaki 3:16.

Katika karne ya tano K.W.K., Malaki alipokuwa akitoa unabii huu, hali ya maadili na ya kidini ilikuwa mbaya sana katika Israeli. Makuhani walipuuza kazi yao, na watu kwa ujumla wakafanya matendo yasiyomheshimu Mungu kama vile ushirikina, uzinzi, na udanganyifu. (Malaki 2:8; 3:5) Licha ya hali hiyo mbaya, bado kulikuwa na kikundi cha Waisraeli walioendelea kuwa waaminifu. Walikuwa wakifanya nini?

“Wale wenye kumwogopa Yehova wakasemezana,” Malaki anaeleza. Kumwogopa Mungu ni sifa nzuri. Hapa, Malaki anazungumzia Waisraeli ambao walimheshimu sana Mungu na kuogopa kumchukiza. Ona kwamba wale waliomwogopa Mungu ‘walisemezana.’ Bila shaka, walikusanyika ili kuzungumzia uzuri wa Yehova na kutiana moyo, la sivyo wangevunjika moyo au kuchafuliwa na upotovu uliokuwa umeenea.

Waisraeli waaminifu walionyesha heshima yao kwa Yehova katika njia nyingine ya maana: Walikuwa ‘wakilifikiria jina lake.’ Tafsiri nyingine husema “waliliheshimu jina Lake.” Watu hao waliomwogopa Mungu walimheshimu Yehova hata katika mawazo yao. Moyoni mwao, walifikiria kwa uthamini, au walitafakari juu ya Yehova na jina lake kuu. Je, Yehova aliona yale waliyokuwa wakifanya?

Malaki anasema: “Yehova akaendelea kutoa uangalifu na kusikiliza.” Kutoka katika makao yake yaliyo juu mbinguni, kwa kweli Yehova alitega sikio lake na kusikiliza kila neno la kumsifu ambalo waabudu wake walisemezana. Pia, alikazia uangalifu mambo yote waliyotafakari faraghani. (Zaburi 94:11) Lakini alifanya mengi zaidi ya kusikiliza tu maneno na mawazo yao mazuri.

“Kitabu cha kumbukumbu kikaanza kuandikwa mbele zake,” anasema Malaki. Kitabu hicho ni kumbukumbu ya wale wote wamemtumikia Yehova kwa uaminifu. Ona kwamba kinaitwa “kitabu cha kumbukumbu.” * Hilo linaonyesha kwamba Yehova hatawasahau kamwe waabudu wake waaminifu na yote waliyofanya ili kumtukuza yeye​—kila tendo jema, neno jema, na wazo jema. Hata hivyo, Mungu ana sababu ya kuwakumbuka. Anawaahidi zawadi ya uzima wa milele wote ambao majina yao yameandikwa bila kufutwa katika kitabu chake cha kumbukumbu. *​—Zaburi 37:29.

Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova huthamini yote tunayofanya ili kumwabudu katika njia inayokubalika! Maneno ya Malaki 3:16 hutupa sababu nzuri ya kufikiria kwa uzito. Ni vizuri kujiuliza, ‘Je, jina langu limo katika “kitabu cha kumbukumbu” cha Mungu?’ Litakuwepo ikiwa tu, tutajitahidi kutenda, kusema, na kufikiri kila siku katika njia ambayo Yehova atataka kukumbuka.

Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa kwa Mwezi wa Desemba:

Nahumu 1-3Malaki 1-4

^ fu. 8 Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “kumbukumbu” humaanisha mengi zaidi ya kukumbuka jambo fulani. Pia, linaweza kumaanisha kuchukua hatua fulani kuhusu kile kinachokumbukwa.

^ fu. 8 Kwa maelezo zaidi kuhusu ahadi ya Mungu ya uzima wa milele, ona sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.