Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maneno “uhai katika yeye mwenyewe” yanamaanisha nini?

Biblia husema kwamba Yesu Kristo ana “uhai katika yeye mwenyewe” na wanafunzi wake kuwa wana ‘uhai katika wao wenyewe.’ (Yohana 5:26; 6:53) Hata hivyo, maandiko hayo mawili hayana maana sawa.

Yesu alisema, “Kama vile Baba alivyo na uhai katika yeye mwenyewe, ndivyo pia amemruhusu Mwana kuwa na uhai katika yeye mwenyewe.” Kabla ya kutaja maneno hayo muhimu, Yesu alisema: “Kwa kweli kabisa mimi nawaambia nyinyi, Yeye ambaye husikia neno langu na kumwamini yeye aliyenituma ana uhai udumuo milele . . . Saa inakuja, nayo ipo sasa, wakati wafu watakapoisikia sauti ya Mwana wa Mungu na wale ambao wamemsikiliza wataishi.” Hapa Yesu alikuwa akizungumzia nguvu za pekee alizopewa na Baba, yaani, nguvu za kuwawezesha wanadamu kuwa na msimamo unaokubalika mbele za Mungu. Isitoshe, Yesu ana uwezo wa kuwafufua wale waliolala katika kifo na kuwapa uhai. Yesu kuwa na “uhai katika yeye mwenyewe” humaanisha kwamba amepewa nguvu hizo. Kama Baba, Mwana pia ana ‘zawadi ya uhai katika yeye mwenyewe.’ (Yohana 5:24-26) Namna gani wafuasi wake?

Baada ya muda wa mwaka mmoja hivi, Yesu aliwaambia hivi wasikilizaji wake: “Kwa kweli kabisa mimi nawaambia, Nyinyi msipoula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uhai katika nyinyi wenyewe. Yeye ambaye hula mwili wangu na kunywa damu yangu ana uhai udumuo milele, nami nitamfufua kwenye siku ya mwisho.” (Yohana 6:53, 54) Hapa Yesu analinganisha kuwa na “uhai katika nyinyi wenyewe” na kupata “uhai udumuo milele.” Maneno ambayo yana muundo huohuo wa kisarufi kama vile kuwa na “uhai katika nyinyi wenyewe” yanapatikana mahali penginepo katika Maandiko ya Kigiriki. Mifano miwili ya maneno hayo ni, “Iweni na chumvi ndani yenu wenyewe” na “kupokea katika wao wenyewe malipo kamili.” (Marko 9:50; Waroma 1:27) Katika mifano hiyo, maneno hayo hayamaanishi kuwa na uwezo wa kuwapa wengine chumvi au kutoa malipo. Badala yake yanamaanisha ukamili. Hivyo, maneno “uhai katika nyinyi wenyewe” yanayotumiwa katika Yohana 6:53 yanamaanisha tu kupata uhai kamili.

Aliposema kwamba wafuasi wake wana uhai katika wao wenyewe, Yesu alitaja mwili na damu yake. Baadaye alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, Yesu alizungumza tena kuhusu mwili na damu yake naye akawaagiza wafuasi wake ambao wangekuwa katika agano jipya wale mifano ya mkate usiotiwa chachu na kunywa divai. Je, hilo linamaanisha kwamba Wakristo watiwa-mafuta pekee, walio katika agano jipya pamoja na Yehova Mungu, ndio wanaopata uhai kamili? La. Matukio hayo mawili yalitofautiana kwa muda wa mwaka mmoja. Wale waliosikia maneno ya Yesu yaliyomo katika Yohana 6:53, 54 hawakujua kuhusu mwadhimisho wa kila mwaka uliohusisha mifano iliyowakilisha mwili na damu ya Kristo.

Kulingana na Yohana sura ya 6, kwanza Yesu analinganisha mwili wake na mana akisema: “Baba zenu wa zamani walikula mana nyikani na bado wakafa. Huu ndio mkate ambao huteremka kutoka mbinguni, ili yeyote apate kula kutokana nao na asife. Mimi ndio mkate ulio hai ulioteremka kutoka mbinguni; yeyote akila kutokana na mkate huu ataishi milele.” Mwili wa Yesu, pamoja na damu yake, ulimaanisha zaidi ya mana halisi. Jinsi gani? Katika maana ya kwamba mwili wake ulitolewa kwa ajili ya “uhai wa ulimwengu,” ili wanadamu waweze kuishi milele. * Kwa hiyo, maneno katika Yohana 6:53 juu ya kuwa na “uhai katika nyinyi wenyewe” yanahusu wote wale wanaopokea uhai udumuo milele mbinguni au duniani.—Yohana 6:48-51.

Wafuasi wa Kristo hupokea uhai katika wao wenyewe, au hupata uhai kamili wakati gani? Warithi wa Ufalme waliotiwa mafuta hupokea uhai huo wanapofufuliwa kwenda kuishi mbinguni wakiwa viumbe wa roho wasioweza kufa. (1 Wakorintho 15:52, 53; 1 Yohana 3:2) “Kondoo wengine” wa Yesu hupata uhai huo kamili mwishoni mwa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja. Wakati huo watakuwa wamejaribiwa, wakapatikana kuwa waaminifu, na kutangazwa kuwa waadilifu kwa ajili ya uhai udumuo milele katika Paradiso duniani.—Yohana 10:16; Ufunuo 20:5, 7-10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Wakiwa nyikani, Waisraeli na “kundi kubwa la watu waliochangamana” walihitaji mana ili kuendelea kuwa hai. (Kutoka 12:37, 38; 16:13-18) Vivyo hivyo, ili kuishi milele, ni lazima Wakristo wote, wawe watiwa-mafuta au la, wakubali mana kutoka mbinguni kwa kuonyesha imani katika nguvu ya kukomboa ya mwili na damu ya Yesu iliyotolewa dhabihu.—Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 1988, ukurasa wa 30-31.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wakristo wote wa kweli wana ‘uhai katika wao wenyewe’