Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwalea Watoto Katika Nchi ya Kigeni—Magumu na Thawabu

Kuwalea Watoto Katika Nchi ya Kigeni—Magumu na Thawabu

Kuwalea Watoto Katika Nchi ya Kigeni—Magumu na Thawabu

MAMILIONI ya watu huhamia nchi nyingine wakitumaini kuishi maisha mazuri. Zaidi ya watu milioni 20 wamehamia Ulaya, zaidi ya milioni 26 wanaishi Marekani, na zaidi ya asilimia 21 ya wakazi wa Australia wanatoka nchi nyingine. Mara nyingi, familia hizo huwa na kazi ngumu ya kujifunza lugha mpya na kuzoea utamaduni mpya.

Kwa kawaida, watoto hujifunza kwa wepesi lugha mpya nao huanza kufikiri katika lugha hiyo. Huenda wazazi wao wakachukua muda mrefu zaidi kujifunza lugha mpya. Watoto wanapokulia katika nchi ya kigeni, matatizo ya mawasiliano yasiyoweza kutatuliwa kwa urahisi yanaweza kuzuka kati yao na wazazi wao.

Lugha mpya huathiri njia ya watoto ya kufikiri nao utamaduni mpya unaweza kuathiri hisia zao. Huenda wazazi wakashindwa kuwaelewa watoto wao. Kwa hiyo, wazazi waliohamia nchi za kigeni ambao wanajaribu kuwalea watoto wao katika “nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova” hukabili magumu yasiyo ya kawaida.—Waefeso 6:4.

Tatizo la Kugusa Moyo na Akili

Wazazi Wakristo wana hamu na wajibu wa kuwafundisha watoto wao “lugha iliyo safi” ya kweli za Biblia. (Sefania 3:9) Lakini wazazi wanawezaje kukazia sheria ya Yehova katika mioyo ya watoto wao ikiwa watoto hawafahamu vyema lugha ya wazazi wao na iwapo wazazi hawafahamu vyema lugha ambayo watoto wao wanazungumza? (Kumbukumbu la Torati 6:7) Huenda watoto wakaelewa maneno ya wazazi wao lakini iwapo mambo yanayosemwa hayagusi mioyo yao, huenda watoto wakawa kama wageni nyumbani mwao.

Pedro na Sandra walihamia Australia kutoka Amerika Kusini, nao wanakabili tatizo hilo wanapowalea vijana wao wawili matineja. * Pedro anasema hivi: “Mambo ya kiroho yanahusiana na moyo na hisia. Unahitaji kufundisha mambo mazito na yenye maana sana, kwa hiyo ni lazima ufahamu lugha vyema zaidi.” Sandra aongezea hivi: “Ikiwa watoto wetu hawaelewi vizuri lugha yetu ya asili, basi wanaweza kudhoofika kiroho. Huenda wasielewe kanuni inayokaziwa katika mambo wanayojifunza na hivyo kukosa kuithamini kweli. Huenda wasifanye maendeleo ya kiroho na uhusiano wao na Yehova unaweza kuharibika.”

Gnanapirakasam na Helen walihamia Ujerumani kutoka Sri Lanka na sasa wana watoto wawili. Wanakiri hivi: “Tunaona ni muhimu sana watoto wetu wazungumze lugha yetu ya asili mbali na kujifunza Kijerumani. Ni muhimu waweze kutueleza hisia zao na kuzungumza nasi waziwazi na kutoka moyoni.”

Miguel na Carmen, waliohamia Uruguay kutoka Australia wanasema hivi: “Ni lazima wazazi waliohamia nchi nyingine wajitahidi sana. Ni lazima wajifunze ama lugha mpya vyema sana hivi kwamba wanaweza kufahamu na kufundisha mambo ya kiroho kwa lugha hiyo au wawafundishe watoto wao lugha yao.”

Uamuzi wa Familia

Ili hali ya kiroho ya familia yoyote iliyohamia nchi nyingine iwe nzuri, ni lazima waamue lugha ambayo watatumia ‘kufundishwa na BWANA.’ (Isaya 54:13) Familia inaweza kuamua kujiunga na kutaniko la karibu linalotumia lugha yao ya asili. Kwa upande mwingine, wanaweza kuamua kuhudhuria kutaniko ambalo linatumia lugha kuu ya nchi ambayo wamehamia. Watazingatia mambo gani wanapofanya uamuzi huo?

Demetrios na Patroulla, waliohamia Uingereza kutoka Cyprus na kulelea watoto watano huko, wanaeleza kilichowasaidia kufanya uamuzi: “Mwanzoni, familia yetu ilihudhuria kwenye kutaniko la Kigiriki. Sisi wazazi tulinufaika sana kuwa kwenye kutaniko hilo lakini ilikuwa vigumu kwa watoto wetu kufanya maendeleo ya kiroho. Walifahamu Kigiriki kidogo lakini haikuwa rahisi kwao kuelewa mafundisho fulani ya kiroho yenye kina. Ukuzi wao wa polepole wa kiroho ulidhihirisha hilo. Tulihamia kwenye kutaniko la Kiingereza, na watoto wetu wakafanya maendeleo mara moja. Wamekuwa thabiti kiroho. Haikuwa rahisi kuhama, lakini huo ulikuwa uamuzi wa hekima kwa familia yetu.”

Bado familia hiyo iliendelea kutumia lugha yao ya asili na ilipata baraka nyingi sana. Watoto wao wanasema hivi: “Kujua lugha kadhaa ni muhimu sana. Ingawa tunatumia hasa Kiingereza, tumegundua kwamba kujua Kigiriki kumeimarisha na kuboresha uhusiano wetu wa familia, hasa pamoja na babu zetu na nyanya. Kumetusaidia pia kuwahurumia zaidi watu waliohamia nchi nyingine, na kumetusadikishia kwamba tunaweza kujifunza lugha nyingine. Kwa hiyo tulipokuwa wakubwa kidogo, familia yetu ilihamia kutaniko la Kialbania lenye uhitaji.”

Christopher na Margarita pia walihamia Cyprus kutoka Uingereza, ambako walilelea watoto watatu. Waliamua kujiunga na kutaniko la Kigiriki. Mwana wao, Nikos, ambaye ni mzee katika kutaniko la Kigiriki akumbuka: “Tulitiwa moyo kujiunga na kutaniko jipya la Kigiriki. Familia yetu iliuona kuwa mgawo kutoka kwa Mungu.”

Margarita anasema hivi: “Wavulana wetu wawili walipokuwa na umri wa miaka 7 na 8, walijiunga na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Sisi wazazi tulikuwa na wasiwasi kidogo kwa sababu hawakujua vyema lugha ya Kigiriki. Hata hivyo, tuliuona kila mgawo kuwa daraka la familia nzima, na tuliwasaidia kwa saa nyingi kutayarisha hotuba zao.”

Binti yao Joanna anasema hivi: “Ningali nakumbuka jinsi Baba alivyotufundisha Kigiriki kwa kuandika alfabeti kwenye ubao nyumbani, na tulijifunza kabisa alfabeti hiyo. Watu wengi, hujifunza lugha fulani kwa miaka mingi sana, lakini kwa msaada wa Mama na Baba tulijifunza Kigiriki kwa muda mfupi tu.”

Familia nyingine hujiunga na makutaniko yanayotumia lugha zao kwa sababu wazazi wanaona kwamba wakifundishwa kwa lugha yao ya asili, wataweza kusitawisha ‘ufahamu wa kiroho’ na kufanya maendeleo. (Wakolosai 1:9, 10; 1 Timotheo 4:13, 15) Au huenda familia ikatumia lugha yao kuwasaidia wahamiaji wengine wanaoitumia kujifunza kweli.

Kwa upande mwingine, familia inaweza kuamua kwamba watafaidika zaidi wakijiunga na kutaniko linalotumia lugha kuu ya nchi wanamoishi. (Wafilipi 2:4; 1 Timotheo 3:5) Baada ya kujadiliana jambo hilo mkiwa familia, kichwa cha familia anapaswa kufanya uamuzi baada ya kusali. (Waroma 14:4; 1 Wakorintho 11:3; Wafilipi 4:6, 7) Ni madokezo yapi yanayoweza kusaidia familia hizi?

Madokezo Fulani Yanayofaa

Pedro na Sandra, waliotajwa awali, wanasema: “Ili tusisahau lugha yetu ya Kihispania, tumeweka sheria ya kuzungumza Kihispania pekee nyumbani. Ni vigumu sana kufuata sheria hiyo, kwa sababu wana wetu wanajua kwamba tunafahamu Kiingereza. Lakini tusipofanya hivyo, wanaweza kusahau lugha ya Kihispania.”

Miguel na Carmen, ambao pia walinukuliwa awali, wanapendekeza hivi: “Wazazi wakiongoza funzo la familia kwa ukawaida na kuzungumzia andiko la siku kwa kutumia lugha yao ya asili, basi watoto watajifunza mambo mengi mbali na kujua lugha ya wazazi wao—watajifunza kueleza mambo ya kiroho kwa lugha hiyo.”

Miguel pia anadokeza hivi: “Jitahidini kufanya kazi ya kuhubiri iwe yenye kufurahisha. Eneo letu linatia ndani sehemu kubwa sana ya jiji, nasi husafiri sana kwa gari tukitafuta watu wanaozungumza lugha yetu. Sisi hucheza michezo ya Biblia na kuzungumzia mambo muhimu tunaposafiri. Mimi hujaribu kupanga vyema safari hizo za kuhubiri ili tufanye ziara kadhaa za kurudia zenye matokeo. Siku iishapo watoto wetu huwa wamekuwa na mazungumzo yenye maana angalau na mtu mmoja.”

Kukabiliana na Tofauti za Kitamaduni

Neno la Mungu linawatia moyo vijana: “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, wala usiiache sheria ya mama yako.” (Mithali 1:8) Lakini matatizo yanaweza kutokea iwapo mafundisho ya baba na “sheria” ya mama itategemea utamaduni ulio tofauti kabisa na utamaduni ambao watoto wamezoea.

Bila shaka, kila kichwa cha familia anapaswa kuamua jinsi atakavyoongoza familia yake, na si lazima aige familia nyingine. (Wagalatia 6:4, 5) Hata hivyo, mawasiliano kati ya wazazi na watoto yanaweza kufanya iwe rahisi kwa wazazi kukubali utamaduni mpya.

Lakini, tamaduni na desturi nyingi ambazo zimeenea katika nchi zilizoendelea ni hatari sana kwa hali ya kiroho ya Wakristo. Kwa kawaida, matendo machafu ya kingono, pupa, na uasi huchochewa kupitia muziki na burudani zinazopendwa. (Waroma 1:26-32) Wazazi Wakristo hawapaswi kamwe kupuuza wajibu wao wa kuwasaidia watoto wao kuchagua muziki na burudani eti kwa sababu wazazi hawafahamu lugha vizuri. Ni lazima waweke sheria thabiti. Hata hivyo, huenda isiwe rahisi.

Carmen anasema: “Mara nyingi hatuelewi maneno ya muziki ambao watoto wetu husikiliza. Muziki waweza kuwa mtamu, lakini hatujui iwapo maneno yake yana maana nyingine tofauti au ni maneno machafu ya mitaani.” Wameshindaje tatizo hilo? Miguel anasema: “Tunatumia muda mwingi kuwafundisha watoto wetu kuhusu hatari za muziki mchafu, nasi hujitahidi kuwasaidia kuchagua muziki ambao unakubaliwa na Yehova.” Naam, ni muhimu kuwa waangalifu na kuwa na busara ili kukabiliana na tofauti za kitamaduni.—Kumbukumbu la Torati 11:18, 19; Wafilipi 4:5.

Thawabu

Hapana shaka yoyote kwamba kuwalea watoto katika nchi nyingine kunahitaji muda na jitihada nyingi. Lakini wazazi na watoto wanaweza kupata thawabu nyingi wakifanya hivyo.

Azzam na mkewe, Sara, walitoka Uturuki na kuhamia Ujerumani, ambako walilea watoto watatu. Mwana wao wa kwanza sasa anatumikia kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Selters, Ujerumani. Azzam asema: “Faida kubwa kwa watoto ni kwamba wanaweza kukuza sifa muhimu sana kutokana na tamaduni zote mbili.”

Antonio na Lutonadio walihamia Ujerumani kutoka Angola, na wana watoto tisa. Familia hiyo huongea Kilingala, Kifaransa, na Kijerumani. Antonio asema: “Kujua lugha mbalimbali kunaisaidia familia yetu kuwahubiria watu kutoka nchi nyingi. Hilo hutufurahisha kwelikweli.”

Watoto wawili wa wazazi Wajapani waliohamia Uingereza wanasema kwamba wananufaika sana kujua Kijapani na Kiingereza. Vijana hao wanasema hivi: “Kujua lugha mbili kulitusaidia kupata kazi. Tumefaidika kuhudhuria makusanyiko makubwa ya lugha ya Kiingereza. Vilevile, tuna pendeleo la pekee la kutumikia katika kutaniko la Kijapani lenye uhitaji mkubwa.”

Unaweza Kufaulu

Watumishi wa Yehova tangu nyakati za Biblia wamekabili tatizo la kulea watoto miongoni mwa watu wenye utamaduni tofauti. Wazazi wa Musa walifaulu, ijapokuwa alilelewa nchini Misri. (Kutoka 2:9, 10) Idadi kubwa ya Wayahudi waliokuwa uhamishoni huko Babiloni walilea watoto ambao walikuwa tayari kurudi Yerusalemu ili kuanzisha tena ibada ya kweli.—Ezra 2:1, 2, 64-70.

Vivyo hivyo leo, wazazi Wakristo wanaweza kufaulu. Huenda wakafurahi kuwasikia watoto wao wakisema maneno kama haya ambayo watoto fulani waliwaambia wazazi wao: “Familia yetu ina umoja kwa sababu Baba na Mama wanatutunza kwa upendo, sikuzote tumewasiliana vizuri pamoja nao. Tunafurahi kuwa washiriki wa familia ya ulimwenguni pote ya watumishi wa Yehova.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 24]

Kuzungumza tu lugha yenu ya asili nyumbani huwasaidia watoto wenu kujua mambo ya msingi ya lugha hiyo

[Picha katika ukurasa wa 24]

Uhusiano kati ya babu, nyanya na wajukuu huimarika wanapozungumza lugha moja

[Picha katika ukurasa wa 25]

Kujifunza Biblia pamoja na watoto wako hukuza ‘ufahamu wao wa kiroho’