Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msamaha wa Yehova Unamaanisha Nini Kwako?

Msamaha wa Yehova Unamaanisha Nini Kwako?

Msamaha wa Yehova Unamaanisha Nini Kwako?

‘Yehova ni Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira, anasamehe kosa na ubaya na dhambi.’​—KUT. 34:6, 7.

TAFUTA MAJIBU

Yehova alishughulikiaje dhambi za Daudi na Manase, na kwa nini?

Kwa nini Yehova hakulisamehe taifa la Israeli kwa ujumla?

Tunawezaje kupata msamaha wa Yehova?

1, 2. (a) Yehova alithibitika kuwa Mungu wa aina gani kwa taifa la Israeli? (b) Ni swali gani linalojibiwa katika makala hii?

KATIKA siku za Nehemia, Walawi fulani walikubali katika sala ya hadharani kwamba mara nyingi mababu zao ‘walikataa kusikiliza’ amri za Yehova. Hata hivyo, Yehova alithibitika tena na tena kuwa ‘Mungu wa matendo ya kusamehe, mwenye neema na rehema, asiye mwepesi wa hasira na mwingi wa fadhili zenye upendo.’ Yehova aliendelea kuwaonyesha fadhili zisizostahiliwa wahamishwa hao waliorudishwa katika siku za Nehemia.​—Neh. 9:16, 17.

2 Kila mmoja wetu anaweza kujiuliza hivi: ‘Msamaha wa Yehova unamaanisha nini kwangu?’ Ili tupate jibu la swali hilo muhimu, acheni tuchunguze jinsi Mungu alivyoshughulika na wanaume wawili ambao walifaidika kutokana na msamaha wa Yehova, yaani, wafalme wawili, Daudi na Manase.

DHAMBI NZITO ZA DAUDI

3-5. Ni nini kilichomfanya Daudi atende dhambi nzito?

3 Ingawa Daudi alikuwa mtu anayemwogopa Mungu, alitenda dhambi nzito. Mbili kati ya dhambi hizo zilihusisha wenzi wa ndoa, Uria na Bath-sheba. Matokeo ya dhambi hizo yaliwaumiza sana wote waliohusika. Hata hivyo, njia ambayo Mungu alitumia kumrekebisha Daudi inafunua mengi kuhusu msamaha wa Yehova. Fikiria kilichotukia.

4 Daudi alilituma jeshi la Israeli ili lizingire Raba, mji mkuu wa Waamoni. Mji huo ulikuwa kilomita 80 hivi upande wa mashariki wa Yerusalemu, ng’ambo ya Mto Yordani. Wakati huo, Daudi alikuwa juu ya dari ya nyumba yake ya kifalme huko Yerusalemu naye akamwona Bath-sheba, mke wa Uria, akioga. Mume wake hakuwapo. Daudi aliwaka tamaa alipomwona Bath-sheba hivi kwamba akawatuma wajumbe ili wamlete katika nyumba yake, ambamo alifanya naye uzinzi.​—2 Sam. 11:1-4.

5 Daudi alipopata habari kwamba Bath-sheba ana mimba, aliagiza mume wake, Uria, arudishwe Yerusalemu akitarajia kwamba angefanya ngono na Bath-sheba mkewe. Lakini Uria alikataa kuingia nyumbani mwake ingawa Daudi alijaribu sana kumhimiza afanye hivyo. Kwa hiyo, mfalme alituma barua ya siri kwa kiongozi wa jeshi lake akimwagiza amweke Uria “mbele ya mashambulio makali zaidi ya kivita” na kuhakikisha kwamba askari-jeshi wenzake wanamwacha peke yake. Uria alishambuliwa kwa urahisi, naye akapigwa na kufa vitani, kama tu Daudi alivyopanga. (2 Sam. 11:12-17) Kwa hiyo, dhambi ya uzinzi ya mfalme huyo ilizidi kuwa mbaya zaidi alipomuua mwanamume asiye na hatia.

DAUDI ABADILI MTAZAMO WAKE

6. Mungu alichukua hatua gani kuelekea dhambi za Daudi, na hilo linaonyesha nini kumhusu Yehova?

6 Bila shaka, Yehova aliona kila kitu kilichotokea. Hakuna jambo asiloweza kuona. (Met. 15:3) Ingawa baadaye Mfalme Daudi alimwoa Bath-sheba, “lile jambo ambalo Daudi alikuwa amefanya likawa baya machoni pa Yehova.” (2 Sam. 11:27) Basi Mungu alichukua hatua gani kuelekea dhambi nzito alizotenda Daudi? Alimtuma nabii Nathani kwa Daudi. Akiwa Mungu anayesamehe, ni wazi kwamba Yehova alitafuta msingi wa kuonyesha rehema. Je, huchangamshwi moyo na hatua hiyo ambayo Yehova alichukua? Hakumlazimisha Daudi aungame dhambi zake bali alimtuma Nathani aliyemsimulia mfalme huyo hadithi iliyoonyesha ubaya wa dhambi hizo. (Soma 2 Samweli 12:1-4.) Hali hiyo ngumu ilishughulikiwa kwa njia nzuri kama nini!

7. Daudi alitendaje aliposikia mfano uliosimuliwa na Nathani?

7 Mfano uliosimuliwa na Nathani ulichochea hisia ya mfalme ya kutaka haki itekelezwe. Daudi alimkasirikia mwanamume tajiri katika hadithi hiyo na kumwambia Nathani hivi: “Kama Yehova anavyoishi, mtu huyo aliyefanya hivyo anastahili kufa!” Isitoshe, Daudi alisema kwamba yule mtu aliyetendewa isivyo haki anapaswa kulipwa kwa sababu ya hasara aliyopata. Kisha Nathani akamwambia hivi waziwazi: “Wewe mwenyewe ndiye yule mwanamume!” Halafu akamwambia Daudi kwamba kwa sababu ya matendo yake, “upanga” hautaondoka nyumbani mwake na msiba utaikumba familia yake. Angeaibishwa pia hadharani kwa sababu ya makosa yake. Daudi alitambua uzito wa yale aliyofanya na kukiri hivi kwa majuto: “Nimemtendea Yehova dhambi.”​—2 Sam. 12:5-14.

SALA YA DAUDI NA MSAMAHA WA MUNGU

8, 9. Zaburi ya 51 inafunuaje hisia za moyoni za Daudi, na inatufundisha nini kumhusu Yehova?

8 Maneno ya wimbo ambao Mfalme Daudi alitunga baadaye yanafunua jinsi alivyojuta kutoka moyoni. Zaburi ya 51 ina sihi zenye kugusa moyo ambazo Daudi alimtolea Yehova na inaonyesha wazi kwamba alifanya mengi zaidi kuliko kukiri tu makosa yake. Alitubu pia dhambi zake. Daudi alihangaikia hasa uhusiano wake na Mungu. Aliungama hivi: “Dhidi yako wewe, wewe peke yako, nimetenda dhambi.” Akamsihi Yehova: “Uumbe moyo safi ndani yangu, Ee Mungu, na kuweka ndani yangu roho mpya, iliyo imara. . . . Unirudishie shangwe ya wokovu wako, nawe unitegemeze kwa roho ya kupenda.” (Zab. 51:1-4, 7-12) Je, wewe pia unazungumza na Yehova kwa unyoofu na kwa bidii kuhusu makosa yako?

9 Yehova hakuondoa matokeo yenye kuumiza ya dhambi za Daudi. Madhara hayo yangeendelea kumsumbua muda wote wa maisha yake. Hata hivyo, Yehova alimsamehe Daudi kwa sababu alionyesha toba, yaani, Daudi alikuwa na “moyo uliovunjika na kupondwa.” (Soma Zaburi 32:5; Zab. 51:17) Mungu Mweza-Yote anajua mtazamo na nia ambayo humchochea mtu kutenda dhambi. Badala ya kuagiza wazinzi hao wahukumiwe kifo na waamuzi wanadamu kulingana na Sheria ya Musa, kwa rehema Yehova aliingilia kati na kushughulikia mwenyewe kisa cha Daudi na Bath-sheba. (Law. 20:10) Mungu hata alimfanya mwana wao Sulemani kuwa mfalme wa Israeli baada ya Daudi.​—1 Nya. 22:9, 10.

10. (a) Huenda Yehova alitumia msingi gani kumsamehe Daudi? (b) Ni mamb o gani yanayomchochea Yehova kusamehe?

10 Labda jambo lingine lililomfanya Yehova amsamehe Daudi ni jinsi Daudi mwenyewe alivyokuwa amemwonyesha rehema Sauli. (1 Sam. 24:4-7) Kama Yesu alivyoeleza, Yehova anatutendea kama tunavyowatendea wengine. Yesu alisema hivi: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa; na kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi.” (Mt. 7:1, 2) Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova atatusamehe dhambi zetu, hata dhambi nzito kama vile uzinzi au uuaji! Atatusamehe tukiwa na roho ya kusamehe, tukiungama dhambi zetu mbele yake, na tukionyesha kwamba tumebadili mtazamo wetu kuelekea matendo yetu mabaya. Watenda-dhambi wanapotubu kikweli wanapata “majira ya kuburudisha” kutoka kwa Yehova.​Soma Matendo 3:19.

MANASE ATENDA DHAMBI NZITO LAKINI ATUBU

11. Ni katika njia zipi Mfalme Manase alifanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Mungu?

11 Fikiria simulizi lingine la Kimaandiko linaloonyesha jinsi Yehova alivyo tayari kusamehe. Miaka 360 hivi baada ya Daudi kuanza kutawala, Manase alitawazwa kuwa mfalme wa Yuda. Uovu ulienea sana wakati wa utawala wake wa miaka 55, na mazoea yake yenye kuchukiza sana yalishutumiwa na Yehova. Kati ya mambo mengine, Manase alijenga madhabahu za Baali, akaabudu “jeshi lote la mbinguni,” akawapitisha wanawe motoni, na kuendeleza mazoea ya kuwasiliana na pepo. Kwa kweli, “alifanya kwa kiasi kikubwa yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova.”​—2 Nya. 33:1-6.

12. Manase alimrudiaje Yehova?

12 Hatimaye, Manase alitekwa kutoka katika nchi yake na kutupwa gerezani huko Babiloni. Akiwa huko, huenda alikumbuka maneno haya ambayo Musa aliwaambia Waisraeli: “Utakapokuwa katika dhiki kali na maneno yote haya yawe yamekupata mwishoni mwa siku hizo, basi utarudi kwa Yehova Mungu wako na kuisikiliza sauti yake.” (Kum. 4:30) Manase alimrudia Yehova. Jinsi gani? ‘Aliendelea kujinyenyekeza sana’ na ‘kuendelea kusali’ kwa Mungu (kama picha inavyoonyesha kwenye ukurasa wa 21). (2 Nya. 33:12, 13) Hatujui maneno hususa ambayo Manase alisema katika sala hizo, lakini tunaweza kuwazia kwamba huenda alisema maneno kama ya Mfalme Daudi, yaliyoandikwa katika Zaburi ya 51. Kwa vyovyote vile, moyo wa Manase ulibadilika kabisa.

13. Kwa nini Yehova alimsamehe Manase?

13 Yehova aliitikiaje sala za Manase? “Yeye akakubali kusihiwa [na Manase] kisha Yeye akasikia ombi lake la kutaka kibali.” Kama Daudi alivyofanya awali, Manase alitambua uzito wa dhambi zake naye akatubu kikweli. Kwa sababu hiyo, Mungu alimsamehe Manase na kumweka tena kuwa mfalme huko Yerusalemu. Kwa hiyo, “Manase akapata kujua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.” (2 Nya. 33:13) Inatia moyo pia kujifunza kutokana na mfano huo kwamba Mungu wetu mwenye rehema huwasamehe wale wanaotubu kikweli.

JE, MSAMAHA WA YEHOVA HAUNA MIPAKA?

14. Yehova huamuaje ikiwa atawasamehe watenda-dhambi?

14 Leo, watu wengi wa Mungu huenda wasihitaji kuomba msamaha kwa ajili ya kufanya dhambi nzito kama zile za Daudi na Manase. Hata hivyo, uhakika wa kwamba Yehova aliwasamehe wafalme hao wawili unatusaidia kutambua kwamba Mungu wetu yuko tayari kusamehe hata dhambi nzito sana ikiwa mtenda-dhambi anatubu kikweli.

15. Tunajuaje kwamba Yehova hawasamehi wanadamu wote dhambi zao bila kujali?

15 Bila shaka, hatuwezi kwa hakika kusema kwamba Yehova anawasamehe wanadamu wote dhambi zao bila kujali. Kuhusu hilo, acheni tulinganishe mtazamo ambao Daudi na Manase walikuwa nao na mtazamo waliokuwa nao watu waasi wa Israeli na Yuda. Mungu alimtuma Nathani ili amkabili Daudi na kumpa nafasi ya kubadili mtazamo wake. Daudi alithamini nafasi hiyo na kukubali shauri. Manase alipokuwa katika dhiki kali, alichochewa kutubu kutoka moyoni. Hata hivyo, mara nyingi wakaaji wa Israeli na Yuda hawakutubu. Kwa hiyo, Yehova hakuwasamehe. Badala yake, aliwatuma tena na tena manabii wake ili wawajulishe maoni yake kuhusu mwenendo wao wa kutotii. (Soma Nehemia 9:30.) Hata baada ya wahamishwa waliotoka Babiloni kurudi katika nchi yao, Yehova aliendelea kuwatuma wajumbe waaminifu, kama vile kuhani Ezra na nabii Malaki. Watu walipotenda kulingana na mapenzi ya Yehova, walipata shangwe kubwa.​—Neh. 12:43-47.

16. (a) Ilikuwaje kwa taifa la Israeli kwa ujumla kwa sababu ya kutotubu? (b) Wazao mmoja-mmoja wa taifa la kale la Israeli wana nafasi gani?

16 Baada ya Yesu kutumwa duniani na dhabihu moja kamilifu ya fidia kutolewa, Yehova hakukubali tena dhabihu za wanyama zilizotolewa na Waisraeli. (1 Yoh. 4:9, 10) Akiwa mwanadamu, Yesu alidhihirisha maoni ya Baba yake aliposema maneno haya yenye kugusa moyo: “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na ambaye huwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwake,​—ni mara ngapi nilitaka kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga vyake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka.” Kwa hiyo, Yesu akatangaza hivi: “Tazama! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mt. 23:37, 38) Basi, Israeli la kiroho lilichukua mahali pa taifa hilo lenye dhambi na lisilotubu. (Mt. 21:43; Gal. 6:16) Lakini vipi kuhusu watu mmoja-mmoja ambao ni Waisraeli wa asili? Wanaalikwa ili wafaidike kutokana na msamaha na rehema ya Yehova kwa kudhihirisha imani katika Mungu na katika dhabihu ya Yesu Kristo. Watu waliokufa bila kutubu dhambi zao ambao watafufuliwa katika dunia iliyosafishwa, watapewa pia nafasi hiyo.​—Yoh. 5:28, 29; Mdo. 24:15.

KUFAIDIKA KUTOKANA NA MSAMAHA WA YEHOVA

17, 18. Tunawezaje kupata msamaha wa Yehova?

17 Tunapaswa kuitikiaje utayari wa Yehova wa kusamehe? Bila shaka, tunapaswa kutenda kama Daudi na Manase. Tunapaswa kutambua hali yetu ya dhambi, kutubu makosa yetu, kumsihi sana Yehova atusamehe, na kumwomba aumbe moyo safi ndani yetu. (Zab. 51:10) Ikiwa tumetenda dhambi nzito, tunapaswa pia kutafuta msaada wa kiroho kutoka kwa wazee. (Yak. 5:14, 15) Licha ya hali zetu, inafariji kukumbuka kwamba Yehova ana sifa zilezile alizomwambia Musa, yaani, yeye ni “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo na kweli, anayehifadhi fadhili zenye upendo kwa ajili ya maelfu, anayesamehe kosa na ubaya na dhambi.” Yehova hajabadilika.​—Kut. 34:6, 7.

18 Akitumia mfano wenye nguvu, Yehova aliwaahidi Waisraeli waliotubu kwamba angeondoa kabisa doa lao la dhambi, na angefanya dhambi zao “nyekundu” ziwe nyeupe kama “theluji.” (Soma Isaya 1:18.) Kwa hiyo basi, msamaha wa Yehova unamaanisha nini kwetu? Unamaanisha kwamba anatusamehe kabisa dhambi na makosa yetu, maadamu tunaonyesha mtazamo wa shukrani na wa kutubu.

19. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

19 Kwa kuwa tumesamehewa na Yehova, tunawezaje kumwiga tunaposhughulika na wengine? Tunawezaje kuepuka kuwa na mtazamo wa kutowasamehe wengine wanaotenda dhambi nzito lakini wanatubu kikweli? Makala inayofuata itatusaidia kuichunguza mioyo yetu ili tuwe kama Baba yetu, Yehova, ambaye ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’​—Zab. 86:5.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kwa sababu ya msamaha wa Yehova, Manase aliwekwa tena kuwa mfalme huko Yerusalemu