Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Shamba ‘Jeupe kwa Ajili ya Kuvunwa’

Shamba ‘Jeupe kwa Ajili ya Kuvunwa’

Shamba ‘Jeupe kwa Ajili ya Kuvunwa’

Rasi ya Guajira iko kwenye ncha ya kaskazini ya Amerika ya Kusini. Iko upande wa kaskazini wa Kolombia na upande wa kaskazini-magharibi wa Venezuela. Eneo hilo ambalo ni kavu kama jangwa, linapigwa na jua kali na halipati mvua ya kutosha. Viwango vya joto vinafikia nyuzi 43 Selsiasi. Hata ingawa hali ya hewa iko hivyo, watu wa eneo hilo ni wakulima wenye bidii wanaozalisha mazao mengi. Pepo zinazovuma daima kutoka baharini na pepo za msimu kutoka kaskazini-mashariki zinafanya maisha yawe mazuri, na hivyo wageni wanaweza kufurahia mazingira yenye kuvutia na fuo maridadi.

UNAKARIBISHWA kwenye nchi ya Wahindi wa kabila la Wayuu. Kuna Wayuu 305,000, na 135,000 kati yao wanaishi nchini Kolombia. Kabila hilo limeishi nchini humo kwa miaka mingi sana kabla ya ukoloni wa Wahispania.

Wayuu wanategemea sana ufugaji na ukulima ili kupata riziki yao. Pia, wanafanya uvuvi na biashara pamoja na nchi jirani. Wanawake wanafuma kwa ustadi sana vitu vyenye rangi za kuvutia ambavyo vinapendwa sana na watalii.

Wayuu wanajulikana kwa sababu ni wanyoofu na wakaribishaji-wageni. Hata hivyo, wao pia wanaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Umaskini ni moja ya matatizo makubwa yanayowakumba, na umesababisha matatizo mengine kama vile kutojua kusoma na kuandika, utapiamlo wa watoto wachanga, ukosefu wa matibabu, na uhalifu katika sehemu nyingine.

Kwa makumi ya miaka, makanisa ya dini zinazodai kuwa za Kikristo yametuma wamishonari kuishi miongoni mwa Wayuu. Kwa hiyo, shule nyingi za walimu na shule za bweni zinasimamiwa na makanisa. Wayuu wengi wamekubali zile zinazoitwa desturi za Kikristo, kama vile kuabudu sanamu na kuwabatiza watoto wachanga. Lakini hawajaacha imani na mila zao ambazo zinategemea hadithi za kitamaduni na ushirikina.

Kwa ujumla, Wayuu ni watu wanaomwogopa Mungu na wanakubali kweli za Biblia ambazo wanafundishwa na Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni mwa miaka ya 1980, kulikuwa na Mashahidi Wayuu saba peke yake huko Guajira, watatu kati yao waliishi katika mji mkuu, Ríohacha. Wahubiri wengine 20 walihubiri habari njema ya Ufalme katika Kihispania pamoja na Mashahidi hao wenyeji.

Ujumbe Katika Lugha Yao

Wayuu wengi wanaoishi Ríohacha wanaongea lugha yao ya asili, Kiwayuunaiki na pia Kihispania kidogo. Mwanzoni, kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme haikufanikiwa sana. Ni kana kwamba wenyeji waliwaepuka arijuna. Wayuu wanawaita hivyo watu ambao si wa kabila lao. Mashahidi walipowatembelea nyumbani kwao, Wayuu wengi walijibu tu kwa lugha yao wala si Kihispania. Mashahidi waliondoka tu na kwenda kwenye nyumba nyingine.

Hata hivyo, kufikia mwishoni mwa 1994, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imetuma kikundi cha mapainia wa pekee, au walimu wa Biblia wa wakati wote, watumike katika Kutaniko la Ríohacha. Mapainia hao walimwomba Shahidi mmoja wa kabila la Wayuu awafundishe Kiwayuunaiki. Baada ya kujifunza maneno machache ili kutoa ujumbe wa Biblia katika lugha hiyo, wahudumu hao walienda kwenye eneo na mara moja wakaona kwamba watu wanaitikia vizuri zaidi. Hata ingawa walimu hao wa Biblia walikuwa wakiongea Kiwayuunaiki bila ufasaha, wenye-nyumba walifurahi na kushangaa nao walikuwa tayari kusikiliza, na nyakati nyingine waliendeleza mazungumzo kwa uchangamfu wakitumia Kihispania kidogo walichojua!

‘Jeupe kwa Ajili ya Kuvunwa’

Mtume Paulo alilinganisha kazi ya Kikristo ya kufanya wanafunzi na kazi ya kulima shamba. Wayuu wanaelewa kwa urahisi ulinganisho huo kwa sababu ni wakulima. (1 Wakorintho 3:5-9) Kwa njia ya mfano, shamba la Wayuu kwa kweli ni ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’—Yohana 4:35.

Neil, Mhindi wa kabila la Wayuu ambaye aliishi Manaure, alizaliwa akiwa na ulemavu fulani. Neil alimlaumu Mungu na kushuka moyo hivi kwamba akajaribu kujiua. Shahidi mmoja ambaye alihubiri nyumba kwa nyumba alipokuwa akitembelea miji mbalimbali kwa sababu za kikazi alizungumza na Neil kuhusu Ufalme wa Yehova. Neil alikuwa na umri wa miaka 14 tu. Alipotambua kwamba Neil anapendezwa, Shahidi huyo alianza kujifunza Biblia pamoja naye. Neil alifurahi kujifunza kuhusu utu wenye upendo wa Yehova, naye akakata kauli kwamba si Mungu aliyemletea mateso. Aliguswa moyo sana aliposoma ahadi ya Mungu ya kuifanya dunia kuwa paradiso, na kwamba magonjwa hayatakuwapo tena!—Isaya 33:24; Mathayo 6:9, 10.

Wakati huo, familia ya Neil ilikuwa ikizozana na familia nyingine. Watu wa ukoo wa Neil walifanya matambiko fulani ya kabila lao ili kujaribu kujilinda. Neil anakumbuka hivi: “Mwanzoni, niliogopa kuijulisha familia yangu kuhusu imani yangu mpya, hasa wazee wa familia yetu ambao wanaheshimiwa sana.” Wazazi wa Neil walikasirika waliposikia kwamba hatafuata kamwe imani ambazo hazipatani na maandiko wala kushiriki katika desturi zinazohusiana na pepo. Halafu Neil akahamia Ríohacha na kuanza kushirikiana na kutaniko la huko. Baadaye alibatizwa. Mwaka wa 1993 aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma, na miaka mitatu baadaye akawa painia wa kawaida. Kisha, mwaka wa 1997 akawekwa rasmi kuwa mzee wa kutaniko. Mwaka wa 2000, alipanua huduma yake na kuwa painia wa pekee.

Pia, fikiria kisa cha Teresa, ambaye ni wa kabila la Wayuu. Alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Daniel, ambaye aliishi naye bila kufunga ndoa, alimdhihaki na kumtendea vibaya kimwili pamoja na watoto wao watatu. Hata ingawa baadaye alikubali kujifunza Biblia pamoja na Teresa, mara nyingi alienda kulewa pamoja na marafiki wake, na nyakati nyingine alikaa huko kwa siku nne au tano. Familia yake ilibaki maskini. Teresa aliendelea kujifunza kwa uaminifu na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Hilo lilimsaidia Daniel kuona umuhimu wa kujifunza Biblia. Kisha, mmoja wa watoto wake alianguka katika maji yaliyokuwa yakichemka na akachomeka. Mtoto huyo alikufa kutokana na majeraha aliyopata. Zaidi ya kuvumilia huzuni kubwa ya kufiwa na mwana wake, Teresa alisukumwa na marafiki na majirani kushiriki katika desturi za mazishi ambazo hazipatani na maandiko.

Katika kipindi hicho kigumu, Teresa na mume wake walipokea msaada wenye kutia moyo na faraja kutoka kwa washiriki wa makutaniko ya karibu. Baada ya mazishi, waliendelea kutembelewa na kufarijiwa na washiriki wa kutaniko la karibu la Kiwayuunaiki. Alipoona upendo wa Kikristo ukionyeshwa kwa matendo, Daniel alichochewa kufanya maendeleo ya kiroho. Aliacha kunywa pombe na kumtesa Teresa. Daniel na Teresa walifunga ndoa, naye Daniel akaanza kujitahidi kuitafutia familia yake riziki. Walifanya maendeleo ya kiroho na wakabatizwa mwaka wa 2003. Wote wawili wanaongoza mafunzo kadhaa ya Biblia. Kwa sababu ya ushahidi mzuri ambao Teresa aliwatolea washiriki wa familia yake, sasa watu wake wa ukoo wanawasikiliza Mashahidi wanapowatembelea. Mpwa mmoja wa kiume wa Daniel ni mhubiri ambaye hajabatizwa, na wapwa wake wawili wa kike wanajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Shemeji ya Teresa, ambaye mwana wake pia alikufa katika msiba, na familia yake wanapendezwa na funzo la Biblia.

Chakula cha Kiroho Katika Kiwayuunaiki

Mnamo mwaka wa 1998, kijitabu Furahia Maisha Katika Paradiso Duniani! * kilitolewa katika Kiwayuunaiki. Kijitabu hicho kilikuwa muhimu sana katika kuhubiri eneo la Wayuu na kuongoza mafunzo ya Biblia. Mipango ilifanywa mwaka wa 2003 ili ndugu kadhaa wazoezwe kutafsiri vichapo vya Mashahidi wa Yehova katika Kiwayuunaiki. Kwa sababu ya jitihada za kikundi cha watafsiri huko Ríohacha, broshua zaidi zimetayarishwa, na broshua hizo zimewasaidia wanafunzi wanaozungumza Kiwayuunaiki wafanye maendeleo ya kiroho.

Kuanzia mwaka wa 2001, sehemu fulani za programu ya kusanyiko la wilaya zimetafsiriwa katika Kiwayuunaiki. Wanafunzi wa Biblia wanachochewa kiroho wanaposikia programu katika lugha yao wenyewe. Wanatazamia siku ambayo wataona drama za Biblia katika lugha yao.

Shamba Lenye Kusitawi

Uribia ni mji ulio kilomita 100 hivi kaskazini-mashariki ya Ríohacha. Kutaniko la Uribia Wayuu lina wahubiri 16 wa Ufalme, wengi wao wanajitahidi zaidi kuwahubiria Wahindi wanaoishi katika maeneo ya mashambani. Mmoja wa wazee wa kutaniko hilo anasema hivi kuhusu safari moja kama hiyo ya kutoa ushahidi: “Tulitembelea shamba moja lenye nyumba 12 hivi ambazo ni fupi na zenye madirisha madogo. Mbele ya kila nyumba kuna paa tambarare lililojengwa kwa yotojolo, shina la ndani la mmea wa dungusi-kakati. Katika nyumba hizo, familia na wageni wanalindwa kutokana na jua kali. Tulifurahi kuona kwamba watu wengi walipendezwa sana, basi tukafanya mipango ya kurudi ili kuanzisha mafunzo ya Biblia. Tuliporudi, tuligundua kwamba wengi hawajui kusoma wala kuandika. Walituambia kwamba kuna shule moja iliyofungwa kwa sababu ya ukosefu wa pesa. Kwa fadhili, msimamizi wa shule hiyo alituruhusu kutumia darasa moja kuwafundisha watu kusoma na kuandika na kuongoza mafunzo ya Biblia. Watu sita wa kabila la Wayuu wamejifunza kusoma na kuandika na wanafanya maendeleo katika funzo lao la Biblia. Tunaguswa moyo na uthamini ambao wanaonyesha. Kwa hiyo, tunapanga kufanya mikutano kwenye shamba hilo.”

Mashahidi kadhaa ambao si wenyeji wamejifunza Kiwayuunaiki, na msaada wao unathaminiwa sana. Leo, katika Rasi ya Guajira, kuna makutaniko manane na vikundi viwili vya lugha hiyo.

Ni wazi kwamba Yehova anabariki jitihada hizo. Hapana shaka kwamba mambo mengi zaidi yanaweza kutimizwa katika kazi ya kuhubiri habari njema miongoni mwa Wayuu. Tunatazamia matokeo mazuri kadiri wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho wanavyokuwa wanafunzi Wakristo. Basi, Yehova na awatume wahudumu zaidi ili wafanye kazi katika shamba hilo, ambalo ni ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’—Mathayo 9:37, 38.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 18 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Ramani katika ukurasa wa 16]

 

VENEZUELA

KOLOMBIA

LA GUAJIRA

Manaure

Ríohacha

Uribia

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 16]

Wayuu camp below: Victor Englebert