Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Wengine Kufanya Yote Wawezayo

Wasaidie Wengine Kufanya Yote Wawezayo

“Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”ZAB. 32:8.

1, 2. Yehova ana maoni gani kuhusu watumishi wake duniani?

WAZAZI wanapowatazama watoto wao wakicheza, kwa kawaida wanashangaa kuona uwezo wao wa kiasili. Je, umejionea jambo hilo? Huenda ikaonekana kwamba mtoto mmoja atakuwa mwanariadha hodari, na mwingine atakuwa msanii stadi. Hata hivyo, licha ya kwamba watoto hao wana vipaji tofauti, wazazi huthamini uwezo wao mbalimbali.

2 Yehova pia anapendezwa kabisa na watoto wake duniani. Anawaona watumishi wake leo kuwa “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote.” (Hag. 2:7) Ni wenye kutamanika hasa kwa sababu ya imani na ujitoaji wao. Hata hivyo, huenda umegundua kwamba Mashahidi wenzetu leo wana vipaji mbalimbali. Baadhi ya ndugu wana kipaji cha kuwahutubia watu, ilhali wengine ni stadi katika kupanga mambo. Dada wengi wana uwezo wa kujifunza lugha za kigeni haraka na kuzitumia katika huduma, ilhali wengine wanaweka vielelezo bora katika kuwategemeza wale wanaohitaji kitia-moyo au kuwatunza wagonjwa. (Rom. 16:1, 12) Je, hatuthamini kuwa na Wakristo hao wote kutanikoni?

3. Ni maswali gani tutakayozungumzia katika makala hii?

 3 Hata hivyo, baadhi ya waamini wenzetu, kutia ndani vijana au ndugu na dada waliobatizwa hivi karibuni, huenda wanahisi kwamba hawawezi kutimiza mengi kutanikoni. Tunawezaje kuwasaidia kufanya yote wawezayo? Kwa nini tunapaswa kujitahidi kutafuta sifa zao nzuri na hivyo kuwaona kama Yehova anavyowaona?

YEHOVA HUONA SIFA NZURI ZA WATUMISHI WAKE

4, 5. Simulizi la Waamuzi 6:11-16 linaonyeshaje kwamba Yehova huona uwezo wa watumishi wake?

4 Masimulizi mengi ya Biblia yanaonyesha wazi kwamba Yehova haoni tu sifa nzuri za watumishi wake bali pia mambo wanayoweza kutimiza. Kwa mfano, Gideoni alipochaguliwa ili awaokoe Waisraeli kutokana na uonevu wa Wamidiani, ni wazi kwamba alishangaa malaika alipomwambia hivi: “Yehova yupo pamoja nawe, Ee mwanamume shujaa na mwenye nguvu.” Ni wazi kwamba Gideoni hakujiona kamwe kuwa “mwenye nguvu” wakati huo. Alikiri kwamba hana uwezo wa kuwaokoa watu wa Mungu. Lakini kama mazungumzo yaliyofuata yalivyofunua, bila shaka Yehova aliona kwamba Gideoni angeweza kufanya hivyo ingawa yeye alijiona hafai.Soma Waamuzi 6:11-16.

5 Yehova alikuwa na hakika kwamba Gideoni angewaokoa Waisraeli kwa sababu Aliona ustadi wake. Kwanza, malaika wa Yehova aliona jinsi Gideoni alivyopura ngano kwa nguvu zake zote. Pia, malaika huyo aliona jambo lingine. Katika nyakati za Biblia, kwa kawaida wakulima walipepeta nafaka mahali palipo wazi ili makapi yapeperushwe na upepo. Inashangaza kwamba Gideoni alipepeta ngano yake kwa siri katika shinikizo la divai ili Wamidiani wasione kiasi kidogo alichovuna. Alitumia mbinu ya werevu sana! Ndiyo sababu Yehova alimwona Gideoni kuwa mkulima mwenye busara—mtu mwerevu. Naam, Yehova aliona uwezo wake na kumsaidia kuutumia.

6, 7. (a) Maoni ya Yehova kuhusu nabii Amosi yalitofautianaje na maoni ya Waisraeli fulani? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Amosi alikuwa mtu mwenye elimu?

6 Vivyo hivyo, ni wazi kwamba Yehova alitambua uwezo wa mtumishi wake, nabii Amosi, hata ingawa huenda alionwa na wengi kuwa mtu duni au wa hali ya chini. Amosi alisema kwamba yeye ni mchungaji wa kondoo na mminyaji wa tini za mikuyu zilizoonwa kuwa chakula cha maskini. Yehova alipomchagua Amosi kuonya ufalme wa Israeli wa makabila kumi, huenda Waisraeli fulani walifikiri kwamba Mungu alichagua mtu asiyestahili.Soma Amosi 7:14, 15.

7 Amosi alitoka katika kijiji cha mashambani, lakini alijua mengi kuhusu desturi na watawala wa wakati huo. Inaelekea kwamba alijua vizuri hali katika Israeli, na huenda alijua mengi kuhusu mataifa jirani kwa sababu ya kushughulika na wafanyabiashara waliotoka nchi nyingine. (Amo. 1:6, 9, 11, 13; 2:8; 6:4-6) Wasomi fulani wa Biblia wanasema kwamba Amosi alikuwa mwandishi stadi. Nabii huyo alichagua maneno rahisi na yenye nguvu na pia alitumia vizuri mifano na tamathali za usemi. Amosi alimjibu kwa ujasiri kuhani Amazia aliyekuwa mwovu, na hivyo kuthibitisha kwamba Yehova alichagua mtu anayefaa, aliyetumia uwezo wake ambao haukuonekana waziwazi mwanzoni.Amo. 7:12, 13, 16, 17.

8. (a) Yehova alimhakikishia nini Daudi? (b) Kwa nini maneno ya Zaburi 32:8 yanawatia moyo wale wanaohisi kwamba hawastahili au hawana ustadi?

8 Naam, Yehova huona uwezo wa kila  mmoja wa watumishi wake. Alimhakikishia Mfalme Daudi kwamba angemwongoza daima ‘jicho Lake likiwa linamtazama.’ (Soma Zaburi 32:8.) Je, unaona kwa nini maneno hayo yanapaswa kututia moyo? Hata ingawa huenda tukahisi kwamba hatustahili, Yehova anaweza kutusaidia kutimiza mambo tuliyofikiri hatuwezi kamwe kufanya. Yehova yuko tayari kutuongoza tunapofanya maendeleo ya kiroho kama vile mwalimu anavyomsaidia kwa makini mwanafunzi asiye na uzoefu kufanya maendeleo hatua kwa hatua. Huenda Yehova akawatumia pia waamini wenzetu kutusaidia kufanya yote tuwezayo. Jinsi gani?

TAFUTA SIFA NZURI ZA WENGINE

9. Tunawezaje kutumia shauri la Paulo la ‘kuendelea kuangalia’ faida za wengine?

9 Paulo aliwahimiza Wakristo wote ‘waendelee kuangalia’ faida za waamini wenzao. (Soma Wafilipi 2:3, 4.) Paulo anatushauri tutambue vipaji vya wengine na kuwapongeza. Tunahisije mtu anapoona maendeleo tunayofanya na kutupongeza? Kwa kawaida, tunachochewa kufanya maendeleo zaidi na kujitahidi kadiri tuwezavyo. Vivyo hivyo, tunapothamini jitihada za waamini wenzetu, tunawasaidia kusitawi na kukua kiroho.

10. Ni nani hasa anayehitaji uangalifu wetu?

10 Ni nani hasa anayehitaji uangalifu wetu? Bila shaka, sote tunahitaji uangalifu wa pekee mara kwa mara. Hata hivyo, tunahitaji kuwafanya watoto au ndugu na dada waliobatizwa karibuni kuhisi kwamba wanahusishwa katika utendaji wa kutaniko. Hilo litawasaidia kuona kwamba kwa kweli wao pia ni sehemu ya kutaniko. Hata hivyo, tusipowaonyesha kwamba tunawathamini, huenda wakavunjika moyo na kutojitahidi kufikia mapendeleo zaidi kama Neno la Mungu linavyowahimiza wafanye.1 Tim. 3:1.

11. (a) Mzee mmoja alimsaidiaje kijana aliyekuwa mwenye haya? (b) Unajifunza nini kutokana na kisa cha Julien?

11 Ludovic, mzee wa kutaniko aliyefanya maendeleo baada ya kuonyeshwa upendezi kama huo akiwa kijana, anasema hivi: “Ninapopendezwa kikweli na ndugu, anafanya maendeleo ya haraka zaidi.” Ludovic anasema hivi kuhusu Julien, kijana aliyekuwa mwenye haya: “Nyakati nyingine Julien alitenda kwa njia isiyofaa ili atambuliwe. Lakini niliona kwamba alikuwa mwenye fadhili sana na alitamani kuwasaidia wengine kutanikoni. Hivyo, badala ya kutilia shaka nia yake, nilikazia fikira sifa zake nzuri, na kujitahidi kumtia moyo.” Baada ya muda, Julien alistahili kuwa mtumishi wa huduma, na sasa anatumika akiwa painia wa kawaida.

WASAIDIE KUFANYA YOTE WAWEZAYO

12. Tunahitaji sifa gani yenye thamani ili kumsaidia mtu afanye yote awezayo? Toa mfano.

12 Ni kweli kwamba ili tuwasaidie wengine kufanya yote wawezayo, tunahitaji kuwa na utambuzi. Kama mfano wa Julien unavyoonyesha, ili tutambue sifa nzuri na ustadi unaoweza kusitawishwa, huenda tukahitaji kutokazia fikira udhaifu wa wengine. Hivyo ndivyo Yesu alivyoshughulika na mtume Petro. Ingawa nyakati nyingine Petro alionekana hategemeki, Yesu alimpa jina Kefa au Petro kuonyesha kwamba angekuwa imara kama mwamba.Yoh. 1:42.

13, 14. (a) Barnaba alionyeshaje utambuzi kuhusiana na kijana Marko? (b) Ndugu mmoja kijana alinufaikaje aliposaidiwa kama Marko? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 28.)

13 Barnaba alionyesha utambuzi kama huo aliposhughulika na Yohana, aliyeitwa Marko katika Kiroma. (Mdo. 12:25) Paulo alipoandamana na Barnaba katika safari yake ya kwanza ya umishonari, Marko alikuwa “akiwatumikia,” labda aliwasaidia  kufanya kazi za nyumbani. Hata hivyo, walipofika Pamfilia, kwa ghafla Marko aliwaacha na kwenda zake. Walilazimika kusafiri bila Marko kwenda kaskazini kupitia eneo lililojaa wanyang’anyi. (Mdo. 13:5, 13) Hata hivyo, inaonekana kwamba Barnaba alikazia fikira sifa nzuri za Marko badala ya udhaifu wake, na baadaye alitumia nafasi aliyopata kumzoeza kikamili. (Mdo. 15:37-39) Mazoezi hayo yalimsaidia kijana huyo kuwa mtumishi mkomavu wa Yehova. Miaka mingi baadaye, Marko alikuwa Roma pamoja na Paulo, aliyekuwa mfungwa. Marko aliwatumia pia salamu Wakristo wa kutaniko la Kolosai, na mtume Paulo alimsifu. (Kol. 4:10) Wazia jinsi Barnaba alivyofurahi Paulo alipoomba Marko aende kumsaidia.2 Tim. 4:11.

14 Alexandre, aliyewekwa hivi karibuni kuwa mzee wa kutaniko, anakumbuka jinsi ndugu mmoja mwenye utambuzi alivyomsaidia: “Nilipokuwa kijana, niliogopa sana kusali hadharani. Mzee akanionyesha jinsi ya kujitayarisha na kupata utulivu zaidi. Badala ya kuninyima pendeleo la kutoa sala, alinipa nafasi za kusali kwa ukawaida kwenye mikutano ya utumishi wa shambani. Baada ya muda, nikapata ujasiri zaidi.”

15. Paulo alionyeshaje kwamba aliwathamini ndugu zake?

15 Tunapoona sifa nzuri ya Mkristo mwenzetu, je, tunamwambia jinsi tunavyoithamini sifa hiyo? Katika Waroma sura ya 16, Paulo aliwapongeza waamini wenzake zaidi ya 20 na kutaja sifa zao zilizofanya awapende kutoka moyoni. (Rom. 16:3-7, 13) Kwa mfano, Paulo alikiri kwamba Androniko na Yunia walimtumikia Kristo kwa muda mrefu kuliko yeye, akikazia uvumilivu wao wa Kikristo. Paulo alimsifu pia mama ya Rufu, labda kwa sababu alimtunza kwa upendo.

Frédéric (kushoto) alimtia moyo Rico kuendelea kumtumikia Yehova (Tazama fungu la 16)

16. Kumpongeza kijana kunaweza kumchochea jinsi gani?

16 Tukiwapongeza wengine kutoka moyoni tunaweza kuwachochea kufanya maendeleo. Mfikirie Rico, mvulana mdogo huko Ufaransa. Rico alivunjika moyo kwa sababu baba yake ambaye hakuwa Shahidi hakutaka abatizwe. Rico alifikiri kwamba angelazimika kungoja afikie umri wa miaka 18 ili amtumikie Yehova kikamili. Alihuzunika pia kwa sababu alidhihakiwa shuleni. Frédéric, mzee wa kutaniko aliyeombwa ajifunze Biblia na mvulana huyo anasema hivi: “Nilimpongeza Rico na kumwambia kwamba alipingwa kwa sababu alitetea imani yake kwa ujasiri.” Maneno hayo yalimsaidia Rico kuazimia kuendelea kufanya maendeleo na kudumisha urafiki na baba yake. Rico alibatizwa akiwa na umri wa miaka 12.

Jérôme (kulia) alimsaidia Ryan kustahili kuwa mmishonari (Tazama fungu la 17)

17.(a) Tunawezaje kuwasaidia ndugu zetu kufanya maendeleo? (b) Mmishonari mmoja alipendezwa kibinafsi jinsi gani na ndugu vijana, na matokeo yalikuwa nini?

17 Kila mara tunapowapongeza waamini wenzetu wanapojitahidi au wanapotimiza vizuri migawo yao, tunawachochea  kumtumikia Yehova kikamili zaidi. Sylvie, * ambaye amekuwa akitumika katika Betheli ya Ufaransa kwa miaka mingi, alisema kwamba dada wanahitaji pia kuwapongeza akina ndugu. Alisema kwamba mara nyingi akina dada huona na kuthamini jitihada au mambo madogo-madogo. Hivyo, “wanaweza kujiunga na ndugu wenye uzoefu katika kuwatia wengine moyo.” Aliongezea hivi: “Ni wajibu wangu kuwapongeza wengine.” (Met. 3:27) Jérôme, mmishonari katika nchi ya French Guiana, amewasaidia vijana wengi kustahili kuwa wamishonari. Anasema hivi: “Nimegundua kwamba ninapowapongeza ndugu vijana kwa sababu ya jambo hususa wanalotimiza katika huduma au maelezo mazuri wanayotoa, wanatiwa moyo na kuchochewa kufanya maendeleo zaidi.”

18. Kwa nini ni vizuri kufanya kazi pamoja na ndugu vijana?

18 Tunaweza pia kuwachochea waamini wenzetu kufanya maendeleo ya kiroho kwa kushirikiana nao katika utendaji mbalimbali. Mzee anaweza kumwomba ndugu kijana anayejua kutumia kompyuta amchapishie makala kutoka katika tovuti ya jw.org inayoweza kuwatia moyo ndugu na dada waliozeeka ambao hawana kompyuta. Au ikiwa unafanya kazi fulani kwenye Jumba la Ufalme, kwa nini usimwalike ndugu kijana akusaidie? Ukifanya hivyo utapata fursa ya kuwatazama vijana, kuwapongeza, na kuona wakifanya maendeleo.Met. 15:23.

KUWAZOEZA WENGINE WATUMIKE WAKATI UJAO

19, 20. wa nini tunapaswa kuwasaidia wengine kufanya maendeleo?

19 Yehova alipomweka rasmi Yoshua awaongoze Waisraeli, alimwamuru Musa ‘amtie moyo na kumwimarisha.’ (Soma Kumbukumbu la Torati 3:28.) Watu wengi zaidi wanajiunga nasi katika kutaniko la ulimwenguni pote. Mbali na wazee wa kutaniko, Wakristo wote wenye uzoefu wanaweza kuwasaidia ndugu vijana na wapya kufanya yote wawezayo. Hivyo, wengi zaidi watakuwa watumishi wa wakati wote na “kustahili vya kutosha kufundisha wengine.”2 Tim. 2:2.

20 Iwe kutaniko letu ni kubwa au ni kikundi kidogo kinachofanya maendeleo ili kuwa kutaniko, acheni tuwazoeze wengine ili watumike wakati ujao. Ili kufanya hivyo, ni lazima tumwige Yehova ambaye hutafuta sifa nzuri za watumishi wake.

^ fu. 17 Jina limebadilishwa.