Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utanufaikaje kwa Kumjua Mungu?

Utanufaikaje kwa Kumjua Mungu?

Kufikia sasa, tumechunguza hatua kadhaa zinazoweza kutusaidia kumjua Mungu. Kwanza, tuliona Biblia inasema kwamba jina lake ni Yehova na upendo ndio sifa yake kuu zaidi. Pia, tuliona mambo ambayo tayari amefanya na yale atakayofanya ili kuwanufaisha wanadamu wote. Ingawa bado kuna mambo mengi ya kujifunza kumhusu Mungu, bila shaka ungependa kujua jinsi utakavyonufaika kwa kumjua vizuri zaidi.

Yehova anaahidi kwamba “ukimtafuta, atakuruhusu umpate.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Ukimtafuta Mungu na kumjua, utapata zawadi yenye thamani sana—“urafiki wa karibu pamoja na Yehova”! (Zaburi 25:14) Uhusiano huo utakunufaishaje?

Utapata furaha ya kweli. Biblia inasema kwamba Yehova ni “Mungu mwenye furaha.” (1 Timotheo 1:11) Kuwa rafiki yake wa karibu na kuiga njia zake kutafanya uwe na furaha ya kweli itakayokunufaisha kihisia, kiakili, na kimwili pia. (Zaburi 33:12) Vilevile, utakuwa na maisha yenye furaha ikiwa utaepuka mazoea yasiyofaa, utasitawisha mazoea mazuri, na kudumisha uhusiano mzuri na wengine. Hatimaye, utakuwa na mtazamo kama wa mtunga zaburi aliyesema: “Kumkaribia Mungu ni jambo jema kwangu.”—Zaburi 73:28.

Mungu atakutunza na kukujali. Yehova aliwaahidi hivi watumishi wake: “Nitakupa ushauri jicho langu likikutazama.” (Zaburi 32:8) Hiyo inamaanisha kwamba Yehova anamjali kila mtumishi wake, na humtegemeza kila mmoja wao kulingana na uhitaji wake. (Zaburi 139:1, 2) Ukisitawisha uhusiano mzuri na Yehova, utatambua kwamba yeye ni mshikamanifu na hatakuacha kamwe.

Utakuwa na maisha mazuri wakati ujao. Zaidi ya kukuonyesha jinsi unavyoweza kuwa na maisha yenye furaha na yanayoridhisha sasa, Yehova Mungu anataka uwe na maisha mazuri wakati ujao. (Isaya 48:17, 18) Biblia inasema: “Uzima wa milele ndio huu, wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Katika siku hizi zenye misukosuko, tumaini ambalo Mungu ametupatia linaweza kuwa kama nanga inayotuwezesha kubaki tukiwa “hakika na imara.”—Waebrania 6:19.

Makala hii imetaja sababu chache tu kati ya sababu nyingi za msingi zinazotuchochea kujifunza kumhusu Mungu na kusitawisha uhusiano wa karibu na yeye. Ili kupata habari zaidi, unaweza kuzungumza na Shahidi wa Yehova au kutembelea tovuti ya jw.org.