Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Amenifungua Macho

Yehova Amenifungua Macho

Yehova Amenifungua Macho

LIMESIMULIWA NA PATRICE OYEKA

Siku moja jioni, baada ya kushinda siku nzima nikiwa nimevunjika moyo kwa sababu ya kuwa kipofu, mpweke, na kusikiliza tu redio, niliamua kujiua. Nilichanganya aina fulani ya sumu na maji ndani ya kikombe na kukiweka juu ya meza iliyokuwa mbele yangu. Nilitaka kwanza kuoga kwa mara ya mwisho, kisha nivae vizuri kabla sijanywa sumu hiyo ili nijimalize kabisa. Kwa nini nilitaka kujiua? Na imekuwaje kwamba bado niko hai nikisimulia habari hii?

NILIZALIWA mnamo Februari 2, 1958, katika mkoa wa Kasaï Oriental, katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Baba yangu alikufa nilipokuwa na umri wa miaka tisa, hivyo kaka yangu alinitunza nilipoendelea kukua.

Baada ya kumaliza masomo yangu, nilipata kazi katika shamba la miti ya mpira. Asubuhi moja katika mwaka wa 1989, nilipokuwa nikitayarisha ripoti fulani katika ofisi yangu, kwa ghafla nilijipata katika giza totoro. Kwanza, nilifikiri kwamba hakukuwa na umeme, lakini jenereta ilikuwa ikinguruma na ilikuwa asubuhi! Nikiwa nimejawa na hofu, nilitambua kwamba singeweza kuona chochote, hata karatasi zilizokuwa mbele yangu!

Mara moja, nikamwita mmoja wa wasaidizi wangu ili anipeleke kwa mtu aliyekuwa akisimamia idara ya wagonjwa na watu walioumia. Msimamizi huyo alipendekeza nipelekwe kwa daktari mwenye ujuzi zaidi, huko jijini. Baada ya kuona kwamba retina za macho yangu zilikuwa zimeharibika kabisa na hali yangu ilikuwa mbaya, daktari huyo aliagiza nipelekwe katika jiji kuu, Kinshasa.

Maisha Jijini Kinshasa

Nilipokuwa Kinshasa, nilipelekwa kwa madaktari wengi wa macho lakini hakuna hata mmoja aliyeweza kunitibu. Baada ya kukaa siku 43 hospitalini, madaktari walisema kwamba ningeendelea kuwa kipofu kwa maisha yangu yote! Watu wa familia yangu walinipeleka kwenye makanisa mengi wakitazamia kwamba nitaponywa kimuujiza, lakini sikuwahi kupona.

Mwishowe, nilikata tamaa ya kwamba nitawahi kuona tena. Kila jambo katika maisha yangu lilikuwa lenye kuvunja moyo. Nilipoteza uwezo wangu wa kuona na nikafutwa kazi. Pia, mke wangu aliniacha na akaenda na kila kitu tulichokuwa nacho ndani ya nyumba yetu. Niliaibika kutoka nje au kushirikiana na watu wengine. Nilijitenga na watu na nilikuwa nikishinda ndani ya nyumba kila siku. Nilikuwa mpweke na nilihisi kwamba sifai kabisa.

Nilijaribu kujiua mara mbili. Kisa cha pili ni kile kilichotajwa mwanzoni mwa simulizi hili. Niliokolewa na mtoto mdogo ambaye alikuwa wa familia yetu. Nilipokuwa nikioga, mtoto huyo alichukua kikombe hicho bila kukusudia na kumwaga ile sumu. Ninashukuru kwamba hakuinywa. Lakini nilihuzunika sana kwa sababu sikupata kile kikombe. Mwishowe, niliwaeleza washiriki wa familia yangu kwa nini nilikuwa nikikitafuta na jambo nililokusudia kufanya.

Ninamshukuru Mungu na familia yangu kwa kunitunza. Mpango wangu wa kujiua haukufanikiwa.

Nilipata Furaha Maishani Tena

Jumapili moja katika mwaka wa 1992, nilipokuwa nimeketi nyumbani nikivuta sigara, Mashahidi wawili wa Yehova walinitembelea walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba. Walipotambua kwamba nilikuwa kipofu, walinisomea andiko la Isaya 35:5 linalosema, “Wakati huo macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa.” Nilishangilia sana moyoni niliposikia maneno hayo! Kinyume na yale niliyokuwa nimesikia katika makanisa niliyotembelea, Mashahidi hawakuahidi kuniponya kimuujiza. Badala yake, walinifafanulia kwamba ikiwa tu ningemjua Mungu ningepata uwezo wa kuona tena katika ulimwengu mpya ambao ameahidi. (Yohana 17:3) Mara moja, nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi tukitumia kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani. Pia, nilianza kuhudhuria mikutano yote ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme lililokuwa karibu na nikafanya mabadiliko maishani. Niliacha kuvuta sigara.

Lakini sikufanya maendeleo ya kiroho haraka kwa sababu ya hali yangu ya kuwa kipofu. Kwa hiyo, nilienda katika taasisi ya vipofu ili nijifunze kusoma na kuandika maandishi ya vipofu. Hilo liliniwezesha kushiriki mazoezi ya kihuduma katika Jumba la Ufalme. Muda si muda, nilianza kuwahubiria majirani wangu. Kisha, nilianza kupata furaha tena katika maisha yangu. Nikafanya maendeleo zaidi na kujitoa kumtumikia Yehova maishani. Nilibatizwa mnamo Mei 7, 1994.

Kadiri nilivyozidi kumpenda Yehova na watu, ndivyo nilivyositawisha tamaa ya kuanza utumishi wa wakati wote. Tangu Desemba 1, 1995, nimekuwa nikitumika nikiwa painia wa kawaida, mhubiri wa wakati wote. Pia, nimekuwa na pendeleo la kutumika nikiwa mzee katika kutaniko letu tangu Februari 2004. Nyakati nyingine, mimi hualikwa kutoa hotuba zinazotegemea Biblia kwenye makutaniko mengine katika eneo letu. Baraka hizo zote zinaniletea shangwe nyingi na kunikumbusha kwamba hakuna ulemavu unaoweza kutuzuia tusitimize tamaa yetu ya kumtumikia Yehova Mungu.

Yehova Amenipa “Macho”

Kama nilivyotaja awali, mke wangu aliniacha kwa sababu nilikuwa kipofu. Lakini nimepata baraka nyingine kutoka kwa Yehova. Kwa njia ya pekee alinipa uwezo wa kuona. Anny Mavambu, ambaye alikubali nimwoe licha ya ulemavu wangu, amekuwa macho yangu. Kwa kuwa yeye pia ni mhubiri wa wakati wote, sikuzote anaambatana nami katika kazi ya kuhubiri. Pia, yeye hunisomea habari nitakazotumia kutoa hotuba ili niandike maandishi yangu ya vipofu. Yeye ni baraka ya kipekee kwangu. Kwa sababu yake nimeona ukweli wa maneno ya andiko la Methali 19:14: “Urithi kutoka kwa akina baba ni nyumba na mali, lakini mke mwenye busara hutoka kwa Yehova.”

Pia, Yehova ametubariki mimi na Anny kwa kutupatia watoto wawili—mvulana na msichana. Ninatamani sana kuona nyuso zao katika Paradiso! Baraka nyingine ambayo nimepata ni kwamba kaka yangu ambaye ameturuhusu tuishi kwake, alikubali kweli za Biblia na kubatizwa! Sisi sote tuko katika kutaniko moja.

Ingawa mimi ni mlemavu, bado ninatamani kufanya mengi zaidi katika kumtumikia Mungu kwa sababu amenibariki sana. (Malaki 3:10) Kila siku, ninasali kwamba Ufalme wake uje na kuondoa mateso yote duniani. Tangu nilipomjua Yehova ninaweza kusema hivi kwa uhakika: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”—Methali 10:22.

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nikitoa hotuba inayotegemea Biblia; nikiwa pamoja na familia yangu na ndugu yangu