Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi”

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi”

“Mimi Nipo Pamoja Nanyi”

“Mjumbe wa Yehova akaendelea kuwaambia: . . . ‘“Mimi nipo pamoja nanyi,” asema Yehova.’”—HAGAI 1:13.

1. Yesu alizungumzia unabii gani unaohusu nyakati zetu?

TUNAISHI wakati muhimu katika historia. Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba tangu mwaka wa 1914 tumekuwa katika “siku ya Bwana.” (Ufunuo 1:10) Huenda umejifunza unabii mbalimbali kuhusu “siku [hiyo] ya Bwana.” Hivyo, unajua kwamba Yesu alisema “siku za Mwana wa binadamu” katika mamlaka ya Ufalme ni kama “siku za Noa” na “siku za Loti.” (Luka 17:26, 28) Biblia inaonyesha kwamba mambo yaliyotukia siku za Noa na za Loti ni unabii unaohusu nyakati zetu. Hata hivyo, kuna unabii mwingine kuhusu nyakati zetu ambao tunapaswa kufikiria kwa uzito.

2. Yehova aliwapa Hagai na Zekaria kazi gani?

2 Acheni tuzungumzie hali fulani iliyokuwapo katika siku za manabii Waebrania, Hagai na Zekaria. Manabii hao wawili waaminifu walikuwa na ujumbe gani ambao unahusu watu wa Yehova wa siku zetu? Hagai na Zekaria walikuwa ‘wajumbe wa Yehova’ kwa Wayahudi waliorudi kutoka utekwani Babiloni. Walipewa utume wa kuwahakikishia Waisraeli kwamba Mungu angewategemeza katika kazi ya kujenga upya hekalu. (Hagai 1:13; Zekaria 4:8, 9) Ingawa vitabu ambavyo Hagai na Zekaria waliandika ni vifupi, vitabu hivyo ni sehemu ya “andiko lote [ambalo] limeongozwa na roho ya Mungu [na] lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.”—2 Timotheo 3:16.

Tunapaswa Kukazia Fikira Unabii Huo

3, 4. Kwa nini tunapaswa kupendezwa na ujumbe wa Hagai na Zekaria?

3 Bila shaka, ujumbe wa Hagai na Zekaria uliwafaidi Wayahudi wa siku zao, na unabii wao ulitimizwa kwa kiasi fulani wakati huo. Hata hivyo, tunawezaje kuwa na hakika kwamba vitabu hivyo viwili vinatuhusu leo? Andiko la Waebrania 12:26-29 linatusaidia kupata jibu. Hapo mtume Paulo ananukuu andiko la Hagai 2:6 linalosema kwamba Mungu ‘anatikisa mbingu na dunia.’ Mwishowe, kutikisa huko ‘kutakipindua kiti cha falme na kuangamiza nguvu za falme za mataifa.’—Hagai 2:22.

4 Anaponukuu Hagai, Paulo anaeleza kile kitakachopata “falme za mataifa” na anakazia ukuu wa Ufalme usiotikisika ambao Wakristo watiwa-mafuta watapokea. (Waebrania 12:28) Basi, maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba unabii wa Hagai na Zekaria unahusu kipindi cha baadaye, baada ya kitabu cha Waebrania kuandikwa katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida. Bado kungali na mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta duniani leo, ambao watatawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa Kimasihi. Hivyo, unabii wa Hagai na Zekaria unahusu nyakati zetu.

5, 6. Ni mambo gani yaliyotukia kabla ya unabii wa Hagai na Zekaria?

5 Kitabu cha Ezra kinaeleza mambo yaliyotukia kabla ya unabii wa Hagai na Zekaria. Baada ya Wayahudi kurudi kutoka utekwani Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., Gavana Zerubabeli na Kuhani Mkuu Yoshua (au Yeshua) walisimamia kuwekwa kwa msingi wa hekalu jipya mwaka wa 536 K.W.K. (Ezra 3:8-13; 5:1) Ingawa tukio hilo lilipaswa kutokeza shangwe nyingi, baada ya muda Wayahudi walianza kuogopa. Andiko la Ezra 4:4 linasema kwamba adui, au ‘watu wa nchi walizidi kuilegeza mikono ya watu wa Yuda na kuwavunja moyo wasijenge.’ Adui hao, hasa Wasamaria, walitoa madai ya uwongo dhidi ya Wayahudi. Wapinzani hao walimchochea mfalme wa Uajemi apige marufuku ujenzi wa hekalu.—Ezra 4:10-21.

6 Bidii ya kazi ya ujenzi ilididimia. Wayahudi wakafuatia mambo ya kibinafsi. Hata hivyo, mwaka wa 520 K.W.K., miaka 16 baada ya kuwekwa kwa msingi wa hekalu, Yehova aliwatuma Hagai na Zekaria ili wawahimize watu waanze tena kulijenga hekalu. (Hagai 1:1; Zekaria 1:1) Kwa kuwa Wayahudi walichochewa na wajumbe wa Mungu na kuthibitishiwa kwamba Yehova angewasaidia, walianza tena kazi ya kujenga hekalu, nao wakalimaliza mwaka wa 515 K.W.K.—Ezra 6:14, 15.

7. Hali katika siku za Hagai na Zekaria zinalinganaje na hali za leo?

7 Je, unajua mambo yote hayo yanatuhusuje? Tuna kazi ya kuhubiri “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Kazi hiyo ilitiliwa maanani zaidi baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Kama vile Wayahudi wa kale walivyowekwa huru kutoka utekwani Babiloni, watu wa Yehova wa leo waliwekwa huru kutoka katika utekwa wa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini za uwongo. Watiwa-mafuta wa Mungu walifanya kwa bidii kazi ya kuhubiri, kufundisha, na kuelekeza watu kwenye ibada ya kweli. Kazi hiyo inaendelea leo kwa kadiri kubwa hata zaidi, na huenda unaifanya. Huu ndio wakati wa kuifanya kwa kuwa mwisho wa mfumo huu mbovu uko karibu! Lazima kazi hiyo tuliyopewa na Mungu iendelee mpaka aingilie kati shughuli za wanadamu wakati wa “dhiki kuu.” (Mathayo 24:21) Wakati huo uovu utakomeshwa, na hilo litawezesha ibada ya kweli kusitawi kila mahali duniani.

8. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu atatusaidia katika kazi yetu?

8 Kama vile unabii wa Hagai na Zekaria unavyoonyesha, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia na kutubariki tunapoendelea kufanya kazi hiyo kwa moyo wote. Licha ya jitihada za wengine za kuwazuia watumishi wa Mungu au kupiga marufuku kazi waliyopewa, hakuna serikali ambayo imefaulu kukomesha kazi ya kuhubiri. Fikiria jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi ya Ufalme kwa kuleta ongezeko kwa miaka mingi tangu Vita vya Kwanza vya Ulimwengu mpaka wakati huu. Lakini, bado kuna mengi ya kufanya.

9. Tunapaswa kufikiria hali gani iliyotukia kale, na kwa nini?

9 Mambo tunayojifunza katika unabii wa Hagai na Zekaria yanaweza kutuchocheaje hata zaidi kutii amri ya Mungu ya kuhubiri na kufundisha? Acheni tuone mambo kadhaa ambayo tunaweza kujifunza kutokana na vitabu hivyo viwili vya Biblia. Kwa mfano, fikiria mambo machache kuhusiana na kazi ya ujenzi wa hekalu ambayo Wayahudi waliorudishwa walipaswa kufanya. Kama ilivyotajwa, Wayahudi waliorudi Yerusalemu kutoka Babiloni hawakuendelea kufanya kazi ya ujenzi wa hekalu. Baada ya kuweka msingi wa hekalu, bidii yao ilididimia. Walianza kuwa na maoni gani yasiyofaa? Nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na hilo?

Maoni Yanayofaa Kuhusu Mali

10. Wayahudi walisitawisha maoni gani yasiyofaa, na matokeo yakawaje?

10 Wayahudi waliorudishwa walikuwa wakisema: “Wakati haujaja.” (Hagai 1:2) Walipoanza kazi ya kujenga hekalu, kwa kuweka msingi mwaka wa 536 K.W.K., hawakusema “wakati haujaja.” Lakini, baada ya muda usio mrefu waliruhusu upinzani kutoka kwa majirani na serikali uwaathiri. Wayahudi walianza kuhangaikia nyumba zao na starehe zao wenyewe. Kwa kuwa nyumba zao zilizofunikwa kwa mbao bora zilikuwa tofauti sana zikilinganishwa na hekalu ambalo halikuwa limemalizika, Yehova aliuliza hivi: “Je, huu ni wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenu zilizofunikwa kwa mbao, huku nyumba hii ikiwa imeharibika?”—Hagai 1:4.

11. Kwa nini Yehova aliwashauri Wayahudi wa siku za Hagai?

11 Naam, Wayahudi walibadili maoni yao kuhusu mambo yaliyo muhimu. Badala ya kutanguliza kusudi la Yehova la kujenga hekalu, watu wa Mungu walijihangaikia wenyewe na nyumba zao. Walipuuza ujenzi wa nyumba ya Mungu ya ibada. Neno la Yehova kwenye Hagai 1:5 liliwahimiza Wayahudi ‘waweke moyo wao juu ya njia zao.’ Yehova alitaka watafakari mambo waliyokuwa wakifanya na kufikiria hasara walizokuwa wakipata kwa sababu ya kutotanguliza ujenzi wa hekalu maishani mwao.

12, 13. Andiko la Hagai 1:6 linaelezaje hali ya Wayahudi, na mstari huo unamaanisha nini?

12 Kwa kuwa Wayahudi walitanguliza mambo yasiyofaa, walipata hasara wao wenyewe. Ona maoni ya Mungu kwenye Hagai 1:6: “Mmepanda mbegu nyingi, lakini mavuno ni kidogo. Mnakula chakula, lakini hamshibi. Mnakunywa, lakini hamlewi. Mnavaa nguo, lakini hakuna yeyote anayepata joto; na yeye anayeajiriwa, anaajiriwa kwa ajili ya mfuko wenye matundu.”

13 Ingawa Wayahudi walikuwa katika nchi ambayo Mungu alikuwa amewapa, haikutokeza mazao kama walivyotazamia. Yehova hakuwabariki, kama alivyokuwa ameonya mapema. (Kumbukumbu la Torati 28:38-48) Bila msaada wake, Wayahudi walipanda mbegu lakini wakapata mavuno kidogo, naam, chakula kidogo ambacho hakikuwashibisha. Bila baraka zake, hawangeweza kujivika nguo zenye joto. Ni kana kwamba pesa walizochuma zilitiwa katika mfuko uliojaa matundu, kwa kuwa hazikuwafaidi wale waliozichuma. Namna gani maneno haya: “Mnakunywa, lakini hamlewi”? Kwa kuwa Mungu anashutumu ulevi, maneno hayo hayamaanishi kwamba kulewa kungeonyesha baraka zake. (1 Samweli 25:36; Methali 23:29-35) Badala yake, maneno hayo yanakazia tena jinsi Wayahudi walivyokosa baraka za Mungu. Kiasi chochote cha divai ambacho wangetengeneza kingekuwa kidogo, kisichoweza kulewesha. Biblia Habari Njema hutafsiri Hagai 1:6 hivi: “Mnakunywa divai, lakini hamtosheki.”

14, 15. Tunajifunza nini katika Hagai 1:6?

14 Mambo tunayojifunza kuhusu nyumba za Wayahudi, hayatufundishi kupamba nyumba. Muda mrefu kabla ya Wayahudi kupelekwa uhamishoni, nabii Amosi aliwakemea matajiri katika Israeli kwa sababu ya “nyumba [zao] za pembe za tembo” na jinsi ‘walivyojilaza katika vitanda vya pembe za tembo.’ (Amosi 3:15; 6:4) Nyumba hizo zenye madoido na vyombo vya mbao vilivyopambwa hazikudumu. Vitu hivyo vyote viliporwa na maadui waliowashinda. Hata hivyo, miaka mingi baadaye, baada ya kuwa uhamishoni kwa miaka 70, wengi kati ya watu wa Mungu hawakuwa wamejifunza kutokana na matukio hayo. Je, sisi tutajifunza? Inafaa kila mmoja wetu ajiulize: ‘Mimi huhangaikia nyumba yangu na mapambo yake kwa kadiri gani? Namna gani kupata elimu ya ziada ili kupandishwa cheo kazini ingawa jambo hilo litanichukua miaka mingi na kunizuia nisifanye mambo muhimu ya kiroho?’—Luka 12:20, 21; 1 Timotheo 6:17-19.

15 Mambo tunayoyasoma kwenye Hagai 1:6 yanapaswa kutuonyesha kwamba tunahitaji baraka za Mungu maishani mwetu. Wayahudi hao wa kale walikosa baraka hizo, nao wakaumia. Iwe tuna mali nyingi au la, tukikosa baraka za Yehova, hakuna shaka kwamba tutaathiriwa kiroho. (Mathayo 25:34-40; 2 Wakorintho 9:8-12) Lakini, tunaweza kupataje baraka hizo?

Yehova Hutoa Msaada Kupitia Roho Yake

16-18. Andiko la Zekaria 4:6 lilimaanisha nini kwa Wayahudi wa kale?

16 Zekaria, aliyekuwa nabii kama Hagai, alichochewa kukazia njia ambayo Yehova alitumia kuwachochea na kuwabariki watu waliojitoa kwake wakati huo. Jambo hilo linaonyesha jinsi atakavyokubariki pia. Tunasoma hivi: “‘Si kwa jeshi, wala kwa nguvu, bali kwa roho yangu,’ Yehova wa majeshi amesema.” (Zekaria 4:6) Huenda umesikia andiko hilo likinukuliwa mara nyingi, lakini lilimaanisha nini kwa Wayahudi wa siku za Hagai na Zekaria, nalo lina umuhimu gani kwako?

17 Kumbuka kwamba maneno ya Hagai na Zekaria yaliyoongozwa kwa roho ya Mungu yalikuwa na matokeo mazuri wakati huo. Mambo ambayo manabii hao wawili walisema yaliwaimarisha Wayahudi waaminifu. Hagai alianza kutoa unabii katika mwezi wa sita, mwaka wa 520 K.W.K. Zekaria alianza kutoa unabii katika mwezi wa nane mwaka huohuo. (Zekaria 1:1) Kulingana na Hagai 2:18, kazi ya kuweka msingi ilianza tena kwa bidii katika mwezi wa tisa. Kwa hiyo, Wayahudi walichochewa kutenda, nao walimtii Yehova wakiwa na hakika kwamba angewategemeza. Naam, maneno ya Zekaria 4:6 yanazungumzia msaada wa Mungu.

18 Wayahudi waliporudi katika nchi yao mwaka wa 537 K.W.K., hawakuwa na jeshi. Hata hivyo, Yehova aliwalinda na kuwaongoza walipokuwa safarini kutoka Babiloni. Isitoshe, roho yake ilikuwa ikielekeza mambo walipoanza ujenzi wa hekalu muda mfupi baadaye. Ikiwa wangerudia kazi hiyo kwa bidii tena, angewasaidia kupitia roho yake takatifu.

19. Roho ya Mungu ilishinda uvutano gani wenye nguvu?

19 Kupitia mfululizo wa maono manane, Zekaria alihakikishiwa kwamba Yehova angekuwa pamoja na watu wake ambao wangeendelea kwa uaminifu kufanya kazi ya kujenga hekalu na kuimaliza. Maono ya nne, yaliyoandikwa katika sura ya 3, yanaonyesha kwamba Shetani alikuwa anajitahidi kuzuia jitihada za Wayahudi za kumaliza kujenga hekalu. (Zekaria 3:1) Bila shaka, Shetani hangefurahi kumwona Kuhani Mkuu Yoshua akiwatumikia watu kwenye hekalu jipya. Ingawa Ibilisi alijitahidi kuwazuia Wayahudi wasijenge hekalu, roho ya Yehova ilitimiza sehemu muhimu katika kuondoa vizuizi na kuwaimarisha Wayahudi waendelee na kumaliza ujenzi wa hekalu.

20. Roho takatifu iliwasaidiaje Wayahudi kufanya mapenzi ya Mungu?

20 Kulikuwa na upinzani mwingi uliokuwa kama mlima kutoka kwa maofisa wa serikali ambao walipiga marufuku kazi ya ujenzi. Hata hivyo, Yehova aliahidi kwamba “mlima” huo ungeondolewa na kuwa “nchi tambarare.” (Zekaria 4:7) Hivyo ndivyo ilivyokuwa! Mfalme Dario wa Kwanza alifanya uchunguzi, naye akagundua hati ya Koreshi ya kumbukumbu, ambayo iliwaruhusu Wayahudi kujenga upya hekalu. Basi, Dario akaondoa marufuku hayo, naye akaamuru kwamba Wayahudi wapewe pesa kutoka katika hazina ya kifalme ili kulipia gharama za ujenzi. Hilo lilikuwa badiliko lililoje! Je, roho ya Mungu ilihusika? Bila shaka. Ujenzi wa hekalu ulikamilishwa mwaka wa 515 K.W.K., katika mwaka wa sita wa utawala wa Dario wa Kwanza. —Ezra 6:1, 15.

21. (a) Katika nyakati za kale, Mungu ‘alitikisaje mataifa yote,’ na “vitu vyenye kutamanika” vilitokaje? (b) Unabii huo umetimiaje leo?

21 Kwenye Hagai 2:5, nabii huyo aliwakumbusha Wayahudi agano ambalo Mungu alikuwa amefanya pamoja nao katika Mlima Sinai wakati “mlima wote ulikuwa ukitetemeka sana.” (Kutoka 19:18) Katika siku za Hagai na Zekaria, Yehova alikusudia kutikisa mambo tena, kama mstari wa 6 na 7 unavyoonyesha. Milki ya Uajemi ingekumbwa na misukosuko, lakini kazi ya ujenzi wa hekalu ingesonga mbele mpaka ikamilike. Watu fulani ambao hawakuwa Wayahudi, yaani, vile “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote,” wangejiunga na Wayahudi kumtukuza Mungu katika mahali hapo pa ibada. Leo, kwa njia kubwa, Mungu ‘ametikisa mataifa’ kupitia kazi yetu ya kuhubiri, na “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote” vimeingia kumwabudu Mungu pamoja na mabaki ya watiwa-mafuta. Naam, sasa watiwa-mafuta na kondoo wengine wanaijaza nyumba ya Yehova utukufu. Waabudu hao wa kweli wanatazamia kwa imani wakati ambapo Yehova ‘atatikisa mbingu na dunia’ katika njia nyingine. Hilo litafanywa ili kupindua na kuangamiza nguvu za falme za mataifa. —Hagai 2:22.

22. Mataifa ‘yanatikiswaje,’ na matokeo ni nini, na ni mambo gani yatakayotukia wakati ujao?

22 Unabii huo unatukumbusha misukosuko ambayo imetokea katika sehemu mbalimbali zinazofananishwa na “mbingu na dunia na bahari na nchi kavu.” Kwanza, Shetani Ibilisi na roho waovu wake walitupwa duniani. (Ufunuo 12:7-12) Isitoshe, kazi ya kuhubiri inayoongozwa na watiwa-mafuta wa Mungu imetikisa sehemu za kidunia za mfumo huu wa mambo. (Ufunuo 11:18) Licha ya hayo yote, “umati mkubwa” wa vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote umejiunga na Waisraeli wa kiroho katika kumtumikia Yehova. (Ufunuo 7:9, 10) Umati huo mkubwa unashirikiana na Wakristo watiwa-mafuta katika kuhubiri habari njema kwamba hivi karibuni Mungu atayatikisa mataifa kwenye Har–Magedoni. Tukio hilo litawezesha ibada ya kweli ifanywe kuwa kamilifu duniani pote.

Je, Unakumbuka?

• Hagai na Zekaria walitumikia wakati gani na katika hali gani?

• Unaweza kutumiaje ujumbe wa Hagai na Zekaria?

• Kwa nini andiko la Zekaria 4:6 linatia moyo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 20]

Maandishi ya Hagai na Zekaria yanatuhakikishia kwamba Mungu atatusaidia

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Je, huu ni wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenu zilizofunikwa kwa mbao, huku nyumba hii ikiwa imeharibika?”

[Picha katika ukurasa wa 24]

Watu wa Yehova huwafikia ‘watu wenye kutamanika wa mataifa’