Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilipata ‘Maombi ya Moyo Wangu’

Nilipata ‘Maombi ya Moyo Wangu’

Simulizi la Maisha

Nilipata ‘Maombi ya Moyo Wangu’

LIMESIMULIWA NA DOMINIQUE MORGOU

Mwishowe, nilifika Afrika mnamo Desemba 1998! Ndoto yangu ya utotoni ilitimia. Nilivutiwa na maeneo makubwa yasiyo na kitu ya Afrika pamoja na wanyama wa pori wenye kustaajabisha wanaopatikana huko. Sasa nilikuwa nimefika Afrika! Wakati huohuo, ndoto yangu nyingine pia ilikuwa imetimia. Sasa nilikuwa mhubiri wa wakati wote katika nchi ya kigeni. Kwa watu wengi, hilo lingeonekana kuwa jambo lisilowezekana. Siwezi kuona vizuri, nami hutembea kwenye barabara za mchanga katika vijiji vya Afrika huku nikiongozwa na mbwa aliyezoezwa kuwaongoza vipofu katika barabara za majiji ya Ulaya. Acha niwaeleze jinsi ambavyo nilianza kutumikia huko Afrika na jinsi ambavyo Yehova alinipa ‘maombi ya moyo wangu.’—Zaburi 37:4.

NILIZALIWA mnamo Juni 9, 1966, kusini mwa Ufaransa. Mimi ni kitinda-mimba katika familia yenye watoto saba, wavulana wawili na wasichana watano. Sote tulitunzwa na wazazi wenye upendo. Hata hivyo, kuna jambo fulani lenye kuhuzunisha lililonipata nilipokuwa mtoto. Kama nyanya yangu, mama yangu, na dada yangu mmoja, nimerithi ugonjwa ambao hatimaye humfanya mtu kuwa kipofu.

Kabla ya kufikisha umri wa miaka 20, nilikabili ubaguzi, chuki, na unafiki, na mambo hayo yalifanya niwe mwasi katika jamii. Katika kipindi hicho kigumu tulihamia eneo la Hérault. Tukiwa huko, jambo la pekee lilitendeka.

Jumapili moja asubuhi, Mashahidi wa Yehova wawili walikuja nyumbani kwetu. Mama yangu aliwajua, naye akawakaribisha ndani. Mmoja wa wanawake hao alimuuliza Mama ikiwa anakumbuka kwamba wakati fulani aliahidi angekubali kujifunza Biblia. Mama alikumbuka, kisha akauliza, “Tutaanza wakati gani?” Walipanga wakutane kila Jumapili asubuhi, na hivyo ndivyo mama yangu alivyoanza kujifunza “kweli ya habari njema.”—Wagalatia 2:14.

Kupata Ufahamu

Mama alijitahidi sana kuelewa na kukumbuka mambo aliyojifunza. Kwa kuwa alikuwa kipofu, ilimbidi aweke kila kitu akilini. Mashahidi walimvumilia sana. Mashahidi hao walipokuja, nilikuwa nikijificha chumbani mwangu hadi walipoondoka. Hata hivyo, alasiri moja, tulikutana na mmoja wa Mashahidi hao anayeitwa Eugénie, naye akazungumza nami. Aliniambia kwamba Ufalme wa Mungu utakomesha kabisa unafiki, chuki, na ubaguzi uliomo ulimwenguni. Aliniambia hivi, “Ni Mungu tu aliye na suluhisho.” Kisha akaniuliza ikiwa ningependa kujua mengi zaidi. Siku iliyofuata, nikaanza kujifunza Biblia.

Mambo yote niliyojifunza yalikuwa mapya kwangu. Sasa nilielewa kwamba Mungu anaruhusu uovu duniani kwa muda fulani kwa sababu nzuri. (Mwanzo 3:15; Yohana 3:16; Waroma 9:17) Pia, nilielewa kwamba Yehova hajatuacha bila tumaini. Ametupa ahadi nzuri ya uzima wa milele katika paradiso duniani. (Zaburi 37:29; 96:11, 12; Isaya 35:1, 2; 45:18) Katika Paradiso hiyo, nitapata tena uwezo wa kuona, ambao nilikuwa nikipoteza pole kwa pole.—Isaya 35:5.

Kuanza Utumishi wa Wakati Wote

Mnamo Desemba 12, 1985, nilionyesha kwamba nimejiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa katika maji, kama vile dada yangu Marie-Claire alivyokuwa amefanya. Baadaye, ndugu yangu Jean-Pierre alibatizwa, halafu mama yangu mpendwa akachukua hatua hiyo pia.

Katika kutaniko nililoshirikiana nalo, kulikuwa na mapainia wa kawaida kadhaa, yaani, wahubiri wa wakati wote. Shangwe na shauku yao kwa ajili ya huduma ilinitia moyo. Hata Marie-Claire, ambaye alilazimika kuvaa kifaa cha kurekebisha kasoro za mifupa kwenye mguu mmoja huku akiwa na ugonjwa wa macho, alianza utumishi wa wakati wote. Hadi leo, anaendelea kunitia moyo kiroho. Kwa kuwa nilishirikiana na mapainia katika kutaniko na katika familia, nilisitawisha tamaa kubwa ya kuwa mtumishi wa wakati wote. Hivyo, mnamo Novemba 1990, nilianza kutumikia nikiwa painia huko Béziers.—Zaburi 94:17-19.

Kukabiliana na Hali ya Kuvunjika Moyo

Nilipokuwa katika huduma, mapainia wengine walinitunza. Hata hivyo, mara kwa mara, nilivunjika moyo kwa sababu singeweza kutimiza mambo fulani, nami nilitamani kufanya zaidi. Lakini Yehova alinitegemeza nilipovunjika moyo. Nilifanya utafiti katika kitabu Watch Tower Publications Index, na kutafuta masimulizi ya maisha ya mapainia ambao walikuwa na matatizo ya kuona kama mimi. Nilishangaa kupata masimulizi mengi sana! Masimulizi hayo yenye kutia moyo yalinifundisha kuthamini mambo ambayo ningeweza kutimiza na kutambua mipaka yangu.

Ili kutosheleza mahitaji yangu, nilisafisha maduka makubwa pamoja na Mashahidi wengine. Siku moja nilitambua kwamba wafanyakazi wenzangu walirudia kusafisha sehemu ambazo nilikuwa nimesafisha. Ni wazi kwamba nilikuwa nikiacha uchafu mwingi. Nilienda kumwona Valérie, painia ambaye alisimamia kikundi chetu cha usafishaji, nami nikamwomba anieleze waziwazi ikiwa nilikuwa nikiwatatiza. Valérie aliacha niamue wakati ambapo nilihisi kwamba singeweza tena kufanya kazi hiyo. Mnamo Machi 1994, niliacha kazi hiyo ya usafishaji.

Kwa mara nyingine tena, nilihisi kwamba mimi ni bure. Nilisali kwa Yehova kwa bidii, nami ninajua kwamba alisikiliza sala zangu. Nilipata msaada mkubwa kwa kujifunza Biblia na vichapo vya Kikristo. Ingawa macho yangu yalikuwa yakizidi kudhoofika, tamaa yangu ya kumtumikia Yehova ilizidi kuimarika. Ningefanya nini?

Kungoja Kwanza, Kisha Kufanya Uamuzi wa Haraka

Nilituma ombi ili nizoezwe katika Kituo cha Kuwasaidia Vipofu na Watu Wenye Matatizo ya Kuona huko Nîmes, na baadaye nikakubaliwa kupokea mazoezi kwa miezi mitatu. Mazoezi hayo yalinisaidia sana. Nilielewa tatizo langu na jinsi ninavyoweza kukabiliana nalo. Kushirikiana na watu waliokuwa na magonjwa mbalimbali kulinisaidia kutambua jinsi tumaini langu la Kikristo lilivyo lenye thamani sana. Angalau nilikuwa na kusudi maishani, nami ningeweza kutimiza jambo fulani muhimu. Isitoshe, nilijifunza maandishi ya vipofu ya Kifaransa.

Niliporudi nyumbani, watu wa familia walitambua kwamba mazoezi hayo yalinisaidia sana. Hata hivyo, sikufurahia ile fimbo nyeupe niliyolazimika kutumia. Ilikuwa vigumu kwangu kukizoea “kijiti” hicho. Nilitamani kupata msaada mwingine, kama vile kuongozwa na mbwa.

Nilijiandikisha ili nipate mbwa lakini nikaambiwa watu wengi sana wamejiandikisha. Isitoshe, shirika ambalo lingenipa mbwa lilipaswa kufanya uchunguzi kwanza. Si mtu yeyote tu anayepewa mbwa wa kumwongoza. Siku moja mwanamke anayesimamia shirika fulani la vipofu aliniambia kwamba kilabu fulani cha mchezo wa tenisi kinakusudia kutoa mbwa wa kumwongoza kipofu au mtu mwenye matatizo ya kuona katika eneo letu. Alisema kwamba alikuwa amenifikiria. Je, ningekubali msaada huo? Nilitambua kwamba Yehova ndiye aliyeongoza mambo, nami nikakubali msaada huo. Hata hivyo, ilinibidi nisubiri kabla ya kupata mbwa huyo.

Naendelea Kufikiria Afrika

Nilipokuwa nikisubiri, nilianza kufikiria jambo lingine. Kama ilivyotajwa awali, tangu utotoni nilivutiwa sana na Afrika. Ingawa uwezo wangu wa kuona ulikuwa ukidhoofika, tamaa yangu ya kwenda Afrika ilizidi hasa niliposikia kwamba watu wengi huko Afrika wanapenda Biblia na wanapenda kumtumikia Yehova. Kitambo kidogo, nilikuwa nimemwambia Valérie kimchezo kwamba ningependa kutembelea Afrika. Je, angekubali kwenda pamoja nami? Alikubali, nasi tukaandikia ofisi kadhaa za tawi za Mashahidi wa Yehova katika nchi za Afrika zinazozungumza Kifaransa.

Tulipokea jibu kutoka Togo. Nilisisimuka sana, nami nikamwomba Valérie anisomee barua hiyo. Barua hiyo ilinitia moyo sana. Basi, Valérie akasema: “Kwa nini tusiende?” Baada ya kuwasiliana na akina ndugu katika ofisi ya tawi ya Togo, nilielekezwa kwa Sandra, painia anayeishi katika jiji kuu la Lomé. Tuliamua kuanza safari yetu Desemba 1, 1998.

Mambo yalikuwa tofauti sana, lakini yalifurahisha! Tulipofika Lomé, tulitoka ndani ya ndege na kuhisi joto jingi la Afrika. Sandra alikuja kutupokea. Hatukuwa tumewahi kuonana, lakini mara moja tulihisi kwamba sisi ni marafiki wa miaka mingi. Muda mfupi baada ya kufika, Sandra na painia mwenzake, Christine, walikuwa wamewekwa kuwa mapainia wa pekee huko Tabligbo, mji mdogo ulio nje ya jiji kuu. Sasa tulipata pendeleo la kujiunga nao katika mgawo wao mpya. Tulikaa huko kwa miezi miwili hivi, na tulipoondoka, nilijua ningerudi.

Nafurahia Kurudi

Nilipofika Ufaransa, mara moja nilianza kujitayarisha kwa ajili ya safari ya pili ya kwenda Togo. Kwa msaada wa watu wa familia yetu, niliweza kufanya mipango ili nikae huko kwa miezi sita. Hivyo, mnamo Septemba 1999, nilipanda ndege tena kwenda Togo. Hata hivyo, wakati huu nilisafiri peke yangu. Hebu wazia jinsi watu wa familia yetu walivyohisi waliponiona nikiondoka peke yangu ingawa sikuweza kuona vizuri! Lakini hawakuwa na sababu ya kuhangaika. Niliwahakikishia wazazi wangu kwamba rafiki zangu, ambao tayari walikuwa kama watu wa familia kwangu, wangeningojea huko Lomé.

Nilifurahia sana kurudi katika eneo lenye watu wengi sana wanaopendezwa na Biblia! Ni kawaida kuona watu wakisoma Biblia barabarani. Huko Tabligbo, watu wanaweza kukuita ili mzungumzie tu Biblia. Lilikuwa pendeleo kubwa sana kuishi pamoja na dada hao wawili ambao ni mapainia wa pekee katika makao yao madogo! Nilipata kufahamiana na utamaduni tofauti, na mtazamo wangu ukabadilika. Kwanza kabisa, nilitambua kwamba ndugu na dada zangu Wakristo huko Afrika hutanguliza mambo ya Ufalme maishani mwao. Kwa mfano, hawakosi kuhudhuria mikutano ingawa wanalazimika kutembea kilometa nyingi. Pia, nilijifunza mambo mengi kutokana na shauku na ukarimu wao.

Siku moja tulipokuwa tukitoka kwenye huduma ya shambani, nilimweleza Sandra kwamba sikutaka kurudi Ufaransa. Tatizo langu la kuona lilikuwa limezidi. Nilifikiri kuhusu barabara zilizosongamana na zenye kelele huko Béziers, ngazi zilizo kwenye majengo ya orofa, na kuhusu mambo mengine mengi yanayoweza kumhangaisha mtu asiyeweza kuona vizuri. Lakini, ijapokuwa barabara za Tabligbo hazijatiwa lami, zina utulivu na hakuna watu wengi wala magari mengi. Ningewezaje kufaulu kuishi Ufaransa baada ya kuzoea kuishi Tabligbo?

Siku mbili baadaye, mama yangu alinipigia simu kunijulisha kwamba nilikuwa nikisubiriwa na shule ya kuwazoeza mbwa wa kuwaongoza vipofu. Sasa ningeongozwa na mbwa mchanga aina ya Labrador anayeitwa Océane. Kwa mara nyingine tena, mahitaji yangu yalitoshelezwa na mahangaiko yangu yakatoweka. Baada ya kutumikia kwa furaha kwa miezi sita huko Tabligbo, nilirudi Ufaransa ili kukutana na Océane.

Baada ya kuzoezwa kwa miezi kadhaa, nilikabidhiwa Océane. Mwanzoni, haikuwa rahisi. Ilitubidi tujifunze kuelewana. Hata hivyo, hatua kwa hatua nilitambua kwamba nilimhitaji sana Océane. Sasa Océane amekuwa sehemu ya maisha yangu. Watu wa Béziers walitendaje waliponiona nikiwatembelea nikiwa na mbwa? Walinitendea kwa heshima nyingi na fadhili. Océane akawa kipenzi cha watu katika eneo hilo. Kwa kuwa watu wengi huwa na wasiwasi wanapokuwa pamoja na mtu mwenye kasoro fulani, kutembea na mbwa kulinisaidia kuzungumza kuhusu tatizo langu bila wasiwasi. Watu walitulia na kunisikiliza. Naam, Océane akawa njia bora ya kuanzisha mazungumzo.

Naenda Afrika Pamoja na Océane

Sikuwa nimesahau Afrika, na sasa nilijitayarisha kurudi kwa mara ya tatu. Wakati huo, nilienda pamoja na Océane. Pia, nilienda pamoja na wenzi wa ndoa vijana walioitwa Anthony na Aurore, na vilevile rafiki yangu Caroline, ambao ni mapainia kama mimi. Mnamo Septemba 10, 2000, tulifika Lomé.

Mwanzoni, watu wengi walimwogopa Océane. Ni watu wachache tu huko Lomé ambao walikuwa wamemwona mbwa mkubwa hivyo, kwa kuwa mbwa wengi wa Togo ni wadogo. Walipoona mshipi wa kumwongoza, wengine walifikiri ni mnyama mkali ambaye anahitaji kuzuiwa. Océane alikuwa tayari kunilinda kutokana na kitu chochote ambacho aliona ni hatari. Hata hivyo, baada ya muda usio mrefu, Océane alizoea hali hiyo mpya. Anapofungwa mshipi, yeye huwa mtiifu na mwenye kutegemeka, huku akiwa kando yangu. Anapofunguliwa, yeye hupenda kucheza na hata huwa mtukutu. Sisi hufurahia sana kucheza pamoja.

Sote tulialikwa kukaa pamoja na Sandra na Christine huko Tabligbo. Ili kuwasaidia ndugu na dada wa eneo hilo kumzoea Océane, tuliwaalika watutembelee na kuwaeleza kusudi la mbwa wa kumwongoza kipofu, sababu iliyofanya nimhitaji, na jinsi wanavyopaswa kutenda wanapokuwa karibu naye. Wazee walikubali Océane aandamane nami kwenye Jumba la Ufalme. Kwa kuwa huo ulikuwa mpango mpya huko Togo, kutaniko lilitangaziwa jambo hilo. Océane aliandamana nami kwenye huduma nilipokuwa nikifanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia tu—katika hali ambazo watu wangeweza kuelewa kwa nini ninaandamana na mbwa.

Inafurahisha sana kuhubiri katika eneo hili. Sikuzote niliguswa moyo nilipoona jinsi watu walivyonijali kupitia matendo yao ya fadhili, kama vile kunipa kiti. Mnamo Oktoba 2001, mama yangu alisafiri pamoja nami katika safari yangu ya nne ya kwenda Togo. Baada ya majuma matatu, alirudi Ufaransa huku akiwa na furaha na uhakika kwamba mimi ni mzima.

Namshukuru sana Yehova kwamba nimeweza kutumikia nchini Togo. Nina hakika kwamba Yehova ataendelea kunipa ‘maombi ya moyo wangu’ ninapoendelea kutumia yote niliyo nayo ili kumtumikia. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 37 Dada Morgou alirudi Ufaransa, kisha akarudi Togo kuanzia Oktoba 6, 2003 hadi Februari 6, 2004. Kwa kusikitisha, kwa sababu ya matatizo ya afya, huenda hataweza kurudi Togo katika mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, bado tamaa yake kubwa zaidi ni kumtumikia Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Nilivutiwa na maeneo makubwa yasiyo na kitu ya Afrika pamoja na wanyama wa pori wenye kustaajabisha wanaopatikana huko

[Picha katika ukurasa wa 10]

Océane aliandamana nami katika ziara za kurudia

[Picha katika ukurasa wa 11]

Wazee walikubali niende mikutanoni pamoja na Océane