Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumfundisha Kristi Kumpenda Mungu

Kumfundisha Kristi Kumpenda Mungu

Kumfundisha Kristi Kumpenda Mungu

BINTI yetu Kristi alizaliwa mwaka wa 1977. Muda mfupi baadaye, daktari alituambia habari zenye kuhuzunisha: Kristi alipozaliwa hakuwa na uwezo wa kusikia naye alikuwa na ugonjwa wa kupooza pia. Hatukujua maisha yetu yangekuwaje.

Miezi michache baadaye, mimi na mume wangu Gary tulianza kuhudhuria masomo ya pekee katika jiji la Melbourne, nchini Australia, ambako tulijifunza jinsi ya kuwasiliana na binti yetu. Pia tulitembelea Maabara ya Kitaifa ya Sauti ya Melbourne. Akiwa huko, Kristi alipewa vifaa vya kumsaidia kusikia akiwa na umri wa miezi kumi. Hakupenda vifaa hivyo, na kwa kuwa vilikuwa na nyaya, aliving’oa mara tu tulipoviingiza kwenye masikio yake madogo! Pia, alipaswa kuvaa mshipi wa kushikilia betri ambazo zilikuwa nzito sana.

Kwa sababu ya ugonjwa wake wa kupooza, ilikuwa vigumu kwa Kristi kujifunza kutembea. Kwa hiyo alihitaji kuzoezwa kila juma na daktari wa kunyoosha viungo. Lakini akiwa na umri wa miaka mitatu, Kristi alianza kutembea ingawa alianguka mara nyingi. Aliendelea kupewa mazoezi mpaka alipokuwa na umri wa miaka mitano. Wakati huohuo, tulihamia mji ulio karibu na Benalla, ambapo Gary aliendesha biashara yake.

Elimu ya Kristi

Mwalimu wa viziwi alitueleza kuhusu elimu ya pekee ambayo Kristi angepata. Hiyo ilitulazimu tuhamie jiji la Bendigo ambalo lilikuwa na shule ya viziwi. Kwa kuwa nilikuwa mjamzito nikitarajia mtoto wa pili, tuliahirisha kuhama mpaka Kristi alipokuwa na umri wa miaka minne, na Scott mwana wetu aliyezaliwa karibuni akiwa na umri wa miezi mitano. Katika hospitali huko Bendigo, mazoezi ya kila juma ya kujifunza kuongea yalianza na yaliendelea kwa miaka kumi. Mimi na Gary tulianza pia kujifunza lugha ya ishara.

Tulihangaikia hasa hali ya kiroho ya Kristi. Kwa kuwa mimi na Gary ni Mashahidi wa Yehova, tulitaka kumlea Kristi “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Lakini tungefanyaje hivyo? Mwalimu mkuu wa shule ya Kristi alisema: “Kumfundisha Kristi kumhusu Mungu kutakuwa jambo gumu zaidi. Huwezi kumwona Mungu, kwa hiyo utamwelezaje kumhusu?” Tulikuwa na kibarua kigumu! Tuligundua kwamba tungehitaji subira, kujifunza, na muda mrefu.

Mwanzoni tulitumia picha na michoro, na tulijaribu kutumia lugha rahisi. Tulimpeleka kwenye mikutano ya Kikristo na katika kazi ya kuhubiri, ijapokuwa hakuelewa kinachoendelea. Kristi alipojua lugha ya ishara, maisha yake yalibadilika sana! Hata hivyo, ilikuwa vigumu kueleza maneno, semi, na mafundisho mengi katika Biblia. Kimojawapo cha vitabu alivyopenda ni Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, * kilichoandikwa hasa kwa ajili ya watoto. Picha zenye rangi nzuri pamoja na michoro tuliyochora ilisaidia sana. Muda si muda, Kristi akaanza kusitawisha upendo kwa Mungu.

Kwa fadhili, mwalimu mkuu wa shule ya Kristi alitujulisha kuhusu Mashahidi wengine wenye watoto viziwi. Tulifanya maendeleo makubwa Mashahidi hao walipotueleza jinsi viziwi wanavyoweza kuwahubiria watu wanaoweza kusikia. Njia moja ni kuwapa kadi iliyo na ujumbe wa Maandiko. Kwa hiyo, Kristi angeweza kuwaeleza wengine kweli za Biblia kwa urahisi! Akawa mhubiri wa habari njema asiyebatizwa akiwa na umri wa miaka 14. Alibatizwa mwaka wa 1994 akiwa na umri wa miaka 17.

Kristi alihitaji marafiki wazuri, lakini ilikuwa vigumu kukuza urafiki na Mashahidi wanaoweza kusikia. Kwa hiyo, mimi na Gary tukaanza kuwafundisha lugha ya ishara washiriki wa kutaniko letu waliotaka kuwasaidia viziwi. Baadhi ya wale tuliofundisha walipata kazi ya kuwatafsiria viziwi. Lakini zaidi ya yote, wengi waliojifunza lugha ya ishara walifurahia sana kuzungumza na Kristi. Sasa Kristi akafaidika zaidi kutokana na mikutano na makusanyiko ya Kikristo. Mpaka sasa anashiriki sana kwenye mikutano hiyo. Kristi anashukuru kwa upendo ambao akina ndugu wamemwonyesha.

Siku moja Kristi alituambia kwamba anatamani kuwa painia wa kawaida au mhubiri wa wakati wote. Gary alimsaidia Kristi kupata leseni ya kuendesha gari, na baada ya kupanga mambo mengine, Kristi aliwekwa rasmi kuwa painia wa kawaida mwaka wa 1995. Mwaka wa 2000, alipata kazi ya muda katika shule ya msingi ambapo anawafundisha watoto viziwi.

Mimi, Kristi, Gary, na mwana wetu Scott, sasa tunafurahi kutumikia tukiwa mapainia wa kawaida. Tunafurahi kutumia wakati kuwafundisha watu kumhusu Mungu wetu, Yehova!

‘Maombi ya Mioyo Yetu’

Sisi sote tunakabili hali ngumu kwa sababu ya hali ya Kristi ya kutoweza kusikia. Wakati mwingine Kristi anapokuwa katika huduma ya Kikristo, hana mtu wa kumtafsiria wala wa kumweleza mawazo na hisia zake. Kristi anasema: “Ni kana kwamba ninaishi katika nchi ambayo kila mtu anazungumza lugha tofauti.” Hata hivyo, sote tumejifunza kukabiliana na hali yake vizuri.

Tunafarijiwa na maneno haya ya Zaburi 37:4: “Upate furaha tele katika Yehova, naye atakupa maombi ya moyo wako.” Kristi anatamani sana kusikiliza muziki na sauti za asili na kuzungumza na wapendwa wake. Natamani siku ambayo Kristi ataweza kusikia sauti yangu. Tuna hakika kwamba maombi hayo ya mioyo yetu yatatimizwa karibuni kama vile Biblia inavyoahidi.—Isaya 35:5.—Tumetumiwa makala hii.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Kristi, akiwa ameshika “Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia” akiwa na umri wa miezi 14

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kristi anahubiri habari njema akitumia kadi yenye ujumbe

[Picha katika ukurasa wa 15]

Scott, Kristi, Gary, na Heather Forbes leo