Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | KUKABILIANA NA MAJANGA

Kufiwa na Mpendwa Wako

Kufiwa na Mpendwa Wako

Ronaldo, anayeishi Brazili, alikuwa kwenye gari lililopata aksidenti na kusababisha vifo vya watu watano wa familia yake kutia ndani baba na mama yake. Anasema hivi: “Baada ya kulazwa hospitalini kwa miezi miwili, niliambiwa kwamba walikufa kwenye ile aksidenti.”

“Mwanzoni, sikuamini kwamba walikuwa wamekufa. Kwa nini wote wafe? Nilipogundua kwamba ni kweli, nilishtuka sana. Sikuwahi kuhisi uchungu kama huo. Katika siku zilizofuata sikuona faida ya kuishi bila wao. Nililia kila siku kwa miezi kadhaa! Nilijilaumu kwa kumruhusu mtu mwingine aendeshe gari. Kama ningeendesha, huenda wangekuwa hai.

“Miaka kumi na sita imepita, na nimefaulu kuendelea na maisha kama kawaida. Hata hivyo, kifo chao kimeacha pengo kubwa maishani mwangu ambalo haliwezi kuzibwa.”

KUKABILIANA NA MAJANGA

Si vibaya kuomboleza. Biblia inasema kuna “wakati wa kuomboleza.” (Mhubiri 3:1, 4) Ronaldo anasema: “Kila nilipohisi kulia, nililia. Nilishindwa kujizuia, na baada ya kulia nilitulia.” Ni kweli kwamba watu huomboleza kwa njia tofauti. Hivyo, kama huonyeshi majonzi kwa nje, hilo halimaanishi kwamba huna huzuni au kwamba ujilazimishe kulia.

Usijitenge na watu. (Methali 18:1) “Niliepuka kujitenga na watu,” anasema Ronaldo. “Watu waliponitembelea niliwakaribisha. Pia, nilimweleza mke wangu na rafiki zangu wa karibu jinsi nilivyokuwa nikihisi.”

Uwe mtulivu mtu fulani anaposema maneno yenye kuumiza. Kwa mfano, huenda mtu akasema “Ni sawa tu.” Ronaldo anakumbuka, “Baadhi ya maneno yaliyokusudiwa kunifariji yalinivunja moyo.” Badala ya kukazia fikira maneno yanayoumiza, fuata ushauri huu wa Biblia: “Usiweke moyoni mwako maneno yote ambayo huenda watu wakasema.”—Mhubiri 7:21.

Jifunze ukweli kuhusu hali ya wafu. Ronaldo anasema hivi: “Kwenye andiko la Mhubiri 9:5, Biblia inaonyesha kwamba wafu hawateseki, na ukweli huo hunipa utulivu moyoni. Pia, Biblia inafundisha kwamba kutakuwa na ufufuo, na wale waliokufa wataishi tena. Kwa hiyo, mimi huwafikiria wapendwa wangu waliokufa kana kwamba wamesafiri.” —Matendo 24:15.

Je, wajua? Biblia inaahidi kwamba wakati ujao Mungu “atameza kifo milele.” *Isaya 25:8.

^ fu. 11 Kwa habari zaidi, ona sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Kinapatikana katika Intaneti kwenye www.jw.org/sw.