Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Baraza la Jiji Hali Paswi Kupiga Ubwana”

“Baraza la Jiji Hali Paswi Kupiga Ubwana”

“Baraza la Jiji Hali Paswi Kupiga Ubwana”

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI KANADA

HATI ya Haki na Uhuru ya Kanada hulinda haki za raia wote wa Kanada. Uhuru wa kusema, wa vyombo vya habari, na wa ibada huidhinishwa kisheria na kutekelezwa na mahakama.

Hivyo, wakati jiji la Blainville, lililo kaskazini-magharibi mwa Montreal, lilipotoa pendekezo la kubadili sheria yake ili kuzuia ‘ziara za kidini’ zinazofanywa nyumba kwa nyumba bila kibali, Mashahidi wa Yehova walichukua kwa uzito jambo hilo. Badiliko hilo lingeathiri huduma yao ya nyumba kwa nyumba. (Matendo 20:20, 21) Lakini kwa nini badiliko hilo lilipendekezwa? Maofisa wa jiji walidai kwamba watu wengi walilalamika kuhusu ziara za nyumba kwa nyumba za Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, kulingana na rekodi za idara ya polisi, hakukuwa hata lalamiko moja kuhusu shughuli za Mashahidi wa Yehova katika muda wa miaka mitano iliyotangulia!

Hata hivyo, badiliko hilo likakubaliwa kisheria mwaka wa 1996. Mawakili wa Mashahidi wa Yehova wa Blainville walilijulisha jiji hilo kwamba ingekuwa kinyume cha sheria kwa jiji hilo kutumia sheria hiyo kuzuia shughuli za Mashahidi wa Yehova kwa sababu katiba inaruhusu uhuru wa kidini. Maofisa wa jiji walipuuza jambo hilo na kutoa hati 17 zilizowaamuru Mashahidi wafike mahakamani kujibu mashtaka. Mawakili wa Mashahidi waliamua kuwasilisha kesi mahakamani ili kuzuia jiji la Blainville lisikandamize uhuru wa kidini na wa kusema, ambazo ni haki za raia wote wa Kanada.

Kesi hiyo ilisikilizwa katika Mahakama Kuu ya Quebec mbele ya Jaji Jean Crépeau, mnamo Oktoba 3 na 4, 2000. Baada ya kuchunguza mambo yote, jaji huyo alifanya uamuzi uliowaunga mkono Mashahidi wa Yehova. Jaji Crépeau alikubali kwamba “Mashahidi wa Yehova wanafuata kielelezo cha kutaniko la Kikristo la kwanza kwa kwenda nyumba kwa nyumba katika ujirani wao ili kuwatia watu moyo kudumisha maadili ya juu na hali nzuri ya kiroho. . . . Kutembelea nyumba za watu ni huduma ya Kikristo kwa jamii. Mashahidi wa Yehova huwatembelea raia wa Blainville angalau mara moja kila miezi minne ili kuzungumza nao kuhusu mambo yanayojenga na yanayowapendeza watu.” Katika uamuzi wake, Jaji Crépeau alisema: “[Mahakama] inatangaza kwamba Mashahidi wa Yehova hawako chini ya wajibu wa kupata kibali ili kufanya huduma yao.”

Jiji la Blainville lilikata rufani dhidi ya uamuzi wa Jaji Crépeau katika Mahakama ya Rufaa ya Quebec. Kesi ya rufani ilisikilizwa mnamo Juni 17, 2003, na uamuzi uliopatana na uamuzi wa jaji wa kwanza ukatolewa mnamo Agosti 27, 2003. Ikinukuu Hati ya Haki na Uhuru ya Kanada, ambayo hulinda uhuru wa kidini na inahusisha haki ya kufundisha na kusambaza imani za kidini, Mahakama hiyo ilitoa taarifa iliyosema hivi: “Sheria hiyo inayotiliwa shaka inazuia kabisa uhuru wa kidini wa Mashahidi wa Yehova na uhuru wa mawazo, uhuru wa imani, uhuru wa maoni, na uhuru wa kusema wa raia wa Blainville . . . Uthibitisho unaonyesha kwamba wakazi wa Blainville hawakulalamika kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiwasumbua kwa kwenda nyumba kwa nyumba, bali walikuwa wakilalamika kuhusu ziara za wachuuzi na wafanyabiashara wengi. Hakukuwa na uhitaji mkubwa na wa lazima wa kuzuia ziara za nyumba kwa nyumba zinazofanywa kwa makusudi ya kidini. Isitoshe, sheria hiyo haikutungwa kwa uangalifu na iliidhinishwa haraka-haraka kabla ya kupata maoni ya watu, na haipatani na akili wala lengo lililotajwa la kulinda faragha ya raia. . . . Katika jamii huru na ya kidemokrasia, baraza la jiji halipaswi kupiga ubwana kwa kujaribu kuamua ni nani watakaotembelea raia jioni au mwishoni mwa juma. Jaji wa kwanza hakukosea kutangaza kwamba sheria hiyo haipaswi kuwaathiri Mashahidi wa Yehova.”

Mashahidi wa Yehova wanafurahi kwamba mahakama za Quebec zimetumia Hati ya Haki ya Kanada ili kulinda uhuru wa kidini wa raia wote wa Quebec dhidi ya ukandamizaji.

[Ramani katika ukurasa wa 24]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

KANADA

Blainville

Montreal

MAREKANI

[Picha katika ukurasa wa 24]

Hati ya Haki na Uhuru ya Kanada hulinda haki za raia wote wa Kanada

[Picha katika ukurasa wa 25]

Sasa Mashahidi wanaweza kutimiza kwa uhuru huduma yao ya hadharani huko Blainville. Ndani: Mkutano kwenye Jumba la Ufalme la kwao