Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

KUTOKA KATIKA HIFADHI YA VITU VYETU VYA KALE

“Msiruhusu Kitu Chochote Chini ya Jua Kiwazuie!”

“Msiruhusu Kitu Chochote Chini ya Jua Kiwazuie!”

ULIKUWA wakati wa majira ya kuchipua ya mwaka wa 1931. Wajumbe kutoka nchi 23 walimiminika katika ukumbi maarufu wa burudani wa Pleyel jijini Paris. Magari yalishusha watu waliovaa vizuri mbele ya ukumbi, na punde si punde ukumbi ukajaa. Watu 3,000 hivi walikuja, si ili kuhudhuria tamasha la muziki, bali kusikiliza hotuba ya Joseph F. Rutherford, aliyekuwa akiongoza kazi yetu ya kuhubiri wakati huo. Hotuba zake zenye kusisimua zilitafsiriwa katika Kifaransa, Kijerumani, na Kipolandi. Sauti nzito ya Ndugu Rutherford ilisikika katika ukumbi wote.

Kusanyiko hilo lilikuwa muhimu sana katika historia ya kazi ya kuhubiri nchini Ufaransa. Ndugu Rutherford alitoa wito kwa wahudhuriaji, hasa vijana Wakristo, watumikie wakiwa makolpota nchini Ufaransa. John Cooke, kijana aliyetoka Uingereza, hakusahau himizo hili lenye kusisimua: “Msiruhusu kitu chochote chini ya jua kiwazuie ninyi vijana kuwa makolpota!” *

Zaidi ya John Cooke, ambaye baadaye alikuwa mmishonari, wengine wengi waliitikia himizo hilo la kwenda Makedonia. (Mdo. 16:9, 10) Kwa kweli, idadi ya makolpota nchini Ufaransa iliongezeka kutoka makolpota 27 mwaka wa 1930, hadi makolpota 104 mwaka wa 1931. Hilo lilikuwa ongezeko la pekee ndani ya mwaka mmoja. Kwa kuwa wengi wa mapainia hao hawakujua Kifaransa, wangekabilianaje na changamoto ya lugha, hali ngumu ya kiuchumi, na upweke?

KUKABILIANA NA CHANGAMOTO YA LUGHA

Makolpota wageni walitegemea kadi za ushuhuda ili kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Ndugu kutoka Ujerumani ambaye alihubiri kwa ujasiri jijini Paris anakumbuka hivi: “Tulijua kwamba Mungu wetu ana nguvu. Mioyo yetu ilipodunda kwa woga tulipokuwa utumishi, haikuwa kwa sababu ya kuwaogopa wanadamu, bali kwa sababu ya kuogopa kusahau maneno haya: ‘Voulez-vous lire cette carte, s’il vous plaît? [Naomba usome kadi hii tafadhali.]’ Tulikuwa na uhakika kwamba kazi yetu ilikuwa muhimu sana.”

Makolpota walitumia baiskeli na pikipiki kueneza habari njema nchini Ufaransa

Walipokuwa wakihubiri katika majengo ya ghorofa yenye wapangaji, mara nyingi makolpota walifukuzwa na walinzi. Siku moja, dada wawili Waingereza wasiojua vizuri Kifaransa walikutana na mlinzi mwenye hasira, ambaye aliwauliza wanataka kumwona nani. Walipokuwa wakijaribu kumtuliza mlinzi huyo, dada mmoja aliona kibandiko fulani mlangoni. Kilikuwa na maneno haya: “Tournez le bouton [Bonyeza kengele].” Akidhani kwamba hilo ni jina la mwenye nyumba, dada huyo alisema hivi kwa shauku: “Tumekuja kumtembelea ‘Tournez le bouton.’” Jambo hilo lenye kuchekesha liliwasaidia sana makolpota hao wenye bidii!

HAWAKUVUNJWA MOYO NA HALI NGUMU YA KIUCHUMI WALA UPWEKE

Miaka ya 1930, watu wengi nchini Ufaransa walikuwa na hali ngumu ya kiuchumi, na makolpota wageni walikabili hali hiyo pia. Mona Brzoska, painia kutoka Uingereza, alieleza hali ngumu ambayo yeye na painia mwenzake walikabili. Alisema hivi: “Kwa ujumla nyumba tulizoishi zilikuwa mbaya, na ilikuwa vigumu sana kuzipasha joto katika majira ya baridi kali. Mara nyingi tulilazimika kuishi katika chumba chenye baridi kali, ambapo asubuhi tulihitaji kuvunja mabonge ya barafu ili kupata maji ya kunawa.” Je, hali hiyo ngumu iliwavunja moyo mapainia hao? La hasha! Mmoja wao alieleza hivi: “Hatukuwa na kila kitu, lakini hatukukosa chochote.”—Mt. 6:33.

Mapainia kutoka Uingereza waliohudhuria kusanyiko jijini Paris mwaka wa 1931

Makolpota hao jasiri walihitaji pia kushinda tatizo la upweke. Mwanzoni mwa miaka ya 1930, idadi ya wahubiri wa Ufalme nchini Ufaransa haikuzidi watu 700, na wengi kati yao walitawanyika katika maeneo mbalimbali nchini humo. Ni nini kilichowasaidia makolpota hao kudumisha shangwe yao? Mona, dada aliyekabili changamoto hiyo akiwa na painia mwenzake, alieleza hivi: “Tulihitaji kupambana na upweke kwa kujifunza kwa ukawaida machapisho ya Sosaiti. Kwa kuwa siku hizo [hatukufanya ziara za kurudia wala kuongoza mafunzo ya Biblia], tulitumia wakati wa jioni kuwaandikia barua watu wa familia na mapainia wengine, ili kusimulia mambo yaliyoonwa na kutiana moyo.”—1 The. 5:11.

Makolpota hao waliojidhabihu walidumisha mtazamo mzuri licha ya hali ngumu. Mtazamo wao mzuri ulionekana wazi katika barua walizoandikia ofisi ya tawi miaka mingi baada ya kufanya upainia nchini Ufaransa. Akikumbuka wakati huo, Annie Cregeen, dada mtiwa-mafuta aliyesafiri maeneo mengi nchini Ufaransa pamoja na mume wake, kuanzia mwaka wa 1931 hadi 1935, aliandika hivi: “Tulikuwa na maisha yenye furaha na yenye mambo mengi! Tukiwa mapainia, tulishirikiana kwa ukaribu. Ni kama tu mtume Paulo alivyosema, ‘Mimi nilipanda, Apolo akatia maji, lakini Mungu akaendelea kuikuza.’ Tunafurahia sana jambo hilo kwa kuwa tulipata fursa ya kuwasaidia watu wengi.”—1 Kor. 3:6.

Kwa kweli, mapainia hao wa zamani waliacha historia nzuri ya uvumilivu na bidii kwa wote wanaotaka kuongeza utumishi wao. Leo, kuna mapainia wa kawaida 14,000 hivi nchini Ufaransa. Wengi wao wanatumikia katika vikundi au makutaniko ya lugha za kigeni. * Kama mapainia waliowatangulia, wao pia hawaruhusu kitu chochote chini ya jua kiwazuie!—Kutoka katika hifadhi ya vitu vyetu vya kale nchini Ufaransa.

^ fu. 4 Kuhusu kazi ya kuhubiri iliyofanywa na Wapolandi waliohamia nchini Ufaransa, tazama makala yenye kichwa “Yehova Aliwaleta Ufaransa ili Mjifunze Kweli,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 15, 2015.

^ fu. 13 Mwaka 2014, kulikuwa na makutaniko na vikundi zaidi ya 900 vya lugha za kigeni katika eneo linalosimamiwa na ofisi ya tawi ya Ufaransa, vikiwasaidia watu wanaozungumza lugha zipatazo 70 wajifunze kweli.