Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maisha Yenye Kuridhisha Licha ya Maumivu ya Moyoni

Maisha Yenye Kuridhisha Licha ya Maumivu ya Moyoni

Simulizi la Maisha

Maisha Yenye Kuridhisha Licha ya Maumivu ya Moyoni

LIMESIMULIWA NA AUDREY HYDE

Ninapokumbuka miaka zaidi ya 63 katika huduma ya wakati wote—miaka 59 nikiwa kwenye makao makuu ya ulimwengu ya Mashahidi wa Yehova—ninaweza kusema kwamba maisha yangu yamekuwa yenye kuridhisha sana. Ni kweli kwamba niliumia sana moyoni kuona mume wangu wa kwanza akidhoofika na kufa kutokana na kansa, kisha mume wangu wa pili akiteseka kutokana na ugonjwa wa Alzheimer (unaoathiri akili). Lakini acheni niwaeleze jinsi nimedumisha shangwe licha ya misiba hiyo.

NILIKULIA katika shamba karibu na mji mdogo wa Haxtun kwenye nyanda za kaskazini-mashariki mwa Colorado, karibu na mpaka wa Nebraska. Nilikuwa mtoto wa tano kati ya watoto sita wa Orille na Nina Mock. Russell, Wayne, Clara, na Ardis walizaliwa kati ya mwaka wa 1913 na 1920, mimi nikazaliwa mwaka uliofuata, naye Curtis akazaliwa mwaka wa 1925.

Mnamo 1913, Mama alipata kuwa Mwanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyoitwa wakati huo. Mwishowe, sote katika familia tukawa Mashahidi.

Maisha Bora Kwenye Nyanda

Baba alipendezwa na mambo mapya. Nyumba zetu zote za mashambani zilikuwa na umeme, jambo ambalo halikuwa la kawaida siku hizo. Pia tulifurahia vitu vilivyotokana na ufugaji—mayai yaliyotagwa na kuku wetu, maziwa, malai, na siagi iliyotokana na ng’ombe wetu. Tulitumia farasi kulima, nasi tulikuza matunda ya stroberi, viazi, ngano, na pia mahindi.

Baba aliamini kwamba watoto wake wote walipaswa kuzoezwa kufanya kazi. Hata kabla sijaenda shuleni, nilizoezwa kufanya kazi shambani. Ninakumbuka nikipalilia kwa jembe bustani yetu wakati wa jua kali la kiangazi. Nilikuwa nikijiuliza, ‘Je, nitamaliza?’ Nilikuwa nikitokwa na jasho jingi, nao nyuki walikuwa wakiniuma. Nyakati nyingine, nilijihurumia kwa sababu watoto wengine hawakuwa wakifanya kazi nyingi kama sisi. Hata hivyo, ninapokumbuka utoto wangu, ninashukuru kwamba tulifundishwa kufanya kazi.

Sote tulikuwa na migawo. Ardis alikama ng’ombe vizuri zaidi kuliko mimi, hivyo kazi yangu ilikuwa kusafisha mabanda ya farasi zizini, nikitoa mbolea kwa sepetu. Hata hivyo, tulikuwa pia na nyakati za kujifurahisha na kucheza. Mimi na Ardis tulicheza besiboli katika timu ya kwetu. Nilicheza namba ya tatu, naye Ardis namba ya kwanza.

Usiku wenye anga lisilo na mawingu ulikuwa maridadi katika nyanda. Maelfu ya nyota yalinikumbusha Muumba wetu, Yehova Mungu. Hata nilipokuwa mdogo, nilifikiria andiko la Zaburi 147:4, linalosema: “[Yehova] anahesabu idadi ya nyota; zote anaziita kwa majina yake.” Mara nyingi wakati wa usiku wenye anga lisilo na mawingu, mbwa wetu, Judge, angeweka kichwa chake juu ya mapaja yangu na kukaa pamoja nami. Wakati wa alasiri niliketi mara nyingi kwenye varanda yetu na kufurahia kutazama ngano kwenye mashamba wakati upepo ulipovuma juu ya mashamba hayo na kuyafanya yafanane na fedha katika mwangaza wa jua.

Kielelezo Kizuri cha Mama

Mama alikuwa mke mwaminifu sana. Sikuzote Baba alijiendesha kama kichwa cha familia naye Mama alitufunza kumheshimu. Mnamo 1939, yeye pia akawa Shahidi wa Yehova. Tulijua kwamba Baba alitupenda ingawa wakati mwingine alitufanyiza kazi ngumu na hakutuendekeza. Mara nyingi wakati wa majira ya baridi kali alifunga farasi wawili pamoja na kutubeba kwa sleji. Tulifurahia sana theluji iliyometameta.

Hata hivyo, Mama ndiye aliyetufundisha kumpenda Mungu na kuiheshimu Biblia. Tulijifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova na kwamba yeye ndiye Chanzo cha uhai. (Zaburi 36:9; 83:18) Pia, tulijifunza kwamba Mungu ametupa mwongozo wa kutunufaisha bali si wa kutunyima furaha. (Isaya 48:17) Sikuzote mama alikazia kwamba tuna kazi ya pekee ya kufanya. Tulijifunza kwamba Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Katika miaka hiyo ya utotoni, nilikuwa nikienda kumtafuta mama kama singemkuta nyumbani niliporudi kutoka shuleni. Pindi moja nilipokuwa na umri wa miaka sita au saba hivi, nilimkuta katika ghala la nafaka. Kisha mvua kubwa ikaanza kunyesha. Tulikuwa katika sehemu ya juu ya ghala la kuwekea nyasi kavu, nami nikamuuliza ikiwa Mungu alikuwa ameleta Gharika nyingine. Alinihakikishia kwamba Mungu aliahidi kuwa hataiharibu dunia tena kwa gharika. Ninakumbuka mara nyingi nikikimbilia mahali pa kujificha, kwani haikuwa kawaida kwa upepo mkali kuvuma.

Hata kabla sijazaliwa, Mama alikuwa akishiriki katika kazi ya kuhubiri. Kikundi fulani kilikusanyika nyumbani kwetu, na wote walikuwa na tumaini la kuishi pamoja na Kristo mbinguni. Ingawa Mama aliona kuhubiri nyumba kwa nyumba kuwa jambo gumu, hata hivyo upendo wake kwa Mungu ulishinda woga wake. Alikuwa mwaminifu hadi alipokufa Novemba 24, 1969, alipokuwa na umri wa miaka 84. “Mama, unaenda mbinguni, nawe utakuwa pamoja na wale unaowajua,” nikamnong’onezea sikioni. Nilifurahi kama nini kuwa pamoja na Mama siku aliyokufa na kumweleza uhakika wangu kuhusu tumaini hilo! Alisema kwa wororo, “Wewe ni mwema kwangu.”

Tulianza Kuhubiri

Mnamo 1939, Russell alianza kuhubiri akiwa painia, kama waeneza-injili wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Alifanya upainia huko Oklahoma na Nebraska hadi mwaka wa 1944 alipoalikwa kutumika kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova (yanayoitwa Betheli), huko Brooklyn, New York. Nilianza upainia Septemba 20, 1941, nami nilitumika katika maeneo mbalimbali huko Colorado, Kansas, na Nebraska. Miaka hiyo ya upainia ilikuwa yenye furaha, si kwa sababu tu ningeweza kuwasaidia wengine kujifunza kumhusu Yehova, bali pia kwa sababu nilijifunza kumtegemea.

Karibu wakati ambapo Russell alianza upainia, Wayne, alikuwa akisoma kwenye chuo kikuu kaskazini-mashariki mwa Amerika, baada ya kufanya kazi kwa muda. Baadaye, alialikwa Betheli. Alitumika kwa miaka kadhaa kwenye Shamba la Ufalme, karibu na Ithaca, New York. Huko, chakula kilikuzwa kwa ajili ya familia ndogo iliyoishi humo na wafanyakazi 200 hivi wa Betheli ya Brooklyn. Wayne alitumia ustadi na uzoefu wake kumtumikia Yehova hadi alipokufa mwaka wa 1988.

Dada yangu Ardis aliolewa na James Kern, nao wakazaa watoto watano. Ardis alikufa mwaka wa 1997. Dada yangu mkubwa, Clara, ameendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova hadi leo, na wakati wa likizo mimi humtembelea nyumbani kwake huko Colorado. Ndugu yetu mdogo, Curtis, alikuja Betheli ya Brooklyn katikati ya miaka ya 1940. Alikuwa akiendesha lori toka Brooklyn hadi Shamba la Ufalme akiwa na bidhaa na mazao. Hakuwahi kuoa, naye alikufa mwaka wa 1971.

Nilitamani Kutumika Betheli

Ndugu zangu wakubwa walikuwa wametangulia kwenda kutumika Betheli, nami pia nilitamani kutumika huko. Nina hakika kwamba kielelezo chao kizuri ndicho kilichofanya nialikwe Betheli. Kumsikiliza mama akizungumza kuhusu tengenezo la Mungu na kujionea mwenyewe utimizo wa unabii wa Biblia kuhusu siku za mwisho kulinisaidia kukuza tamaa ya kutumika Betheli. Niliweka nadhiri kwa Yehova katika sala kwamba ikiwa angeniwezesha kutumika Betheli, singeondoka huko kamwe isipokuwa niwe na madaraka ya Kikristo ya kutimiza.

Nilifika Betheli Juni 20, 1945, na kupewa kazi ya kutunza nyumba. Nilisafisha vyumba 13 na kutandika vitanda 26 kila siku. Nilisafisha pia kumbi, ngazi, na madirisha. Ilikuwa kazi ngumu. Kila siku nilipokuwa nikifanya kazi, nilijiambia, ‘Kweli, umechoka, lakini upo Betheli, nyumba ya Mungu!’

Naolewa na Nathan Knorr

Tangu miaka ya 1920, wanabetheli waliotaka kufunga ndoa waliombwa waondoke Betheli na kwenda kufanya kazi ya Ufalme mahali pengine. Lakini katika miaka ya mapema ya 1950, wachache kati ya wale waliokuwa wametumika Betheli kwa muda mrefu walikubaliwa kufunga ndoa na kubaki huko. Kwa hiyo, Nathan H. Knorr, ambaye wakati huo aliongoza kazi ya Ufalme duniani pote, alipopendezwa nami, niliwaza, ‘Sasa, huyu atabaki Betheli!’

Nathan alikuwa na madaraka mengi ya kusimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova duniani pote. Kwa hiyo, alizungumza nami waziwazi, akinipa sababu nyingi ambazo nilipaswa kufikiria kwa makini kabla ya kukubali ombi lake la kufunga ndoa nami. Siku hizo, alisafiri sana kutembelea Mashahidi wa Yehova duniani pote, na mara nyingi alisafiri kwa majuma mengi. Hivyo akanieleza kwamba hatungekuwa pamoja kwa vipindi virefu.

Kama msichana, nilitamani sana kuolewa wakati wa vuli na baada ya arusi kusafiri kwenye visiwa vya Pasifiki vya Hawaii. Tulifunga ndoa Januari 31, 1953, wakati wa majira ya baridi kali kisha tukaenda fungate huko New Jersey ambako tulikaa Jumamosi hiyo alasiri na Jumapili. Tulirudi kazini Jumatatu. Hata hivyo, juma moja baadaye, tulienda likizo kwa muda wa juma moja.

Mwenzi Mwenye Bidii

Nathan alikuwa na umri wa miaka 18 alipofika Betheli mwaka wa 1923. Alizoezwa vizuri na watu wenye uzoefu kama vile Joseph F. Rutherford, ambaye alichukua uongozi wa kazi ya Mashahidi, na Robert J. Martin, aliyekuwa msimamizi wa idara ya uchapishaji. Ndugu Martin alipokufa Septemba 1932, Nathan akawa msimamizi wa idara hiyo. Mwaka uliofuata, Ndugu Rutherford aliandamana na Nathan alipotembelea ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova huko Ulaya. Ndugu Rutherford alipokufa Januari 1942, Nathan alipewa daraka la kusimamia kazi ya duniani pote ya Mashahidi wa Yehova.

Nathan ni mtu aliyependa maendeleo sana, sikuzote alipanga mambo kimbele kwa ajili ya mpanuko wa wakati ujao. Kwa sababu mwisho wa mfumo wa mambo ulifikiriwa kuwa umekaribia sana, wengine waliona mipango hiyo kuwa isiyofaa. Hivyo, ndugu mmoja aliyeona ratiba ya Nathan ya uchapaji alimuuliza: “Hii ni nini Ndugu Knorr? Je, huamini kwamba mwisho umekaribia?” Alimjibu: “Ndiyo, ninaamini, lakini ikiwa mwisho hautakuja haraka kama tunavyotarajia, tutakuwa tayari.”

Jambo moja ambalo Nathan aliamini kabisa ni kuanzisha shule ya mishonari. Hivyo, mnamo Februari 1, 1943, shule ya mishonari ilianzishwa kwenye Shamba la Ufalme ambako ndugu yangu Wayne alikuwa akitumikia wakati huo. Ingawa shule hiyo ilihusisha kujifunza Biblia kwa bidii kwa miezi mitano hivi, Nathan alihakikisha kwamba wanafunzi walikuwa na vipindi vya kujiburudisha. Mnamo miaka ya kwanza ya shule, alicheza besiboli pamoja na wanafunzi, lakini baadaye akaacha kucheza akiogopa kuumia, jambo ambalo lingemzuia kuhudhuria makusanyiko ya wilaya wakati wa kiangazi. Badala yake, alichagua kuwa refarii. Wanafunzi walifurahia wakati alipobadili waziwazi kanuni za mchezo kwa kuwapendelea wanafunzi wageni waliocheza.

Kusafiri Pamoja na Nathan

Mwishowe, nilianza kusafiri ng’ambo pamoja na Nathan. Nilifurahia kushiriki mambo yaliyoonwa pamoja na mishonari na wanabetheli kwenye ofisi za tawi. Nilijionea upendo na ujitoaji wao, na kujua ratiba yao na hali za maisha katika nchi walikotumwa. Kwa miaka mingi nimeendelea kupokea barua za shukrani kwa ajili ya ziara hizo.

Ninapofikiria safari zetu, ninakumbuka mambo mengi yaliyoonwa. Kwa mfano, tulipotembelea Poland, dada wawili walikuwa wakinong’onezeana mbele zangu. Nikawauliza, “Kwa nini mnanong’onezeana?” Waliomba radhi na kunieleza kwamba walikuwa wamezoea kunong’onezeana kwa kuwa kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku nchini Poland na wakati nyumba zao zilipokuwa zimetegwa kwa vifaa vya kunasa sauti.

Dada Adach ni mmoja wa wale waliotumika chini ya marufuku huko Poland. Sehemu ya nywele zake zenye mawimbi-mawimbi ilikuwa imefunika kipaji cha uso wake. Aliinua nywele zake na kunionyesha kovu kubwa ambalo lililotokana na kupigwa na mtesaji fulani. Nilihuzunika kujionea mwenyewe matokeo ya ukatili ambao ndugu na dada zetu walitendewa.

Mbali na Betheli, ile sehemu nyingine ninayopenda zaidi ni Hawaii. Ninakumbuka kusanyiko lililofanywa katika jiji la Hilo mwaka wa 1957. Kusanyiko hilo lilikuwa tukio muhimu, nao watu waliohudhuria walikuwa wengi zaidi kuliko hudhurio lilikuwa kubwa zaidi ya jumla ya hesabu ya Mashahidi wa mahali hapo. Meya wa jiji hata alimpa Nathan ufunguo wa jiji. Wengi walikuja kutusalimu, na kutupamba kwa mashada ya maua.

Kusanyiko lingine lenye kuvutia lilifanywa Nuremberg, Ujerumani, mwaka wa 1955, mahali ambapo Hitler alikuwa akifanyia gwaride. Inajulikana vizuri kwamba Hitler aliapa kuwaangamiza watu wa Yehova nchini Ujerumani, lakini sasa uwanja huo ulikuwa umejaa Mashahidi wa Yehova! Nilitokwa na machozi. Jukwaa lilikuwa kubwa na nyuma yake kulikuwa na nguzo kubwa 144. Nilikuwa kwenye jukwaa na ningeweza kuona wahudhuriaji zaidi ya 107,000. Jukwaa lilikuwa mbali sana na sehemu ya nyuma ya uwanja hivi kwamba singeweza kuwaona vizuri watu walioketi safu ya mwisho.

Tungeweza kuona utimilifu wa ndugu wa Ujerumani na nguvu walizopata kutoka kwa Yehova wakati wa mateso chini ya utawala wa Nazi. Azimio letu la kuendelea kuwa washikamanifu na watimilifu kwa Yehova liliimarishwa. Nathan alitoa hotuba ya kumalizia, na mwishoni mwa hotuba hiyo, akawaaga wahudhuriaji kwa kuwapungia mkono. Waliitikia papo hapo kwa kupeperusha vitambaa vyao ili kutuaga. Uwanja ulionekana kama shamba maridadi la maua.

Pia siwezi kusahau ziara yetu huko Ureno mnamo Desemba 1974. Tulikuwa miongoni mwa wahudhuriaji kwenye kusanyiko la kwanza la Mashahidi huko Lisbon baada ya kazi ya kuhubiri kutambuliwa kisheria. Kazi hiyo ilikuwa imepigwa marufuku kwa miaka 50! Ingawa wakati huo kulikuwa na watangazaji wa Ufalme 14,000 tu nchini, watu zaidi ya 46,000 walihudhuria makusanyiko mawili yaliyofanywa. Nilitokwa na machozi ndugu waliposema: “Hatuhitaji tena kujificha. Tuko huru.”

Tangu nilipoanza kusafiri na Nathan hadi leo, ninapendezwa na mahubiri yasiyo rasmi—ndani ya ndege, mikahawani—na mahubiri ya barabarani. Sikuzote mimi hubeba vichapo ili kutoa ushahidi. Siku moja tulipokuwa tukingojea ndege ambayo ilikuwa imechelewa, mwanamke mmoja aliniuliza nilikuwa nikifanya kazi wapi. Swali hilo lilitokeza mazungumzo kati yangu na yeye na wengine waliokuwa karibu nasi ambao walikuwa wakisikiliza. Utumishi wa Betheli na kazi ya kuhubiri imenisaidia kuwa mwenye shughuli na mwenye furaha sana.

Ugonjwa na Kitia Moyo cha Kuniaga

Mwaka wa 1976, Nathan alishikwa na ugonjwa wa kansa, nami pamoja na wafanyakazi wengine wa Betheli, tulimsaidia kukabiliana na hali hiyo. Licha ya kuzorota kwa afya yake, tuliwaalika chumbani mwetu washiriki wa ofisi za tawi kutoka ulimwenguni ambao walikuwa Brooklyn kwa ajili ya mazoezi. Ninakumbuka ziara za Don na Earlene Steele, Lloyd na Melba Barry, Douglas na Mary Guest, Martin na Gertrud Poetzinger, Pryce Hughes, na wengine wengi. Mara kwa mara walitueleza mambo yaliyoonwa katika nchi zao. Nilichochewa hasa na mambo yaliyoonwa na ndugu zetu waliobaki imara chini ya mateso.

Nathan alipoona kwamba anakaribia kufa, alinitolea mashauri fulani ili kunisaidia kukabiliana na ujane. Alisema: “Tumekuwa na ndoa yenye furaha. Wengi hawapati furaha kama hiyo katika ndoa.” Jambo moja lililofanya ndoa yetu iwe yenye furaha ni kwamba Nathan alikuwa mwenye kunifikiria. Kwa mfano, tulipokutana na watu tofautitofauti safarini, alikuwa akiniambia: “Audrey, ikiwa nyakati nyingine siwajulishi wewe ni nani, ni kwa sababu nimesahau majina yao.” Nilifurahi sana kwamba aliniambia hivyo mapema.

Nathan alinikumbusha: “Baada ya kifo tumaini letu huwa hakika na hatutateseka tena.” Kisha akanisihi: “Kaza macho mbele, kwani huko ndiko kuna thawabu yako. Usiendelee kufikiria wakati uliopita, ingawa utakuwa na kumbukumbu hizo. Utapona kadiri wakati unavyosonga. Usiwe mwenye uchungu na kujisikitikia. Shangilia kwamba umepata furaha na baraka hizo. Mwishowe, utaona kwamba kumbukumbu hizo zitakuletea furaha. Kumbukumbu ni zawadi ambayo Mungu ametupatia.” Akaongeza: “Uwe na mengi ya kufanya, yaani, jaribu kutumia maisha yako ili kufanya jambo fulani kwa ajili ya wengine. Hilo litakusaidia kuishi kwa furaha.” Hatimaye, Nathan aliyekuwa na tumaini la kwenda mbinguni, alikufa Juni, 8, 1977.

Nafunga Ndoa na Glenn Hyde

Nathan aliniambia kwamba ningeweza kuendelea kufikiria wakati uliopita au kuanzisha maisha mapya. Kwa hiyo, mwaka wa 1978, baada ya kuhama na kwenda katika Mashamba ya Watchtower huko Wallkill, New York, nilifunga ndoa na Glenn Hyde, mwanamume mnyamavu, mtulivu, na mwenye sura nzuri sana. Kabla ya kuwa Shahidi, alitumika katika jeshi la wanamaji wakati Marekani ilipokuwa ikipigana na Japani.

Glenn alikuwa kwenye mashua ya ulinzi ya kijeshi ya kurusha makombora, naye alifanya kazi kwenye chumba cha injini. Kwa sababu ya mlio wa injini, uwezo wake wa kusikia uliathiriwa. Baada ya vita, akawa zimamoto. Kwa miaka mingi alikuwa akiota ndoto zenye kutisha kwa sababu ya mambo aliyoona vitani. Alijifunza ukweli wa Biblia kutoka kwa karani wake wa kike, aliyemhubiria kwa njia isiyo rasmi.

Baadaye, mwaka wa 1968, Glenn aliitwa Betheli kutumikia akiwa zimamoto huko Brooklyn. Kisha, Mashamba ya Watchtower yalipopata gari la kuzima moto, akahamishwa kwenda huko mwaka wa 1975. Baada ya muda, alipatwa na ugonjwa wa Alzheimer. Baada ya miaka kumi ya ndoa yetu, Glenn akafa.

Ningekabilianaje na hali hiyo? Kwa mara nyingine tena mashauri ambayo Nathan alinipa alipojua kwamba atakufa yalinifariji. Niliendelea kusoma yale aliyoniandikia kuhusu jinsi ya kukabiliana na ujane. Bado ninashiriki maelezo hayo na wengine wanaofiwa na wenzi wa ndoa, nao pia hufarijiwa na mashauri ya Nathan. Naam, kama Nathan alivyonitia moyo kufanya, ni vizuri kufikiria wakati ujao.

Undugu Wenye Thamani

Ndugu na dada wapendwa katika familia ya Betheli wamefanya maisha yangu yawe yenye furaha na yenye kuridhisha. Mmoja wao ni Esther Lopez, ambaye alihitimu darasa la tatu la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead) mnamo 1944. Alirudi Brooklyn Februari 1950 kutumikia kama mtafsiri wa vichapo vyetu vya Biblia katika Kihispania. Mara nyingi Nathan alipokuwa safarini, Esther ndiye aliyekuwa mwandamani wangu wa karibu. Yeye pia anaishi kwenye Mashamba ya Watchtower. Sasa akiwa na umri wa miaka 90 na kitu, afya yake inadhoofika, naye anatunzwa katika chumba chetu cha wagonjwa.

Kati ya watu wa familia yangu ya karibu, Russell na Clara tu ndio wako hai. Russell ana miaka zaidi ya 90 na anatumikia kwa uaminifu kwenye Betheli ya Brooklyn. Alikuwa kati ya ndugu wa kwanza walioruhusiwa kubaki Betheli baada ya kuoa. Mnamo 1952, alimwoa mwanabetheli mwenzake, Jean Larson. Max, ndugu yake Jean, alikuja Betheli mwaka wa 1939, naye akachukua nafasi ya Nathan kama msimamizi wa idara ya uchapishaji mnamo 1942. Max anaendelea kushughulikia madaraka mengi Betheli, kutia ndani kusaidia kumtunza mke wake mpendwa, Helen, ambaye anaugua ugonjwa wa neva.

Ninapokumbuka miaka 63 ambayo nimemtumikia Yehova wakati wote, ninaweza kusema kwamba maisha yangu yamekuwa yenye kuridhisha. Betheli imekuwa makao yangu, na ninaendelea kutumika hapa kwa shangwe. Ninawashukuru wazazi wangu kwa kutufunza umuhimu wa kuwa na mazoea mazuri ya kazi na nia ya kumtumikia Yehova. Lakini jambo linalofanya maisha yawe yenye kuridhisha ni undugu wetu mzuri na tumaini la kuishi pamoja na ndugu na dada zetu katika paradiso duniani, tukimtumikia milele Muumba wetu Mkuu, Mungu wa pekee wa kweli, Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Wazazi wangu siku ya arusi yao mnamo Juni 1912

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kutoka kushoto hadi kulia: Russell, Wayne, Clara, Ardis, mimi, na Curtis mwaka wa 1927

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nimesimama kati ya Frances na Barbara McNaught, nilipokuwa nikifanya upainia mwaka wa 1944

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa Betheli mwaka wa 1951. Kutoka kushoto hadi kulia: Mimi, Esther Lopez, na dada-mkwe wangu, Jean

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na Nathan na wazazi wake

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na Nathan mwaka wa 1955

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nikiwa na Nathan huko Hawaii

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nikiwa na mume wangu wa pili, Glenn