Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Inamaanisha Nini Kuwa Kichwa cha Familia?

Inamaanisha Nini Kuwa Kichwa cha Familia?

Maoni ya Biblia

Inamaanisha Nini Kuwa Kichwa cha Familia?

KULINGANA na Biblia, “kichwa cha mwanamke ni mwanamume.” (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:23) Lakini wengi wanaodai kuiheshimu Biblia wanahisi kwamba kanuni hiyo ya mwanamume kuwa kichwa ni ya kale na hatari pia. Wenzi fulani wa ndoa walisema hivi: “Fundisho la kwamba wanawake wanapaswa ‘kujitiisha [chini ya waume zao] kwa kupenda’ likitumiwa vibaya, linaweza kusababisha dhuluma ya kimwili na ya kihisia.” Kwa kusikitisha, matumizi mabaya ya ukichwa yameenea sana. Mwandishi mmoja alisema kwamba “katika nchi nyingi kumpiga mke huonwa kuwa jambo linalokubalika na pia kuwa ni haki ya wanaume, na nyimbo, methali, na sherehe za arusi hutukuza maoni hayo.”

Watu wengi wanadai kwamba kanuni ya Biblia ya ukichwa imesababisha dhuluma hiyo. Je, fundisho la Biblia la ukichwa huwashusha wanawake na kuchochea jeuri ya nyumbani? Inamaanisha nini kuwa kichwa cha familia? *

Ukichwa Si Kupiga Ubwana

Ukichwa wa Kimaandiko ni mpango wenye upendo unaotofautiana sana na kupiga ubwana. Kutotii mamlaka iliyotoka kwa Mungu ndiko kulikosababisha wanaume wawatawale wanawake kikatili mara nyingi. (Mwanzo 3:16) Tangu katika shamba la Edeni, mara nyingi wanaume wametumia mamlaka yao vibaya, wakiwakandamiza wengine kikatili, kutia ndani wanawake na watoto.

Hata hivyo, hilo halikuwa kusudi la Mungu. Yehova huwachukia wale wanaotumia mamlaka yao vibaya. Aliwashutumu wanaume Waisraeli waliowatendea wake zao “kwa hila.” (Malaki 2:13-16) Zaidi ya hilo, Mungu husema kwamba “mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia.” (Zaburi 11:5) Kwa hiyo, wale wanaowapiga au kuwadhulumu wake zao, hawapaswi kutumia Biblia kutetea jeuri yao.

Ukichwa Unaofaa Unahusisha Nini?

Ukichwa ni mpango wa msingi ambao Mungu anatumia kudumisha utaratibu katika ulimwengu wote. Kila mtu, isipokuwa Mungu, yuko chini ya mtu fulani. Waume wako chini ya Kristo, watoto wako chini ya wazazi, na Wakristo wote wako chini ya serikali. Hata Kristo yuko chini ya Mungu.—Waroma 13:1; 1 Wakorintho 11:3; 15:28; Waefeso 6:1.

Kujitiisha kwa ukichwa ni kwa lazima ili kuwe na utaratibu katika jamii. Vivyo hivyo, kujitiisha chini ya kichwa cha familia ni kwa lazima ili kujenga familia iliyo imara, yenye furaha, na yenye amani. Kanuni hiyo haibadiliki hata kama familia haina baba au mume. Katika familia za aina hiyo mama ndiye kichwa. Ikiwa wazazi wote wawili hawapo, mtoto mkubwa au mtu mwingine wa ukoo anaweza kuwa kichwa cha familia. Katika hali hizo zote, washiriki wa familia hunufaika wanapoonyesha heshima inayofaa kwa yule mwenye mamlaka ya kuongoza.

Basi, jambo muhimu si kukataa kanuni ya ukichwa, bali ni kujifunza kuutumia ukichwa kwa njia inayofaa na kuwa na maoni mazuri kuhusu mpango huo. Mtume Paulo anawahimiza waume Wakristo kuwa vichwa vya familia zao “kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko.” (Waefeso 5:21-23) Hivyo, Paulo anaonyesha jinsi Kristo alivyoshughulika na kutaniko akiwa mfano mkamilifu wa ukichwa. Kristo aliweka mfano gani?

Yesu akiwa Masihi na Mfalme wa wakati ujao, alikuwa amepewa mamlaka na Mungu mwenyewe na alikuwa na akili na ujuzi mwingi maishani kuliko wanafunzi wake. Hata hivyo, yeye alikuwa mwenye upendo, shauku, na huruma. Kamwe hakuwa mkatili, asiyebadilika kulingana na hali, au mwenye kudai mengi mno. Hakuwatawala wengine na kuwakumbusha daima kwamba alikuwa Mwana wa Mungu. Yesu alikuwa mnyenyekevu moyoni. Hivyo, ‘nira yake ilikuwa laini na mzigo wake mwepesi.’ (Mathayo 11:28-30) Alikuwa mwenye urafiki na alikubali maoni ya wengine. Isitoshe, Paulo anasema kwamba Yesu alilipenda kutaniko sana hivi kwamba ‘akajitoa mwenyewe kwa ajili yake.’—Waefeso 5:25.

Mtu Anawezaje Kuiga Ukichwa wa Yesu?

Vichwa vya familia wanawezaje kuiga sifa za Kristo? Kichwa cha familia anayechukua madaraka kwa uzito hujali mahitaji ya kimwili na ya kiroho ya familia yake. Yeye hujitoa kwa kutenga wakati wa kutosha ili kushughulikia mahitaji ya mshiriki mmoja-mmoja au ya familia nzima. Yeye hutanguliza faida za mwenzi wake na za watoto wake. * (1 Wakorintho 10:24; Wafilipi 2:4) Mume anapotumia kanuni na mafundisho ya Biblia maishani mwake kila siku, yeye huheshimiwa na kutegemezwa na mke na watoto wake. Chini ya ukichwa wake wenye upendo, jitihada za pamoja za familia za kushinda magumu zinaweza kufanikiwa. Hivyo, kwa kutumia ukichwa wake kulingana na Maandiko, mume hujenga familia yenye furaha inayomletea Mungu utukufu na sifa.

Kichwa cha familia mwenye hekima ni mnyenyekevu pia. Inapohitajiwa, ataomba msamaha kwa hiari, ingawa huenda ikawa vigumu kukubali kwamba alikosea. Biblia husema kwamba kuna wokovu “kwa wingi wa washauri.” (Methali 24:6) Naam, unyenyekevu utamchochea kichwa cha familia kusikiliza na kuomba maoni ya mke na watoto wake inapofaa. Kwa kumwiga Yesu, kichwa cha familia Mkristo atahakikisha kwamba ukichwa wake hauleti tu furaha na usalama katika familia yake, bali pia unamheshimu na kumtukuza Mwanzilishi wa familia, Yehova Mungu.—Waefeso 3:14, 15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Ingawa makala hii inazungumzia hasa daraka la mume na baba katika familia, akina mama wasio na wenzi na yatima wanaowatunza ndugu zao wadogo wanaweza pia kunufaika na kanuni zinazotolewa kwa vichwa vya familia.

^ fu. 14 Kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova, kina mapendekezo mazuri kuhusu kutunza familia kwa upendo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Mume mwenye busara hufikiria maoni ya mke na watoto wake