Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?

Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Ufalme wa Mungu Umo Moyoni Mwako?

Watu wengi leo wanaamini kwamba jibu la swali hilo ni ndiyo. Kwa mfano, kitabu kimoja (The Catholic Encyclopedia) kinadai hivi: “Ufalme wa Mungu unamaanisha . . . jinsi Mungu anavyotawala mioyo yetu.” Makasisi wengi wanafundisha jambo hilo. Je, kweli Biblia inafundisha kwamba Ufalme wa Mungu umo ndani ya mioyo ya wanadamu?

Watu fulani wanafikiri kuwa Yesu ndiye aliyefundisha kwamba Ufalme wa Mungu umo ndani ya mioyo ya wanadamu. Yesu alisema: “Tazama! ufalme wa Mungu umo katikati yenu.” (Luka 17:21) Tafsiri fulani zinasema hivi: “Ufalme wa Mungu umo ndani yenu.” Je, tafsiri hizo zinatafsiri kwa usahihi maneno ya Yesu? Je, kweli alimaanisha kwamba Ufalme wa Mungu umo ndani ya mioyo ya wanadamu?

Kwanza, fikiria jinsi moyo wa mwanadamu ulivyo. Unapozungumziwa katika Biblia, moyo wa mfano unamaanisha mtu wa ndani, chanzo cha mawazo, mitazamo, na hisia za mtu. Huenda wazo la kwamba kitu kitakatifu kama Ufalme wa Mungu kinaweza kukaa moyoni mwa mwanadamu, katika maana ya kwamba unabadili na kuwaboresha watu likapendeza, lakini je, linapatana na akili?

Biblia inatuambia hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Yesu mwenyewe alisema hivi: “Kutoka ndani, kutoka katika moyo wa watu, hutoka mawazo mabaya: uasherati, wizi, mauaji, uzinzi, kutamani, matendo ya uovu.” (Marko 7:20-22) Fikiria hili: Je, mateso mengi tunayoona ulimwenguni leo hayatoki katika mioyo ya wanadamu yenye dhambi? Hivyo basi, Ufalme mkamilifu wa Mungu ungeweza namna gani kutoka katika chanzo kama hicho? Kwa kweli, moyo wa mwanadamu hauwezi kutokeza Ufalme wa Mungu kama vile tu mchongoma usivyoweza kuzaa tini.—Mathayo 7:16.

Pili, fikiria watu ambao Yesu alikuwa akizungumza nao aliposema maneno hayo yaliyo katika Luka 17:21. Mstari unaotangulia unasema hivi: “Alipoulizwa na Mafarisayo ufalme wa Mungu ungekuja wakati gani, akawajibu.” (Luka 17:20) Mafarisayo walikuwa maadui wa Yesu. Yesu alisema kwamba wanafiki hao hawangeingia katika Ufalme wa Mungu. (Mathayo 23:13) Sasa ikiwa Mafarisayo hawangeingia katika Ufalme wa Mungu, je, Ufalme huo ungekuwa ndani ya mioyo yao? Haiwezekani hata kidogo! Hivyo basi, Yesu alimaanisha nini?

Zinapotafsiri maneno hayo ya Yesu, tafsiri fulani za Biblia zilizo sahihi zinatumia maneno sawa na ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Tafsiri fulani zinasema Ufalme umo “miongoni mwenu” au “kati yenu.” Ufalme wa Mungu ulikuwa jinsi gani katikati ya watu walioishi wakati huo, kutia ndani Mafarisayo? Kumbuka kwamba, Yesu ndiye yule ambaye Yehova Mungu alimweka rasmi awe Mfalme wa Ufalme. Yesu, akiwa Mfalme Aliyechaguliwa, alikuwa papo hapo katikati yao. Alifundisha kuhusu Ufalme wa Mungu na hata akafanya miujiza, ili kuwaonyesha kimbele yale ambayo Ufalme huo utatimiza. Hivyo, katika maana halisi kabisa, Ufalme huo ulikuwa katikati yao.

Kwa wazi, hakuna msingi wowote wa Kimaandiko unaounga mkono wazo la kwamba Ufalme wa Mungu umo ndani ya mioyo ya wanadamu. Badala yake, Ufalme wa Mungu ni serikali halisi ambayo italeta mabadiliko makubwa duniani, kama vile manabii walivyotabiri.—Isaya 9:6, 7; Danieli 2:44.