Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kifo Kimemezwa Milele”

“Kifo Kimemezwa Milele”

“Kifo Kimemezwa Milele”

WAZIA kwamba unasoma gazeti lililo na kichwa kilicho juu badala ya kusoma kumhusu msichana mdogo ambaye amejiua. Ni wazi kwamba hakuna gazeti ambalo limewahi kuwa na kichwa kama hicho. Lakini maneno hayo yanapatikana katika kitabu kilichoandikwa maelfu ya miaka iliyopita, yaani, Biblia.

Ukweli kuhusu kifo unaelezwa waziwazi katika Maandiko. Isitoshe, Biblia haielezi tu kwa nini tunakufa, bali pia inaeleza hali ya wafu na tumaini la wapendwa wetu waliokufa. Kisha, inaonyesha kwamba siku moja itawezekana kusema hivi: “Kifo kimemezwa milele.”—1 Wakorintho 15:54.

Biblia inazungumzia kifo kwa kutumia maneno rahisi wala si maneno magumu yasiyoeleweka. Kwa mfano, mara nyingi inalinganisha kifo na “usingizi,” na inasema kwamba wafu ‘wanalala usingizi katika kifo.’ (Zaburi 13:3; 1 Wathesalonike 4:13; Yohana 11:11-14) Kifo kinatajwa pia kuwa “adui.” (1 Wakorintho 15:26) Jambo muhimu zaidi ni kwamba Biblia inatuwezesha kuelewa kwa nini kifo kinalinganishwa na usingizi, kwa nini wanadamu hufa, na jinsi adui huyo atakavyoshindwa hatimaye.

Kwa Nini Tunakufa?

Kitabu cha kwanza katika Biblia kinaeleza kwamba Mungu alimuumba mtu wa kwanza, Adamu, na kumpa makao katika paradiso. (Mwanzo 2:7, 15) Baada ya kuumbwa, Adamu alipewa kazi, na vilevile sheria iliyomkataza katakata asile matunda ya mti fulani katika bustani ya Edeni. Mungu alimwambia hivi kuhusu matunda ya mti huo: “Usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.” * (Mwanzo 2:17) Kwa hiyo, Adamu alielewa kwamba angeweza kuepuka kifo. Angekufa tu kama angevunja sheria ya Mungu.

Inahuzunisha kwamba Adamu na mkewe Hawa hawakutii. Waliamua kupuuza mapenzi ya Muumba wao, nao wakapatwa na matokeo mabaya ya uamuzi wao. Alipotaja matokeo ya dhambi hiyo Mungu alisema hivi: “Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Walitiwa dosari kubwa, yaani, kutokamilika. Wangekufa kwa sababu ya kutokamilika au dhambi.

Wazao wa Adamu na Hawa, yaani wanadamu wote, walirithi dosari hiyo ya dhambi. Kwa hiyo, dhambi inaweza kulinganishwa na ugonjwa unaorithiwa. Adamu alipoteza taraja la kuishi milele bila kufa, na wazao wake walirithi kutokamilika kutoka kwake. Wanadamu wakaja kuwa watumwa wa dhambi. Biblia inasema hivi: “Hiyo ndiyo sababu, kama vile kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 5:12.

“Dhambi Iliingia Katika Ulimwengu”

Dosari hiyo inayorithiwa, au dhambi, si kitu kinachoonekana. “Dhambi” ni kasoro ya maadili na ya kiroho ambayo sisi tumerithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza nayo inaathiri miili yetu. Hata hivyo, Biblia inafunua kwamba Mungu ameandaa suluhisho. Mtume Paulo anaeleza hivi: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” (Waroma 6:23) Katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, Paulo anaongeza uhakikisho huu aliouona kuwa muhimu sana: “Kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.”—1 Wakorintho 15:22.

Ni wazi kwamba Yesu Kristo ana sehemu muhimu katika mpango wa kumaliza dhambi na kifo. Alisema kwamba alikuja duniani “kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Hali hiyo inafanana na utekaji-nyara. Mtu aliyetekwa nyara huachiliwa tu baada ya kiasi fulani cha pesa kulipwa kama fidia. Fidia inayoweza kutuweka huru na dhambi na kifo ni uhai mkamilifu wa Yesu. *Matendo 10:39-43.

Ili kuandaa fidia, Mungu alimtuma Yesu duniani atoe uhai wake uwe dhabihu. “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini . . . awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Kabla hajafa na kutoa uhai wake uwe dhabihu, Kristo ‘alitoa ushahidi juu ya ile kweli.’ (Yohana 18:37) Na wakati wa huduma yake duniani, alitumia nafasi mbalimbali kufunua ukweli kuhusu kifo.

“Msichana Mdogo . . . Analala Usingizi”

Kifo hakikuwa jambo geni kwa Yesu alipokuwa duniani. Alishikwa na majonzi wakati watu aliowafahamu walipokufa, na alijua kwamba yeye mwenyewe angeuawa. (Mathayo 17:22, 23) Yaelekea, Lazaro aliyekuwa rafiki wa karibu wa Yesu alikufa miezi michache kabla ya Yesu kuuawa. Tukio hilo linatusaidia kuelewa maoni ya Yesu kuhusu kifo.

Punde baada ya kupata habari kwamba Lazaro amekufa, Yesu alisema hivi: “Lazaro rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda huko ili kumwamsha kutoka usingizini.” Wanafunzi walidhani kwamba ikiwa Lazaro anapumzika tu, atapona. Kwa hiyo, Yesu akasema wazi: “Lazaro amekufa.” (Yohana 11:11-14) Ni wazi kwamba Yesu alikiona kifo kuwa kama usingizi. Ingawa inaweza kuwa vigumu kuelewa kifo ni nini, tunaelewa usingizi. Tunapolala fofofo, hatujui kwamba wakati unapita wala hatufahamu mambo yanayotendeka. Hivyo ndivyo Biblia inavyofafanua hali ya wafu. Andiko la Mhubiri 9:5 linasema hivi: ‘Wafu hawajui lolote kamwe.’

Pia, Yesu alilinganisha kifo na usingizi kwa sababu kwa nguvu za Mungu watu wanaweza kuamshwa kutoka katika kifo. Siku moja Yesu alitembelea familia yenye huzuni. Msichana mdogo katika familia hiyo alikuwa amekufa. Yesu alisema: “Msichana mdogo hakufa, bali analala usingizi.” Kisha akamkaribia yule msichana aliyekufa na kushika mkono wake, naye mshichana huyo “akainuka,” yaani akafufuka kutoka kwa wafu.—Mathayo 9:24, 25.

Yesu pia alimfufua rafiki yake, Lazaro. Lakini kabla hajafanya muujiza huo, alimfariji Martha, dada ya Lazaro, kwa maneno haya: “Ndugu yako atafufuka.” Martha alisema hivi bila kusita: “Ninajua atafufuka katika ufufuo siku ya mwisho.” (Yohana 11:23, 24) Yaelekea alitarajia kwamba watumishi wote wa Mungu watafufuliwa wakati ujao.

Ufufuo unamaanisha nini? Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ufufuo” (a·naʹsta·sis) linamaanisha “kusimama tena.” Linahusisha kuinuka kutoka kwa wafu. Huenda ikawa vigumu kwa watu fulani kuamini jambo hilo, lakini Yesu alipotaja kwamba wafu wangesikia sauti yake, aliongeza hivi pia: “Msistaajabie jambo hili.” (Yohana 5:28) Masimulizi ya Biblia kuwahusu watu ambao Yesu aliwafufua alipokuwa duniani, yanatuthibitishia kwamba wafu walio katika kumbukumbu ya Mungu wataamka kutoka katika “usingizi” wao wa muda mrefu, kama Biblia inavyoahidi. Andiko la Ufunuo 20:13 linatabiri hivi: “Bahari ikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake, na kifo na Kaburi vikawatoa wale wafu waliokuwa ndani yake.”

Je, hao wafu watafufuliwa ili tu wazeeke na kufa tena, kama Lazaro? Hilo si kusudi la Mungu. Biblia inatuhakikishia kwamba wakati ujao “kifo hakitakuwapo tena,” kwa hiyo hakuna yeyote atakayezeeka na kufa.—Ufunuo 21:4.

Kifo ni adui. Wanadamu wana maadui wengi, kama vile magonjwa na uzee, ambao pia huwafanya wateseke sana. Mungu ameahidi atawashinda wote, na hatimaye kumhukumu adui mkuu wa wanadamu. “Adui wa mwisho atakayeangamizwa ni kifo.”—1 Wakorintho 15:26.

Baada ya ahadi hiyo kutimizwa, wanadamu watakuwa na maisha makamilifu ambayo hayatatiwa dosari na dhambi na kifo. Tunapongojea pindi hiyo, tunafarijika kwa kujua kwamba wapendwa wetu waliokufa wanapumzika, na wale walio katika kumbukumbu ya Mungu watafufuliwa wakati wa Mungu utakapowadia.

Kujua Ukweli Kuhusu Kifo Hutupa Kusudi Maishani

Kujua vizuri ukweli kuhusu kifo na tumaini la wafu kunaweza kubadili mtazamo wetu juu ya maisha. Ian, aliyetajwa katika makala ya kwanza, alipata kuelewa kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu kifo alipokuwa na miaka 20 na kitu. Anasema hivi: “Niliamini kwamba baba yangu alikuwa hai mahali fulani lakini sikuwa na hakika hata kidogo. Kwa hiyo, nilipojifunza kwamba analala tu katika kifo, nilivunjika moyo.” Hata hivyo, Ian aliposoma kuhusu ahadi ya Mungu ya kuwafufua wafu, alifurahi sana kujua kwamba ataweza kumwona baba yake tena. Anasema: “Kwa mara ya kwanza maishani nilikuwa na amani.” Alipojua ukweli kuhusu kifo alipata amani ya akili iliyomtuliza.

Steven, mwenye umri wa miaka 21, ambaye ni mwana wa Clive na Brenda, alikufa katika ule msiba uliotajwa katika makala ya kwanza. Ijapokuwa walijua yale ambayo Biblia inasema kuhusu kifo, walihuzunika sana mwanao alipokufa ghafula. Kifo ni adui na mchomo wake unaumiza. Lakini kwa sababu walijua yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu hali ya wafu huzuni yao ilipungua pole kwa pole. Brenda anasema: “Kwa sababu tunajua ukweli kuhusu kifo tumeweza kurudia maisha ya kawaida na tuna amani ya akili. Hata hivyo, kila siku tunafikiri kuhusu wakati ambapo Steven ataamka kutoka katika usingizi wake mzito.”

“Kifo, Uko Wapi Mchomo Wako?”

Ni wazi kwamba kuelewa hali ya wafu kunaweza kutusaidia kuwa na mtazamo unaofaa kuhusu maisha. Inawezekana kujua ukweli kuhusu kifo. Tunaweza kufurahia maisha bila kuogopa sana kifo. Na kwa kuwa tunatambua kwamba mtu akifa anaweza kuishi tena, tunaepuka tamaa ya kuponda raha kwa sababu ya kuona kwamba “maisha ni mafupi sana.” Tunafarijiwa na kutamani kuendelea kuishi tunapojua kwamba wapendwa wetu waliokufa, ambao wamo katika kumbukumbu ya Mungu, wanalala usingizi katika kifo wakingojea ufufuo.

Naam, tunaweza kuwa na hakika tunapotarajia wakati ujao, Yehova Mungu aliye Chanzo cha uhai, atakapomeza kifo milele. Tutafurahi sana tutakapoweza kuuliza hivi: “Kifo, uko wapi ushindi wako? Kifo, uko wapi mchomo wako?”—1 Wakorintho 15:55.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Hapa ndipo mahali pa kwanza ambapo kifo kinatajwa katika Biblia.

^ fu. 11 Fidia iliyolipwa ilikuwa uhai mkamilifu wa mwanadamu kwa sababu Adamu alipoteza uhai mkamilifu wa mwanadamu. Kwa kuwa watu wote walikuwa wenye dhambi, hakuna mwanadamu yeyote asiyekamilika ambaye angeweza kulipa fidia. Hivyo, Mungu alimtuma Mwana wake kutoka mbinguni kwa kusudi hilo. (Zaburi 49:7-9) Maelezo zaidi kuhusu habari hiyo yanapatikana katika sura ya 7 ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kutotii kwa Adamu na Hawa kulisababisha kifo

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yesu alishika mkono wa msichana aliyekufa na msichana huyo akainuka

[Picha katika ukurasa wa 7]

Wengi hutarajia wakati ambapo wapendwa wao ambao wamekufa wataamka kama Lazaro