Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Mnagusa Mioyo ya Wazazi Wenu

Vijana Mnagusa Mioyo ya Wazazi Wenu

Vijana Mnagusa Mioyo ya Wazazi Wenu

“SINA sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli,” akaandika mtume Yohana. (3 Yohana 4) Ijapokuwa watoto wanaotajwa katika mstari huo wa Biblia ni wanafunzi Wakristo, wazazi wanaomwogopa Mungu wanaweza kwa urahisi kuelewa hisia hizo za Yohana. Wazazi wanaweza kufanya maisha ya watoto wao yawe mazuri sana, nao watoto wanaweza kufanya maisha ya wazazi wao yawe mazuri.

Mfalme Sulemani wa Israeli alijua jinsi watoto wanavyoweza kugusa sana mioyo ya wazazi wao. Aliandika hivi: “Mwana mwenye hekima ndiye anayemfanya baba ashangilie, naye mwana mjinga ni huzuni ya mama yake.” (Methali 10:1) Kwa hiyo, inafaa watoto wote, hata wale wenye umri mkubwa, wafikirie jinsi matendo yao yatakavyogusa maisha ya baba na mama yao. Kwa nini inafaa kufanya hivyo?

Hebu fikiria jitihada zote ambazo wazazi wako wanaomwogopa Mungu wamefanya katika kukulea! Walianza kukuhangaikia na kusali kwa ajili yako muda mrefu kabla hujazaliwa. Baada ya wewe kuzaliwa, wazazi wako walifurahia kujenga uhusiano wa karibu pamoja nawe na inaelekea kwamba walimshukuru Mungu kwa sababu ya pendeleo kubwa na wajibu mzito wa kukulea. Ukiwa mtoto mdogo asiyejiweza, ulikuwa sasa chini ya utunzaji wao, na wakiwa waabudu wa Yehova, walichukua wajibu huo kwa uzito.

Kwa kuwa wazazi wako ni Wakristo wa kweli, walichunguza Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia ili wapate mwongozo unaotegemeka, na pia waliwaomba mashauri wale ambao tayari wamelea watoto. Pia, waliendelea kumjulisha Mungu mahangaiko yao katika sala. (Waamuzi 13:8) Kadiri ulivyokua, wazazi wako walitambua uwezo wako na pia waliona udhaifu wako. (Ayubu 1:5) Ulipokuwa kijana matatizo mapya yalitokea. Huenda uliasi mara kwa mara, na wazazi wako walisali zaidi, wakajifunza zaidi, na kufikiri zaidi jinsi ya kukusaidia kuendelea kumwabudu Baba yako wa mbinguni, Yehova.

Wazazi wako wataendelea daima kuwa baba na mama yako. Wanaendelea kuhangaikia hali yako njema ya kimwili, kiakili, kihisia, na kiroho hata baada ya wewe kuwa mtu mzima. Hata hivyo, nyakati zote wanakumbuka kwamba wewe una uhuru wa kujiamulia mambo na kwamba hawawezi kuwa na uhakika kabisa kuhusu jinsi maisha yako yatakavyokuwa mwishowe. Ni lazima ufanye uamuzi wako mwenyewe kuhusu njia utakayofuata maishani.

Ikiwa wazazi hawana “sababu nyingine kubwa zaidi ya kuwa na shukrani” kuliko kusikia kwamba watoto wao “wanaendelea kutembea katika kweli,” je, si jambo linalopatana na akili kusema kwamba watoto wasipotembea katika kweli wazazi watahuzunika? Kwa kweli, watoto wanaotenda kwa ujinga wanawahuzunisha wazazi wao. Sulemani alisema: “Mwana mjinga ni huzuni kwa baba yake na ni uchungu kwa mama aliyemzaa.” (Methali 17:25) Wazazi wanahuzunika kama nini mtoto anapoacha ibada ya Mungu wa kweli!

Kwa wazi, ninyi vijana mna uvutano mkubwa ndani na nje ya familia yenu. Mwenendo wenu unagusa sana mioyo ya wazazi wenu. Mkimwacha Mungu na kukataa kanuni zake, wazazi wenu wataumia. Hata hivyo, mkiendelea kuwa waaminifu na watiifu kwa Yehova, wazazi wenu watashangilia. Azimieni kufanya mioyo ya wazazi wenu ishangilie! Mnaweza kuwapa wazazi wenu wanaowalea, kuwalinda na kuwapenda zawadi gani yenye thamani kubwa kuliko hiyo?