Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

3 Jifunze Ukweli Kumhusu Yesu

3 Jifunze Ukweli Kumhusu Yesu

3 Jifunze Ukweli Kumhusu Yesu

“Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

KWA NINI INAWEZA KUWA VIGUMU? Watu fulani wanasema kwamba Yesu hakuwa mtu halisi. Wengine wanakubali kwamba Yesu alipata kuishi lakini wanasema alikuwa mtu wa kawaida tu ambaye alikufa zamani.

UNAWEZA KUFAULU JINSI GANI? Unaweza kufaulu kwa kumwiga mwanafunzi Nathanaeli. * Rafiki yake Filipo alimwambia kwamba alifikiri alikuwa amempata Masihi—“Yesu, mwana wa Yosefu, kutoka Nazareti.” Lakini Nathanaeli hakuyaamini tu maneno ya Filipo, badala yake, alimuuliza: “Je, kitu chochote kilicho chema kinaweza kutoka Nazareti?” Lakini Filipo alipomwambia, ‘Njoo ujionee’ mwenyewe, Nathanaeli alikubali. (Yohana 1:43-51) Wewe pia utanufaika kwa kujichunguzia mwenyewe uthibitisho uliopo kumhusu Yesu. Unaweza kufanya nini?

Chunguza habari za kihistoria zinazothibitisha kwamba Yesu alikuwa mtu halisi. Yosefo na Tasito ni wanahistoria wa karne ya kwanza wenye kuheshimiwa ambao hawakuwa Wakristo. Wanamtaja Yesu Kristo kuwa mtu halisi aliyepata kuishi. Tasito aliandika hivi alipoeleza jinsi Maliki Mroma Nero alivyowalaumu Wakristo kwamba walianzisha moto jijini Roma mwaka wa 64 W.K.: “Nero aliwalaumu watu walioitwa Wakristo ambao walichukiwa na Waroma kwa sababu ya mazoea yao, naye aliwatesa kikatili sana. Jina Wakristo linatokana na jina la Kristo, ambaye gavana wetu Pontio Pilato alimhukumia kifo, wakati wa utawala wa Tiberio.”

Kitabu Encyclopædia Britannica, Chapa ya 2002, kinasema hivi kuhusiana na mambo ambayo wanahistoria wa karne ya kwanza na ya pili walisema kumhusu Yesu na Wakristo wa mapema: “Masimulizi hayo mbalimbali yanathibitisha kwamba zamani za kale hata wapinzani wa Ukristo hawakutilia shaka kwamba Yesu alikuwa mtu halisi. Jambo hilo lilibishaniwa kwa mara ya kwanza na bila sababu nzuri mwishoni mwa karne ya 18, katika karne ya 19, na mwanzoni mwa karne ya 20.” Mnamo 2002, gazeti The Wall Street Journal lilisema: “Wasomi wengi, isipokuwa wale wachache ambao wanaamini kwamba hakuna Mungu, wamekubali Yesu wa Nazareti kuwa mtu halisi.”

Fikiria uthibitisho wa kwamba Yesu alifufuliwa. Yesu alipokamatwa na wapinzani wake, marafiki wake wa karibu walimwacha na kutawanyika, na rafiki yake Petro alikana kumjua kwa sababu ya woga. (Mathayo 26:31, 55, 56, 69-75) Kisha kwa ghafula, wanafunzi wake wakaanza kutenda kwa bidii. Petro na Yohana waliwakabili kwa ujasiri watu walewale waliopanga njama ya kumuua Yesu. Wanafunzi wa Yesu walichochewa kiasi cha kwamba walieneza mafundisho yake kotekote katika Milki ya Roma, wakiona ni afadhali kufa kuliko kutenda kinyume cha mambo waliyoamini.

Ni nini kilichowachochea wanafunzi hao wabadili mtazamo wao jinsi hiyo? Mtume Paulo anaeleza kwamba Yesu alifufuliwa na “alimtokea Kefa [Petro], kisha wale kumi na wawili.” Paulo anaendelea kusema: “Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mmoja.” Watu wengi waliojionea kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa walikuwa bado hai wakati Paulo alipoandika maneno hayo. (1 Wakorintho 15:3-7) Ingekuwa rahisi kwa watu wenye shaka kupuuza ushuhuda wa mtu mmoja au wawili. (Luka 24:1-11) Lakini ushuhuda wa watu zaidi ya 500 ulithibitisha kwamba Yesu alifufuliwa.

UTAPATA THAWABU GANI? Wale wanaomwamini Yesu na kumtii wanaweza kusamehewa dhambi zao na wanaweza kuwa na dhamiri safi. (Marko 2:5-12; 1 Timotheo 1:19; 1 Petro 3:16-22) Wakifa, Yesu anaahidi atawafufua “katika siku ya mwisho.”—Yohana 6:40.

Ili kupata habari zaidi, ona sura ya 4, “Yesu Kristo Ni Nani?,” na sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 4 Katika vitabu vya Injili vya Mathayo, Marko, na Luka yaonekana Nathanaeli anaitwa Bartholomayo.

^ fu. 10 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kama Nathanaeli, chunguza mambo yanayothibitisha kwamba Yesu alikuwa mtu halisi