Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA I UUMBAJI

Uumbaji

Uumbaji

Je, Mungu aliiumba dunia kwa siku sita zenye urefu wa saa 24, kama watu fulani wanavyodai?

“Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” —Mwanzo 1:1.

BIBLIA INASEMA NINI

Mungu aliumba ulimwengu kutia ndani dunia, muda mrefu uliopita, yaani, “hapo mwanzo,” linasema andiko la Mwanzo 1:1. Wanasayansi wa kisasa wanakubali kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Katika miaka ya hivi karibuni, wanasayansi wamekadiria kwamba dunia imekuwepo kwa miaka bilioni 14 hivi.

Biblia inataja pia kuhusu “siku” sita za uumbaji. Hata hivyo, haisemi kwamba zilikuwa siku zenye urefu wa saa 24. (Mwanzo 1:31) Biblia inatumia neno “siku” kurejelea vipindi vya wakati vyenye urefu tofauti. Kwa mfano, inarejelea kipindi chote cha uumbaji kuwa “siku ambayo Yehova Mungu aliifanya dunia na mbingu.” (Mwanzo 2:4) Inaonekana kwamba “siku” hizo za uumbaji zilikuwa na urefu wa maelfu ya miaka.—Zaburi 90:4.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Maoni yasiyo sahihi kwamba dunia iliumbwa kwa siku sita zenye urefu wa saa 24 yanaweza kukufanya uipuuze Biblia. Kwa upande mwingine, ikiwa masimulizi ya Biblia kuhusu uumbaji ni sahihi, utafaidika kutokana na “hekima inayotumika” iliyo katika Biblia.—Methali 3:21.

 Je, Mungu alitumia mageuzi kuumba uhai duniani?

“Mungu akaendelea kusema: ‘Dunia na itokeze nafsi zilizo hai kulingana na aina zake.’” —Mwanzo 1:24.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mungu hakuumba viumbe duni kisha akaviruhusu vijigueze na kuwa viumbe vya hali ya juu. Badala yake, aliumba mimea na wanyama wa hali ya juu wa “aina” ileile, kisha wakazaana “kulingana na aina zake.” (Mwanzo 1:11, 21, 24) Viumbe hivyo vimeendelea kuzaana mpaka leo na hivyo kuijaza dunia “aina” zilezile za viumbe vilivyoumbwa na Mungu hapo mwanzo.—Zaburi 89:11.

Biblia haielezi unamna-namna unaoweza kutokea katika jamii fulani ya viumbe, kama vile wanyama wa aina tofauti katika jamii moja wanapozaana na kubadilika kulingana na mazingira. Ingawa huenda wengine wakadhani mabadiliko hayo ni mageuzi, hakuna kiumbe kipya kinachotokezwa. Utafiti wa kisasa unathibitisha kwamba kwa kipindi kirefu jamii za wanyama na mimea hazijabadilika sana.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Usahihi wa kisayansi wa Biblia kuhusu “aina” za viumbe unathibitisha kwamba Biblia ni sahihi kihistoria na pia kiunabii.

Vitu vilivyotumiwa kutengeneza ulimwengu vilitoka wapi?

“Mikono yangu mwenyewe imezitandaza mbingu.”—Isaya 45:12.

BIBLIA INASEMA NINI?

Mungu ndiye Chanzo cha nguvu au nishati isiyo na kikomo. (Ayubu 37:23) Hilo ni jambo muhimu kwa sababu wanasayansi wamegundua kwamba nishati inaweza kugeuzwa na kuwa kitu chenye uzani. Biblia inasema kwamba Mungu ndiye Chanzo cha “nguvu zenye msukumo” zilizotokeza ulimwengu. (Isaya 40:26) Mungu ameahidi kwamba atatumia nguvu zake kutegemeza uumbaji wake, kwa kuwa Biblia inasema hivi kuhusu jua, mwezi, na nyota: “[Mungu] huendelea kuvisimamisha milele, mpaka wakati usio na kipimo.”—Zaburi 148:3-6.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Wakati mmoja mtaalamu wa nyota, Allan Sandage alisema sayansi haiwezi kuthibitisha jinsi ulimwengu ulivyotokea. Biblia inaeleza uumbaji kwa njia inayopatana na sayansi na pia inajibu maswali ambayo sayansi imeshindwa kujibu, kama vile, Mungu ana kusudi gani kwa dunia na wanadamu? *

^ fu. 16 Ili upate habari zaidi ona sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.