Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dunia Isiyokuwa na Mabomu ya Ardhini

Dunia Isiyokuwa na Mabomu ya Ardhini

Dunia Isiyokuwa na Mabomu ya Ardhini

NI NANI awezaye kutatua tatizo la mabomu ya ardhini? Kama tulivyokwisha kuona, wanadamu hawawezi kukomesha chuki, ushupavu, na pupa. Hata hivyo, wanafunzi wa Biblia hung’amua kwamba Muumba anaweza kutatua tatizo hilo kabisa. Atalitatuaje?

Kutokeza Jamii Yenye Amani

Watu ndio wanaopigana vita, si silaha. Kwa hiyo, chuki inayowatenganisha wanadamu kwa vikundi vya kijamii, kikabila, na kitaifa sharti ikomeshwe kabisa iwapo twataka amani. Mungu aahidi kuikomesha kupitia kwa Ufalme wake, ambao mamilioni ya watu duniani wamefunzwa kusali juu yake.—Mathayo 6:9, 10.

Biblia humtaja Yehova kuwa “Mungu apaye amani.” (Waroma 15:33) Amani anayotoa Mungu haitegemei marufuku na mikataba, wala haitegemei hofu ya ulipizaji kisasi wa taifa adui lenye silaha kali. Kinyume cha hilo, amani itokayo kwa Mungu huhusisha mabadiliko katika njia ya watu ya kufikiri na mitazamo yao kuelekea wanadamu wenzao.

Yehova Mungu atawafundisha wanyenyekevu njia zake za amani. (Zaburi 25:9) Neno lake, Biblia, huahidi wakati ambapo wote walio hai “watafundishwa na BWANA; na amani ya watoto wako itakuwa nyingi.” (Isaya 54:13) Jambo hilo tayari linatukia kwa kadiri fulani. Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wana sifa ya kudumisha amani hata miongoni mwa watu wenye malezi mbalimbali. Watu wanaofundishwa kanuni bora za Biblia hujitahidi kuishi kwa umoja bila kujali maswala yanayoweza kuwatenganisha. Elimu ya Biblia hubadili kabisa mtazamo wa chuki waliokuwa nao kuwa wa upendo.—Yohana 13:34, 35; 1 Wakorintho 13:4-8.

Mbali na elimu, uhitaji wa ushirikiano wa ulimwenguni pote umeonwa kwa muda mrefu kuwa jambo muhimu katika kuharibu silaha. Kwa mfano, Shirika la Kimataifa la Msalaba Mwekundu linapendekeza kwamba jumuiya ya kimataifa ishirikiane katika kudumisha hali zitakazozuia na kukomesha kabisa tisho la mabomu ya ardhini.

Yehova anaahidi kutimiza mengi zaidi. Nabii Danieli alitabiri hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele. . . . Utavunja falme hizi zote [zilizopo] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

Ufalme wa Mungu utatimiza mambo ambayo mwanadamu hawezi kutimiza. Kwa mfano, Zaburi 46:9 yatabiri: “[Yehova] avikomesha vita hata mwisho wa dunia. Avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.” Ufalme wa Mungu utatokeza mazingira ambamo mwanadamu atafurahia kabisa amani kati yake na Muumba wake na mwanadamu mwenzake.—Isaya 2:4; Sefania 3:9; Ufunuo 21:3, 4; 22:2.

Augusto, aliyetajwa mwanzoni mwa makala iliyotangulia, hufarijiwa na ujumbe huo wa Biblia. Wazazi wake, ambao ni Mashahidi wa Yehova, wanamsaidia kujenga imani katika ahadi nzuri ajabu za Biblia. (Marko 3:1-5) Bila shaka, hana budi kuvumilia sasa maumivu yanayotokana na mlipuko wa bomu la ardhini lililomlemaza. Hata hivyo, Augusto atazamia wakati ambapo ahadi ya Mungu ya paradiso duniani itakapotimizwa. “Ndipo,” akatabiri nabii Isaya, “macho ya vipofu yatafumbuliwa, na . . . mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu.”—Isaya 35:5, 6.

Katika Paradiso ijayo, mabomu ya ardhini hayatahatarisha tena uhai na viungo vya mwili. Badala yake, watu wataishi kwa usalama duniani kote. Nabii Mika alisema hivi: “Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu; kwa kuwa kinywa cha BWANA wa majeshi kimesema hivi.”—Mika 4:4.

Je, ungependa kujifunza mengi juu ya ahadi za Mungu zilizo katika Neno lake Biblia? Wasiliana na Mashahidi wa Yehova walio karibu nawe, au andika kwa anwani ifaayo iliyoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Chini ya Ufalme wa Mungu, mabomu ya ardhini hayatakuwa tisho tena