Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sahihi Kisayansi

Sahihi Kisayansi

“Je, kufikia sasa sikukuandikia mashauri na ujuzi, nikuonyeshe ukweli wa maneno ya kweli, ili urudishe maneno yaliyo kweli.”​—METHALI 22:20, 21.

BIBLIA INATOFAUTIANAJE NA VITABU VINGINE? Vitabu vya kale vina habari zisizotegemeka na mawazo hatari ambayo sayansi ya kisasa imethibitisha kuwa ni ya uwongo. Hata leo, waandishi wengi wanalazimika kubadili habari zilizo katika vitabu vyao ili zipatane na uvumbuzi wa kisasa. Lakini Biblia inadai kwamba ilitungwa na Muumba na Neno lake “linadumu milele.”​—1 Petro 1:25.

MFANO: Sheria ya Musa iliwaamuru Waisraeli wachimbe na kufunika mavi yao “nje ya kambi.” (Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Ikiwa wangegusa mnyama au mwanadamu aliyekufa, Waisraeli walipaswa kujisafisha kwa maji. (Mambo ya Walawi 11:27, 28; Hesabu 19:14-16) Watu waliokuwa na ugonjwa wa ukoma walitengwa hadi uchunguzi wa kitiba ulipothibitisha kwamba hawangewaambukiza watu wengine.​—Mambo ya Walawi 13:1-8.

MAMBO AMBAYO TIBA YA KISASA IMETHIBITISHA: Kuondoa kinyesi kwa njia inayofaa, kunawa mikono, na kutenga wagonjwa bado ndiyo njia bora ya kupambana na magonjwa. Ikiwa hakuna vyoo karibu au mfumo wa kuondoa maji machafu na takataka, Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani (CDC) vinatoa ushauri huu: “Funika mavi angalau mita 30 hivi kutoka mahali penye maji.” Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, watu wanapohakikisha kwamba wanaondoa kinyesi kwa njia inayofaa, wanapunguza magonjwa ya kuharisha kwa asilimia 36. Miaka isiyozidi 200 iliyopita, madaktari waligundua kwamba waliwaambukiza wagonjwa wengi wakati walipowagusa kabla ya kunawa mikono baada ya kugusa maiti. CDC inasema kwamba kunawa mikono ndiyo “njia pekee iliyo na matokeo zaidi katika kuzuia kusambaa kwa magonjwa.” Vipi kuhusu kuwatenga watu walio na ukoma au magonjwa mengine? Hivi karibuni, jarida linaloitwa Saudi Medical Journal lilisema hivi: “Janga la ugonjwa wa kuambukiza linapokumba eneo fulani, mbinu pekee ya kuzuia kusambaa kwa ugonjwa huo ni kuwatenga watu ambao tayari wameambukizwa.”

UNA MAONI GANI? Je, ungetazamia kitabu kingine chochote kitakatifu na cha kale kiwe na habari zinazopatana na sayansi ya kisasa? Au je, Biblia ni kitabu cha kipekee?

“Ni jambo lenye kuvutia kusoma mambo yanayohusu usafi yaliyofuatwa wakati wa Sheria ya Musa.”​—KITABU MANUAL OF TROPICAL MEDICINE, CHA DAKT. ALDO CASTELLANI NA DAKT. ALBERT J. CHALMERS