Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujifunza Siri ya Kutosheka

Kujifunza Siri ya Kutosheka

Kujifunza Siri ya Kutosheka

Katika barua yenye kutia moyo kwa Wakristo Wafilipi, mtume Paulo aliandika hivi: “Nimejifunza, kuwa mwenye ujitoshelevu, mwenyewe katika hali zozote nilimo. . . . Katika kila jambo na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji.”—Wafilipi 4:11, 12.

Siri ya Paulo ya kutosheka ilikuwa nini? Kwa sababu ya gharama ya juu ya maisha na msukosuko wa kiuchumi nyakati zetu, ingefaa Wakristo wa kweli wajifunze kutosheka ili wakazie fikira utumishi wao kwa Mungu.

MWANZONI mwa barua yake, Paulo alitaja kazi yenye mafanikio aliyokuwa akifanya awali. Alisema hivi: “Ikiwa mtu yeyote mwingine hufikiri ana sababu za kuwa na uhakika katika mwili, mimi ni zaidi: katahiriwa siku ya nane, katokana na ukoo wa familia ya Israeli, wa kabila la Benyamini, Mwebrania aliyezaliwa kutoka kwa Waebrania; kwa habari ya sheria, Farisayo; kwa habari ya bidii, nikilinyanyasa kutaniko; kwa habari ya uadilifu ulio kwa njia ya sheria, mmoja aliyejithibitisha mwenyewe kuwa bila lawama.” (Wafilipi 3:4-6) Zaidi ya hayo, akiwa Myahudi mwenye bidii, Paulo alitumwa na kuungwa mkono na makuhani wakuu wa Yerusalemu. Kwa hiyo, Paulo alikuwa na nafasi ya kupata sifa na mamlaka—kisiasa, kidini, na bila shaka pesa nyingi—katika mfumo wa Kiyahudi.—Matendo 26:10, 12.

Hata hivyo, mambo yalibadilika kabisa Paulo alipoamua kuwa mhubiri Mkristo mwenye bidii. Aliacha kwa hiari kazi yake yenye mafanikio na mambo yote yaliyoonwa kuwa muhimu ili ahubiri habari njema. (Wafilipi 3:7, 8) Sasa angepataje riziki? Je, angelipwa mshahara akiwa mhubiri? Mahitaji yake ya kibinafsi yangetimizwaje?

Paulo alifanya huduma yake bila malipo. Ili asiwe mzigo kwa wale aliowahubiria, alijiunga na Akila na Prisila katika kazi ya kutengeneza mahema huko Korintho, na alifanya kazi nyingine ili kujiruzuku. (Matendo 18:1-3; 1 Wathesalonike 2:9; 2 Wathesalonike 3:8-10) Paulo alifunga safari tatu za mbali za mishonari, na aliyatembelea pia makutaniko yaliyokuwa na uhitaji. Kwa kuwa alijishughulisha sana na utumishi wa Mungu, alikuwa na vitu vichache vya kimwili. Mara nyingi akina ndugu walimpa alichohitaji. Ingawa hivyo, nyakati nyingine hakuwa na chochote kwa sababu ya hali ngumu. (2 Wakorintho 11:27; Wafilipi 4:15-18) Hata hivyo, Paulo hakulalamika kamwe kwa sababu ya hali yake, na wala hakutamani vitu vya wengine. Alijitolea kwa furaha kufanya kazi kwa bidii ili awasaidie Wakristo wenzake. Kwa kweli, Paulo ndiye aliyenukuu maneno haya ya Yesu yanayojulikana sana: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” Alikuwa kielelezo bora kama nini kwetu sote!—Matendo 20:33-35.

Maana ya Kutosheka

Paulo alikuwa mwenye furaha na mwenye kuridhika kwa sababu alitosheka. Lakini ni nini maana ya kutosheka? Kwa ufupi, kutosheka humaanisha kuridhika na vitu vya lazima maishani. Kuhusiana na hilo, Paulo alimwambia hivi Timotheo, mwandamani wake katika huduma: ‘Kwa hakika, ni njia ya kupata faida kubwa, ujitoaji-kimungu huu pamoja na ujitoshelevu. Kwa maana hatukuleta kitu katika ulimwengu, wala hatuwezi kupeleka kitu chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.’—1 Timotheo 6:6-8.

Ona kwamba Paulo alihusianisha kutosheka na ujitoaji-kimungu. Alitambua kwamba furaha ya kweli hutokana na ujitoaji-kimungu, yaani, kutanguliza utumishi wetu kwa Mungu, wala si mali au utajiri. Kuwa na “riziki na cha kujifunika” kungemsaidia kuendelea kufuatia ujitoaji-kimungu. Kwa hiyo, Paulo alijua kwamba siri ya kutosheka ni kumtegemea Yehova katika hali zozote zile.

Watu wengi leo huwa na mahangaiko mengi na kukosa furaha kwa sababu hawajui siri hiyo au huipuuza. Badala ya kutosheka, wao hutumaini pesa na vitu vinavyoweza kununuliwa. Matangazo ya biashara na vyombo vya habari huwafanya watu wahisi kwamba hawawezi kuwa na furaha wasiponunua upesi bidhaa na vifaa vya kisasa vya bei ghali. Na hivyo watu wengi huanguka katika mtego wa kutafuta pesa na mali. Badala ya kupata furaha na uradhi, wao “huanguka ndani ya kishawishi na mtego na tamaa nyingi zisizo za akili na zenye kuumiza, ambazo hutumbukiza watu ndani ya uharibifu na uangamizo.”—1 Timotheo 6:9, 10.

Wamejifunza Siri

Je, kweli siku hizi tunaweza kupata furaha na uradhi tukiwa na ujitoaji-kimungu na kutosheka? Inawezekana. Mamilioni ya watu leo wamefaulu. Wamejua siri ya kuwa na furaha kwa kutosheka na vitu walivyo navyo. Wao ni Mashahidi wa Yehova waliojiweka wakfu kwa Mungu, wakifanya mapenzi yake na kuwafundisha watu kila mahali kuhusu kusudi lake.

Kwa mfano, wafikirie wale ambao wamejitolea kuzoezwa na kutumwa wakiwa mishonari kwenye nchi za kigeni kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Mara nyingi, wao hutumwa katika nchi ambazo hazina ufanisi kama nchi zao. Kwa mfano, mishonari walipowasili katika nchi moja ya Asia mapema mwaka wa 1947, kulikuwa na hali mbaya zilizosababishwa na vita na nyumba nyingi hazikuwa na umeme. Katika nchi nyingi, mishonari walipata kwamba nguo hufuliwa mtoni kwenye miamba badala ya kutumia mashine za kufua. Kwa kuwa walikuja kuwafunza watu kweli ya Biblia, walizoea kuishi kama wenyeji na wakaendelea na huduma yao.

Wengine wanafanya utumishi wa wakati wote au wamehamia kwenye maeneo ambayo hayajahubiriwa habari njema. Adulfo amefanya utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 50 katika sehemu mbalimbali za Mexico. Anasema: “Kama mtume Paulo, mimi na mke wangu tumejifunza kuishi kupatana na hali. Kwa mfano, tulitembelea kutaniko ambalo halikuwa karibu na soko au jiji lolote. Kila siku, akina ndugu walikula chapati ndogo kavu iliyopakwa mafuta kidogo ya nguruwe, chumvi, na kunywa kikombe cha kahawa. Hawakula chakula kingine ila chapati tatu kila siku. Kwa hiyo tuliishi kama wao. Nimefurahia pindi nyingi kama hizo kwa miaka 54 ambayo nimemtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote.”

Florentino akumbuka jinsi yeye na familia yake walivyokabiliana na magumu. Anasema hivi kuhusu maisha yake ya utotoni: “Baba yangu alikuwa mfanyabiashara mwenye ufanisi. Alimiliki mashamba mengi. Bado ninakumbuka meza iliyokuwa kwenye duka letu la mboga na matunda. Meza hiyo ilikuwa na kabati yenye upana wa sentimeta 50 na kimo cha sentimeta 20, na ilikuwa na sehemu nne. Humo ndimo tulimoweka pesa za kila siku. Kila jioni, kabati hiyo ilijaa sarafu na noti.

“Kisha kwa ghafula, tulipoteza vitu vyote na tukawa maskini. Tulipoteza kila kitu isipokuwa nyumba yetu. Zaidi ya hayo, ndugu yangu alipatwa na aksidenti na hatimaye akapooza miguu. Mambo yalibadilika kabisa. Kwa muda nilifanya kazi ya kuuza matunda na nyama. Pia nilivuna pamba, zabibu, na njegere, na nilifanya kazi ya kumwagilia mashamba maji. Watu fulani waliniita mjuzi wa kazi zote. Mara nyingi mama alitutia moyo kwa kutuambia kwamba tuna kweli, utajiri wa kiroho ambao wengi hawana. Kwa hiyo nilizoea kila hali maishani. Sasa baada ya kumtumikia Yehova katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 25, ninaweza kusema kwamba siku kwa siku ninafurahi kujua kwamba nimechagua njia bora ya maisha, yaani, kumtumikia Yehova kwa wakati wote.”

Biblia hutuambia kwa mkazo kwamba “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” Kwa sababu hiyo, inatusihi hivi: “[Acha] wale washangiliao [wawe] kama wale wasioshangilia, na wale wanunuao kama wale wasio na kitu, na wale wanaoutumia ulimwengu kama wale wasioutumia kwa ukamili.”—1 Wakorintho 7:29-31.

Huu ndio wakati wa kujichunguza kwa makini. Ikiwa una vitu vichache, jihadhari usiwe na uchungu wala wivu. Kwa upande mwingine, ikiwa una vitu vya kimwili, ni hekima kutovitanguliza maishani visije vikakutawala. Kama mtume Paulo alivyoshauri, usiweke kamwe tumaini lako “juu ya mali zisizo hakika, bali juu ya Mungu, ambaye hututolea sisi vitu vyote kwa utajiri kwa ajili ya ufurahio wetu.” Ukifanya hivyo, wewe pia waweza kusema kwamba umejifunza siri ya kutosheka.—1 Timotheo 6:17-19.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Paulo alifanya kazi kwa mikono yake mwenyewe ili asiwe mzigo kwa wengine

[Picha katika ukurasa wa 10]

Maelfu wanafurahia maisha ya “ujitoaji-kimungu pamoja na ujitoshelevu”