Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acha Neno la Mungu Liongoze Hatua Zako

Acha Neno la Mungu Liongoze Hatua Zako

Acha Neno la Mungu Liongoze Hatua Zako

“Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.” —ZABURI 119:105.

1, 2. Kwa nini wanadamu wengi wameshindwa kupata amani na furaha ya kweli?

JE, UNAWEZA kukumbuka wakati fulani ulipohitaji kumwomba mtu akuonyeshe njia? Huenda ulikuwa umekaribia mahali ambapo ulikuwa unaenda lakini hukuwa na hakika ufuate njia gani. Au huenda ulikuwa umepotea kabisa na ulihitaji kufuata njia tofauti kabisa. Kwa vyovyote vile, je, halingekuwa jambo la hekima kufuata mwelekezo wa mtu anayejua eneo hilo? Mtu kama huyo angeweza kukusaidia kufika mahali unapoenda.

2 Kwa maelfu ya miaka, wanadamu kwa ujumla wamejaribu kuongoza maisha yao bila msaada wa Mungu. Hata hivyo, wanadamu wasio wakamilifu hawawezi kufanikiwa hata kidogo wasiposaidiwa. Kwa ufupi, hawawezi kamwe kupata njia inayoongoza kwenye amani na furaha ya kweli. Kwa nini wameshindwa kabisa kufanikiwa? Miaka zaidi ya 2,500 iliyopita, nabii Yeremia alisema hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Bila shaka, yeyote anayejaribu kuongoza hatua yake bila kukubali msaada wa mtu anayestahili atakatishwa tamaa kabisa. Kwa kweli, wanadamu wanahitaji kuongozwa!

3. Kwa nini Yehova Mungu ndiye anayestahili zaidi kuwaongoza wanadamu, naye ameahidi nini?

3 Yehova Mungu ndiye anayestahili kabisa kutuongoza. Kwa nini? Kwa sababu anaelewa vizuri kuliko mtu mwingine yeyote jinsi wanadamu walivyoumbwa. Pia, anajua vizuri kabisa jinsi jamii ya wanadamu ilivyopotoka na kupotea. Anajua pia kile kinachohitajiwa ili kuwasaidia warudi kwenye njia inayofaa. Zaidi ya hayo, akiwa Muumba, nyakati zote Yehova anajua mambo yanayotufaa zaidi. (Isaya 48:17) Hivyo, tunaweza kutegemea kabisa ahadi yake iliyoandikwa katika Zaburi 32:8: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.” Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova anatoa mwongozo bora zaidi. Lakini anatuongoza jinsi gani?

4, 5. Maneno ya Mungu yanaweza kutuongoza jinsi gani?

4 Mtunga-zaburi alisema hivi katika sala kwa Yehova: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.” (Zaburi 119:105) Maneno na vikumbusho vya Mungu vinapatikana katika Biblia, navyo vinaweza kutusaidia kushinda vizuizi tunavyopata katika maisha yetu. Kwa kweli, tunaposoma Biblia na kuacha ituongoze, maneno haya ya Isaya 30:21 yanatimia katika maisha yetu: “Masikio yako yatasikia neno nyuma yako likisema: ‘Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.’”

5 Hata hivyo, ona kwamba Zaburi 119:105 inaonyesha makusudi mawili yanayohusiana ya Neno la Mungu. Kwanza, ni taa ya mguu wetu. Tunapokabili matatizo ya kila siku, kanuni za Biblia zinapaswa kuongoza hatua zetu ili tufanye maamuzi ya hekima na kuepuka mitego ya ulimwengu huu. Pili, vikumbusho vya Mungu ni nuru kwa barabara yetu, navyo vinatusaidia kufanya maamuzi yanayopatana na tumaini letu la kuishi milele katika paradiso iliyoahidiwa na Mungu. Barabara yetu ikiwa na mwangaza wa kutosha, tutaweza kutambua ikiwa njia fulani italeta matokeo mazuri au mabaya. (Waroma 14:21; 1 Timotheo 6:9; Ufunuo 22:12) Acheni tuone kwa undani jinsi maneno ya Mungu yaliyo katika Biblia yanavyoweza kuwa taa ya mguu wetu na nuru kwa barabara yetu.

“Taa ya Mguu Wangu”

6. Maneno ya Mungu yanaweza kuwa taa ya mguu wetu katika hali gani?

Kila siku, tunafanya maamuzi. Huenda maamuzi fulani yakaonekana kuwa madogo, lakini nyakati nyingine tunaweza kukabili hali inayojaribu maadili, unyoofu, au msimamo wetu wa kutokuwamo. Ili tupambane kwa mafanikio na hali hizo, ni lazima ‘nguvu zetu za ufahamu zizoezwe kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Tukipata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu na kuelewa kanuni zake, tunazoeza dhamiri yetu ili tuweze kufanya maamuzi yanayompendeza Yehova.—Methali 3:21.

7. Eleza hali inayoweza kumfanya Mkristo atake kushirikiana na wafanyakazi wenzake ambao si waamini.

7 Fikiria mfano huu. Je, wewe ni mtu mzima unayejitahidi kikweli kufanya moyo wa Yehova ushangilie? (Methali 27:11) Ikiwa ndivyo, unastahili kupongezwa. Lakini wazia kwamba wafanyakazi wenzako wanakupa tikiti ili uende nao kwenye mchezo fulani. Wanafurahia kushirikiana nawe kazini na pia wangependa kushirikiana nawe katika mahali pengine. Huenda ukasadiki kabisa kwamba watu hao si wabaya. Huenda hata wana sifa fulani nzuri. Utafanya nini? Je, kuna hatari yoyote ya kukubali mwaliko wao? Chini ya hali hiyo, Neno la Mungu linaweza kukusaidia jinsi gani kufanya uamuzi mzuri?

8. Ni kanuni gani za Kimaandiko zinazoweza kutusaidia kufanya uamuzi kuhusu mashirika?

8 Fikiria kanuni chache za Kimaandiko. Kanuni ya kwanza unayoweza kukumbuka inapatikana katika andiko la 1 Wakorintho 15:33, linalosema: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” Je, kufuata kanuni hiyo kunamaanisha kwamba unapaswa kuepuka kabisa watu ambao si waamini? Kulingana na Maandiko, jibu ni hapana. Hata mtume Paulo mwenyewe aliwahangaikia kwa upendo “watu wa namna zote,” kutia ndani wale wasio waamini. (1 Wakorintho 9:22) Kulingana na kanuni za Ukristo tunapaswa kupendezwa na wengine, kutia ndani wale ambao si waamini wenzetu. (Waroma 10:13-15) Kwa wazi, tunaweza jinsi gani kufuata shauri la ‘kuwatendea wote mema’ ikiwa tungejitenga na watu ambao huenda wakahitaji msaada wetu?—Wagalatia 6:10.

9. Ni shauri gani la Biblia linalotusaidia kuwa na usawaziko katika uhusiano wetu na wafanyakazi wenzetu?

9 Hata hivyo, kuna tofauti kubwa kati ya kuwa mwenye urafiki kumwelekea mfanyakazi mwenzako na kuwa rafiki yake wa karibu. Inapohusu urafiki wa karibu, kanuni nyingine ya Kimaandiko inahusika. Mtume Paulo aliwaonya Wakristo hivi: “Msifungwe nira isivyo sawa pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14) Maneno “msifungwe nira isivyo sawa” yanamaanisha nini? Tafsiri fulani za Biblia zinatumia maneno “msijiunge pamoja na,” “msijaribu kufanya mambo pamoja kana kwamba mko sawa,” au “komeni kujenga mahusiano yasiyofaa.” Ni wakati gani urafiki na mfanyakazi mwenzako unakuwa usiofaa? Ni wakati gani uhusiano huo unapokuwa sawa na kufungiwa nira isivyo sawa? Neno la Mungu, Biblia, linaweza kuongoza hatua zako katika hali hiyo.

10. (a) Yesu alichagua marafiki wake jinsi gani? (b) Ni maswali gani yanayoweza kumsaidia mtu kufanya uamuzi mzuri kuhusu mashirika?

10 Fikiria mfano wa Yesu, ambaye aliwapenda wanadamu tangu walipoumbwa. (Methali 8:31) Alipokuwa duniani alijenga uhusiano wa karibu sana pamoja na wafuasi wake. (Yohana 13:1) Hata ‘alimpenda’ mtu fulani aliyekuwa amepotoshwa kidini. (Marko 10:17-22) Lakini Yesu aliweka pia mipaka iliyo wazi kuhusu uchaguzi wake wa marafiki wa karibu. Hakusitawisha urafiki wa karibu na watu ambao hawakupenda kikweli kufanya mapenzi ya Baba yake. Wakati mmoja, Yesu alisema: “Ninyi ni rafiki zangu ikiwa mnafanya ninalowaamuru ninyi.” (Yohana 15:14) Kweli, huenda una uhusiano mzuri pamoja na mfanyakazi mwenzako. Lakini jiulize: ‘Je, mtu huyu yuko tayari kufanya yale ambayo Yesu anaamuru? Je, anataka kujifunza kumhusu Yehova, yule ambaye Yesu alitufundisha tumwabudu? Je, anaishi kulingana na viwango vya maadili ambavyo mimi nikiwa Mkristo ninafuata?’ (Mathayo 4:10) Unapozungumza na wafanyakazi wenzako na kusisitiza kufuata viwango vya Biblia, majibu ya maswali hayo yataonekana wazi.

11. Toa mifano ya hali ambazo maneno ya Mungu yanapaswa kuongoza hatua zetu.

11 Maneno ya Mungu yanaweza kuwa taa ya mguu wetu katika hali nyingine nyingi. Kwa mfano, huenda Mkristo ambaye hana kazi akapata kazi anayohitaji sana. Hata hivyo, pengine kazi hiyo itachukua muda wake mwingi na kumchosha sana, na akiikubali, atakosa mikutano fulani ya Kikristo na hataweza kushiriki katika utendaji mwingine wa ibada ya kweli. (Zaburi 37:25) Huenda Mkristo mwingine akashawishiwa sana kutazama mambo yanayopingana waziwazi na kanuni za Biblia. (Waefeso 4:17-19) Huenda mwingine akakasirishwa kwa urahisi sana na udhaifu wa waamini wenzake. (Wakolosai 3:13) Katika hali hizo zote, tunapaswa kuacha Neno la Mungu liwe taa ya mguu wetu. Kwa kweli, kwa kufuata kanuni za Biblia, tunaweza kupambana kwa mafanikio na hali yoyote ngumu tunayopata maishani. Neno la Mungu ni “lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.”—2 Timotheo 3:16.

“Nuru kwa Barabara Yangu”

12. Maneno ya Mungu ni nuru kwa barabara yetu jinsi gani?

12 Zaburi 119:105 inasema pia kwamba maneno ya Mungu ni nuru kwa barabara yetu, yakiangaza njia iliyo mbele yetu. Kuhusu wakati ujao, hatumo katika giza kwa kuwa Biblia inaeleza kwa nini kuna hali zenye kufadhaisha ulimwenguni na jinsi mambo yatakavyokuwa mwishowe. Ndiyo, tunatambua kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu mbovu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5) Kujua mambo yatakayotukia wakati ujao kunapaswa kuwa na uvutano mkubwa kuhusu jinsi tunavyoishi sasa. Mtume Petro aliandika hivi: “Kwa kuwa hivyo vitu vyote vitayeyushwa jinsi hiyo, ninyi mnapaswa kuwa watu wa namna gani katika matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu, mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova!”—2 Petro 3:11, 12.

13. Uharaka wa nyakati tunamoishi unapaswa kuwa na uvutano gani juu ya mawazo na mtindo wetu wa maisha?

13 Mawazo na mtindo wetu wa maisha unapaswa kuonyesha kuwa tunasadiki kabisa kwamba “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake.” (1 Yohana 2:17) Kufuata mwongozo wa Biblia kutatusaidia kufanya maamuzi ya hekima kuhusu miradi yetu ya wakati ujao. Kwa mfano, Yesu alisema: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mathayo 6:33) Vijana wengi wanaoonyesha imani katika maneno hayo ya Yesu kwa kufuatia utumishi wa wakati wote wanastahili kupongezwa sana! Wengine, kutia ndani familia nzima-nzima, wamejitolea kuhamia katika nchi zenye uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme.

14. Familia moja ya Kikristo ilipanua huduma yao jinsi gani?

14 Fikiria familia moja ya Kikristo yenye washiriki wanne waliotoka Marekani na kuhamia katika Jamhuri ya Dominika ili wasaidie kutaniko lililo katika mji wenye wakaaji 50,000. Kutaniko hilo lina wahubiri 130 hivi wa Ufalme. Lakini, mnamo Aprili 12, 2006, watu 1,300 hivi walihudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo! Shamba katika eneo hilo ni ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa’ hivi kwamba baada ya miezi mitano tu, wote katika familia hiyo, yaani, baba, mama, mwana, na binti walikuwa wakiongoza jumla ya mafunzo 30 ya Biblia. (Yohana 4:35) Baba huyo anaeleza hivi: “Kutaniko lina ndugu na dada 30 ambao wamehamia hapa ili kusaidia. Karibu 20 kati yao wametoka Marekani, na wengine wametoka Bahamas, Hispania, Italia, Kanada, na New Zealand. Wanakuja wakiwa na hamu ya kushiriki katika huduma na wanawachochea sana ndugu wenyeji.”

15. Umepata baraka gani kwa kutanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yako?

15 Inaeleweka kwamba wengi hawawezi kuhamia nchi nyingine ili kutumika mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. Lakini wale wanaoweza kuhamia mahali penye uhitaji mkubwa, au wale wanaoweza kurekebisha hali zao ili wahamie maeneo hayo, bila shaka watapata baraka nyingi kwa kushiriki katika sehemu hiyo ya huduma. Na hata iwe unatumikia wapi, usijinyime shangwe unayoweza kupata kwa kumtumikia Yehova kwa nguvu zako zote. Ukitanguliza mambo ya Ufalme katika maisha yako, Yehova anaahidi kuwa ‘atakufungulia wewe malango ya mbinguni na kukumwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’—Malaki 3:10.

Kufaidika Kutokana na Mwongozo wa Yehova

16. Tutafaidika kwa njia gani tukiacha maneno ya Mungu yatuongoze?

16 Kama tulivyoona, maneno ya Yehova yanatuongoza kwa njia mbili zinazohusiana. Maneno hayo ni taa ya mguu wetu, yakitusaidia kusonga mbele kuelekea upande unaofaa na kutuongoza tunapofanya maamuzi. Nayo ni nuru kwa barabara yetu, yakitusaidia kuona waziwazi mambo yatakayotukia wakati ujao. Yanatuwezesha kufuata himizo hili la Petro: “Kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji, tunzeni akili zenu kwa ukamili; kazeni tumaini lenu juu ya fadhili zisizostahiliwa zitakazoletwa kwenu wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.”—1 Petro 1:13.

17. Kujifunza Biblia kutatusaidia jinsi gani kufuata mwongozo wa Mungu?

17 Hapana shaka kwamba Yehova anatoa mwongozo. Lakini swali ni, Je, utafuata mwongozo wake? Ili uelewe mwongozo ambao Yehova anatoa, azimia kusoma sehemu fulani ya Biblia kila siku. Tafakari mambo unayojifunza, jaribu kufahamu mapenzi ya Yehova kuhusu mambo, na ufikirie njia mbalimbali za kutumia habari hiyo katika maisha yako. (1 Timotheo 4:15) Kisha, tumia ‘nguvu zako za kufikiri’ unapofanya maamuzi ya kibinafsi.—Waroma 12:1.

18. Tunapata baraka gani tukiacha Neno la Mungu lituongoze?

18 Tukiacha kanuni za Neno la Mungu zituongoze, tutapata ujuzi na mwongozo tunaohitaji tunapofanya maamuzi kuhusu njia tunayopaswa kufuata maishani. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba maneno ya Yehova yaliyoandikwa “humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” (Zaburi 19:7) Tukiacha Biblia ituongoze, tutakuwa na dhamiri safi na uradhi kwa sababu tunampendeza Yehova. (1 Timotheo 1:18, 19) Tukiacha maneno ya Mungu yaongoze hatua zetu kila siku, Yehova atatuthawabisha kwa kutupa baraka kuu kuliko zote, yaani, uzima wa milele.—Yohana 17:3.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini ni jambo la maana kumwacha Yehova Mungu aongoze hatua zetu?

• Maneno ya Mungu yanaweza kuwa taa ya mguu wetu kwa njia gani?

• Maneno ya Mungu yanaweza kuwa nuru kwa barabara yetu jinsi gani?

• Kujifunza Biblia kutatusaidia namna gani kufuata mwongozo wa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ni wakati gani inapokuwa si hekima kushirikiana na mtu ambaye si mwamini?

[Picha katika ukurasa wa 16]

Marafiki wa karibu wa Yesu walikuwa watu waliofanya mapenzi ya Yehova

[Picha katika ukurasa wa 17]

Je, mtindo wetu wa maisha unaonyesha kwamba tunatanguliza mambo ya Ufalme?