Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Miaka Mia Moja ya Utawala wa Ufalme!

Miaka Mia Moja ya Utawala wa Ufalme!

“Mungu wa amani . . . awape ninyi vifaa vyema vya kila namna ili kufanya mapenzi yake.”—EBR. 13:20, 21.

NYIMBO: 136, 14

1. Kazi ya kuhubiri ilikuwa muhimu kadiri gani kwa Yesu? Fafanua.

YESU alipenda kuzungumzia Ufalme wa Mungu. Masimulizi ya Biblia yanaonyesha kwamba alizungumzia Ufalme kuliko jambo lingine lolote; aliutaja zaidi ya mara 100 katika huduma yake. Kwa kweli, Ufalme ulikuwa jambo muhimu sana maishani mwake.—Soma Mathayo 12:34.

2. Inaelekea ni watu wangapi walikuwepo Yesu alipotoa amri iliyo kwenye Mathayo 28:19 na 20? Na kwa nini tunafikia mkataa huo? (Tazama maelezo ya chini.)

2 Muda mfupi baada ya kufufuliwa, Yesu alikutana na watu zaidi ya 500, ambao baadaye wangekuwa watangazaji wa Ufalme. (1 Kor. 15:6) Inaelekea hapo ndipo Yesu aliwapa amri ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme kwa “watu wa mataifa yote,” kazi iliyokuwa kubwa sana wakati huo. * Yesu alitabiri kwamba kazi hiyo ingeendelea kufanywa mpaka “umalizio wa mfumo wa mambo,” na hivyo ndivyo ilivyo leo. Kwa hiyo, unapohubiri habari njema, unashiriki kutimiza utume na unabii huo.—Mt. 28:19, 20.

3. Ni mambo gani matatu yametusaidia tutimize utume wa kuhubiri habari njema?

3 Baada ya kutoa utume huo wa kuhubiri, Yesu aliwaahidi hivi wafuasi wake: “Mimi nipo pamoja nanyi.” (Mt. 28:20) Hivyo, kazi hiyo kubwa ya kuhubiri ingefanywa chini ya mwongozo wake. Mungu wetu ametupatia “vifaa vyema vya kila namna” ili kutusaidia tutimize utume huo. (Ebr. 13:20, 21) Katika makala hii, tutazungumzia mambo matatu: (1) vifaa ambavyo tumepewa, (2) njia ambazo tumetumia, na (3) mazoezi ambayo tumepata. Kwanza, acheni tufikirie baadhi ya vifaa ambavyo tumetumia katika miaka 100 iliyopita.

MFALME AWAPA VIFAA WATUMISHI WAKE ILI WAHUBIRI

4. Kwa nini tumetumia vifaa mbalimbali katika kazi yetu ya kuhubiri?

4 Yesu alilinganisha “neno la ufalme” na mbegu ambayo imepandwa katika aina mbalimbali za udongo. (Mt. 13:18, 19) Mkulima anaweza kutumia aina mbalimbali za vifaa ili kutayarisha shamba lake kwa ajili ya kupanda mbegu. Vivyo hivyo, Mfalme wetu ametupatia vifaa vinavyotusaidia kutayarisha mioyo ya watu ili wakubali ujumbe wa Ufalme. Baadhi ya vifaa vilitumika kwa miaka michache ilhali vingine vinatumika mpaka leo. Lakini vifaa vyote hivyo vimetusaidia kuboresha ustadi wetu wa kuhubiri.

5. Kadi ya ushuhuda ni nini? Na ilitumiwa jinsi gani?

5 Kifaa kimoja ambacho kiliwasaidia wengi waanze kuhubiri ni kadi ya ushuhuda, ambayo ilianza kutumiwa mwaka wa 1933. Kadi hiyo ilikuwa na ukubwa wa sentimeta 8 kwa 13, na ilikuwa na ujumbe mfupi wa Biblia. Kadi yenye ujumbe mpya wa Biblia ilitolewa kila baada ya muda fulani. Ilikuwa rahisi sana kutumia kadi hiyo! C. W. Erlenmeyer alikuwa na umri wa miaka kumi hivi alipohubiri kwa mara ya kwanza kwa kutumia njia hii. Alieleza hivi: “Utangulizi uliotumika ulikuwa, ‘Naomba usome kadi hii tafadhali!’ Baada ya mwenye nyumba kumaliza kusoma, tungempa machapisho na kuondoka.”

6. Kadi ya ushuhuda iliwasaidiaje wahubiri?

6 Kadi ya ushuhuda iliwasaidia wahubiri katika njia mbalimbali. Wahubiri fulani walitamani sana kuhubiri lakini walikuwa wenye haya na hawakujua jambo la kusema. Wengine walikuwa na mambo mengi ya kusema. Wangemweleza mwenye nyumba kila jambo walilojua kwa dakika chache tu, hata hivyo si mara zote njia yao ilikuwa yenye busara. Tofauti na hilo, kadi ya ushuhuda ilikuwa na ujumbe rahisi na unaoeleweka, hivyo ni kana kwamba “ilizungumza” kwa niaba ya mhubiri.

7. Wahubiri walikabili changamoto gani walipokuwa wakitumia kadi ya ushuhuda?

7 Njia hiyo ilikuwa na changamoto zake pia. Grace A. Estep, ambaye alimtumikia Yehova kwa miaka mingi alikumbuka hivi: “Nyakati nyingine tuliulizwa, ‘Kadi hiyo inasema nini? Huwezi tu kunieleza kile inachosema?’” Isitoshe, baadhi ya wenye nyumba hawangeweza kusoma ujumbe uliokuwa kwenye kadi. Wengine walifikiri kuwa tunawapa kadi hiyo, hivyo waliichukua na kufunga mlango. Ikiwa tungemkuta mwenye nyumba anayepinga vikali ujumbe wetu, basi angeichanachana kadi hiyo. Hata hivyo, ndugu zetu walijifunza jinsi ya kuwahubiria watu na kujitambulisha waziwazi kuwa wahubiri wa Ufalme.

8. Eleza jinsi gramafoni ilivyotumika. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

8 Gramafoni ni kifaa kingine kilichotumiwa katika miaka ya 1930 na mwanzoni mwa miaka ya 1940. Baadhi ya akina ndugu waliipa jina la utani Haruni, kwa sababu mashine hiyo ilizungumza kwa niaba yao. (Soma Kutoka 4:14-16.) Ikiwa mwenye nyumba angekubali kusikiliza, basi mhubiri angecheza hotuba ya Biblia ya dakika nne na nusu, kisha angemwachia machapisho kadhaa. Nyakati nyingine, familia zilikusanyika ili kusikiliza ujumbe wa Biblia uliorekodiwa. Mwaka wa 1934, Shirika la Watch Tower Society lilianza kutengeneza gramafoni zilizobebeka kwa urahisi ili zitumiwe katika huduma. Hatimaye, akina ndugu walirekodi hotuba 92 zilizozungumzia mambo mbalimbali.

9. Gramafoni ilikuwa na matokeo gani?

9 Mwenye nyumba mmoja aitwaye Hillary Goslin aliposikia hotuba za Biblia zilizorekodiwa, alimwomba mhubiri amwachie gramafoni yake kwa juma moja ili awaeleze jirani zake ujumbe huo wa Ufalme. Mhubiri huyo aliporudi, alikuta watu kadhaa waliopenda ujumbe wa Ufalme wakimsubiri. Baada ya muda, baadhi yao walijiweka wakfu kwa Yehova, na mabinti wawili wa Hillary walihudhuria Shule ya Gileadi na kupewa mgawo wa kutumikia wakiwa wamishonari. Kama vile kadi ya ushuhuda, gramafoni pia iliwasaidia wengi waanze kuhubiri. Baadaye, Mfalme angetumia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kuwafundisha watu wake jinsi ya kuhubiri.

KUTUMIA KILA NJIA KUWAFIKIA WATU

10, 11. Watu wa Mungu walitumiaje magazeti na redio kuwafikishia watu kweli za Biblia? Na njia hizo zilikuwa na matokeo gani?

10 Chini ya mwongozo wa Mfalme, watu wa Mungu wametumia njia mbalimbali ili kuwafikishia watu habari njema. Jambo hilo lilikuwa muhimu hasa kulipokuwa na ‘wafanyakazi wachache.’ (Soma Mathayo 9:37.) Mwanzoni mwa karne ya 20, magazeti ya habari yalitumiwa kuwafikia watu wengi katika maeneo ambayo watu wa Yehova walikuwa wachache. Kila juma Charles Taze Russell alituma hotuba ya Biblia katika shirika fulani la magazeti. Kisha, shirika hilo lilituma hotuba hiyo katika magazeti nchini Marekani, Kanada, na Ulaya. Inakadiriwa kwamba kufikia mwaka wa 1913, hotuba za Ndugu Russell ziliwafikia wasomaji 15,000,000 kupitia magazeti 2,000!

11 Baada ya kifo cha Ndugu Russell, njia nyingine ya kueneza habari njema ilianza kutumika. Aprili 16, 1922, Joseph F. Rutherford alitoa moja kati ya hotuba zake za kwanza katika kituo cha redio, na inakadiriwa kwamba watu 50,000 walisikiliza hotuba hiyo. Kisha, Februari 24, 1924, kituo cha kwanza cha redio (WBBR) kilichomilikiwa na tengenezo, kilianza kurusha matangazo yake. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Desemba 1, 1924, lilisema hivi kuhusu njia hiyo mpya ya kuhubiri: “Tunaamini kwamba kati ya mbinu zote ambazo zimewahi kutumiwa, redio ndiyo njia isiyogharimu pesa nyingi na yenye matokeo mazuri zaidi katika kueneza ujumbe wa kweli.” Kama magazeti, redio pia ilitusaidia kuwafikia watu wengi katika maeneo ambayo yalikuwa na wahubiri wachache wa Ufalme.

Wahubiri wengi wa Ufalme wanafurahia mahubiri ya hadharani na kuwaelekeza watu kwenye tovuti yetu, jw.org (Tazama fungu la 12 na 13)

12. (a) Ni sehemu gani ya mahubiri ya hadharani unayofurahia zaidi? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia tushinde woga wa kushiriki katika mahubiri ya hadharani?

12 Leo, nguvu nyingi zimeelekezwa kwenye mahubiri ya hadharani: katika vituo vya mabasi na treni, maeneo ya umma, maegesho ya magari, na kwenye masoko. Je, kushiriki katika mahubiri ya hadharani kunakufanya uwe na wasiwasi? Basi sali na utafakari kile ambacho Angelo Manera, Jr., mwangalizi wa mzunguko ambaye ametumikia kwa muda mrefu, alisema: “Tuliona kushiriki katika kila njia mpya ya kuhubiri kuwa fursa nyingine ya kumtumikia Yehova, fursa nyingine ya kuonyesha ushikamanifu wetu kwake, jaribu lingine la uaminifu wetu, na tulikuwa na hamu kubwa ya kuthibitisha kwamba tuko tayari kumtumikia Yehova kwa njia yoyote anayotaka.” Kushiriki katika njia mpya ya kuhubiri, hata kama hatuifurahii, kunatusaidia tumtumaini na kumwamini zaidi Yehova, na kuendelea kukomaa kiroho.—Soma 2 Wakorintho 12:9, 10.

13. Tovuti yetu imekuwa na matokeo gani? Nawe umejionea mambo gani kwa kuwaelekeza watu kwenye tovuti hiyo?

13 Wahubiri wengi hufurahia kuwaelekeza watu kwenye tovuti yetu, jw.org, ambapo wanaweza kusoma na kupakua machapisho katika lugha zaidi ya 700. Kila siku, zaidi ya watu milioni 1.6 hutembelea tovuti yetu. Kama vile redio, tovuti yetu inawasaidia watu kila mahali kupata habari njema.

KUWAZOEZA WAHUDUMU WA HABARI NJEMA

14. Wahubiri wa Ufalme walihitaji mazoezi gani? Na ni shule gani imewasaidia wawe walimu stadi?

14 Tumezungumzia vifaa na njia chache ambazo zimetumiwa kueneza habari njema. Hata hivyo, wahudumu wamepokea mazoezi gani? Wazia ikiwa mwenye nyumba angepinga mambo aliyosikia kwenye gramafoni au angefurahishwa na ujumbe aliosoma kwenye kadi ya ushuhuda. Wahubiri walihitaji kujua jinsi ya kuzungumza kwa busara na watu waliopinga ujumbe wetu, na jinsi ya kuwafundisha kwa ustadi watu wanyofu. Bila shaka, roho ya Mungu ilimchochea Nathan H. Knorr aone uhitaji wa kuwazoeza wahubiri ili wajue jinsi ya kuzungumza na wenye nyumba katika huduma. Hivyo, mwaka wa 1943, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ilianzishwa makutanikoni. Shule hiyo imetusaidia tuwe walimu stadi.

15. (a) Wanafunzi fulani walikabili hali gani walipokuwa wakitoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? (b) Ni kwa njia gani umejionea utimizo wa ahadi ya Yehova iliyo kwenye Zaburi 32:8?

15 Ilichukua muda kwa wahubiri wengi kuzoea kuzungumza mbele ya watu. Julio S. Ramu alikumbuka hotuba yake ya kwanza aliyotoa mwaka wa 1944. Katika hotuba hiyo, alimzungumzia Doegi, mwanaume anayetajwa katika mistari minne tu ya Biblia! Julio alisema hivi: “Magoti yangu yaligongana gongana, mikono ilitetemeka, na meno yaligongana gongana.” Mbali na hilo, alihitaji kutayarisha hotuba nzima kwa kutumia mistari hiyo minne tu. Julio aliongeza hivi: “Nilitoa hotuba yangu kwa dakika tatu. Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kutoa hotuba jukwaani, lakini sikukata tamaa.” Watoto pia walijiunga na shule hiyo, hata ingawa haikuwa rahisi kwa baadhi yao kutoa hotuba kutanikoni. Angelo Manera, aliyetajwa awali, alikumbuka hotuba ya kwanza iliyotolewa na mvulana mdogo aliyetoka tu kuanza shule ya msingi. Alisema hivi: “Alikuwa na wasiwasi mwingi sana hivi kwamba alipoanza kutoa hotuba yake, alianza kutokwa na machozi. Lakini kwa kuwa aliazimia kuitoa, alitokwa na machozi mpaka mwisho wa hotuba.” Je, umewahi kushindwa kujibu au kutimiza mgawo fulani kwa sababu ya aibu au kuhisi kwamba huwezi kufanya hivyo? Mwombe Yehova akusaidie ushinde woga. Utaona jinsi Yehova atakavyokusaidia kama tu alivyowasaidia wanafunzi wa mapema wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.—Soma Zaburi 32:8.

16. (a) Shule ya Gileadi ilitimiza nini zamani? (b) Shule hiyo imetimiza nini tangu mwaka 2011?

16 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni moja tu kati ya shule ambazo zimekusudiwa kuwazoeza watu wa Yehova. Wamishonari na wahubiri wengine wamefaidika sana kwa kuhudhuria Shule ya Gileadi. Mwalimu mmoja wa Gileadi alisema kwamba kusudi la shule hiyo ni “kuchochea tamaa ya wanafunzi ili wawe waeneza injili wenye bidii.” Shule ya Gileadi ilianzishwa mwaka wa 1943, na tangu wakati huo wanafunzi zaidi ya 8,500 wamezoezwa na kutumwa katika nchi 170 hivi. Tangu mwaka 2011, wanaoalikwa katika shule hiyo ni wale tu walio katika utumishi wa pekee wa wakati wote, yaani, mapainia wa pekee, waangalizi wa mzunguko, Wanabetheli, au wamishonari ambao bado hawajahudhuria.

17. Mazoezi ya Shule ya Gileadi yamekuwa na matokeo gani?

17 Mazoezi ya Shule ya Gileadi yamekuwa na matokeo gani? Fikiria mfano mmoja. Mnamo Agosti 1949, kulikuwa na wahubiri wasiozidi kumi nchini Japani. Kufikia mwishoni mwa mwaka huo, kulikuwa na wamishonari 13 kutoka Gileadi wakihubiri kwa bidii. Leo, kuna wahubiri 216,000 hivi nchini Japani, na karibu nusu ya wahubiri ni mapainia!

18. Taja shule nyingine ambazo zimewasaidia watu wa Yehova wakue kiroho.

18 Shule nyingine, kama vile Shule ya Huduma ya Ufalme, Shule ya Utumishi wa Painia, Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, Shule ya Waangalizi wa Mzunguko na Wake Zao, na Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Wake Zao, zimeboresha sana hali ya kiroho na ustadi wa watu wa Yehova. Bila shaka, Mfalme anaendelea kuwazoeza watu wake!

19. Charles Taze Russell alisema nini kuhusu kazi ya kuhubiri? Na maneno yake yametimiaje?

19 Zaidi ya miaka 100 imepita tangu Ufalme wa Mungu uanze kutawala. Mfalme wetu, Yesu Kristo, anaendelea kutuzoeza. Muda mfupi kabla ya kifo chake mwaka wa 1916, Charles Taze Russell aliamini kwamba habari njema ingehubiriwa katika dunia yote. Alimwambia hivi mshirika wake wa karibu: “Kazi inaongezeka kwa kasi sana, na itaendelea kuongezeka, kwa kuwa kuna kazi inayohitaji kufanywa ulimwenguni pote ya kuhubiri ‘injili ya ufalme.’” (Faith on the March, cha A. H. Macmillan, uku. 69) Ndugu Russell alikuwa sahihi kabisa! Tunamshukuru sana Mungu wa amani ambaye anaendelea kutupatia vifaa tunavyohitaji ili tufanye kazi hii inayotupatia shangwe kubwa. Naam, anatupatia “vifaa vyema vya kila namna” ambavyo tunahitaji ili tufanye mapenzi yake!

^ fu. 2 Kuna sababu ya kuamini kwamba watu wengi waliokuwepo wakati huo walikuja kuwa Wakristo. Katika barua yake kwa Wakorintho, Paulo anawaita “ndugu zaidi ya mia tano.” Isitoshe, anaongeza hivi: “Walio wengi kati yao wapo mpaka sasa, lakini wengine wamelala usingizi katika kifo.” Hivyo, inaonekana kwamba Paulo na Wakristo wengine wa karne ya kwanza waliwajua watu wengi waliosikia moja kwa moja amri hiyo ilipotolewa.