Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unajua Jinsi ya Kungoja?

Je, Unajua Jinsi ya Kungoja?

Je, Unajua Jinsi ya Kungoja?

WAWEZA kuwazia kiasi cha wakati ambacho watu hutumia kila mwaka wakingoja tu? Wao hungoja kwenye foleni dukani au kwenye kituo cha petroli. Hungoja wahudumiwe mikahawani. Hungoja ili wamwone daktari. Hungoja mabasi na magarimoshi. Naam, mtu hutumia wakati mwingi sana katika maisha yake akingoja mambo yatendeke. Kwa mujibu wa kadirio moja, Wajerumani peke yao hupoteza muda wa saa bilioni 4.7 kila mwaka wakingoja katika misongamano ya magari barabarani! Mtu fulani alikadiria kwamba saa hizo ni sawa na jumla ya muda wanaotazamiwa kuishi watu 7,000.

Kungoja kwaweza kuvunja moyo sana. Leo, ni kana kwamba hakuna wakati wa kutosha kufanya mambo yote, na kuyafikiria mambo hayo mengine tunayopaswa kuwa tukifanya kwaweza kufanya kungoja kuwe jaribu kali. Mwandishi aitwaye Alexander Rose alisema hivi wakati mmoja: “Kungoja ni nusu ya mateso yapatikanayo maishani.”

Mwanasiasa Mmarekani Benjamin Franklin alitambua kwamba kungoja kwaweza kugharimu sana. Alisema hivi zaidi ya miaka 250 iliyopita: “Wakati ni fedha.” Hiyo ndiyo sababu mashirika ya kibiashara hutafuta njia za kuepusha ucheleweshaji usio wa lazima wakati wa kazi. Bidhaa nyingi zikizalishwa kwa wakati mchache, zaweza kuleta faida zaidi. Mashirika ya kibiashara yanayohudumia umma moja kwa moja hujaribu kutoa huduma za haraka—mikahawa, benki zinazotoa huduma ya haraka, na kadhalika—kwa sababu wanajua kwamba kumpendeza mteja hutia ndani kupunguza wakati wa kungoja.

Kupoteza Wakati Bure Maishani Mwetu

Mshairi Mmarekani wa karne ya 19, Ralph Waldo Emerson, siku moja alilalamika: “Sehemu kubwa sana ya wakati wa maisha ya mwanadamu hupotea akingojea!” Juzijuzi, mwandishi Lance Morrow alilalamika juu ya uchovu na usumbufu wa kungoja. Kisha akasema kuhusu “usumbufu usio dhahiri wa kungoja.” Huo ni nini? “Ni mtu kujua kwamba rasilimali yake yenye thamani zaidi, yaani wakati, ambayo ni sehemu ya maisha yake, inapotelea mbali, pasipo tumaini la kupatikana tena.” Yasikitisha, lakini ni kweli. Wakati unaopotea kwa sababu ya kungoja hupotea milele.

Pasipo shaka, ikiwa maisha hayangalikuwa mafupi sana hivi, kungoja hakungalihangaisha sana. Lakini maisha ni mafupi. Maelfu ya miaka iliyopita, mtunga-zaburi wa Biblia alisema hivi: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.” (Zaburi 90:10) Haidhuru twaishi wapi wala sisi ni nani, maisha yetu, yaani siku, saa, dakika zilizo mbele yetu tuzaliwapo, zina kikomo. Ijapokuwa hivyo, hatuwezi kuepuka hali zinazotulazimu kupoteza sehemu ya wakati huo wenye thamani tukingojea matukio au watu.

Kujifunza Jinsi ya Kungoja

Wengi wetu tumewahi kuwa katika gari ambalo dereva anajaribu kila mara kupita gari lililo mbele yake. Mara nyingi hapana haraka—dereva huyo hana jambo la haraka analoenda kufanya. Ingawa hivyo, hawezi kuvumilia dereva mwingine aongoze mwendo wake. Ukosefu wake wa subira waonyesha kuwa hajajifunza kungoja. Eti kujifunza? Naam, ni lazima mtu ajifunze jinsi ya kungoja. Hakuna azaliwaye na sifa hiyo. Watoto wachanga hutaka washughulikiwe mara moja wanapokuwa na njaa au wanaposumbuka. Wanapokua ndipo tu watambuapo kwamba nyakati nyingine ni lazima wangojee wanachotaka. Kwa kweli, kwa vile kungoja ni sehemu isiyoepukika ya maisha, kujua jinsi ya kungoja kwa subira iwapo lazima huonyesha mtu amekomaa.

Hapana shaka kuna hali za dharura ambapo ukosefu wa subira hueleweka. Inaeleweka wakati mume mchanga afanyapo hima-hima na kukataa kucheleweshwa kwa sababu anampeleka hospitali mkewe anayekaribia kujifungua. Malaika waliomsihi Loti aondoke Sodoma hawakuwa tayari kungoja huku Loti akikawia-kawia. Uharibifu ulikuwa karibu, na maisha ya Loti na familia yake yalikuwa hatarini. (Mwanzo 19:15, 16) Hata hivyo, katika hali nyingi, maisha hayawi hatarini wakati watu wanapolazimika kungoja. Katika hali hizo, mambo yangekuwa afadhali zaidi iwapo kila mtu angejifunza kusubiri—hata kama kungoja huko kumesababishwa na uvivu au kutokujali kwa mtu fulani. Zaidi ya hayo, ingekuwa rahisi zaidi kusubiri ikiwa kila mtu angejifunza jinsi ya kutumia kwa faida wakati unaotumiwa kungoja. Sanduku kwenye ukurasa wa 5 lina madokezo fulani ya kufanya kungoja kuvumilike zaidi na kuwe na faida.

Na ikumbukwe kwamba roho isiyo na subira huenda ikafunua mtazamo wenye kiburi, maoni ya kwamba mtu fulani ni muhimu sana asiweze kungojea. Kwa yeyote aliye na mtazamo huo, ni vema ayazingatie maneno ya Biblia: “Heri . . . mvumilivu rohoni kuliko mwenye roho ya kiburi.” (Mhubiri 7:8) Kiburi ni kasoro mbaya ya utu, na mithali ya Biblia yasema hivi: “Kila mwenye moyo wa kiburi ni chukizo kwa BWANA.” (Mithali 16:5) Huenda, basi, kujifunza kusubiri—kujifunza jinsi ya kungoja—kukahitaji tujichunguze kwa makini na pia tuchunguze mahusiano yetu na wengine wanaotuzunguka.

Subira Huvuta Heri

Kwa kawaida sisi huona ni rahisi kungoja iwapo twasadiki kwamba jambo tunalolingojea lafaa, na hata likituchelewesha litakuja hatimaye. Kwa hiyo, yafaa kukumbuka kwamba waabudu wote wa kweli wa Mungu wanangojea kutimia kwa ahadi zake nzuri zilizo katika Biblia. Kwa mfano, twaambiwa katika zaburi iliyopuliziwa na Mungu: “Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” Ahadi hiyo ilirudiwa na mtume Yohana aliposema: “Yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (Zaburi 37:29; 1 Yohana 2:17) Kwa wazi, ikiwa tungeweza kuishi milele, kungoja hakungekuwa tatizo kubwa. Lakini hatuishi milele sasa. Je, kweli ni jambo linalofaa kuongea juu ya uhai udumuo milele?

Kabla ya kujibu, kumbuka kuwa Mungu aliwaumba wazazi wetu wa kwanza wakiwa na tumaini la kuishi milele. Walipofanya dhambi ndipo wakapoteza tumaini hilo, kwao wenyewe na kwa watoto wao—kutia ndani sisi. Hata hivyo, punde baada ya dhambi yao, Mungu alitangaza kusudi lake la kukomesha matokeo ya kutotii kwao. Aliahidi kuja kwa “mbegu” fulani, nayo ikaja kuwa Yesu Kristo.—Mwanzo 3:15 NW; Waroma 5:18.

Lazima tufanye uamuzi wa kibinafsi iwapo twataka kunufaika kutokana na utimizo wa ahadi zake. Subira yahitajika ili kufanya hivyo. Ili kutusaidia kujifunza subira ya aina hiyo, Biblia yatutia moyo tuufikirie mfano wa mkulima. Yeye hupanda mbegu zake na hana budi kungojea kwa subira—akifanya yote awezayo kuilinda mimea yake—hadi wakati wa mavuno. Ndipo subira yake huleta thawabu, naye hupata matunda ya kazi yake. (Yakobo 5:7) Mtume Paulo ataja mfano mwingine wa subira. Atukumbusha juu ya wanaume na wanawake waaminifu wa kale. Walikuwa wakitazamia kutimia kwa makusudi ya Mungu, lakini iliwabidi kungojea wakati rasmi wa Mungu. Paulo atutia moyo tuwaige hao, “ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.”—Waebrania 6:11, 12.

Naam, kungoja ni jambo lisiloepukika maishani. Lakini si lazima kutokeze usumbufu kila mara. Kwa wale wanaongojea kutimia kwa ahadi za Mungu, kungoja kwaweza kuleta shangwe. Waweza kutumia wakati huo wa kungoja kwa kusitawisha uhusiano wa karibu na Mungu na kufanya kazi zinazodhihirisha imani yao. Na kwa sala, funzo, na kutafakari, wanaweza kusitawisha tumaini lisiloweza kuyumba-yumba kwamba mambo yote aliyoahidi Mungu yatatimia kwa wakati wake.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

PUNGUZA USUMBUFU WA KUNGOJA!

Panga mapema! Ukijua kwamba itakubidi kungoja, jitayarishe kusoma, kuandika, kushona, kufuma, au kufanya utendaji mwingine wenye faida.

Tumia wakati huo kutafakari, jambo linalozidi kuwa gumu katika ulimwengu wetu wenye haraka-haraka.

Weka vichapo fulani karibu na simu ili uvisome iwapo waambiwa usubiri; katika muda wa dakika tano au kumi, waweza kusoma kurasa kadhaa.

Unapongojea katika kikundi, tumia nafasi hiyo, iwapo yafaa, kuanzisha mazungumzo na wengine na kubadilishana nao mawazo yanayojenga.

Weka karatasi ya kuandikia au kichapo cha kusoma katika gari lako kwa ajili ya vipindi visivyotarajiwa vya kungojea.

Funga macho, pumzika, au sali.

MARA NYINGI KUNGOJA KWA MAFANIKIO KWATEGEMEA MTAZAMO WAKO NA KUPANGA MAPEMA.