Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa nini niishi kupatana na viwango vya Biblia?

Kwa nini niishi kupatana na viwango vya Biblia?

Vijana Huuliza . . .

Kwa nini niishi kupatana na viwango vya Biblia?

UMEKETI shuleni ukila chakula cha mchana pamoja na wasichana wawili. Mmoja wao anamwangalia kijana fulani.

Msichana wa kwanza anakuambia: “Unajua kijana yule anakupenda. Nilitambua mara moja nilipoona jinsi anavyokutazama. Macho yake hayabanduki!”

Msichana wa pili anasogeza kichwa chake karibu na sikio lako na kusema kwa sauti ya chini: “Acha nikuambie! Hana mpenzi!”

Msichana wa pili anasema: “Ubaya ni kwamba mimi tayari nina mpenzi, la sivyo ningeanzisha uhusiano naye mara moja!”

Kisha msichana wa kwanza anakuuliza swali ambalo huwa linakukera.

“Kwa nini huna mpenzi?”

Ulijua tu atakuuliza swali hilo. Kwa kweli, unatamani kuwa na mpenzi. Lakini umeambiwa kwamba ni bora ungoje kwanza hadi uwe tayari kwa ndoa ndipo uanze kumtafuta mchumba. Kama tu haingekuwa . . .

“Ni kwa sababu ya dini yako, siyo?” msichana wa pili anasema.

Unajiuliza kimoyomoyo, ‘Amejuaje, kwani anaweza kusoma akili yangu?’

“Wewe ni Biblia, Biblia, Biblia, huna hata uhuru,” msichana wa kwanza anakudhihaki. “Kwani huwezi kujifurahisha nyakati nyingine?”

Umewahi kupatwa na hali kama hiyo? Je, watu wamekudhihaki kwa sababu ya kujaribu kuishi kupatana na viwango vya Biblia? Ulijibuje?

▪ Ulitetea viwango vyako vya maadili kwa uthabiti.

▪ Uliaibika, lakini ukaeleza imani yako kwa kadiri ulivyoweza.

▪ Uliamua kwamba marafiki wako hawakuwa wamekosea na kwamba ulikuwa ukikosa mambo mengi yanayoleta raha!

Je, umewahi kujiuliza swali hili, ‘Kweli kuna umuhimu wa kuishi kupatana na kanuni za Biblia?’ Msichana mmoja anayeitwa Deborah alikuwa na maoni kama hayo. * Anasema hivi: “Wasichana wengine wa rika langu wangefanya lolote watakalo. Ni kama hawakuwajibika kwa yeyote. Nilihisi viwango vya Biblia vimenibana. Uhuru ambao marafiki wangu walikuwa nao ulinivutia.”

Je, Ni Vibaya Kuwa na Mashaka?

Mwandikaji wa Biblia Asafu alipitia kipindi fulani maishani mwake ambapo alijiuliza ikiwa ni muhimu kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Mwandikaji huyo aliandika hivi: “Niliwaonea wivu wenye kujisifu, nilipokuwa nikiiona amani ya watu waovu.” Hata alisema: “Hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kuiosha mikono yangu katika kutokuwa na hatia.”—Zaburi 73:3, 13.

Yehova Mungu anaelewa kwamba nyakati fulani watu wanaweza kuwa na mashaka kuhusu umuhimu wa kuishi kupatana na viwango vyake. Hiyo ndiyo sababu aliruhusu maneno ya Asafu yaandikwe katika Biblia. Mwishowe, Asafu aliamua kwamba kuishi kupatana na sheria ya Mungu ndiyo njia bora maishani. (Zaburi 73:28) Alifikia mkataa huo jinsi gani? Asafu alikuwa na hekima. Alifanya uamuzi huo, si kwa sababu ya kupatwa na misiba fulani, bali kwa kujifunza kutokana na makosa ya wengine. (Zaburi 73:16-19) Je, unaweza kufanya hivyo?

Jithibitishie Ukweli

Kinyume na Asafu, Mfalme Daudi alijifunza kutokana na hali ngumu alizopitia kwamba wale wanaopuuza viwango vya Mungu wanapatwa na madhara. Alifanya uzinzi pamoja na mke wa mtumishi wake, kisha akajaribu kuficha dhambi hiyo. Matokeo yakawa kwamba aliwaumiza watu wengine, kutia ndani Mungu, na akafadhaika sana. (2 Samweli 11:1–12:23) Baada ya Daudi kutubu, Yehova kupitia roho yake alimwongoza aeleze hisia zake kwa wimbo na akafanya maneno hayo yahifadhiwe katika Biblia kwa faida yetu. (Zaburi 51:1-19; Waroma 15:4) Kwa hiyo, ni jambo la hekima na linalopatana na Maandiko kujifunza kutokana na makosa ya watu wengine.

Ili kukusaidia uige mfano wa Asafu na uepuke makosa ya Daudi, fikiria maelezo ya vijana kutoka nchi kadhaa ambao kwa muda fulani walikataa viwango vya Biblia. Vijana hao walijihusisha na ngono kabla ya ndoa. Kama ilivyokuwa na Daudi, wao wametubu dhambi zao na sasa wana msimamo mzuri pamoja na Mungu. (Isaya 1:18; 55:7) Fikiria kile walichosema.

Amkeni!: Ni mambo gani yaliyochochea maoni na matendo yako?

Deborah: “Nilipokuwa shuleni niliona kila mtu akiwa na mpenzi, na walionekana kuwa na furaha. Nilipokuwa nao na kuwaona wakikumbatiana na kubusiana, niliona wivu na kujihisi mpweke. Nilijiruhusu kutumia wakati mwingi nikimfikiria kijana fulani niliyevutiwa naye. Hilo lilichochea tamaa ya kuwa naye na nilikuwa tayari kufanya chochote ili nitimize tamaa hiyo.”

Mike: “Nilisoma vitabu na kuona vipindi ambavyo vilitukuza ngono. Kuzungumza kuhusu ngono na marafiki wangu kuliamsha udadisi wangu. Kisha, nilipokuwa peke yangu na msichana nilifikiri kwamba ningeweza kumshika-shika bila kufanya ngono. Nilifikiri kwamba ningeweza kujizuia wakati wowote.”

Andrew: “Nilitazama ponografia (picha au habari za ngono) kwenye Intaneti. Nilianza kunywa kileo kwa wingi sana. Na nilihudhuria karamu pamoja na vijana ambao hawakuheshimu viwango vya maadili vya Biblia.”

Tracy: “Nilipokuwa na umri wa miaka 16, kuwa na mpenzi kulikuwa jambo muhimu zaidi maishani mwangu. Akilini nilijua kwamba kufanya ngono kabla ya ndoa ni dhambi, lakini sikuchukia jambo hilo. Sikukusudia kuwa na uhusiano wa kingono kabla ya ndoa, lakini hisia zangu zilizidi uwezo wangu wa kufikiri. Kwa muda, dhamiri yangu haikunisumbua.”

Amkeni!: Je, njia hiyo ya maisha ilikuletea furaha?

Deborah: “Mwanzoni, nilijihisi huru na nilifurahia kwamba sasa nilipendwa na watu wengine wa rika langu. Lakini hisia hizo hazikudumu. Nilianza kujiona kuwa mchafu, mwenye hatia, na asiye na maana. Nilijuta sana kwamba nilikuwa nimepoteza ubikira, kitu ambacho nisingekipata tena. Tangu wakati huo nimejiuliza mara nyingi, ‘Kwani nilifikiria mimi ni nani nisipatwe na madhara yoyote? Kwa nini—kwa nini nilipuuza viwango vyenye upendo vya Yehova?’”

Mike: “Nilianza kuhisi ni kama sehemu yangu fulani imekufa. Nilijaribu kupuuza jinsi matendo yangu yalivyowaathiri wengine, lakini singeweza. Ilihuzunisha kutambua kwamba katika kufuatia raha, nilikuwa nimewaumiza wengine. Nisingeweza kulala. Mwishowe, raha ya kufanya ngono haramu ilipotea, na mawazo yangu yalitawaliwa na hisia za maumivu na aibu.”

Andrew: “Ilianza kuwa rahisi zaidi kutenda kupatana na tamaa mbaya. Lakini wakati huohuo, nilikuwa nimelemewa na hisia za hatia na nilijichukia sana.”

Tracy: “Haikunichukua muda mrefu kutambua uhalisi wa mambo. Ukosefu wa adili katika ngono ulikuwa umeniharibia ujana wangu. Nilifikiri kwamba mimi na mpenzi wangu tungefurahia maisha. Lakini haikuwa hivyo. Mwishowe tuliumizana, tukasababishiana mateso na kuvunjika moyo. Nilikaa kitandani usiku mmoja baada ya mwingine nikilia na nikitamani kwamba ningefanya mambo kupatana na njia ya Yehova.”

Amkeni!: Ungewapa mashauri gani vijana wengine wanaojiuliza ikiwa viwango vya maadili vya Biblia vinabana?

Deborah: “Hutakuwa na maisha bora zaidi ukipuuza viwango vya Biblia. Hebu fikiria jinsi Yehova atakavyohisi ukifuata mashauri yake. Kisha ufikirie sana kuhusu matokeo ya kupuuza mashauri yake. Kumbuka, matendo yako hayakuathiri wewe tu. Yatawaathiri watu wengine. Ukipuuza mashauri ya Mungu, utajidhuru mwenyewe.”

Mike: “Ni kweli kwamba kijuujuu maisha ya vijana wenzako yanaonekana kuwa yanapendeza. Lakini chunguza mambo kwa undani zaidi. Yehova amekupa vitu vyenye thamani sana kwa kukuwezesha ujiheshimu na usiwe na lawama. Kutupa zawadi hizo kwa sababu huwezi kujizuia ni kujishusha sana. Zungumza na wazazi wako na watu wengine waliokomaa kuhusu matatizo yako. Ukikosea, funua jambo hilo mara moja na urekebishe makosa yako. Ukifanya mambo jinsi Yehova anavyotaka, utapata amani halisi.”

Andrew: “Usipokuwa na uzoefu, unaweza kufikiri kwamba vijana wenzako wana maisha yanayosisimua. Mtazamo wao utakuathiri. Kwa hiyo, chagua marafiki kwa hekima. Mtegemee Yehova, na utaepuka majuto mengi.”

Tracy: “Usijidanganye kwa kufikiri, ‘Jambo kama hilo haliwezi kunipata.’ Mama yangu aliniketisha chini na kuniambia waziwazi kwamba matendo yangu yatakuwa na matokeo mabaya. Niliudhika sana. Nilifikiri kwamba nilikuwa na hekima ya kutosha nisiweze kushawishiwa na mwenendo mbaya. Nilikuwa nimekosea. Ishi kupatana na viwango vya Yehova na ushirikiane na watu wanaofanya vivyo hivyo. Kufanya hivyo kutakuletea furaha zaidi.”

Je, Viwango vya Biblia Ni Pingu au Mkanda wa Usalama?

Iwapo vijana wenzako wanakudhihaki kwa sababu unajaribu kuishi kupatana na viwango vya Biblia, jiulize maswali yafuatayo: ‘Kwa nini hawataki kuishi kupatana na sheria za Biblia kuhusu maadili ya ngono? Je, wameisoma Biblia na kuchunguza faida zinazotokana na kutii amri za Mungu? Je, wamechunguza kwa uangalifu matokeo ya kupuuza viwango hivyo? Au badala yake, je, wanafuata tu kile ambacho kila mtu anafanya?’

Inaelekea kwamba unawafahamu watu ambao ‘wanafuata umati.’ (Kutoka 23:2) Je, hungependa kuwa na utu bora kuliko huo? Unaweza kuwaje tofauti? Kwa kufuata shauri la Biblia la ‘kujihakikishia mwenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ (Waroma 12:2) Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” na angependa uwe na furaha pia. (1 Timotheo 1:11; Mhubiri 11:9) Viwango vilivyo katika Biblia vipo kwa faida yako. Ni kweli kwamba unaweza kuviona kuwa pingu zinazozuia uhuru wako. Lakini ukweli ni kwamba viwango vya maadili vya Biblia ni kama mkanda wa usalama ndani ya gari unaomlinda msafiri asiumie.

Bila shaka, unaweza kuiamini Biblia. Ukichagua kuishi kupatana na viwango vyake, utamfurahisha Yehova na pia utajifaidi mwenyewe.—Isaya 48:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

MAMBO YA KUFIKIRIA

▪ Ni nini kinachoweza kufanya iwe vigumu kwako kuishi kupatana na viwango vya Biblia?

▪ Kwa nini unahitaji kujihakikishia kwamba kuishi kupatana na viwango vya Mungu ndiyo njia bora zaidi ya maisha?